Quantcast
Channel: Rogers Linky - Sports Home
Viewing all 12768 articles
Browse latest View live

HADITHI: WAKILI WA MOYO SEHEMU: 9

$
0
0

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’

ILIPOISHIA:
“Cecy nitakutafuta tuzungumze akili yako ikitulia.”
“Usijisumbue.”
“Lazima nijisumbue kwako kwa vile kuna kitu ndani yako nilichokiona.”
“Colin niache nirudi nyumbani.”
“Unakaa wapi nikupeleke.”
“Colin unataka mama yako aje kuchoka pagala letu, aliona picha ikawa vile vipi anione kwenye gari lako?”
“Hawezi, na ungeniambia alichokifanya ningempa ukweli, tabu ya kina mama wa kiswahili wazungu hawajali vitu vya kijingakijinga.”
“We nenda tu.”
SASA ENDELEA...
Colin alimbembeleza sana Cecy, kwa vile naye alikuwa akimpenda akiingia kwenye gari na kurudishwa nyumbani kwao. Walipomfikisha Colin naye aliteremka na kuongozana hadi kwa kina Cecy ambako kulikuwa na nyumba ya vyumba viwili na sebule. Lakini nyumba ilikuwa ya hali ya chini bati zake zilikuwa na kutu na juu waliweka mawe ili kuzuia bati lisiezuliwe na upepo.
Cecy baada ya kufika eneo la kwao alishukuru na kuanza kuelekea nyumbani, lakini Colin alimsemesha.
“Cecy mbona unaniacha mgeni?”
“Colin nashukuru umenileta, lakini naomba usifike nyumbani.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Nimekueleza mara ngapi kuhusu mama yangu, unataka mama yako aje akitie moto kibanda chetu.”
“Cecy suala la kuhusu mama yangu niachenie mimi, naomba nimsalimie mama mara moja.”
“Mmh! Sawa.”
Waliongozana Cecy na Colin hadi nyumbani kwao ambako alitambulishwa kwa mama yake na kumfanya mama Cecy ashtuke.
“Ha! Wewe ndiye unayenyanyasa mwanangu?”
“Kumnyanyasa kivipi mama?”
Mama Cecy alimweleza mateso yote ya mwanaye juu yake na jinsi mama yake alivyokwenda kuwatukana huku akitishia maisha ya Cecy kama ataharibu ndoa yake na Mage. Colin baada ya kusikilia maneno yale aliyarudia maneno ya Cecy juu ya mapenzi yake kwake.
Ashangaa kuona penzi la Cecy kwake lilikuwa wazi kwa mama yake lakini mhusika mkuu alikuwa hajui kitu zaidi ya kumuona Cecy kama msichana mzuri lakini hakuwa na uwezo wa kumtamkia chochote kutokana na mama yake kumtafutia mwanamke aoe ambaye kwa upande wake aliungana na uchaguzi wa mama yake.
“Mzazi wangu, kwanza niwaombeni radhi kwa yote yaliyotokea kwa mama yangu kuja kuwatukana bila sababu. Naweza kusema labda makosa nimefanya mimi kwa kutomjulisha nini nilichotaka kukifanya na Cecy.
“Najua mama yangu alimpenda Cecy lakini si kuwa mke wa mwanaye bali msichana mzuri anayejiheshimu. Inawezekana kigezo cha elimu ndicho kilichomfanya mama yangu amtafute Mage, nina imani kama Cecy angekuwa na elimu kama ya Mage basi angekuwa chaguo la kwanza la mama.
“ Wasiwasi mkubwa wa mama ilianzia siku alipomuona Cecy kapendeza naweza kusema aliwashinda wote waliokuwa kwenye sherehe yangu. Kilichomshtua mama yangu kunikuta na picha ya Cecy aliyokuwa amependeza sana. Aliamini kabisa ni mpenzi wangu hivyo kujihami kabla mambo hayajaharibika kutokana na harusi yetu kuandaliwa kwa fedha nyingi sana.
“Lakini hakutakiwa kuchukua uamuzi aliochukua bila kuniuliza mimi japokuwa nilimweleza sababu ya kuwa na picha ile. Ila napenda kuwaeleza kitu kimoja kuwa sitauacha upendo wa Cecy upitee hivihivi najitolea kumsomesha ili aongeze elimu na ujuzi.
Baada ya elimu hiyo nitafanya naye kazi ndani na nje ya nchi ambayo naamini itamweka katika maisha mazuri na ramani ya dunia. Pia nitahakikisha naijenga nyumba yenu katika hadhi ya kisasa pia mama nitakufungulia mradi ili muendeshe maisha yenu,” Colin alieleza nia yake nzuri kwa Cecy na mama yake.
“Asante bab..”
“Mama nani kamwambia sisi tuna shida ya vitu hivyo? Kama kilichonitesa nimekikosa, sihitaji kitu kingine toka kwako,” Cecy alimkatisha mama yake na kumjia juu Colin kwa kauli yake.
“Cecy mimi na wewe nani mwenye kosa, ulilolisema leo ungelisema mapema situngefika huku,” Colin alijitetea.
“Muongo! Colin hata ningesema ingekuwa sawa na kazi bure kwa vile tayari mama yako aliisha kuchagulia mwanamke,” Cecy alisema kwa hisia kali.
“Kabla ya kutoa uamuzi ningechagua.”
“Mimi na Mage unampenda nani?”
“Nawapenda wote, ila kwa sasa Mage kwa vile ndiye tupo katika mipango ya ndoa.”
“Kwa kauli hiyo naomba tukomane kila mtu ashike hamsini zake ukinikuta njiani nipite kama nguzo ya umeme,” Cecy alisema kwa hasira.
“Cecy kuwa na adabu, heshimu anachokisema mwenzako...Baba kama una nia hiyo ifanye faida hataiona leo, lakini baadaye atakushukuru.”
“Sawa mama nimekuelewa, Cecy punguza hasira nina nia nzuri na wewe, uzuri wako nitaulinda na baadaye utakuingia fedha nyingi na kumsaidia mama. Utauza ndizi mpaka lini?”
Cecy hakujibu kitu aliinama chini, Colin alimsogelea na kumbembeleza kitu kilichomfanya Cecy aangue kilio na kusema:
“Colin nisamehe kwa yote, hujui kiasi gani penzi lako lilivyouathiri moyo wangu, najua nilikupenda bila kushauriana na moyo wangu. Mnaweza kuniona mdogo lakini nami nina hisia za mapenzi kama wengine,” Cecy alisema huku akimtazama Colin kwa macho yaliyojaa machozi.
“Najua Cecy, isingekuwa mipango ya harusi ningeza kufanya chochote ili ujue nauthamini upendo wako.”
“Sawa Colin nimekuelewa.”
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda Colin aliaga kuwahi nyumbani baada ya kuondoka bila kuaga. Alikwenda kwenye gari na kuwaletea laki moja, walimshukuru naye aliondoka kuelekea nyumbani. Njiani alijikuta akimuwaza Cecy msichana mdogo lakini alikuwa jasiri kuzielezea hisia zake japo aliamini mama yake asingemkubali kutokana na uduni wa maisha na kukosa elimu.
Kwa upande mwingine aliamini kabisa kutokana na kasi ya mabadiliko duniani Mage ndiye mwanamke sahihi kwake. Kwani aliamini maisha ni zaidi ya mapenzi kwa vile maisha yakiwa vizuri kila kitu kinakwenda. Aliamini kwa umbile adimu la Cecy angeweza kuifanya kazi yake vizuri ya maonesho ya mavazi.
