Endelea kulike: www.facebook.com/2jiachie
Tembelea: www.2jiachie.comILIPOISHIA: Alimwalia James kwa macho yaliyojaa furaha, akamkumbatia na kumsogeza kifuani pake kisha kuanza kumpa mabusu mfululizo.
SHUKA NAYO MWENYEWE…
“Mbona umeonekana kuwa na furaha ghafla, vipi kwani?” aliuliza James baada ya kumwona Lina akihema kwa nguvu na kumvutia kwake kumpa mabusu mfululizo…
“Hamna mume wangu jamani, siku hazilingani hata siku moja, nikoje kwani mume wangu?” Sasa Lina alipata hata muda wa kusema neno ‘mume wangu.’
“Uko happy ghafla.”
“Aaah jamani baby. Lina alizidi kumbusu James mpaka wakajikuta wamezama kwenye ulingo mwingine kabisa wa mahaba mazito juu ya kitanda.
Lina siku hiyo alimfanyia mambo makubwa ya kimapenzi James kama siku yao ya kwanza kukutana ilivyokuwa.
Kila hatua, Lina alihakikisha anatoa kilio cha mahaba huku akimsifia James kwamba ni mwanaume bora kwake licha ya kwamba alijua furaha yake inaweza kuwa ya muda mfupi kuliko kilio kitakachofuata mbele yake siku chache zijazo.
Lina alilala kwa furaha siku hiyo, usiku alipata hata muda wa kuchati na mumewe, Semi kwani James aliwahi kulala akijua ana safari ya kumpeleka stendi Lina asubuhi kwa safari ya kwao, Korogwe.
Kulikucha salama, Lina alijiandaa kwa safari, akapakizwa kwenye gari na James hadi Ubungo.
“Baby mpe pole sana mama, mwambie nampenda panapo majaliwa nitamuona siku moja na Mungu atamsaidia afya njema,” alisema James wakati Lina akijiandaa kupanda basi ndani ya stendi ya Ubungo.
Walipeana mabusu ya nguvu ndani, gari lilikuwa na vioo visivyoonwa ndani yaani ‘tintedi.’
Walipanda wote ndani ya basi baada ya kukata tiketi, Lina akakaa kwenye siti yake huku James akisimama pembeni akizidi kumwombea dua njema kwa safari yake. Baada ya dereva kuingia na kuingiza gia, James alimbusu Lina mbele za watu, akashuka.
Cha kwanza baada ya James kushuka, Lina aliingiza mkono kwenye mkoba wake na kutoa kitita cha pesa alizopewa na James kikiwa ndani ya bahasha. Alihesabu mpaka alipoweka kituo, tayari alishajua amepewa shilingi milioni moja na laki tano.
“Mh!” aliguna Lina, akaangalia juu ya gari kisha akawaangalia abiria wenzake na kuwaona hawana maana, maskini wakubwa.
Basi liliondoka Ubungo, likashika Barabara ya Morogoro na kusogelea mataa ya Ubungo. Mungu ibariki, taa zikaruhusu magari kupita, dereva alivusha gari na kuishika njia ya kwenda Kimara…
Ah! Konda samahani, mzigo niliokuwa nakwenda nao Korogwe nimeusahau nyumbani jamani,” alisema kwa sauti Lina huku akiwa ameshasimama na kutembea kwa kasi kuelekea mlango mkubwa.
Abiria wengine walimpa pole wengine walimshangaa kwa kuhoji iweje mtu asafari mpaka ndani ya basi kumbe anachokipeleka amekiacha nyumbani? Waliona ni usanii mtupu.
“Shusha konda, samahani sana,” alisema Lina.
Dereva akaweka gari pembeni maeneo ya Kimara-Rombo, Lina akashuka huku konda akimkazia macho kuamini kwamba huenda atadai nauli lakini wala!
Akiwa chini ya sasa, Lina aliangaza pembeni na kuona Bajaj…
“Tafadhali nipeleke Kijitonyama.”
Lina alipofika nyunbani kwake, yaani kwake na Semi, alizama ndani akiwa haamini kilichotokea. Alishika simu na kumtwangia Eg kumpa mkasa wote, Eg alishangaa sana. Hakuamini kile alichokuwa anasimuliwa na Lina.
“Sasa mpendwa wangu, ukimwambia umefika si atataka kuzungumza na mama?” aliuliza Eg.
“Nitamwambia hawezi kuongea kwani si nimemwambia mama anaumwa, sijasema anafanyiwa bethidei!”
“Hapo sawa. Kwa hiyo sasa upo nyumbani?”
“Nimejaa tele, nabadili nguo nakwenda kazini.”
Ghafla Lina akakumbuka kwamba, James huwa anakwenda sana kazini kwake na ndiko walikokutania, itakuaje akifika na kumkuta?
Alifikiria kutuma udhuru kwa mabosi wake lakini akaona kwamba ataonekana mvivu maana siku mbili tatu zilizopita alishatoa udhuru mwingine.
“Mh! Sasa itakuaje? Hapa mawili, nitoe udhuru au niende. Lakini nikienda akitokea James nimeumbuka,” alisema moyoni Lina.
Muda huohuo meseji ikaingia kwenye simu yake, akajua ni James lakini sivyo, alikuwa bosi wake…
“Lina hakikisha unafika kazini leo, kuna kazi nyingi sana zimelala. Usikose.”
Lina alijishika kichwani, akajikuna kidogo, akahema…
“Nahisi nimepatikana leo, sina ujanja. Miongoni mwa hizo kazi nyingi anazosema bosi ni pamoja na za James,” alisema moyoni Lina huku akikosa amani ya moyo.
