MWANDISHI: NYEMO CHILONGANI
Endelea kulike: www.facebook.com/2jiachie
Tembelea: www.2jiachie.com“Nitamuua mumeo. Ni lazima nimuue” Dominick alimwambia Edith huku machozi yakitiririka mashavuni mwake.
“Usimuue. Nakuomba usimuue…” Edith alimwambia Dominick.
“Nitamuacha vipi mumeo? Ameiangamiza familia yangu kwa kuichoma na moto ndani ya nyumba yangu. Amebadilisha maisha yangu, nimekuwa mtu wa kutanga tanga. Ameuumiza moyo wangu kwa kunifanya kuwa mpweke katika kipindi chote hiki. Hakuna sababu ya kufanya afurahie maisha Ni lazima nimuue tu” Dominick alimwambia Edith huku akiendelea kulia.
Kadri muda ulivyokuwa ukizidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo maisha yake ya nyum yalivyokuwa yakijirudia kichwani mwake kama mkanda wa filamu. Alikumbuka kila kitu, hakuona sababu yoyote ya kumuacha waziri Tumaini hai, ni lazima amuue, tena kwa mkono wake mwenyewe.
“Naomba umsamehe….naomba umsamehe Dominick” Edith alimwambia Dominick.
“Nitaanzia wapi? Hivi familia yangu itanielewa? Haiwezekani kabisa, kama alivyoiangamiza familia yangu, na yeye nitamuangamiza pia” Dominick alimwambia Edith ambaye alikuwa akilia tu.
Dominick akazunguka nyuma ya Edith na kuanza kuzifungua kamba zile ambazo alikuwa amemfunga pale mtini. Edith bado alikuwa akilia huku akiwa haamini kama Dominick yule mpole ambaye alikuwa pamoja nae shuleni ndiye yule ambaye alikuwa nae mahali pale.
Hakuamini kama mumewe alikuwa amehusika katika mauaji yoyote, uovu wa mumewe ulionekana kumsikitisha kupita kawaida. Alimwangalia Dominick mara mbili mbili, Dominick alionekana kuwa na hasira kupita kiasi, matukio mengi ya nyuma ambayo yalitokea nyuma yake yalionekana kumsikitisha.
“Nitamuua. Nitamuua baada ya kupata msaada mkubwa kutoka kwako”Dominick alimwambia Edith.
“Kupata msaada mkubwa kutoka kwangu? Siwezi Dominick kukusaidia. Siwezi” Edith alimwambia Dominick.
Dominick alimwangalia Edith mara mbili mbili, akaonekana kubadilika zaidi, hasira ambazo alikuwa nazo katika kipindi cha nyuma zikaonekana kuongezeka maradufu. Edith akaonekana kuogopa, hakuwahi kumuona Dominick akiwa katika hali ile hata siku moja.
“Nitakuua. Sitojali chochote kile” Dominick alimwambia Edith ambaye akaanza kutetemeka.
“Naomba unisamehe”
“Nitahitaji msaada wako. Msaada wako ndio utakuwa uhai wako. Kama ukienda kinyume. Nitakuua” Dominick alimwambia Edith.
Dominick akaonekana kubadilika. Tayari hasira zilionekana kumkaba rohoni. Hakuonekana kujali tena kwamba yule aliyekuwa akiongea nae alikuwa Edith au nani, kitu ambacho alikuwa akikitaka kwa kipindi hicho ni kusaidiwa tu.
“Nitakusaidia” Edith alisema.
“Sio kwa maneno. Nitahitaji kwa vitendo” Dominick alimwambia Edith.
“Ingia ndani ya gari” Dominick alimwambia Edith na kisha wote kuanza kuingia garini.
Dominick hakuongea kitu chochote kile, alibaki kimya huku macho yake yakiangaia mbele. Alama za machozi ambayo yalikuwa yakimtoka katika kipindi cha nyuma zilikuwa zikionekana mashavuni mwake. Edith nae alibaki kimya, hakuongea kitu chochte kile kwani aliogopa kumkwaza Dominick.
Safari ile iliishia katika jengo bovu bovu lililokuwa katika uwanja wa Tanganyika Pakers. Giza lilikuwa limeanza kuingia mahali hapo. Hakukuwa na watu wengi mahali pale kitu ambacho wakateremka na kuanza kupiga hatua kuelekea katika jengo lile.