Kitu kikubwa aliamini Cecy kama atapata twisheni ya kingereza ataweza kuongeza uwezo wake hata kusafiri nchi za nje kufanya kazi ya maonesho ya mavazi pia kupata tenda ya kupamba majarida. Aliamini akimtumia vizuri Cecy kampuni yake itafika mbali na yeye kujitengezea kipato kikubwa.
Alipanga kuwekeza fedha nyingi kwa Cecy baadaye angevuna fedha nyingi kwa kuamini alikuwa na kitu cha ziada ambacho wasichana wengi hawakuwa nacho. Japokuwa alikuwa na wasiwasi na kikwazo cha mama yake, lakini kwa vile yupo kikazi alijua mama yake angemuelewa tu.
Alipanga ndani ya wiki mbili nyumba ya kisasa ya kina Cecy iwe imesimama huku akimtafutia twisheni nzuri ili kuijua lugha haraka. Alipanga kufungua duka mbele ya nyumba yao ambalo litawafanya waingize kipato kila siku. Kutokana na kuzama kwenye mawazo ya kumuwaza Cecy alijikuta akimsahau Mage mpaka alipofika kwao.
***
Alipoingia ndani alikutana na mama yake ambaye alishangaa kumuona mwanaye akiteremka kwenye gari.
“Colin unatoka wapi?”
Colin ilibidi amweleze mama yake kilichotokea, baada ya kumsikiliza alimuuliza:
“Colin mwanangu umemfanya nini mtoto wa watu?”
“Mama sijamfanya kitu chochote kama nilivyokueleza.”
“Mage si mjinga kulia tu na kukataa kuzungumza na wewe wakati mlikuwa pamoja?”
“Yaani sijui kitu labda uulize wewe utapata jibu.”
“Nitauliza, lakini Colin kuna kitu unanificha haiwezekani Mage aondoke bila kukuaga kisha akatae kuzungumza na wewe wakati usiku mmelala pamoja?”
“Mama piga simu uulize labda utagundua kitu.”
“Mmh! Sasa nimepata jibu,” mama Colin alisema huku akitikisa kichwa kama kakumbuka kitu.
“Jibu gani?”
“Colin lazima kuna kitu Mage amegundua kuhusu wewe na Cecy, nasema hivi ndoa ikivunjika Cecy atanitambua.”
“Mama unamuonea bure mtoto wa watu, toka siku ile ya sherehe sijaonana na Cecy,” Colin alidanganya.
“Muongo umemkataza asilete ndizi ili mkutane sehemu nyingine. Colin Mage akinieleza kuwa amegundua una uhusiano na msichana mwingine pagala lao nakwenda kulitia moto sasa hivi.”
“Mama kwa nini unanihukumu kwa kosa nisilofanya, nimekueleza piga simu uulize unaanza kutengeneza mawazo yako. Cecy amekukosea nini mpaka kumchukuia hivyo, ni wewe ndiye uliyekuwa naye karibu?”
Mama Colin hakusema kitu aliingia ndani kuchukua simu ili ampigie Mage kujua amepatwa na nini.
***
Baada ya Colin kuondoka mama Mage alimfuata mwanaye chumbani aliyekuwa amezama kwenye dimbwi la mawazo juu ya hali ya Hans na familia yake ilivyomtenga na kumuona kama kinyesi. Moyo ulimuuma na kujua hakukuwa na haja ya yeye kwenda hospitali pia kumuacha mchumba wake mumewe mtarajiwa akiwa amelala na kuondoka bila kumuaga.
Alijilaumu kwa kitendo chake cha kumpita Colin bila kumsemesha, alijiuliza atamfikiliaje. Alijiuliza ndoa yake ikivunjia na ijulikane sababu ya Hans mwanaume asiye na mapenzi naye ataiweka wapi sura yake. Lakini alijiuliza angesimama na kuzungumza na Colin angemwambia anatoka wapi na kwa nini hakumuaga?
Akiwa katika dimbwi la mawazo mama yake aliingia na kumkuta amezilaza chali huku ameukumbatia mto wake na wacho yake alikuwa akiangalia darini.
“Mage..Mage.”
“A..a..bee.”
“Mbona sikuelewi mwanangu?”
“Mama nahitaji msaada wako najua nimechanganya madawa.”
“Nikusaidie nini?”
“Sijui Colin atanielewaje maana nilichomfanyia si kitu kizuri.”
“Kwa kweli hatua tuliyofikia huku vikao vikienda vizuri halafu mwenzako abadili uamuzi sijui sura zetu tutaziweka wapi?”
“Hapo ndipo ninapochanganyikiwa, mama kitendo walionifanyia familia ya kina Hans sitawasahau.”
“Umeona eeh, nilikueleza toka zamani familia ile ilikuwa haikupendi kama ungeolewa na Hans ndoa yako isingedumu. Mungu amekuletea mwanaume wa maisha yako unamchanganya.”
“Mama nimeisha fanya kosa naomba msaada wako, nitamweleza nini Colin anielewe.”
“Wala usiwe na wasi kamwambie kuwa ulimtuma Brenda cheni ambayo ulipanga kumpatia kama surprise umekuta hajaitengeneza na kujikuta umekasirika na kuanza kulia.”
“Mmh! Atanielewa? Naona kama utetezi mwepesi.”
“Walaa, ye anajua ulikuwa kwa Brenda, nilimwambia kuna kitu mmeshindwa kuelewana ndiyo maana ulirudi katika hali ile.”
“Mmh! Basi ngoja nifanye hivyo.”
Wakiwa katikati ya mazungumzo simu ya iliita ilikuwa ikitoka kwa mama Colin.
“Mkweo,” mama Mage alisema.
“Mmh! Lazima ataulizia kilichotokea.”
“Ngoja nimsikilize,” alisema huku akibofya cha kupolelea na kuweka simu sauti ya nje.
“Haloo mama Colin.”
“Eeh! Dada kuna nini huko?”
“Kwani vipi?”
“Naona Colin ananichanyanyia maneno wala simuelewi.”
“Wala hakuna kitu cha kutisha bali mkweo aliudhiwa na shoga yake, lakini kwa sasa yupo sawa na wakati wowote atakuja huko.”
“Mmh! Afadhali maana nilikuwa na wasiwasi.”
“Wa nini?”
“Nilijua Colin kisha mtibua mkwe wangu.”
“Walaa, sema mkweo ana hasira za kitoto kitu kidogo analia kama kafiwa.”
“Basi nikuacheni muendelee na mambo mengine.”
Baada ya simu kukatwa mama Mage alimgeukia mwanaye na kumwambia.
“Unaona ulivyotaka kumsababishia matatizo mwenzako?”
“Mama lazima niende sasa hivi najua mpenzi wangu hayupo kwenye hali nzuri.”
“Fanya hivyo na...” mama Mage alinyamaza baada ya mlango kugongwa.
“Unasemaje?” aliuliza kwa sauti.
“Kuna wageni.”
“Nakuja,” mama Mage alitoka nje kwenda kumsikiliza mgeni.
Alitoka hadi getini na kukutana wa wanaume wawili na mwanamke mmoja, aliwatazama walikuwa wageni kwake.
“Karibuni.”
“Asante.”
Aliwakaribisha hadi sebuleni, baada ya kuketi mama Mage alitaka kujua wana shida gani.
“Ndiyo jamani mna shida gani?”
“Sisi ni maafisa wa polisi,” walitoa vitambulisho vyao.
“Ndiyo, mna shida gani?”
“Tuna imani hapa ndipo anaishi Magreth Chogo.”
“Ndiyo.”
“Yupo?”
“Mna shida gani?”
Kabla hajajibu Mage alitoka chumbani ili awaone wageni ni kina nani, askari mmoja baada ya kumuona alijua ni Mage alibahatisha kwa kumwita jina.
“Mage.”
“Abee.”
“Upo chini ya ulinzi,” alisema askari wa kike.
“He! Kwa kosa gani?” Mage alishtuka.
“Kutokana na tukio lililomtokea mpenzi wako wa zamani.”
INAENDELEA HAPA