Lina alibadili nguo, akaondoka kuelekea kazini. Ile anaingia tu ndani ya geti, James anapaki gari nje…
“Mungu wangu ndiyo mambo niliyoyakataa haya,” alisema Lina akikimbilia ndani, akaenda kuingia kwenye chumba cha kuchemshia chai ambako mchemsha chai alimshangaa…
“Lina vipi tena, unakimbizwa?”
“We acha tu! Naomba utoke, mfuatilie kaka mmoja anaingia, naamini atakuwa ameshika brifkesi, jua anaingia wapi, anatoka muda gani,” aliagiza Lina.
“Pole na kuumwa mama?”
“Aaa…santé saa…na.”
“Basi sawa mama, we pumzika tutawasiliana tena baadaye.”
“Ha…haya…aa.”
Lina aliipokea simu na kuangua kicheko ambapo mwanamke huyo naye aliungana naye kwa usanii walioufanya.
“Daa! Jamani! Ama kweli dunia tambara bovu,” alisema mama mpika chai…
“Umeona ee?”
“Nimeona Lina.”
“Sasa mama wewe utanisaidiaje katika hili?”
“Hili suala ni gumu sana mwanangu, tena gumu kwelikweli. Ila cha kufanya wewe kuwa muwazi kwa James, mwambie ukweli wako.”
“Hee! Si atanipeleka polisi?”
“Akupeleke polisi kwa kosa gani?”
“Nimemtapeli.”
“Sasa unadhani nini kitafuata katika maisha hayo ya kukwepakwepa, kujifichaficha? Kwanza unaelewa kuwa huyo James karibu kila baada ya siku mbili anakuja hapa ofisini…”
“Ndiyo hapo sasa mama.”
“Ndiyo maana nimekwambia hivyo au we una mawazo gani Lina?”
Lina alitulia kidogo kisha akamkodolea macho mama mpika chai na kumwambia…
“Nimuue mmoja.”
“Eti?” alishtuka mama mpika chai.
“Bila hivyo hili suala haliwezi kumalizika kirahisi hata siku moja, mi najua.”
“Sasa unataka kumuua nani kati ya James na Semi?”
“Hapo ndipo penye mtihani mkubwa.”
“Mh! Lakini hilo wazo umelitoa wapi wewe binti?”
“Mimi mwenyewe nimewaza hivyo. Unajua hii ni kesi kama nitaamua kumuweka wazi James na ni kweli ndiye anayetakiwa kuwekwa wazi…”
“Basi kama ni hivyo hata kumuua muue yeye,” mpika chai alisema.
Lina alionekana kusita kukubaliana na maneno ya mama huyo kwamba kama ni kufa afe James…
“Lakini mama, unajua mimi nahisi kama mapenzi yangu makubwa yapo kwa James na si Semi…”
“Una kichaa?”
“Kwa nini?”
“Sasa huo si ndiyo usaliti! Unampenda mwanaume wa pembeni zaidi kuliko mumeo? Ndiyo maana ndoa zinawashinda siku hizi.”
Lina alirudi kwenye meza yake bila kupata mwafaka wa namna ya kumaliza utapeli wake kwa James huku kichwa kikiwa kimejaa mawazo…
“Ukweli pale nimejibu sivyo, lakini ndiyo uhalisia wenyewe. Lazima mwanaume mmoja afe ndipo mimi niweze kuwa huru na si vinginevyo. Nani atanielewa siku ikijulikana nini kilitokea? Nitaonekana mwanamke wa ajabu sana mimi.”
***
Mchana wa siku hiyo, James alikutana na Kindaundau mjini, yule mwanaume aliyekwenda kuchukua mzigo ofisini kwa Lina ulioachwa na mume wa Lina, Semi…
“Bwana leo afadhali tumeonana, nataka tuzungumze,” alisema Kindaundau…
“Hebu tukakae kwenye mgahawa wa maana,” alisema James. Kila mmoja aliingia kwenye gari lake na kwenda kwenye mgahawa mmoja maarufu kwa jina la Mashefa!
“Kwanza nina swali lilelile la siku zile,” alianza kusema Kindaundau…
“Lipi?”
“Kuhusu mwanamke uliyemuoa…”
“Kwani Kindaundau unataka kujua nini zaidi rafiki yangu?”
“Nina wasiwasi na jambo fulani.”
“Kuhusu mke wangu?”
“Ndiyo…”
“Kuwa..?”
“Unasema anaitwa Lina si ndiyo?”
“Ndiyo! Anaitwa Lina Joseph Ambakucha, ni mzaliwa na Kijiji cha Kilole, Korogwe mkoani Tanga…”
“Sasa sikia James, mimi nina rafiki yangu anaitwa Semi…”
“Semi?” alihoji kwa mshtuko James…
“Ndiyo, Semi.”
James akakumbuka aliona jina la Bro Semi kwenye simu ya Lina…
“Enhe, kafanyaje?”
“Semi ana mke, anaitwa Lina Joseph Ambakucha. Mimi sijawahi kumwona ila kuna wakati Semi alikuwa anafukuzia mkopo mkubwa benki, Lina alikuwa mmoja wa watu wanaotakiwa kutia sahihi kwenye fomu. Kwa sababu tulikuwa tukienda benki kila siku nikalizoea hilo jina.
“Halafu juzi nadhani, nilikwenda kuchukua mzigo wangu ofisini kwa huyo Lina aliuacha mumewe, huyo Semi…”
Endelea kulike: www.facebook.com/2jiachie
Tembelea: www.2jiachie.comITAENDELEA SIKU YA KESHO