MTUNZI: ALLY MBETU
Endelea kulike: www.facebook.com/2jiachie
Tembelea: www.2jiachie.com“Dada una mimba?”
“Ndiyo mdogo wangu.”
“Mmh, Mungu mkubwa.”
“Basi mdogo wangu siri uliyokuwa huijui ndiyo hiyo, nasikia sasa havi mambo yote hayaendi vizuri kabisa na wamechanganyikiwa.”
“Ni kweli dada sasa hivi kila siku baba analalamika na kusema angekuwa na uwezo angekuulia mbali.”
“Sasa aniue kwa sababu gani? Kwa watoto wa mzee Makumiyane ni mimi peke yangu? Niliwaeleza mmoja ajitoe akichukue kidonda change lakini kila mmoja alikaa nyuma kukikimbia kidonda. Basi mdogo wangu nikifa leo ujue nimekufa kwa kukikataa kidonda.
3
“Siogopi kufa hata siku moja, kila kiumbe kitakufa! Kama nitakufa kwa kukataa kidonda nipo tayari, ila namuomba Mungu aniue baada ya kumzaa mwanangu ili niache jina langu,” dada alisema huku machozi yakimtoka, moyo wangu uliingia baridi ya woga wa ajabu kwa yote niliyoelezwa na dada juu ya siri nzito ya utajiri wetu iliyokuwa ikibebwa na kidonda cha dada.
Kingine kilichonitisha kilikuwa kusikia kuwa dada eti atakufa baada ya kukikataa kidonda. Machozi ya dada yaliniumiza sana moyo wangu na kumuonea huruma.
“Dada kwa nini usikubali kuliko kukubali kufa?”
“Masalu wewe hujui lolote katika maisha, lakini unakumbuka haya niyasemayo hata kama nikifa leo utayakumbuka maneno yangu. Kwa vile wote wameshazaa na kufanya mapenzi hawawezi kupatwa na kidonda. Wasiwasi wangu kikitoka kwangu kinaweza kurudi kwako.”
“Ha! Dada mbona unanitisha.”
“Kutokana na siri ya kidonda niliyoelezewa na baba, nakumbuka nilimuuliza kwa mfano nikifa itakuwaje? Alinieleza itabidi atafutwe aliye safi ndani ya familia. Nilimuuliza tena ni kwa mwanamke tu? Alinijibu ni kwa mtu yoyote mwanamke au mwanaume aliye msafi, unafikiri nani atakayekichukua kidonda changu kama si wewe?”
“Mimi sikubali.”
“Masalu huna jeuri ya kumbishia baba.”
“Nitahamia kwako.”
“Uhamie wapi nami umesikia lazima nitakufa?”
“Huwezi kufa dada, ni vitisho.”
“Hata nisipokufa siwezi kukukubali tena hicho kidonda kisicho na faida zaidi ya mateso.”
****
Kwa kweli sikuweza kumshawishi dada kutokana na msimamo wake mkali, jioni ilipofika niliagana na dada kwa kupanda daladala mpaka nyumbani. Nilipofika nyumbani nilikuwa na mawazo mengi juu ya maneno ya dada ambayo sikuamini kama yana ukweli wowote, nilipinga kuwa utajiri wetu si kupitia kidonda chake. Nilipoangalia hali ya maisha yetu ilikuwa ya kawaida tofauti na kauli ya dada ya kusema sasa hivi maisha ni magumu upande wa familia.
Chakula tulikula kama kawaida ambacho kwa kweli hakikuwa na hadhi ya utajiri uliotuzunguka. Lakini kwa muda ule sikushtuka kutokana maisha yale ndiyo yaliyokuwa ya kawaida ya siku zote. Japo kwa mbali nilijawa na maswali iweje nyumbani maisha yetu ya kawaida.
Kingine ambacho alikisema dada kiliniingia akilini kilikuwa kwa mama kuamka kila siku asubuhi na kwenda kulima wakati baba alikuwa na pesa nyingi. Kingine nilichokubaliana na dada ni mama kuokota kuni na kuja kupikia wakati dada zetu wanatumia majiko ya umeme na gesi.