“Mpigie simu mumeo. Mwambie aje mahali hapa, tena akiwa peke yake” Dominick alimwambia Edith.
Edith akachukua simu yake, akawaiwasha na kisha kuanza kumpigia mumewe. Simu ilianza kuita, iliita kwa muda fulani, ikapokelewa. Sauti ya Bwana Tumaini ilisikika kwa wasiwasi, aliongea kama mtu ambaye alikuwa na kigugumizi. Ila baada ya kipindi fulani, ikakaa sawa.
“Umesema uko nae hapo?”
“Ndio. Alitaka kuniua kwa kunichoma moto”
“Mungu wangu! Nakuja sasa hivi” Bwana Tumaini alisema na kisha kukata simu.
Edith alibaki akimwangalia Dominick. Machozi yakaanza kumtoka, alijua fika kwamba kitendo cha mumewe kufika mahali pale basi kingeashiria kwamba angekwenda kuuawa. Alitamani kumuomba Dominick msamaha kwa ajili ya mumewe lakini akaona kuwa ngumu kufanya hivyo.
Dominick akaa kimya. Kadri muda ulivyozidi kwenda na ndivyo ambavyo hasira zake zilivyokuwa zikizidi kuongezeka. Muda aliuona ukienda taratibu sana kuliko siku nyingine, alitamani dakika ziende haraka haraka ili Tumaini afike mahali hapo na kumuua.
***********
Bwana Tumaini alikuwa akitetemeka kwa woga, kitendo cha mke wake kutekwa na mtu mbaye alisadikiwa kuua familia za mawaziri kilionekana kuwa kitendo ambacho kilimuogopesha. Hakutaka kabisa kwenda peke yake huko ambako aliiitwa, kitu alichokitaka ni kwenda pamoja na mapolisi.
Moja kwa moja akaanza kuondoka kuelekea kituo cha polisi. Mapolisi wote wakaonekana kutetemeka mara baada ya kumuona waziri akiingia ndani ya kituo hicho. Bwana Tumaini hakuongea kitu chochote kile, alibaki kimya kwa muda huku akiwaangalia mapolisi ambao walikuwa katika kituo kile.
“Karibu mkuu” polisi mmoja alimkaribisha Tumaini.
“Asante. Nina tatizo na ninahitaji msaada wenu”
“Msaada gani mkuu?”
“Mke wangu ametekwa na mtu ambaye aliua familia za mawaziri wengine” Bwana Tumaini aliwaambia mapolisi ambao walionekana kushtuka.
“Unasemaje?”
“Ndio hivyo. Ameniambia kwamba ni lazima niende Tanganyika Parkers kuonana nae. La si hivyo, atamuua mke wangu” Bwana Tumaini aliwaambia.
Mapolisi wote wakaonekana kuogopa, taarifa ambayo walikuwa wamepewa ilionekana kuwaogopesha kupita kiasi. Walikumbuka baadhi ya mauaji ambayo yalikuwa yamepita katika miezi iliyopita, muuaji hakuonekana kuwa na hurma.
Mapolisi hawakutaka kubaki mahali hapo, moja wa moja wakaingia katika gari lao aina ya Defender na moja kwa moja kuanza safari ya kuelekea katika viwanja vya Tanganyika Parkers. Kila mmoja akaanza bunduki yake vizuri, hawakutakiwa kuuliza kitu chochote mara watakapofika, ni kumkamata muuaji huyo na kumfikisha katika vyombo vya dola.
***********
Muda ulizidi kwenda zaidi na zaidi mpaka giza kuingia. Hakukuwa na mtu yeyote uwanjani pale zaidi ya wao ambao walikuwa wamelipaki gari pembeni. Dakika ziliendelea kwenda mbele, Dominick hakuongea kitu chochote kile zaidi ya kumwangalia Edith ambaye muda wote alikuwa akilia.
Mwanga wa taa ukaanza kuonekana kwa mbali jambo ambalo lilimfanya Dominick kuanza kutabasamu. Sauti ya muungurumo wa gari lile ukaonekana kumshtua. Ingawa muungurumo ule ulikuwa ukisikika kwa mbali lakini alijua vizuri kama gari lile halikuwa lile ambalo alikuwa akiliitaji kufika mahali pale.
Muungurumo ulikuwa mzito, wasiwasi ukaanza kumuingia, akamshika Edith mkono na kuanza kuondoka nae mahali pale. Edith alitamani kukataa lakini kutokana na kuvutwa kwa nguvu, Edith akajikuta akisonga kule ambapo Dominick alitaka waelekee.