HADITHI: WAKILI WA MOYO SEHEMU: 10

$
0
0

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’

ILIPOISHIA:
Kabla hajajibu Mage alitoka chumbani ili awaone wageni ni kina nani, askari mmoja baada ya kumuona alijua ni Mage alibahatisha kwa kumwita jina.
“Mage.”
“Abee.”
“Upo chini ya ulinzi,” alisema askari wa kike.
“He! Kwa kosa gani?” Mage alishtuka.
“Kutokana na tukio lililomtokea mpenzi wako wa zamani.”
SASA ENDELEA...
“Sasa mimi nahusika kivipi?”
“Utajua yote kituoni.”
“Mi siendi,” Mage alitaka kugoma kwenda.
“We nenda wala usihofu, ila jamani chondechonde mwanangu asiguswe wala kulazimisha kusema uongo tutaelewana vibaya.”
“Hakuna tatizo, atakuwa salama baada ya mahojiano atarudi.”
Ilibidi Mage achukuliwe kupelekwa kituo cha kati cha polisi, mama yake alichukua simu na kumpigia mkuu wa polisi ambaye alikuwa rafiki mkubwa wa mzee Chogo baba yake Mage.
“Vipi shemeji?” ulipokewa upande wa pili.
“Mwanao Mage amekamatwa na vijana wako sasa hivi.”
“Kwa kosa gani?”
Alimwelezea kila kitu, baada ya kumsikiliza alimjibu.
“Basi hakuna tatizo shemeji nitalishughulikia mwenyewe, yupo kituo gani?”
“Cha kati.”
“Usiwe na wasi waache wamuhoji watamwachia tu.”
“Sawa shemeji kwa hiyo niende.”
“Hapana nitamfuta mwenyewe.”
“Asante shemeji.”
Mama Mage baada ya kukata simu alijikuta njia panda, alijifikiria kumpigia simu Colin lakini alijiuliza akimpigia atamwambia nini. Aliamua kukaa kimya ili kusubiri hatima yake ndipo ajue afanye nini.
***
Mage alipelekwa hadi kituoni na kuingizwa chumba cha mahojiano, Inspekta Koleta alikaa mbele ya meza aliyokuwa amekaa Mage na kalatasi ili kuandika mahojiano yale.
“Unaitwa nani?”
“Mage.”
“Nataka jina kamili.”
“Magreth Chogo,” Mage alijibu kwa sauti ya chini kidogo.
“Una umri gani?”
“Miaka 24.”
“Unamfahamu vipi Hans?”
“Namfahamu kama mpenzi wangu wa zamani.”
“Ulijuaje amepata matatizo?”
Mage alielezea jinsi alivyopigiwa simu na shoga yake Brenda ambaye alipigiwa simu rafiki yake Hans, Ndubukile.
“Wewe ulikuwa wapi?”
“Kwa mchumba wangu.”
“Anaitwa nani?”
“Colin.”
“Inasemekana mlikuwa ikipendana sana na Hans kwa nini hakukuoa akamuoa msichana mwingine?”
“Alichaguliwa na wazazi wake.”
“Unafikiri kwa sababu gani alichaguliwa msichana mwingine wakati wewe ndiye uliyekuwa mpenzi wake kila mtu alijua.”
“Kwa kweli kwa hiyo siwezi kujua.”
“Hans alipoona mwanamke mwingine wewe ulichukuliaje?”
“Sikuwa na jinsi ila roho ilinikuma sana.”
“Ulifikiria kufanya nini baada ya kuachwa na Hans?”
“Nilipanga kutojishughulisha na mapenzi tena.”
“Hukupanga kulipa kisasi?”
“Kisasi cha nini?”
“Kwa vile ndoto zako zilikuwa kuolewa na Hans.”
“Ni kweli ndoto zangu zilikuwa kuolewa na Hans lakini sikuwa chaguo la wazazi wake.”
“Unafikiria kwa nini unahusishwa na matukio ya mauaji na shambulizi la Hans?”
“Hata mimi nashangaa.”
“Kuna ukweli gani umelipa kisasi cha kuachwa kuolewa?”
“Hakuna ukweli wowote kwa vile sasa hivi nami nipo katika maandalizi ya ndoa yangu, kwanza nifanye vile kwa ajili gani kwa vile Hans sijagombana naye ameoa tukiwa tunapendana. Pia sikuwa na kinyongo na familia yake.”
“Unaweza kufikiria nani aliyefanya vile?”
“Mmh! Kwa kweli sijui kwa vile niliisha kata mawasiliano na Hans toka alipooa.”
“Kuna taarifa mlikuwa na penzi la siri na Hans?”
“Si kweli, mara nyingi Hans alinitafuta kuniomba msamaha nilimkatalia kwa vile yeye ni mume wa mtu sikutaka kuonekana naingilia ndoa yake hasa baada ya familia yake kutonihitaji.”
Wakiwa katika ya mazungumzo mkuu wa polisi aliingilia Mr Clarence, Inspekta Koleta alinyanyuka na kupiga saluti. Mage alipomuona alifurahi kwani siku zote alikuwa mtu wa karibu katika familia yao.
“Shikamoo baba.”
“Marahaba, kuna nini?”
“Mkuu kuna tukio la mauaji na mashambulizi ambayo inaonekana mshukiwa wa kwanza ni huyu binti,” alijibu Inspekta Koleta.
“Hebu nipe hiyo kalatasi ya maelezo.”
Mkuu wa Polisi Mr Clarence aliichukua na kuisoma kisha aliomba kuzungumza na Mage kidogo. Baada ya kupishwa alimuuliza mswali kuhusiana na tukio lile.
“Mage.”
“Abee baba.”
“Naomba uniambie ukweli ili nikusaidie hata kama umehusika niambie ili nijue jinsi ya kukusaidia,” Mr Clarence alimwambia kwa upole.
“Baba haki ya Mungu sijui chochote zaidi ya kupigiwa simu asubuhi nikiwa kwa mkweo, kwa vile Hans ndiye aliyekuwa chaguo la moyo wangu pia sikukosana naye bali penzi letu lilivunjwa kwa nguvu ya wazazi wake nilishtuka sana kupata habari ile. Huwezi kuamini taarifa ile ilisababisha nitoke hata bila kumuaga mkweo hivi ndiyo nilikuwa najiandaa kwenda kuzungumza na mkweo japo sikutaka ajue nimekuja kumuona mpenzi wangu wa zamani.”
“Una muda gani ujaonana na Hans?”
“Mmh! Sasa ni mwaka na nusu.”
“Kwa nini?”
“Baba, yeye kaoa na mimi Mungu kanipa wangu kuna umuhimu gani kuendeleza ukaribu?”
“Nimekuelewa, sasa nitawaambia utoke kazi yote niachie mimi.”
“Asante baba.”
Mkuu wa polisi alimwita Inspekta Koleta na kumweleza amwachie Mage na kumweleza waendelee na upelelezi kwa vile Mage ahusiki na matukio yake. Walikubaliana na Mage aliruhusiwa kutoka. Mkuu wa Polisi Mr Clarence alimchukua Mage na kumrudisha nyumbani.
Mama yake alifurahi kumuona mwanaye na Mr Mulisa.
“Asante shemeji.”
“Kawaida, nina imani Hans akipata nafuu kila kitu kitakuwa wazi.”
“Tena Mungu ampe afya ili kuwaumbua wenye roho mbaya wanataka kuiharibu harusi na mwanangu.”
“Usiwe na wasi kila kitu kitakwenda kilivyopangwa na aliyetenda unyama ule atajulikana mkono wa dola ni mrefu.”
Mkuu wa polisi aliaga na kumuacha Mage na mama yake, baada ya kuondoka Mage aliagungua kilio.
“Mama kosa langu nini? Mbona familia ya kina Hans wameniandama hivyo, jamani mimi nimuue mke wa Hans na mwanaye na kutaka kumuua Hans ili iweje?”
“Ndiyo dunia mwanangu, kwa vile baba yako yupo atakusimamia.”
“Unajua mama mi’ nilikuwa na wasiwasi labda aliyefanya vile ni Colin.”
“Wee! Temea chini tena usirudie kusema kitu kama hicho, Hans na Colin wapi na wapi?” Mama yake alikuwa mkali.
“Basi mama nisamehe ni mawazo tu.”
“Tena umeniudhi sana, wee kidogo ufe kwa presha kwa kusingiziwa unataka kumpaka shombo mtoto wa watu.”
“Basi mama nisamehe ulikuwa wasiwasi wangu.”
“Nataka uoge ubadili nguo uende kwa mwenzio ukamtoe hofu usimweleze ya kupelekwa polisi.”
“Sawa mama.”
Mage alikwenda kuoga na kubadili nguo alichukua gari na kwenda kwa Colin, akiwa njiani alijawa na mawazo juu ya familia ya Hans kumshukia yeye katika tukio lile.
Alijiuliza kipi hasa kilichofanya wamfikirie yeye kwanza.
Aliona jinsi gani familia ile jinsi ilivyokuwa ikimchukia na kuamini kauli ya mama yake kuwa hata kama angeolewa asingedumu kwenye ndoa yake kwa vile hakuwa chaguo lao.
Alijikuta taratibu mapenzi yake yote akiyahamishia kwa Colin na kuuapia moyo wake kumpenda kwa nguvu zake zote na kwa akili zake zote. Alipofika nyumbani kwao Colin baada ya kuteremka kwenye gari aliingia ndani huku akikimbia kama mtu aliyepagawa. Sebuleni alimkuta mama Colin, alishtuka kumuona katika hali ile.
“Vipi Mage?”
“Mama, mume wangu yupo wapi?” aliuliza akionesha kuchanganyiwa.
Wakati huo Colin alikuwa akitokea chumbani kwake kuja sebuleni, alipomuona alikimbilia na kumkumbatia.
“Jamani mume wanguu!”
“Vipi mbona hivyo?” Colin alishtuka uchangamfu wa Mage uliopitiliza.
“Najua nimekuudhi nisamehe sana, mama nimemuudhi sana mume wangu,” Mage alisema huku akilia.
“Hujamuudhi chochote,” mama Colin alisema.
“Najua nimemuudhi, Colin naomba twende chumbani.”
Walishikana mikono na kuelekea chumbani na kumuacha mama Colin akiwatazama na kuchekelea moyoni na kusema kwa sauti ya chini. “Kweli wanapendana.” Aliwatazama mpaka walipopotea machoni kwake.