Lakini kitu ambacho sikukubaliana naye ni imani za kishirikina kwanza maisha yetu yanategemea ushirikina wa kidonda chake. Katika akili yangu niliamini kidonda cha dada hakikuwa kimepata tiba sahihi. Lakini baada ya kupata tiba sahihi kilipona. Niliamini dada alitaka kunijengea uadui na wazazi ili niwaone ni watu wabaya wasiofaa.
Sikutaka kumuamini dada zaidi ya kuona anataka kunipotosha, lakini siri ile nilibaki nayo moyoni sikutaka kumwambia mtu. Siku zilizidi kukatika nami niliendelea na masomo kama kawaida. Pamoja na kuyapuuza ya dada na kuyaona kama ya uchonganishi lakini kuna vitu vilikuwa vikitia wasiwasi. Kuna siku nilimsikia baba akimwambia mama kwa sauti iliyoonesha hawakuniona kutokana na kiza kilichokuwepo.
“Mama Monika nimempa mpa muda mwanao wa kutosha, litakalotokea tusilaumiane.”
“Sasa mimi nitafanyaje kama mwenyewe hajihurumii.”
“Hali ni mbaya tukiendeleza huruma tutaadhirika.”
“Baba Monika mimi mwenyewe nilikwenda kwa Monika, lakini kiburi kimemjaa tena amekosa hata heshima kujua anazungumza na mama yake.”
“Mganga amenipa mwezi huu mwisho la sivyo kihame kwa mwingine.”
“Unafikiri kitaenda kwa nani?”
“Hilo suala tutalizungumza baada ya kushindikana kabisa.”
“Yaani Monika kanichanganya sana.”
“Basi uamuzi ni huo sina mwingine.”
“Utakavyokuwa mimi tena simo kayataka mwenyewe.”
Mazungumzo ya baba na mama kumhusu dada Monika yalinishtua sana na kujiuliza baba alikuwa anataka kufanya nini? Nilijiuliza au ndiyo niliyoelezwa na dada Monika juu ya kumlazimisha aendelee kuwa na kidonda na kama kikihama kitaenda kwa nani?”
Pia nilijiuliza mama alikuwa na maana gani kusema yakimkuta dada Monika hayumo ni mambo gani hayo. Nilijikuta nikiingiwa na wasiwasi wa maneno ya dada Monika kuwa baba alimtishia maisha kuwa kama akikataa kuendelea kuwa na kidonda hatadumu lazima atakufa.
Nilijikuta nikikosa raha na kutamani kwenda kumuomba dada akubali kuliko kutokewa na balaa lile. Kwa mbali nilijikuta njia panda kuamini kuwa kidonda cha dada ndicho kilikuwa kikifanya tuwe matajiri. Nilitamani nizungumze na mama kuhusu kujua baba alikusudia kufanya nini kwa dada.
Japo niliogopa kuulizwa nimejuaje, lakini nilipanga siku ya pili sitakwenda shule na kumfuata mama shambani kumuuliza kuna kitu gani dada Monika anataka kufanyiwa baada ya kukataa kuwa na kidonda kile. Usiku kwangu ulikuwa mzito sana niliota mambo mazito ambayo yalinitisha na kunifanya niamke saa nane za usiku na kukesha bila kulala.
Niliota familia yetu ikifanya sherehe kubwa huku dada Monika akiwa amekufa na mwili wake haukuwa na mguu mmoja uliokuwa ukivuja damu, ule mguu uliokuwa na kidonda. Damu ya dada Monika ndugu zetu walikuwa wakinywa kwa furaha. Niliamka na kukaa kitandani nikitweta. Nilijiuliza ndoto ile ina maana gani.
Baada ya muda usingizi ulinipitia, muda haukupita niliota ndoto nyingine mbaya, niliota nimeoza mguu sehemu ya ndani na kuanza kutoka funza, ajabu ndugu zangu walifurahia kama ndoto ya mwanzo ya kufurahia kifo cha dada Monika kwa kumla na kunywa damu yake.