Wakasimama katika ukuta karibu kabisa na kutoka nje ya uwanja ule. Macho yao yalikuwa yakielekea kule ambapo gari lao lilipokuwa. Mara wakawaona watu wanne wakiteremka kutoka katika gari lile na moja kwa moja kulifuata gari alilokuja nalo Dominick na Edith.
“Amekuja na mapolisi. Vizuri sana. Sidhani kama ataweza kumuona mkewe tena” Dominick alisema maneno ambayo yalisikika vizuri masikioni mwa Edith.
Akamshika mkono Edith na kuanza kuondoka nae mahali hapo. Tayari Edith akaona kwamba ni lazima Dominick angechukua hatua kali zaidi juu yake kwa ajili ya kumkomoa Tumaini. Kwa haraka haraka akaichukua simu yake na kuanza kumpigia mume wake ambaye alikuwa pamoja na mapolisi kule uwanjani.
“Anataka kuniua…..” Edith alimwambia mumewe kwa sauti iliyojaa wasiwasi.
“Naomba niongee nae” Bwana Tumaini alisema huku akihofia.
Dominick akaichukua simu ile, hata kabla hajaongea kitu, akaanza kumwangalia Edith kwa macho ya chuki. Dominick alionekana kukasirika kupita kawaida. Mapenzi yote ambayo alikuwa nayo juu ya Edith yalionekana kupotea kwa wakati huo.
“Nakuombaaa…nakuomba usimuue mke wangu…” Bwana Tumaini alisema.
“Mjanja wewe. Mjanja wewe kwa kuja na mapolisi. Sasa ninataka kukuonyeshea kwamba mimi ni mjanja zaidi yako. Ni lazima nimuue” Dominick alimwambia Bwana Tumaini.
Bwana Tumaini hakuwa na la kuongea, tayari alitambua kwamba alifanya makosa kuja na mapolisi mahali pale. Akazidi kuomba msamaha zaidi lakini Dominick hakuonekana kuelewa zaidi. Kitu ambacho alikuwa akiking’angania kwa wakati huo ni kumuua Edith tu.
“Niambie nije wapi. Sitokuja na mapolisi” Bwana Tumaini alimwambia Dominick.
“Kama umeshidwa kuja peke yako, utaweza kuja peke yako baadae?” Dominick aliuliza.
“Nitawezaaaa..nitawezaaa…”
“Mimi sio mtoto. Hautoweza. Nakwenda kumchoma moto mkeo” Dominick alimwambia Bwana Tumaini ambaye alionekana kuchanganyikiwa zaidi.
“Nakuomba…nakuo…” Bwana Tumaini alisema lakini hata kabla hajamalizia sentensi yake, simu ikakatika.
Dominick akamchukua Edith na kuanza kuondoka nae. Alipofika nje ya eneo la uwanja ule, akaifuata bajaji moja, akaingia ndani pamoja na Edith na kisha dereva kuwasha bajaji na kuondoka mahali hapo.
Bajaji ilisimama karibu na ufukwe wa Msasani. Wote wakateremka na kuanza kuingia ndani ya ukumbi huo. Hawakutaka kukaa ndani ya ukumbi huo, wakapitiliza nakwenda katika sehemu ambayo ilikuwa na idadi kubwa ya miti.
Dominick akachukua simu ile na kisha kuiwasha. Akampigia simu Bwana Tumaini. Simu ilianza kuita, iliita kwa muda mfupi, ikapokelewa.
“Niambie nije wapi….niambie nije wapiiiii…” Bwana Tumaini alisema.
“Njoo Msasani Club huku kulipokuwa na miti. Mara ya mwisho, kama utakuja pamoja na mapolisi, nitamchoma moto mkeo kama nilivyozichoma moto familia za marafiki zako” Dominick alimwambia Bwana Tumaini.
**********
Bwana Tumaini alikuwa amechanganyikiwa, kitendo cha kumkosa mkewe pamoja na muuaji ambaye wala hakuwa akimfahamu katika kipindi hicho kilionekana kumchanganya kupita kiasi. Simu ambayo alikuwa amepigiwa hakutaka kuidharau hata mara moja, akatoka nje ya kituo cha polisi kimya kimya na kuingia garini mwake.