Colin na Mage alikwenda hadi chumbani, alipofika ndani Mage alijifupa kifuani kwa mpenzi wake na kuanza kulia kitu kilichomshtua Colin na kuhoji.
“Vipi mpenzi?”
“Colin nisamehe sana mpenzi wangu.”
“Kwa lipi?”
“Najua leo nimekukosea kwa kuondoka bila kukuaga kitu kilichokufanya usumbuke kunitafuta, kibaya zaidi zijapokea simu zako na kukataa kuzungumza na wewe uliponifuata nyumbani.”
“Kumbe ni hayo? Achana nayo.”
“Hapana najua umenikubalia ili yaishe lakini umejenga picha mbaya juu yangu.”
“Walaa.”
“Colin nihukumu hukumu yoyote lakini elewa nakupenda sana mpenzi wangu, nilitaka kufanya surprise lakini ikaenda ndivyo sivyo. Nilishindwa nikueleze nini kwa vile sikuwa na lakukueleza kwa wakati ule hasa baada ya Brenda kunichanganya.”
“Yote mama alinieleza ndiyo maana nilikuelewa toka asubuhi.”
“Colin lakini si unajua nakupenda?” Mage alimuuliza kwa sauti ya kudeka.
“Najua, ndiyo maana upo hapa.”
“Nashukuru kulifahamu hilo.”
Siku ile Mage alishinda pale na kufanya kazi zote za nyumbani ikiwa pamoja na kupika chakula cha jioni. Colin aljikuta akisahau yote na kujiona kama tayari kaisha muoa Mage.
Siku ile muda wote walikuwa pamoja kama kumbikumbi kwa kufanya kazi kwa kusaidizana. Mama Colin muda wote alikuwa mtu wa tabasamu na kuona ndoa ya mwanaye jinsi itakavyojaa furaha na upendo.
Aliwaangalia walivyopendeza kwa kusaidizana kazi zote za jikoni mtu na mchumba wake. Alifumbata mikono yake na kuomba kwa sauti ya chini.
“Eeh! Mwenyezi Mungu baba nijalie ndoa ya wenetu iwe yenye matunda,” baada ya dua alipiga njia ya msalaba kumshukuru Mungu.
Siku ile ilikuwa ya furaha kwa wapenzi wawili kwa Mage ambaye alihamishia mapenzi yake yote kwa Colin baada ya kujua hata kama angempenda vipi Hans asingekuwa na nafasi ndani ya familia yake. Aliona jinsi gani sivyo mpenda mpaka kumzushia shutuma nzito za mauaji ya shambulio la kuua.
Kingine kilichomuweka njia panda kama Mungu atamsaidia Hans kupona atamchukuliaje, lazima naye atangeamini mhusika ni yeye. Lakini kwa upande wa Hans alijua ni vigumu kumshuku yeye kutokana na ukaribu wao ulivyokuwa.
Angekuwa na wasiwasi kama angekuwa akilipigania penzi la Hans. Kama tatizo lile lingemtokea baada ya kuoa lazima Hans angejua ni yeye, lakini baada ya mkewe kupata ujauzito na kujifungua penzi lake alilizika rasmi.
Aliamini ule ndiyo muda wa kulionesha penzi lake halisi kwa Colin, siku ile alilala tena na kuondoka siku ya pili huku kila mmoja akifurahia penzi la mwenzake.
****
Ukaribu wa Mage na Colin kwa kufuatana muda wote kama kumbikumbi, Ulifanya Colin ashindwe kutekeleza ahadi yake kwa kina Cecy. Baada ya kusubiri kwa wiki bila kuonekana dalili zozote za kutekelezwa ahadi. Cecy aliyekuwa amejilaza kitandani na kukosa usingizi.
Alijikuta akinyanyuka kitandani na kumfuata mama yake aliyeamini ameisha pitiwa usingizi ambaye alikuwa na matumaini ya kuyakimbia maisha ya kulala nyumba ya kuvuja na taa ya kibatari.
Alitoka chumbani kwake na kwenda hadi kwenye mlango wa mama yake na kugonga.
“Mama..mama.”
“Unasemaje Cecy,” alimuuliza bila kuamka kwa vile tayari alikuwa amepitiwa usingizi.
“Kuna jambo nataka tushauliane.”
“Jambo gani, kwani lazima tuzungumze usiku?”
“Ndiyo, asubuhi nikiamka nijue cha kufanya.”
“Mmh! Nakuja.”
Mama yake aliamka na kutoka sebuleni, alimkuta Cecy amesimama, mama yake aliketi kwenye kigoda na kumtazama mwanaye aliyekuwa bado amesimama.
“Unasemaje mama?”
“Mama siku zote japo mdogo lakini huwa nayaamini mawazo yangu japokuwa sina elimu kubwa, lakini busara haina elimu bali kipawa toka kwa Mungu.”
“Ni kweli.”
“Hivi mama tulipokuwa tukifanya biashara zetu tulipungukiwa nini?”
“Hatukupungukiwa kitu, kwani maisha ya mwanadamu Mungu ndiye anayetuongoza.”
“Kwa hiyo hatuwezi kumtegemea mtu?”
“Ndiyo, kwani amelaaniwa kila amtegemea mwanadamu.”
“Nimefurahi sana kulifahamu hilo.”
“Ulikuwa una maanisha nini?”
“Huoni kama tunamkosea Mungu kumtegemea mtu.”
“Tunamtegemea nani?”
“Tumeacha kufanya biashara zetu kwa ajili ya Colin aliyetugeuza watoto kutuahidi pipi, leo ni siku ya ngapi hatufanyi biashara kwa ajili ya kusubiri ahadi yake. Wiki inakatika hakuna cha tofari wala mchanga.”
“Cecy mwanangu Colin, naye binadamu huenda amepatwa na matatizo. Hivyo tulitakiwa kuvuta subira.”
“Mama niliyajua haya mapema, sikutaka kukukata kauli kwa vile wewe ni mtu mzima. Lakini nilijua hakuna kitu, Colin atujengee nyumba kwa kipi cha maana tulichompa?”
“Kwa hiyo ulikuwa unasemaje?”
“Kesho asubuhi nakwenda Mabibo kununua ndizi na kuendelea na kazi yangu inayoniweka mjini.”
“Mmh! Si wazo baya.”
Walikubaliana siku ya pili Cecy aendelee na biashara yake ya ndizi kama kawaida. Kila mmoja alirudi chumbani kwake na kupanda kitandani. Cecy alichelewa kulala huku moyo ukimuuma kwa kitendo cha Colin kuwadhalilisha kwa kuwaahidi kitu kisichowezekana.
Alijikuta akimchukia Colin na kuapa hata zungumza naye siku zote za maisha yake. Kutokana na hasira alijikuta akichelewa kulala.
Siku ya pili Cecy aliamka na mapema na kuwahi kununua ndizi, baadaye alirudi nyumbani na kuoga kisha aliingia chumbani na kuchagua nguo za kuiingia nazo mtaani. Alitafuta gauni lililochoka na upande wa khanga uliopauka na kuvaa.
Alitoka kuelekea nje, alipofika mlangoni alisita kidogo na kujiuliza swali.
“Hivi maisha yangu namtegemea nani? Jibu Mungu, kwa nini niishi maisha kwa ajili ya mtu fulani? Ina maana bila Colin sina maisha? Hapana..hapana,” Cecy alisema huku akirudi chumbani na kuvua nguo chakavu na kufungua sanduku lake na kutoa nguo nzuri na kuzivaa kisha alitoka na kuchukua beseni lake la ndizi na kumuaga mama yake aliingia mtaani kuuza ndizi.
Alishangaa siku ile alimaliza ndizi mapema tofauti na alivyobadili mfumo wa maisha baada ya kuumizwa na penzi la Colin na kuamua kuishi kwa kutojijali. Toka alipoamua kuishi maisha yale biashara yake haikuwa kama awali alijikuta akimaliza biashara zake kwa kutembea umbali mrefu pia kutumia muda mwingi.
Alijikuta akijilaumu kwa kupoteza muda wake mwingi kumuwaza Colin mwanaume asiye na mapenzi naye ambaye tayari alikuwa na mpenzi wake. Moyo wake aliutoa kifungoni na kuwa tayari kupokea penzi jipya ila la mtu atakaye mpenda naye ampende ambaye atakuwa sahihi kwa moyo wake.
Hakuwa tayari kumkubali mwanaume anayetumia umaskini wake kufanya naye ngono. Siku zote aliamini mwenye mapenzi ya kweli hawezi kutanguliza ngono mbele zaidi ya upendo kwanza.
Lakini kwa Colin alikuwa radhi kuupoteza usichana wake hata bila ndoa kwani aliamini penzi la Colin lilizidi furaha ya maisha yake. Baada ya matukio yote aliamini muda wa uvumilivu ulikuwa umepita hivyo alitakiwa kitengeneza mawazo mapya na kuwaza kitu kingine kabisa kigeni katika ubongo wake.
Kila usiku ulipoingia alitumia muda mwingi kuwaza maisha wanayoishi ya kuuza ndizi mwisho wake nini. Aliamini muda ule bado ana nguvu alitakiwa atafute njia mbadala itakayomsaidia kukabiliana na ukali wa maisha aweze kumsaidia mama yake. Wazo lilikuwa kila jioni baada ya kutoka kwenye biashara zake ambazo zilikuwa zikifanya vizuri japokuwa changamoto za wanaume zilikuwa kubwa ambazo alikabiliana nayo.
Wazo kubwa lilikuwa aanze kusoma masomo ya jioni kujifunza kingereza ambacho kingemsaidia kufafuta kazi ya kuajiliwa na kuachana na kazi ya kuzurula huku akila vumbi la barabarani.
Wazo lile alimwambia mama yake ambaye naye aliliafiki, jioni ilipofika alikwenda sehemu moja iliyokuwa ikifundisha twisheni na kuomba kusoma kingereza ambacho aliahidiwa kukijua baada ya miezi mitatu. Alilipa ada na kuanza kusoma siku ileile huku akiwa na ndoto za siku moja naye kuzungumza kingereza.
Itaendelea