*****
Nilishituka usingizini na kuogopa kulala tena mpaka asubuhi, asubuhi nilisingizia naumwa. Sikwenda shule, nilitoka ndani na kwenda kulala sebuleni ili kuogopa kuota ndoto za kutisha. Sebuleni nilipolala sikuota ndoto mpaka nilipoamka kujiandaa kwenda kwa mama shamba baada ya kufungua kinywa.
Nilioga na kufungua kinywa kisha nilielekea shambani kwa mama ili nikamuulize kuna kitu gani dada Monika anataka kufanyiwa na baba, kama kumuua ningepinga kwa nguvu zangu zote.
Nilikwenda hadi shambani na kumkuta mama akiwa katikati ya kilimo, sikumsemesha kitu, nilijiuliza iweje tuwe na pesa majumba na magari mama ateseke kiasi kile. Nilizidi kuingiwa na wasiwasi juu la mambo yaliyokuwa yakifanyika.
Baada ya muda nilimwita mama, aliponiona alishtuka na kuniuliza.
“Masalu kuna usalama?”
“Upo mama.”
“Si unaumwa, umekuja huku kufanya nini?”
”Kuna kitu nataka kuuliza mama.”
“Kitu gani?”
Mama alisema huku akiweka pembeni jembe na kunifuata nilipokuwa nimesimama.
“Masalu una nini mwanangu?”
“Mama jana nimeota ndoto mbaya sana.”
“Ndoto gani mwanangu?”
“Kuhusu dada Monika.”
“Monika! Ndoto inahusu nini?”
Nilimhadithia ndoto niliyoota, mama alishtuka na kutulia kwa muda kisha alisema kwa sauti ya chini.
“Sasa wewe wasiwasi wako nini?”
“Mama kuna maneno nilizungumza siku moja na dada Monika kuhusu baba kumtishia kifo na kunieleza kama akifa nijue baba ndiye aliyehusika.”
“Masalu!” Mama alishtuka.
“Naam mama.”
“Mlifikia wapi mpaka mkazungumza hayo?”
“Kuna siku nilikwenda kwa dada Monika na kumuuliza sababu ya yeye kuhama nyumbani. Mama dada alinieleza mambo mengi ya kutisha sana lakini sikuyaamini.”
“Masalu alikueleza mambo gani Monika?”
Nilimuhadithia baadhi ya mambo kisha nilimueleza ya yeye kulima wakati tuna pesa.
“Eti mama hata kulima kwako amesema ni imani za kishirikina iweje tuwe na pesa wewe ulime wakati ungewalipa watu wakatulimia?”
“Mmh, mbona makubwa!” Mama alizidi kushangaa.
Mama alisema huku akitoka shambani na kunisogeza chini ya mwembe.
“Masalu wewe hayo unayaamini?”
“Siwezi kuyaamini japo kuna mengine yana ukweli.”
“Nakuomba asikubaliane na maneno ya Monika ni ya uongo.”
“Mama mbona baba alisema jana litakalomtokea asilaumiwe, nini kitamtokea dada Monika?”
“Wee Masalu!” Mama alizidi kushtuka kuona ninajua vitu vingi.
Ilionesha mama aliamini siyajui mengi kuhusiana na mambo yaliyokuwa yakitendeka nyumbani. Nilimuona akifuta jasho kwenye paji la uso kisha alinipandisha na kunishusha na kusema.
“Masalu wewe ni mtoto, hujui kitu hata nikikueleza hutanielewa, nakuomba uachane na hayo, swali hili ungemuuliza baba yako mngekosana.”
“Mama hujanijibu, jibu si kukosana bali kupata ukweli nilioelezwa na dada Monika juu ya kukataa kwake kidonda na baba kumtishia kuyakatisha maisha yake.”
“Hilo si kweli, ni ujinga wa dada yako kama kufa atakufa na yake.”