Safari yake ikaanza ya kuelekea katika ufukwe wa Msasani Club. Moyo wake ulikuwa na wasiwasi kwa kuona kwamba angekuta muuaji amekwishamuua mke wake, Edith. Muda wote alikuwa akisali njiani huku akimtaka Mungu Amnusuru mke wake ambaye alikuwa akimpenda kupita kiasi.
Mara baada ya kuliegesha gari lake, moja kwa moja akaanza kuingia ndani ya eneo la ukumbi ule na moja kwa moja kuteremka na kuanza kupiga hatua kuingia ndani ya ukumbi ule. Macho yake hayakutulia sehemu moja, yalikuwa yakiangalia katika kila kona mahali pale.
Akatka kabisa nje ya ukumbi ule na kuelekea katika michanga mingi pembezoni mwa bahari ya Hindi. Akayapeleka macho yake huku na kule, kwa mbali akauona mwanga wa simu. Hakutaka kujiuliza zaidi, moja kwa moja akaanza kuufuata mwanga ule wa simu huku moyo wake ukia na shauku kubwa ya kutaka kumuona mkewe ambaye alikuwa mjauzito.
Bwana Tumaini akaanza kutabasamu, hakuamini kama angemkuta mkewe mzima mahali pale. Kwa furaha kubwa aliyokuwa nayo, akamfuata na kumkumbatia. Edith alikuwa akilia kwa furaha, tukio la kumuona mumewe mahali hapo, aliona ni jinsi gani alikuwa akimthamini.
“Uliiangamiza familia yangu” Dominick alimwambia Bwana Tumaini.
“Wewe ni nani?” Bwana Tumaini aliuliza huku akijaribu kumwangalia vizuri Dominick usoni.
“Najua unanifahamu. Ulisaidiana na wenzako kuiangamiza familia yangu kwa kuichoma moto ndani ya nyumba yangu. Umeuumiza moyo wangu kupita kawaida” Dominick alimwambia Bwana Tumaini.
“Dominick…Dominick..naomba unisamehe…”
“Nitaanza vipi kukusamehe. Nitaanzia wapi. Ni lazima nikuangamize wewe pamoja na familia yako” Dominick alimwambia Bwana Tumaini na kuanza kuikoki bunduki yake na kuwanyooshea.
“Naomba unisamehe”
“Haiwezekani. Ni lazima niwaue wote” Dominick aliwaambia.
Tayari alikuwa amekwishaiokoki bunduki yake. Moyo wake ulikuwa ukimuuma kupita kawaida. Tayari mapenzi kati yake na Edith yalikuwa yamekwisha kabisa. Hakuwana kitu kingine cha kufanya zaidi ya kutaka kuiangamiza familia hiyo. Walijitahidi kuomba msamaha lakini Dominick hakuonekana kuelewa.
“Ni lazima niwaue” Dominick alisema.
Ghafla milio ya risasi ikasikika mahali hapo, damu zikaonekana kutapakaa katika michanga ufukweni hapo na ukimya kutawala kwa muda.
********
Damu zilikuwa zimetapakaa chini. Bwana Tumaini pamoja na mkewe Edith walikuwa chini huku wakirusha rusha miguu yao. Risasi zaidi ya nane zilikuwa zimeingia katika miili yao. Vifua vyao vilikuwa vimetobolewa na risasi ambazo zilipigwa kwa haraka sana.
Dominick akawasogelea na kuwaangalia vizuri, alihitaji kufahamu kama watu hao walikuwa wamekufa kama alivyokusudia au la. Wote walikuwa wamekufa pale pale hasa mara baada ya kuacha kurusha rusha miguu yao. Dominick akaachia tabasamu pana, kitendo kile cha kishujaa kilionekana kumfurahisha kupita kiasi.
Moyoni hakuhuzunika hata mara moja mara baada ya kumuua Edith. Ni kweli alimpenda sana mwanamke yule, lakini kwa kipindi kile, alijiona kuwa na uhitaji wa kufaya jambo lile ili mladi tu kutunza siri na kutokujulikana na mtu yeyote.
Mara baada ya kuwaangalia kwa muda, akaanza kuondoka mahali hapo. Alipofika nje ya ukumbi ule wa Msasani Beach, akakodi bajaji nyingine na kisha kuondoka mahali hapo kuelekea katika hoteli ya La Vista Inn ambayo alikuwa amechukua chumba.