WAKILI WA MOYO SEHEMU: 11

$
0
0

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
ILIPOISHIA:
Wazo lile alimwambia mama yake ambaye naye aliliafiki, jioni ilipofika alikwenda sehemu moja iliyokuwa ikifundisha twisheni na kuomba kusoma kingereza ambacho aliahidiwa kukijua baada ya miezi mitatu. Alilipa ada na kuanza kusoma siku ileile huku akiwa na ndoto za siku moja naye kuzungumza kingereza.
SASA ENDELEA...
***
Mipango ya harusi ya Colin na Mage ilizidi kupamba moto huku kila familia ikijipanga kufanya sherehe ya kufuru. Nayo Hali ya Hans iliendelea vizuri iliyofanya atolewe hospitali na kurudishwa nyumbani. Baada ya kutulia kwa wiki moja aliitwa polisi kutoa maelezo kutokana na tukio lililomtokea lililopeleka kupoteza mke na mtoto.
“Pole sana,” Inspekta Koleta alianza kwa kumpa pole.
“Asante.”
“Unajisikiaje kwa sasa?”
“Namshukuru Mungu sijambo kabisa.”
“Unakumbuka tukio lilivyotokea?”
“Ndiyo, nilikuwa chumbani mke na mwanangu wakiwa sebuleni ghafla nikasikia sauti kama ya amri, mwanzo nilifikiri labda sauti inatoka kwenye tivii kwa vile alikuwa akiangalia tamthilia. Lakini sauti ya maumivu ya mke wangu ilinishtua na kunifanya nitoke chumbani. Nilishtuka kuona mke na mwanangu wamelala chini.
“Nilipotaka kwenda kuwasaidia nilipigwa na kitu kizito kichwani kilichonifanya nipoteze fahamu. Nilipozinduka nilijikuta nipo hospitali na kupewa taarifa za kushtusha za kifo cha mke wangu na mwanangu,” Hans alipofika hapo alianza kulia na kumfanya Inspekta Koleta kumbembeleza.
“Pole sana.”
“Asante, lakini inauma sana heri wangeniua mimi kuliko mke na mwanangu!”
“Najua inauma, unawafahamu waliofanya unyama ule?”
“Kwa kweli siwafahamu kutokana na kuziba nyuso zao na kofia za kuziba kichwa.”
“Unamjua Mage?”
“Mage yupi?”
“Wewe unamjua Mage yupi?”
“Mmh! Mmoja.”
“Yupi?”
“Aliyewahi kuwa mpenzi wangu.”
“Unamfahamu vipi?”
“Alikuwa mpenzi wangu, lakini bahati mbaya nilioa mwanamke mwingine badala yake.”
”Kwa sasabu gani ulioa mwingine na kumuacha mpenzi wako wa muda mrefu?”
“Wazazi wangu walikuwa hawamtaki.”
“Unafikiri kitendo cha wazazi wako kumkataa Mage na kumchukua mwanamke mwingine kilimpandisha Mage hasira na kuamua kukukomoa?”
“Walaa, yule msichana hausiki kabisa.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Sasa hivi yupo katika mipango ya harusi anategemewa kuwa mke wa mtu afanye vile ili iweje?”
“Kwa hiyo huna mtu yeyote unayemshuku?”
“Mmh! Hakuna,” Hans alikataa.
“Basi tukikuhitahi tutakuita.”
“Hakuna tatizo.”
Baada ya mahojiano yale Hans aliruhusiwa kuondoka, alirudi kupumzika nyumbani. Kila alipokaa peke yake moyo aliendelea kuumia bila kuonana na Mage na kumweleza neno lililo moyoni mwake kabla ya kuolewa.
Aliamini kwa vile ulikuwa umebakia mwezi mmoja na nusu harusi ifungwe ingekuwa vigumu kuonana ana kwa ana. Wasiwasi wake ulikuwa kutopata nafasi baada ya kupata taarifa kwenda kumuona hospitali na kufukuzwa kisha kufunguliwa shtaki la kuishambulia familia yake. Aliamini Mage hatakuwa tayari kumsikiliza.
Alijaribu kumpigia shoga yake Brenda ili amsaidie aweze kuzungumza naye hata kwa dakika mbili kisha moyo wake uwe radhi Mage kuolewa. Alichukua simu yake na kumpigia Brenda ambaye aliipokea upande wa pili.
“Haloo.”
“Haloo Brenda.”
“Abee, nani mwenzangu?”
“Hans.”
“Hans yupi?”
“Shemu kweli umenichoka yaani leo unaniuliza hivyo?”
“Ha! Kumbe wewe? Vipi unaendeleaje?”
“Nipo fiti kama chuma.”
“Wewee! Utani huo upo wapi?”
“Nyumbani, kwanza niwapeni pole kwa kitendo cha familia yangu kuwazuia kuniona kimeniuma sana kwa hiyo nakuombeni radhi sana.”
“Hans wewe siku zote huna kosa, familia yako ndiyo kikwazo katika maisha yako.”
“Hilo nalijua.”
“Hans mtoto bado ana mapenzi na wewe baada ya taarifa zile kachanganyikiwa mbio hospitali lakini walichomfanya familia yako hawezi kusahau kibaya zaidi wamempakazia tatizo lako.”
“Yaani wamenichanganya ile mbaya, Brenda naomba unikutanishe na Mage ili nimuombe msamaha.”
“Mmh! Sijui kama utampa kwa vile sasa hivi yupo katika maandalizi ya ndoa yake.”
“Sikiliza Brenda naomba nikupitie kwenu twende hadi nje ya nyumba yao Mage kisha uje naye nizungumze naye kwa dakika tano kisha nikurudishe nyumbani kwenu. Nakuahidi zawadi nzuri ukiniwezesha kumuona Mage kwa dakika hata mbili tu.”
“Mmh! Kwani sasa hivi upo wapi?”
“We nieleze nikufuate wapi?”
“Njoo home basi.”
“Fanya hivi chukua gari la kwenu tukutane Kivukoni.”
“Haina tatizo.”
Hans baada ya kuelezwa vile alitoka na kuingia kwenye gari aina ya Toyota Verosa na kuelekea Kigamboni kwa kina Mage. Alipofika Kivukoni hakukaa sana simu yake iliita ilikuwa ya Brenda, aliipokea.
“Haloo Brenda.”
“Hans nimefika, upo wapi?”
“Nami nimefika umekuja na gari gani?”
“Nissan Patrol nyeupe.”
“Basi tuvuke.”
Walikubaliana kuvuka upande wa pili, baada ya watu na baadhi ya magari kujaa ndani ya kivuko safari ya kuelekea Kigamboni ilianza. Kivuko kiliposimama upande wa Magogoni, watu waliteremka na kuelekea maeneo ya Kigamboni, Mji mwema mpaka Geza ulole na kwingineko.
Brenda alitangulia baadaye aliliona gari la Hans likija nyuma, hakusimama aliendelea na safari mpaka karibia na kwa kina Mage alisimamisha gari pembeni Hans naye alisimamisha pembeni yake na kuteremka.
Hans na Brenda walikumbatiana na kupeana pole upya huku Brenda akiwa haamini kama Hans amepona.
“Dah! Pole sana.”
“Asante.”
“Sasa inakuwaje?”
“Fanya hivi hili gari langu tuliache sehemu salama ili twende na lako tukifika utaingia ndani kwenda kumuita akija utamuingia kwenye gari lako najua atashangaa kuniona lakini nitatumia muda huo kuzungumza naye kisha atarudi ndani mwao na sisi tuondoke.”
“Hakuna tatizo.”