“Mama, baba aliposema kuwa asilaumiwe na wewe kusema shauri yake alikuwa na maana gani?”
“Masalu naomba usiniulize swali kama hilo tena,” mama alikuwa mkali.
Niliona nibadili mada kwa kumuuliza swali lingine.
“Halafu mama kwa nini tusitafute mtu atulimie na wewe kupumzika, tuna faida gani kuwa na pesa na wewe mama unaendelea kuteseka?”
“Masalu nakuomba uondoke, nakuona umekosa maneno ya kuzungumza,” mama alikuwa mkali.
Kila neno nililolisema kwa mama lilimuudhi, sikutaka kuendelea kulumbana naye, niliamua kurudi zangu nyumbani nikiwa bado nipo njia panda. Wazo la haraka lilikuwa kwenda kwa dada Monika kumueleza akubaliane na matakwa ya wazazi ili asije kujutia maisha yake. Nilipofika nyumbani nilijawa na mawazo mengi sana kuhusiana na majibu ya mama.
*****
Nilipanga siku ya pili nitaaga na kwenda shule lakini kituo changu cha kwanza kingekuwa kwa dada Monika kumueleza hali halisi kutokana maneno ya baba. Siku ile sikushinda na furaha kila nilipokumbuka ndoto nilizoota usiku na majibu ya mama.
Japo niliamini mama hawezi kumueleza baba niliyomuuliza, bado nilikuwa na wasiwasi kama atamueleza basi lazima baba angenishikisha adabu kufuatilia mambo yasiyonihusu. Lakini siku ilikatika bila kuulizwa swali lolote na baba zaidi ya mama kuniita na kunionya nisirudie tena kuuliza mambo yale wala kumueleza mtu yoyote.
Nilimuahidi mama sitarudia kumueleza mtu maneno yale, kwa furaha ya mama alinipa pesa za kula shule kitu ambacho hakuwahi kukifanya zaidi ya kila siku kunipa nauli tu. Niliamini ile itanisaidia kuongeza nauli ya kwenda kwa dada. Usiku nilipolala ndoto ya jana yake ilijirudia.
Nilijikuta nikikesha kwa mara nyingine mpaka asubuhi kwa kuogopa kila nilipofumba macho njozi mbaya zilinifuata. Chumba nilikiogopa na kujiuliza njozi zile mbaya za dada Monika kuliwa nyama huku familia yote ikifurahia zilikuwa na maana gani? Kingine kilichonitisha mguu wangu kuoza na kutoa wadudu.
Nilijikuta nikiogopa kufumba macho na kubaki macho mpaka kunakucha, alfajiri nilisikia habari zilizonishtua sana. Nilimsikia baba akimwambia mama:
“Aliyoyataka mwanao yametimia.”
“Unataka kuniambia Monika ame...”
“Ishia hapohapo na sitaki utoe chozi unajua nini tuliambiwa.”
Nilishtuka na kutoka nje na kuwakuta baba na mama sebuleni, mama aliponiona alishtuka tofauti na baba.
“Mama dada Monika kafanya nini?”
“Kwani umesikia nini?” Baba aliniuliza.
“Sijui...ame..”
“Amefanya nini?”
“A..me..mee,” nilijikuta nikipata kigugumizi.
“Hebu ondoka hapa asubuhi yote nini kimekuamsha,” baba alinifokea.
Nilirudi chumbani kwangu nikiwa bado sielewi dada Monika kafanya nini japo bado wasiwasi wangu ulikuwa labda amefariki kutokana na maelezo ya dada Monika na kauli ya baba juu ya dada Monika. Kwa kauli ya baba ambayo aliifunga, niliamini kabisa dada Monika huenda kweli amefariki. Kwa vile muda wa kujiandaa kwenda shule ulikuwa umekaribia nilikwenda kuoga ili nijiandae na shule.