Dominick alikaa chumbani kwa muda, kichwa chake kikaanza kuifikiria familia yake ambayo iliteketezwa kwa moto katika kipindi kirefu kilichopita. Moyo ulimuuma sana lakini wakati mwingine alibaki akitabasamu kutokana na kuanza kulipa kisasi kwa wale wote ambao walikuwa wameiteketeza familia yake.
Bado kazi ya kuwaua watu wawili ndio ilikuwa imebaki mbele yake, alitamani kazi hiyo kuifanya haraka iwezekanavyo ili apumzike na kuishi maisha ya amani. Kila siku alikuwa akielekea katika makaburi ya familia yake na kusimama pembeni kama ishara ya kuwakumbuka kwa kuacha maua kadhaa ambayo yalionyesha kuwa tukio kubwa ambalo alikuwa akilifanya maishani mwake kama kuwaenzi.
Hakujua ni wapi pa kuanzia ingawa aliona kuwa ni lazima watu hao wauawe kwa mkono wake mwenyewe. Hakutaka kuwaacha kwani kama angfanya hivyo basi angeonekana kutowatendea haki. Mikono yake aliiona ikiwa imejaa damu lakini bado hakuonekana kuridhika.
Alihitaji kuwaua wote ili kuiridhisha nafsi yake, hakutaka kumuacha yeyote yule ambaye alikuwa amehusika katika mauaji ya familia yake. Kila siku alikuwa akifikiria namna ya kulipiza kisasi hicho kwa watu hao ambao kwake aliwaona kuwa kama wanyama.
Waliuumiza moyo wake na kuuwekea majeraha ambayo hakujua kama ipo siku majeraha hayo yangekuja kupata nafuu. Alihitaji kuyaponya maumivu ya moyo wake na hata kama angeshindwa kuyaponya basi hata kuyapunguzia maumivu.
Kila siku alikuwa akiuma meno yake kwa hasira katika kipindi ambacho alikuwa akiwaona viongozi wale ambao walikuwa wameiangamiza familia yake. Aliwachukia kuliko alivyomchukia shetani ambaye hakuwa akimuona, hakukuwa na kitu chochote ambacho alikuwa akikihitaji katika kipindi hicho zaidi ya kuwaua viongozi hao wawili ambao walikuwa wamebakia.
“Ni lazima niwaue….tena kwa mikono yangu mwenyewe” Dominick alijisemea huku akivuta shuka na kulala.
*************
Nchi ya Tanzania ikashtuka kupita kiasi. Mauaji ambayo yalikuwa yametokea katika ufukwe wa Msasani yalionekana kumshtua kila mtu. Viongozi wakakosa amani, kila mmoja akajiona kuwa yuko njiani kumfuata marehemu Tumaini na mkewe.
Mauaji yalitotokea ndani ya miezi michache yalionekana kuwasisimua wattanzania. Muuaji alikuwa hajajulikana mpaka katika kipindi hicho. Maswali kadhaa yalikuwa yakimiminika vichwani mwa Watanzania juu ya polisi ambao bado walionekana kuzembea katika kila kitu.
Miili iliyochukuliwa katika ufukwe ule ikapelekwa mpaka katika chumba cha kuhifadhia maiti huku uchunguzi ukiendelea kufanyika kila siku. Kamanda wa polisi alionekana kuchanganyikiwa, kila siku alikuwa akiongea peke yake kana kwamba pembeni yake kulikuwa na mtu.
Matukio ya mauaji ambayo yalitokea mfululizo tena yote yakiwa yakiwahusu viongozi yalionekana kumchanganya kila mtu. Viongozi walitakiwa kuwa makini katika maisha yao ya kila siku hali iliyowafanya kuwaajili walinzi kwa ajili ya kuwalinda katika maisha yao ya kila siku.
Upelelezi ambao bado ulikuwa ukifanyika haukusaidia kitu chochote kile. Mara kwa mara mpelelezi Bugabu alikuwa akiitwa na kuulizwa juu ya mahali ambapo alifikia katika upelelezi wake. Hakuwa na chochote cha kujibu zaidi ya kuomba muda zaidi kwa kuwa kazi ambayo alikuwa akiifanya ilikuwa ngumu tofauti na jinsi ambavyo aliitarajia kabla.
Kila siku waandishi wa habari walikuwa wakielekea katika ofisi ya kamanda mkuu wa jeshi la polisi, Bwana Ngomale huku lengo lao likiwa ni kutaka kufahamu ni kitu gani ambacho kilikuwa kikiendelea kuhusu muuaji ambaye bado alikuwa akiendeea kuua viongozi wa Serikali.