Hans alilipaki gari lake sehemu ya usalama na kuingia kwenye gari la Brenda hadi nyumbani kwao na Mage. Alipofika alilisimamisha gari pembeni ya geti hakutaka kuliingiza ndani na kuteremka. Mlinzi alishangaa kuliacha gari nje na kumuuliza.
“Da’ Brenda mbona huingizi gari ndani?”
“Hapana sikai sana,” Brenda alijibu huku akiingia ndani ya geti.
Alitembea kwa mwendo wa kukimbia hadi ndani, alimkuta msichana wa kazi akiondoa vyombo mezani na kumuuliza.
“Mage yupo wapi?”
“Chumbani kwake.”
Alikwenda hadi chumbani na kugonga.
“Ingia,” sauti ya Mage toka ndani ulisema.
Brenda alisukuma mlango na kuingia ndani Mage alishtuka kumuona shoga yake muda ule, kwa vile hawakuwa na miadi ya kukutana muda ule wakati mchana wa siku ile walikuwa pamoja na kuachana jioni.
“He! Vipi mbona huku muda huu?” Mage alimshangaa Brenda.
“Shoga hebu twende nje mara moja.”
“Kuna nini?”
“Utajua huko, we twende mara moja.”
Mage bila kuongeza neno alinyanyuka kitandani na kuongozana na Brenda hadi nje, alishangaa kuona wanatoka nje ya geti. Lakini hakuhoji alisubiri kuona Brenda kamuitia nini. Alipotoka nje ya geti aliliona gari la Brenda, kwa vile alikuwa akisubiri muda wa kwenda kwa Colin na alichelewa kwenda kutokana na mama yake kutoka alimwambia shoga yake.
“Brenda siwezi kufika mbali namsubiri mama ili niende kwa mume wangu.”
“Hata huendi popote twende ndani ya gari.”
“Kuna nini?”
“Hebu punguza maswali.”
Waliongozana wote hadi kwenye gari.
“Ingia mlango wa nyuma,” Brenda alimwambia Mage, naye hakubisha aliingia.
Ndani ya gari palikuwa giza, Brenda baada ya kuingia mbele aliwasha taa na kumfanya Mage ashtuke kumuona Hans.
“Ha! Hans?”
“Ndiyo mimi Mage samahani kwa kukushtukiza.”
“Bila samahani, kwanza unaendeleaje?”
“Namshukuru Mungu sijambo kabisa.”
“Pole na kufiwa mke na mtoto.”
“Asante, pole na wewe kutokana na ulichotendewa na familia yangu.”
“Hans achana na hayo yameisha pita, nina imani kuna kitu kimekuleta naomba tuzungumze kwa haraka nataka kwenda kwa mume wangu muda si mrefu.”
Hans alijikuta akitulia huku maneno yakigoma kutoka mdomoni, Mage alishangaa kuona mpenzi wa zamani akitokwa na machozi. Brenda alitoka nje ya gari na kuwaacha wapenzi ndani ya gari wazungumze yao.
“Jamani nipo nje.”
“Hakuna tatizo, usikae mbali natoka sasa hivi,” Mage alisema.
Baada ya kutoka Mage alimuuliza Hans aliyekuwa akitokwa machozi.
“Hans ameniita kuona machozi yako au kuna kitu kingine kama ni machozi nimeisha yaona, naomba niende zangu,” Mage alizungumza kwa sauti ya upole huku akimtazama usoni Hans.
“Ma..ma..ge,” Hans alisema kwa kigugumizi.
“Jina langu.”
“Kilichonileta si kuja kukuonesha machozi bali moyo wangu umejaa maumivu makali.”
“Najua inauma kupoteza mke na mtoto si kitu cha kawaida yataka moyo wa chuma kuyashinda maumivu yake lakini Mungu siku zote ni mfariji na kukufanya utayasahau yote kisha atakuletea mke mwingine.”
“Mage mimi na wewe tuliahidiana nini?”
“Kuoana kuwa mke na mume.”
“Baada ya matatizo ya familia yangu nilikueleza nini?”
“Ulisema huwezi kuzaa na yule mwanamke, baadaye utamuacha na kunioa mimi.”
“Kwa nini umekubali kuolewa na mwanaume mwingine?”
“Kwa sababu umevunja ahadi yetu.”
“Mage nina imani unajua jinsi gani ninavyokupenda?”
“Siyo unavyonipenda bali ulivyokuwa ukinipenda.”
“Mage moyo wangu hautachoka kukupenda, nilikueleza nini baada ya kulazimishwa kuoa mwanamke mwingine?”
“Ulisema wakikulazimisha kuoa utajiua.”
“Ulinishauri nini?”
“Nilikuwa radhi uoe lakini si kukupoteza maishani, ulichoniahidi ndicho kilinipa moyo na kuwa radhi kukusubiri hata miaka mia. Lakini wewe ndiye ulivunja mkataba na kuamini sina changu na kuamua nami kutafuta wangu japokuwa ilikuwa sawa na kunimezesha mfupa.”
“Ndiyo sababu ya mimi kuja kuzungumza na wewe, baada ya kunisikiliza uamuzi utakaoutoa hapa sitapingana nao hata kama utaniumiza.”
“Haya niambie hicho kilichokuleta.”
Hans alianza kuzungumza kwa sauti ya chini yenye kusikika huku machozi yakiweka michirizi kwenye mashavu. Mazungumzo yalikuwa (Of air) ambayo hayakutakiwa mtu yeyote kusikia zaidi ya watu wawili tu. Hans alimaliza kuzungumza huku machozi na kamasi zikimtoka chapachapa.
Muda wote Mage alijitahidi kumbembeleza Hans japokuwa naye alikuwa akilia.
“Hans nimekuelewa lakini hukutakiwa kufanya hivyo.”
“Sikuwa na jinsi, hukutaka kunisikiliza nilikuwa na wakati mgumu wa kuweza kunisikiliza. Kama ningekufa bila wewe kuujua ukweli wa moyo wangu ningekuwa nimekufa kibudu. Kama ningeshindwa kabisa ningekuja kujiua kwenye harusi yako ili ujue nilichokuahidi hakitabadilika moyoni mwangu kuwa kifo pekee ndicho kitanitenganisha na wewe.”
“Mmh! Mbona Hans unanipa mtihani mkubwa, japokuwa uamuzi ni wangu lakini dunia itanitenga.”
“Lakini Mage nilikueleza kila kitu juu yetu, wewe ndiye uliyeshikilia uhai wangu kwa mara nyingine wa kuniua au kuniacha hai ni wewe.”
“Hans hata siku moja kifo chako hakitatoka mikononi mwangu, naombani uniache kwa leo mengine tutazungumza kesho kichwa changu kimevurugika hata sielewi jifanye nini.”
“Ila kumbuka uhai wangu umeubeba wewe.”
“Naelewa Hans.”
“Kwa hiyo niondoke na jibu gani?’
“Niache kwa leo, nimekuelewa Hans.”
“Sawa lakini bado nipo njia panda.”
“Hans kuwa muelewa nimekueleza nimekuelewa unataka nini tena?”
“Basi nashukuru.”
“Nikutakie usiku mwema.”
“Na kwako pia.”
Mage aliteremka kwenye gari na kumuaga shoga yake huku akifuta machozi yaliyokosa kizuizi kisha alielekea ndani mwao. Brenda aliingia ndani ya gari na kushangaa kumkuta Hans akifuta machozi wakati Mage naye alitoka akifuta machozi.
“Vipi kuna usalama?”
“Kiasi.”
“Umeelewana?”
“Ndiyo.”
“Kwa hiyo tunaweza kwenda.”
“Ndiyo.”
Brenda aliwasha gari na kuliondoka kuelekea walipokuwa wameliacha gari la Hans, njiani alijaribu kudodosa kwani kila mmoja alionekana kulia.
Itaendelea