Baada ya kuoga nilirudi chumbani kwangu kujiandaa kwenda shule, nikiwa bado nipo katika maandalizi nilishtuka kusikia sauti za ndugu zangu, ujio wao wa asubuhi ile ulinishtua sana.Niijiuliza kuna kitu gani kimetokea au ndiyo niliyokuwa nayafikiria ya kifo cha dada Monika? Sikutaka kutoka haraka, nilimalizia kuvaa nguo za shule, baada ya kuvaa nilitoka ili nijiandae.
Nilishtuka kuwaona dada na kaka zangu wamekaa sebuleni, waliponiona walishtuka na kuniuliza:
“Masalu unakwenda wapi?”
”Shule.”
“Unakwenda shule hujui hapa nyumbani kumetokea nini?”
”Sijui.”
“Mmh, makubwa, Monika amefariki.”
“Eti?
“Monika amefariki.”
“Dada Monika?” Bado sikuamini.
“Eeeh, huyo huyo.”
“Siamini …siamini.”
Bila kujielewa nilijizoa mzimamzima na kujipiga chini na kupoteza fahamu, baada ya huduma ya kwanza nilipata fahamu na kuangua kilio tofauti na wenzangu ambao hakuna hata mtu mmoja aliyemwaga chozi. Juhudi za kunibembeleza zilishindikana. Bila kujielewa nilijikuta nikisema kwa sauti ya juu:
“Yote uliyonieleza dada yangu nilifikiri utani kumbe kweli wamekuua.”
“Alikueleza nini?”
”Baba kwa nini umemuua dada Monika?”
“Wee Msalu maneno gani hayo?”
“Maskini dada yangu kumbe ulikuwa na siri nzito moyoni mwako ambayo imenifumbua leo, ungekufa dada yangu bila kujua lakini Mungu mkubwa.”
“Masalu hebu ondoa uchuro hapa.”
“Siwezi… siwezi, kwa nini lakini umemuua dada Monika?” Niliendelea kulia kwa uchungu huku nikijipigiza chini.
“Nani kamuua Monika?”
“Nyinyi wote kwa tamaa za mali.”
“Masalu unatukosea adabu.”
“Siwakosei adabu bali ukweli ni huo.”
Kaka mkubwa alinichukua na kutoka na mimi uani huku nikiendelea kulia, roho iliniuma kumpoteza kipenzi dada yangu Monika mtu aliyenipenda kuliko yeyote. Kutokuonesha ndugu zangu kuguswa na kifo cha Monika niliamini ndoto niliyoota ilikuwa na maana kubwa. Kama dada Monika wamemla nyama nini maana ya kidonda mguuni kwangu chenye kutoa wadudu?
****
Tulipofika nje kaka alinibembeleza na kunieleza maneno ya busara kuhusiana na kifo cha Monika kuwa kilitokana na uzazi wala hakihusiani na masuala ya ushirikina. Na kutokuonesha kuguswa kila mmoja alikuwa akililia moyoni kwa vile hakuna aliyetegemea.
Kwa vile nilikuwa namheshimu nilimkubalia ili kumridhisha lakini siri ilibakia moyoni mwangu. Wengi walishtuka maneno yangu na kunionya nisiyasikilize ya Monika kwa vile alikuwa ni muongo na mgombanishi, nao nilikubaliana nao ili yaishe.
Ajabu ya mwaka ambayo baada ya akili ya ufahamu kukomaa niligundua kuna kitu kilitendeka mpaka leo hii sijui. Baada ya taarifa za msiba wa dada Monika ambao hakuna aliyefunua mdomo wake kulia zaidi yangu mwenyewe.
Taarifa za msiba ule hata majirani hawakujua nyumbani kulitokea msiba. Mwili wa dada ulifuatwa na kurudishwa nyumbani. Gari lililouleta mwili wa dada ilipita mpaka uani. Waliuteremsha na kuuingiza chumbani kisha ndugu wote walitawanyika kwenda kuendelea na kazi zao kama kawaida. Kitu kile kilinishtua iweje kuwepo na msiba hakuna mtu aliyeguswa wala taarifa kuwafikia majirani.