Bwana Ngomale hakuwa na cha kuongea zaidi ya kuwataka Watanzania wawe wavumilivu kwa kuwaambia kwamba kila kitu kilikuwa kikiendelea kama kilivyopangwa na baada ya muda fulani basi muuaji angeweza kutiwa nguvuni na kufikishwa katika vyombo vya sheria.
Kila siku Watanzania walikuwa wakiendelea kulalamika katika vyombo vya habari kwa kudai kwamba mapolisi walikuwa wameshindwa kumtia nguvuni mtu huyo ambaye bado alikuwa akiendelea kufanya mauaji kuwaua viongozi.
Magazeti ya udaku hayakuishiwa na habari, kila siku yalikuwa yakiandika habari mbalimbali kuusiana na muuaji huyo, huku hata siku nyingine wakithubutu kusema kwamba muuaji alikuwa akikaribia kujulikana, hiyo yote ilikuwa ni njia mojawapo ambayo iliyafanya magazeti yao kununuliwa kila siku.
Hakukuwa na mtu yeyote ambaye alikuwa akimfahamu muuaji ambaye alikuwa amehusika na mauaji yale ya kutisha. Kila siku tetesi zilikuwa zikiendelea kusikika mitaani lakini kiukweli hakukuwa na mtu yeyote ambaye alikuwa akiufahamu ukweli.
Mpelelezi Bugabu bado alikuwa akiendelea na upelelezi wake kama kawaida, kila siku alikuwa akihakikisha anaandika kitu chochote kuhusiana na mambo yote ambayo yalikuwa yakiandikwa magazetini na kuongelewa na watu mbalimbali.
Listi yake ya mauaji ambayo yalikuwa yameitikisa nchi ilikuwa katika mikono yake. Hakutaka kuyawekea maanani mauaji megine ambayo alikuwa ameyaandika katika kitabu chake. Akaanza kuangalia mauaji ya familia ya Bwana Boniface, familia ile ilikuwa imeteketezwa kwa kuchomwa na moto katika ufukwe wa Coco.
Mpelelezi Bugabu hakuishia hapo, akazidi kufuatlia mauajia mengine zaidi, kwa sasa akafikia katika mauaji ya familia ya Bwana Ombeni, nayo kama kawaida ilikuwa imeteketezwa kwa moto. Mpelelezi Bugabu akatikisa kichwa chake juu na chini kwa kuona kwamba upelelezi wake ulikuwa ukienda kufanikiwa.
Akaanza kuyafikiria mauaji ya Bwana Tumaini na familia yake. Mauaji ambayo yalikuwa yamefanyika hayakuwa ya kuchomwa moto, bali yalikuwa ni mauaji ya kupigwa risasi za viafuani na kufa. Hakutaka kuyapuuzia mauaji haya japokuwa yalikuwa tofauti na mauaji mengine.
Akafunga kitabu chake kidogo ambacho kilikuwa na matukio mengi ya mauaji. Akabaki kimya kwa muda huku akionekana kujifikiria. Kuna mauaji mengine yakamjia kichwani, haya yalitokea katika kipindi kirefu cha mwaka mmoja uliopita, haya yalikuwa mauaji ya familia ya Mwandishi Dominick ambayo iliteketezwa kwa moto ndani ya nyumba yao.
Bugabu akakohoa kidogo, akaendelea kufikiria zaidi. Alionekana kuyatilia shaka mauaji yale. Alimfahamu vilivyo Dominick kama mwandishi bora ambaye alikuwa akiandika mambo mengi tofauti tofauti ambayo yalikuwa yakifichua maovu mengi.
Familia yake pia ikateketezwa kwa moto huku baadae nae akisadikiwa kuuawa baada ya kutekwa na wauaji. Kuna vitu ambavyo alitamani sana kuvifahamu kuhusiana na mauaji haya yote ambayo yalikuwa yametokea. Kwanza alitaka kufuatilia makaburi ambayo maiti za familia zote zile zilipozikwa hata kabla hajaamua ni hatua gani ambayo ingefuata baada ya hapo.
Bugabu akaanza kuelekea katika makaburia ambayo yalizikiwa miili ya familia za viongozi. Aliyaangalia kwa muda mrefu na kisha kuondoka zake. Akaanza kuelekea katika makaburi ya familia ya Dominick, kidogo Bugabu akapigwa na mshtuko mara baada ya kuona maua yakiwa juu ya makaburi mawili, kaburi la Christina na Ibrahim.