WAKILI WA MOYO SEHEMU: 12

$
0
0

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’

ILIPOISHIA:
Mage aliteremka kwenye gari na kumuaga shoga yake huku akifuta machozi yaliyokosa kizuizi kisha alielekea ndani mwao. Brenda aliingia ndani ya gari na kushangaa kumkuta Hans akifuta machozi wakati Mage naye alitoka akifuta machozi.
SASA ENDELEA...
“Vipi kuna usalama?”
“Kiasi.”
“Umeelewana?”
“Ndiyo.”
“Kwa hiyo tunaweza kwenda.”
“Ndiyo.”
Brenda aliwasha gari na kuliondoka kuelekea walipokuwa wameliacha gari la Hans, njiani alijaribu kudodosa kwani kila mmoja alionekana kulia.
“Hans, Mage anasemaje?”
“Hana la kusema bali nilitaka tu kumfikishia ujumbe, nashukuru amenisikiliza.”
“Kwa hiyo roho yako umetulia?”
“Nashukuru, tukifika kwenye gari nitakupa zawadi yako niliyokuahidi.”
“Nitashukuru.”
***
Muda ulizidi kukatika bila Mage kuonesha dalili zozote za kutoka kwenda kwa Colin, kitu kiliochomshtua mama yake ambaye aliwahi kurudi kwa ajili ya mwanaye kwenda kwa mchumba wake. Aliangalia saa ya ukutani ilimuonesha inakaribia saa nne usiku, alijiuliza labda mwanaye ametoka bila yeye kujua.
Ilibidi amuulize msichana wa kazi kama Mage ametoka yeye akiwa chumbani.
“Sofi Mage ametoka saa ngapi bila kuniaga?”
“Mmh! Mama sijamuona kutoka.”
“Una maanisha yupo chumbani kwake?”
“Sijajua ila sijamuona.”
Mama Mage alinyanyuka na kwenda chumbani kwa mwanaye, alikuta mlango umerudishwa alisukuma na kuingia bila hodi na kumkuta Mage amejilaza akiwa amekumbatia mtu huku machozi yakimwagika kama maji. Mama yake alishtuka na kutaka kujua kuliko mwanaye kuwa katika hali ile.
“Mage! Nini mwanangu?”
“Mamaa..maamaa,” Mage alishindwa kuzungumza aliangua kilio.
“Mage una nini?” mama yake alizidi kumshangaa.
“M..m..maa..ma,” Mage kila alipotaka kusema maneno yaligoma kutoka mdomoni.
“Mage mwanangu umepatwa na nini, hebu nieleze mimi ndiye mama yako nipo tayari kukusikiliza na kukusaidia.”
“Mama nipo kwenye wakati mgumu sana maishani mwangu.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Najua nitakuudhi wewe mama yangu lakini nina imani ndiyo tiba sahihi ya moyo wangu ambao umekuwa matesoni kwa muda mrefu.”
“Una maanisha nini?” mama yake alishtuka mpaka mapigo ya moyo yalianza kumwenda kasi.
“Mama nitakacho kisema najua kitakuwa sawa na kumng’oa mtu jino bila ganzi.”
“Una maanisha nini?”
“Mama sitaki kuolewa tena.”
“Niniii?” mama alishtuka.
“Mama sitaki kuolewa na Colin.”
“Kwa nini?”
“Si chaguo la moyo wangu.”
“Mwanangu unasema ukweli au unatania?”
“Nasema kweli kabisa.”
“Mmh! Na mipango ya ndoa?”
“Tunasitisha kwa vile muda bado.”
“Na watu tuliowachangisha fedha za send of.”
“Tutawarudishia fedha zao.”
“Wee mwana tutazupata wapi?”
“Mi najua pa kuzipata.”
“Hebu mwanangu nieleza tatizo nini, kama Colin amekukosea bado tuna nafasi ya kuzungumza tukalimaliza.”
“Mama, Colin hajawahi kunikosea toka tujuane, ila mimi ndiye nimekuwa nikimkosea muda wote. Najua ananipenda sana na uamuzi wangu utamchanganya, lakini ukweli utabakia palepale si chaguo la moyo wangu. Nimejilazimisha kumpenda lakini moyo umekataa hivyo sina budi kuusikiliza moyo wangu unachotaka.
“Siku zote moyo wa mtu huwa ndiyo muamuzi kwa jambo lolote kwa vile wenyewe ndiyo unaopokea furaha kwa jambo zuri au huzuri kwa jambo baya.”
“Kwa hiyo unasema hujakosana na Colin?”
“Walaa, najua Colin ananipenda sana na ataumizwa na uamuzi wangu lakini sina jinsi kila ndege hutua mtu aupendao.”
“Mage upo sawa mwanangu?”
“Nipo sawa mama.”
Kauli ile ilimfanya mama yake akae kwenye kitanda baada ya miguu kukosa nguvu.
“Mage mwanangu mbona sikuelewi, kipi kimekusibu mama?”
“Mama najua itakuwa vigumu kunielewa lakini utanielewa tu.”
Mara simu ya Mage iliita, aliichukua na kuitazama na kuirudisha bila kuipokea kitu kilichomfanya mama yake kuuliza.
“Mbona upokei kwani inatoka wapi?”
“Kwa Colin.”
“Sasa kwa nini hupokei?”
“Sasa nitazungumza naye nini?”
“Pokea mwambie leo huwezi kwenda hujisikii vizuri.”
“Siwezi kuzungumza naye kwa leo, nitajisikia vibaya.”
Simu iliita tena lakini haikupokelewa mpaka inakatika, baada ya muda msichana wa kazi alimwita mama Mage kuwa kuna simu yake inaita. Alitoka na kuichukua ilikuwa inatoka kwa mama Colin, aliipokea mara moja.
“Haloo dada.”
“Eeh! Kuna usalama huko?”
“Kiasi.”
“Kulikoni?”
“Mage kichwa kilimshika ghafla.”
“Jamani mkwe wangu! Vipi hali yake?”
“Kidogo hajambo amelala kwa sasa.”
“Basi tunakuja kumuona.”
“Usisumbuke, alitaka kuja nikamzuia hayupo serious sana.”
“Basi augue pole maana mwenzake alikuwa na wasiwasi baada ya kupiga simu isipokelewe.”
“Mwambie asiwe na wasiwasi ni kichwa tu lakini anaendelea vizuri kesho atakuwa hajambo.”
“Basi niwatakie usiku mwema.”
“Na ninyi pia.”
Mama Colin baada ya kumaliza kuzungumza alimgekia mwanaye aliyekuwa pembeni ya mama yake akifuatilia mazungumzo yale.
“Vipi mama?”
“Kumbe kichwa kilimshika ghafla amekunywa dawa kimetulia, alitaka kuja lakini mama yake kamwambia alale kwa leo atakuja kesho.”
“Duh! Afadhali, nilikuwa na wasiwasi sana.”
“Kapumzike, kesho mchumba wako atakuja.”
“Sawa mama.”
Colin alikwenda chumbani kwake, kabla ya kulala alichukua simu yake na kuangalia picha zote alizopiga na Mage na nyingine iliyopigwa siku ile mchana aliyotumiwa na Mage alipokuwa na shoga yake Brenda Mlimani City Samakisamaki. Aliibusu picha picha kubwa ya mpenzi wake aliyokuwa katika tabasamu la kufa mtu na kusema kwa sauti ya chini.
“Mage wewe ndiye mke wa maisha yangu,” aliikumbatia na kujilaza.
***
Mama Mage usingizi uligoma kabisa na kukiona kichwa kikitaka kupasuka kutokana na kuchanganywa na kauli ya mwanaye, alijiuliza kama mwanaye atasimamia uamuzi ule angeuweka wapi uso wake. Wasiwasi wake huenda amemfumania Colin na mwanamke mwingine na kuamua kuvunja uchumba.