Usiku nilipelekwa kwa kaka ambako nililala siku mbili na kurudishwa nyumbani, niliporudi hali ilikuwa ileile na kunifanya niwe na mawazo ni kweli dada alikufa au taarifa zile zilikuwa mgonjwa mahututi? Kwa hiyo yupo hospitali, sikutaka kuhoji haraka baada ya wiki sikuona mabadiliko wala taarifa zozote za dada Monika.
Hata majirani waliotuzunguka hawakujua kitu zaidi ya ndugu wa mpenzi wa dada Monika kuulizia dada alizikwa wapi. Maswali yale kwa kweli yalinichanganya sana. Kila nilivyojitahidi kuchunguza sikupata taarifa zozote zaidi ya watu kufurahia maisha.
Mwezi ulikatika nikiwa bado njia panda kuhusu maswali dada Monika wakiulizia mazishi yake yalifanyika lini na kwa nini baba hakuwataarifu kama kuna msiba, kama majirani wajumuike pamoja katika msiba ule. Siku moja nilikwenda hadi Mkuyuni kwenye nyumba aliyokuwa akikaa dada Monika.
Nilikuta mlango umefungwa, kuuliza nilishindwa kutokana na kuogopa maswali huenda amekufa na kunifahamu mimi ni nani. Niliamua kurudi bila kupata jibu kuhusiana na kupotea kwa dada Monika kwamba amekufa kweli au hali yake ni mbaya. Lakini nilikumbuka kaka mkubwa aliniambia kuwa Monika alikufa kutokana na uzazi.
Nilijiuliza kama alikufa alizikwa wapi na kwa nini majirani hawajui lolote, na kama kweli alikuwa amekufa mazishi yake yalifanyika wapi. Kutokana na kuja mjini muda mrefu mazishi yote tuliyafanyia mjini. Ingekuwa kama wengine mazishi huyafanyia vijiji walikozaliwa lakini dhana ile baba aliikataa.
Bado sikutaka kukubali, nilizunguka kwenye makaburi labda nitaliona kaburi jipya la dada Monika, lakini sikuona kitu chochote zaidi ya makaburi mapya yenye majina tofauti na la dada Monika. Nilibakia njia panda siku zote kujiuliza ni kweli dada Monika alikufa au yupo kwa mganga.
Siku moja nilikutana na shemeji aliyekuwa akikaa na dada Monika, nilimuulizia kitu ambacho kilionekana kituko mbele yake.
“Shemu za siku?”
“Nzuri sijui zako?”
“Eti shemu dada Monika yupo wapi?”
“Masalu swali gani hilo? Ina maana mtu akifa huwa anakwenda wapi?”
“Una maana ni kweli dada Monika amekufa?”
“Masalu kioja gani unataka kunionesha, ina maana wakati Monika anakufa wewe ulikuwa wapi?”
“Sasa kama amekufa maiti yake imezikwa wapi?”
“Mimi nitajua wapi, wakati nilifukuzwa?”
“Kama kazikwa mbona hakuna kaburi lake?”
“Masalu upo sawa?”
“Kwani wewe unanionaje?”
“Nakuona haupo sawa.”
“Nipo sawa na akili timamu.”
“Kama kweli una akili timamu usingeniuliza suala la kifo cha Monika.”
“Shemu kama dada alikufa mbona wewe mumewe haukuwepo msibani?”
“Masalu, nilifukuzwa kama mbwa na kutishiwa maisha, kwanza nikionekana nimesimama na wewe nitajitafutia balaa.”
“Shemu una uhakika Monika amekufa?”
“Ndiyo.”
“Ulimshuhudia kabisa amekufa?”
“Monika amefia mikononi mwangu na kuna mengi alinieleza ya kukueleza lakini sikupata muda wa kuonana na wewe. Kama ni kweli aliyosema Monika basi familia yetu itakuwa ina hatari kubwa.”
“Kuhusu utajiri?” Nijikuta naropoka.