Bugabu hakuishia hapo, aliendelea na uchunguzi wake, moja kwa moja akaelekea katika kaburi la Dominick ambalo wala halikuwa mbali kutoka pale yalipokuwa makaburi yale mawili, alipolifikia, akaanza kuliangalia, hakukuwa na ua lolote jambo ambalo likaanza kumtia mashaka.
“Kuna kitu hapa. Kazi yangu itaanzia hapa” Bugabu alisema.
************
Mawaziri wakaonekana kuogopa, matukio ya mauaji ambayo yalikuwa yametokea kwa mawaziri wenzao yalionekana kuwatisha kupita kawaida. Kila waziri akahakikisha kuandaa ulinzi wa kutosha katika maisha yake ya kila siku.
Wasiwasi ukaanza kuwatawala hasa wale mawaziri kutoka katika chama tawala cha Republic. Kila mmoja alikuwa na hofu kubwa, mauaji yalionekana kuwatisha kupita kawaida.
Mawaziri wawili, Bwana Ombeni na Boniface ndio ambao walikuwa na wasiwasi zaidi. Tayari walikuwa na uhakika kuwa Dominick ndiye ambaye alikuwa amehusika katika mauaji yote ambayo yalikuwa yametokea. Kila siku walikuwa wakijiuliza njia ambazo alizitumia Dominick katika kuwatoroka vijana ambao walikuwa wamewatuma.
Tayari Dominick akaonekana kuwa mtu hatari katika maisha yao, hawakutaka kuongea na waandishi wa habari kuhusu habari yoyote ya Dominick kwa kuogopa maswali zaidi. Kila Mtanzania alijua kwamba Dominick alikuwa ameuawa na watu wasiojulikana, ingekuwaje kama wangesema kwamba Dominick aikuwa hai na ndiye ambaye alikuwa amehusika katika mauaji yote?
Jambo lile la kuwaeleza waandishi wa habari likaonekana kuwa gumu kwa upande wao, kitu ambacho walitakiwa kukifanya kwa wakati huo ni kuyalinda maisha yao kwa kuwaita vijana ambao wangekuwa wakiwalinda usiku na mchana.
Waliogopa maswali kutoka kwa Watanzania juu ya Dominick kama tu wangejaribu kuwaambia kwamba mambo yale yote ambayo yalikuwa yakifanyika yalikuwa yakifanywa na Dominick. Walijuaje kama Dominick ndiye ambaye alikuwa akifanya mauaji yale? Na kwa nini alikuwa akiwauwa mawaziri tu na familia zao na si watu wengine?. Kila walipokuwa wakiyafikiria maswali yale, wakaamua kubaki kimya huku wakijihakikishia ulinzi katika maisha yao.
*************
Ukimya ulikuwa umetawala katika nyumba hii kana kwamba ndani hakukuwa na mtu yeyote yule. Hakukuwa na mtu ambaye alikuwa akizunguka zunguka katika eneo la nyumba ile zaidi ya mlinzi ambaye alikuwa na bunduki katika mkono wake wa kulia.
Giza lilikuwa kubwa huku saa zikisoma kwamba tayari ilikuwa imetimia saa saba usiku. Milio ya mbwa kutoka katika nyumba nyingine za jirani ndio ambayo ilikuwa ikisikika kwa wingi mahali hapo. Mara mwanga wa taa ukaanza kuonekana ukimulika, kwa haraka sana mlinzi akaanza kulisogelea geti na kisha kufungua kitundu kidogo kilichokuwa getini.
Gari aina ya Range ilikuwa imesimama nje. Honi mfululizo zikaanza kusikika kutoka katika gari lile. Bwana Boniface akatoka kutoka ndani ya nyumba yake. Mwili wake ulikuwa ukitetemeka kupita kiasi. Alionekana kuwa na shauku ya kutaka kufahamu kitu kimoja mahali hapo.
Akampa mlinzi ishara ya kufungua geti lile. Mlinzi akafanya hivyo, geti likafunguliwa na gari lile kupita. Mwanaume mmoja ambaye alikuwa na mwili uliokuwa umejazia akateremka kutoka garini na moja kwa moja kumfuata Bwana Boniface na kuongea nae kwa sekunde kadhaa.
Mwanaume yule akaufuata mlango wa nyuma wa gari lile na kisha kuufungua. Mwanaume mwingine akateremka kutoka garini. Kichwa chake hakikuwa na nywele kabisa. Ndevu nyingi zilikuwa kidevuni mwake huku akiwa amevaa miwani ya jua.
Alionekana kuwa kama daktari, hii ilitokana na koti refu jeupe ambalo alikuwa amelivaa pamoja na mashine ya kusikilizia mapigo ya moyo. Bwana Boniface akaanza kumwangalia daktari yule kwa macho yaliyokuwa na shauku ya kutaka kufahamu kile ambacho kilikuwa kinatarajiwa kuongea kutoka kwa mtu huyo.
Mara baada ya kusalimiana, akamkaribisha ndani. Mwanaume yule ambaye alijitambulisha kama dokta Pius akaingia ndani pamoja na Bwana Boniface na yule mwanaume ambaye alionekana kuwa mlinzi wa Bwana Boniface.
“Umenishangaza sana” Bwana Boniface alimwambia dokta Pius.
“Huo ndio ukweli. Ni ukweli kabisa ambao wala hautakiwi maswali yoyote yale” Dokta Pius alimwambia.
“Kwa hiyo una uhakika kwamba mtu anayefanya mauaji haya ni Dominick?” Bwana Boniface aliuliza.
“Asilimia mia moja”
“Umejua vipi?”
“Nilisoma nae shuleni. Ninafahamu mambo mengi sana. Alikuwa akiniamini sana mpaka alipoanza kazi. Alinieleza kila kitu kuhusiana na ninyi jinsi mlivyoiteketeza familia yake” Dokta Pius alimwambia.
Bwana Boniface akashusha pumzi ndefu. Hakuonekana kuamini kama kweli kulikuwa na mtu mwingine zaidi ya Dominick ambaye alikuwa akifahamu kila kitu kilichokuwa kimetokea. Tayari aliiona siri ambayo ilikuwa maishani mwao ikiwa imeanza kuvuja.
Alimwangalia dokta Pius mara mbili mbili huku akionekana kutokuamini. Akasimama na kuanza kutembea tembea mahali pale huku akionekana dhahiri kuchanganyikiwa. Tayari hatari ikaonekana kuanza kumnyemelea, akaanza kuwakumbuka waandishi wa habari kwa kuona kwamba ni lazima habari ile ingeenea na hivyo kuitoa katika vyombo vya habari.
“Naomba msaada wako” Bwana Boniface alimwambia dokta Pius.
“Msaada gani?”
“Yaani haujanielewa? Sitaki siri hii ifichuke. Nahitaji iendelee kuwa siri” Bwana Boniface aimwambia dokta Pius.
“Kuna kitu labda unatakiwa kukifanya”
“Kitu gani?”
“Kumuua Dominick. Hilo ndilo suruhisho la mwisho”
“Sawa. Ila nitaweza vipi kumuua? Sipajui sehemu alipojificha. Yaani sifahamu chochote kile”
“Usijali. Nitakusaidia. Anaishi hotelini kwa sasa” Dokta Pius alimwambia Bwana Boniface.
“Unaijua hoteli yenyewe?”
“Naifahamu. Huwa ninawasiliana nae mara kwa mara. Na sasa anataka kukua wewe na kisha kumuua Bwana Ombeni” Dokta Pius alimwambia Bwana Boniface.
“Mungu wangu! Yupo hoteli gani?”
“La Vista Inn pale Magomeni”
“Sawa. Inatubidi twende. Naomba unisaidie kumuua. Ninakuahidi kukupa kiasi chochote ukitakacho” Bwana Boniface alimwambia dokta Pius.
“Sawa. Kajiandae. Nitakusaidia kila hatua” Dokta Pius alimwambia Bwana Boniface ambaye akanyanyuka na kuanza kuelekea chumbani kwake.
Dokta Pius akabaki sebuleni pale huku akionekana kuwa na mawazo. Mara baada ya kutulia kwa sekunde kadhaa, akainuka na kisha kuanza kuelekea ndani ya chumba cha Bwana Boniface ambako alikuwa amekwenda kujiandaa. Dokta Pius alionekana kuwa mtu mwema ambaye alidhamiria kumsaidia Bwana Boniface.
MWANDISHI: NYEMO CHILONGANI
Endelea kulike: www.facebook.com/2jiachie
Tembelea: www.2jiachie.com