“Nalo hilo alilizungumzia, ila wamemtesa sana mke wangu mpaka kifo chake. Kibaya wamemuua hata mtoto wangu aliyekuwa tumboni bila kosa, yaani siamini familia yako kuna na roho mbaya kiasi hicho. Kama mtu kawapatia utajiri akisema amechoka na yeye anataka maisha yake kuna ubaya gani?” Maskini shemeji yangu alizungumza huku akitokwa na machozi, nilijikuta nikitokwa na mimi machozi bila kupenda.
“Masalu familia yenu haifai, unafikiri maisha ya kuongozwa na nguvu za kishirikina mwisho wake nini? Haya sasa wamemuua Monika nani atafuata na kwa taarifa kidonda alichokikataa dada yako kitahamia kwako. Kabla ya kufa kaitaja familia yenu wote kuwa wanagombania roho yake kasoro wewe pake yako na kuonesha jinsi gani huhusiki na mateso ya mke wangu.”
“Mungu wangu!”
“Huo ndio ukweli wenyewe, hujiulizi kwa nini mama yako bado analima kama sio ushirikina, hivi baba yako hana pesa ya kuwapa watu walime na mama yako na utu uzima wake apumzike?”
“Anaweza.”
“Kama anaongeza majumba na magari kwa nini mama yako usipumzike, hebu angalia ndugu zako wakubwa. Nao wana roho ya tamaa ya mali kushindwa kumuonea huruma mama yenu. Nasikia ndani mwenu kuna chumba kisichofunguliwa, unajua kuna nini?”
“Hata sijui!”
“Kwa taarifa yako kuna maiti ya mtoto mchanga ambayo kila baada ya siku tatu hupakwa mafuta ili isiharibike.”
“Shemuuuu! Umejuaje?” Nilishtuka kusikia habari zile, chumba alichokisema kweli kilikuwepo ambacho sikuwahi kukiona kikifunguliwa.
“Dada yako Monika alikuwa na siri nzito moyoni mwake, nyingine alisema hawezi kuniambia labda ungekuwepo kabla ya kufa kwake.”
“Sasa yeye alijuaje kama kuna maiti ya mtoto?”
“Mara nyingi kazi ile aliifanya yeye, baba na mama yenu. Hakuna mtu mwingine aliyeruhusiwa kuifanya.”
“Mmh! Maiti ya mtoto wa nani?”
“Kama una kumbukumbu, nasikia mtoto wa kwanza wa dada yako ambaye ndiye aliye na pesa kuliko wote alimtoa mtoto wake kafara ili kuongeza utajiri.”
*****
Kauli ile ilinirudisha nyuma na kukumbuka miaka sita iliyopita dada mkubwa alifiwa na mwanaye lakini mazishi yake sikuyaelewa japo msiba ulikuwa nyumbani. Kingine kilichonifungua macho hakikuwa na tofauti na msiba wa Monika kilikuwa cha kifamilia tena ya ndani hata wanandugu hawakujulishwa. Taratibu nilianza kufunguka akili na kuamini kila lililosemwa na Monika lilikuwa na ukweli mkubwa.
“Asante shemu kwa kunifumbua macho,” nilimshukuru ili tuagane, nilipotaka kuondoka aliniuliza kitu.
“Masalu unataka kuniambia hukuwa na habari Monika amekufa au ulitaka kunitega akili?”
“Shemu, huwezi kuamini kila dakika nimekuwa nikichanganyikiwa juu ya taarifa za msiba wa dada Monika. Kweli niliuona mwili ukiteremshwa kwenye gari. Lakini tokea hapo sikuweza kujua nini kilichoendelea mpaka leo hii.”
“Ulipouliza walikujibu nini?”
“Sijauliza bali nilifanya upelelezi wangu, kila kona nilifika lakini sikupata kuona chochote.”
“Ulichunguza nini?”
“Sehemu za makaburi au kupata taarifa kama hajafa yupo wapi?”
“Una uhakika Monika hakuzikwa?”
“Nina uhakika.”
ITAENDELEASIKU YA KESHOOOOOOOOOOOO