Bado aliona kama ni hivyo linazungumzika kwa vile wote wamejuana wakiwa tayari wanayajua mapenzi. Alinyanyuka kitandani na kutoka kwenda kwa mwananaye kupata ukweli kwani alikuwa amechanganyikiwa sana. Alitoka taratibu taa ya sebuleni zilikuwa zimezimwa kulikuwa na hali ya ukimya kutokana na watu wote kuwa wamelala.
Hakutaka kuwasha taa ya sebuleni alitembea taratibu hadi chumba cha Mage alipotaka kuushika mlango alimsikia mwanaye akizungumza na simu alitulia ili asikilize anazungumza nini na nani. Alimsikia mwanaye akisema:
“Kama hivyo nimeisha litibua yote kwa ajili ya mapenzi yangu mazito kwako, kama umemejitoa muhanga kwa ajili yangu nami sina budi kujitoa kwa ajili yako. Najua uamuzi wangu utamchanganya mama na yule mchovu lakini wewe ni zaidi yao wote nakupenda sana zaidi ya kukupenda.
“ Nipo radhi vyote duniani viondoke ubakie peke yako, please mpenzi usinitende kosa lako ni mauti yangu, nashukuru kwa kujali mapenzi yangu kwako. Asante mpenzi wangu naomba ulale usingizi mororo huku ukiniota. I love you and i need you in all my life, mmmmwa.”
Mama Mage alijiuliza mwanaye anazungumza na nani, wazo lake lilipelekea labda ni Hans, lakini hakukubaliana nalo kutokana na maumivu aliyoyapata mwanaye kutoka kwa Hans na familia yake. Wazo lilielekea huenda kapata mpenzi mwingine ambaye kamzidi kete Colin.
Alishangaa mabadiliko yake ya ghafla kwani mpaka saa tatu kasoro usiku mwanaye alikuwa na kimuhemuhe cha kwenda kwa mchumba wake Colin na kumuhimiza kuwahi. Lakini aliporudi alikuwa mambo yamebadilika ghafla kama saa sita mchana ugeuke kiza totoro na watu wasionane.
Alipata wazo la kwenda chumbani kwa Sofia msichana wa kazi kumuuliza kuna kitu gani kilitokea kabla ya kurudi na kusababisha hali ile. Alikwenda kugonga chumba cha msichana wa kazi aliyeamka.
“Abee mama.”
Mama Mage aliingia chumbani bila kusema kitu kisha alirudisha mlango na kumuuliza kwa sauti ya chini.
“Sofi.”
“Abee mama.”
“Eti nilipotoka, Mage alitoka?”
“Hapana hajatoka,” Sofi alikataa huku akitikisa kichwa.
“Colin alikuja?”
“Hapana.”
“Nani alikuja.”
“Mmh! Da’ Brenda.”
“Brenda si alikuja mchana na kuondoka na Mage?”
“Hata usiku alikuja na kwenda chumbani kwa dada Mage kisha walitoka nje baadaye nilimuona dada Mage akirudi peke yake huku ameshikilia kitambaa mkononi kama anafuta machozi lakini sikumtilia maanani.”
“Mmh! Sasa nimeelewa,” mama Mage alisema huku akishika mikono kiunoni.
“Kuna nini mama?” Sofi alishtushwa na kauli ya mama Colin.
“Kawaida, ila nimeelewa,” alisema huku akitoka chumbani kwa Sofi na kurudi chumbani kwake.
Alipoingia chumbani alichukua simu na kumpigia Brenda ili amwambie alimpeleka wapi mwanaye mpaka kugeuka ghafla na kumtia gharama na fedheha kubwa. Baada ya kupiga simu ya Brenda ulipokelewa upande wa pili.
“Haloo mama.”
“Brenda za saizi?”
“Nzuri mama.”
“Eti Brenda kumetokea nini mama?”
“Kuhusu nini?”
“Ulimpekeka wapi Mage?”
“Sijampeleka popote nilitoka naye nje mara moja akarudi ndani kujiandaa kwenda kwa shemeji Colin.”
“Unajua wewe ndiye umevunja ndoa ya Mage?”
“Kivipi mama?” Brenda alishtuka.
“Umemwambia nini Mage mpaka akakataa kuolewa, gharama za harusi utazilipa wewe?”
“Mama kwa nini unasema hivyo?” Brenda alishtuka.
“Haiwezekani kuja wewe ghafla na Mage kubadili uamuzi wa kuolewa.”
“Mamaa! Hebu subiri,” Brenda alikata simu na kumpigia Mage.
Baada ya kuita kwa muda simu ilipokelewa.
“Haloo Brenda afadhali umenipigia.”
“Mage kuna nini?”
“Nimevunja uchumba na Colin.”
“Mungu wangu! Kwa nini tena?”
“Nimepata tiba ya moyo wangu.”
“Mage unajua lawama zote nabebeshwa mimi?”
“Brenda walaa hilo halikuhusu, kila kitu kitaeleweka, nitazungumza na mama muda si mrefu.”
“Mage ndugu yangu naomba usivunje ndoa yako utaniweka mahari pabaya,” Brenda alimbembeleza Mage.
“Nitaolewaje na mtu nisiyempenda?”
“Mage leo yamekuwa hayo? Si ni wewe ndiye ulinihakikishia Colin ndiye tiba ya moyo wako?”
“Hakuwa tiba bali dawa ya kupunguza maumivu lakini Hans ndiye tiba kamili, kama alijitoa kwa ajili yangu nami sina budi kujitoa kwa ajili yake.”
“Colin anajua?”
“Hajajua ila sitaki mtu yeyote amwambie nitamwambia mimi mwenyewe nina imani tutaelewana tu.”
“Mmh! Mbona najuta kiherehere cha kumleta Hans!” Brenda alijua yeye ndiye chanzo cha yote yaliyotokea.
Alijiuliza Hans alimweleza Mage kitu gani kilichomfanya abadili ghafla uamuzi wa kuolewa. Aliamua kumpigia simu Hans kutaka kujua aliwambia nini Mage mpaka kuamua kuvunja uchumba wakati kila kitu kilikuwa kipo katika hatia za mwisho. Lakini simu ya Hans haikuwa hewani, alijikuta akijiuliza atamwambia nini mama Mage mpaka amwelewe. Usiku ulikuwa mrefu kwa Brenda na kujuta kwa nini alimkubalia Hans kwenda kuonana na Mage.
***
Siku ya pili Mage aliamka asubuhi na kuoga na kujipamba kisha alitoka, alimkuta mama yake amekaa sebuleni ameshika tama.
“Mama vipi mbona hivyo?” alimuuliza huku akijilazimisha kujenga tabasamu.
“He! Safari ya wapi?”
“Naenda kwa Colin mama.”
“Kweli?” mama yake alishtuka.
“Ndiyo mama.”
“Haya wasalimie.”
“Sawa mama, ila sitakuwa hewani kwa siku mbili.”
“Kwa nini?”
“Utajua nikirudi.”
“Kwani mnakwenda wapi?”
“Itajua tu mama.”
“Haya mwanangu safari njema.”
“Asante mama.”
Mage kabla ya kutoka alimbusu mama yake na kuelekea nje na kumfanya mama yake kumsindikize kwa macho kisha alinyanyua mikono juu kumshukuru Mungu kwa kuweza kumbadili msimamo wake. Alijiuliza kama angesimamia msimamo wake kwake ingekuwa aibu na fedhea ya kuvunjika harusi aliyoiandaa kwa nguvu kubwa.
Ilikuwa toka aamke alikuwa hajaoga zaidi ya kukaa sebuleni kutafuta njia ya kuinusuru ndoa ya mwanaye ambayo aliamini ni muujiza pekee ndiyo wenye kuiponya kwa kuamini nguvu za kibinaadamu zisikingeweza. Alinyanyuka na kwenda kuoga ili apate kifungua kinywa.
Mage alikwenda kuchukua gari aina ya Prado nyeupe na kutoka kuelekea nyumbani kwa kina Colin. Aliendesha gari taratibu tofauti na siku zote aliendesha kwa fujo. Alirudisha kukumbuka ya muda mfupi ya picha ya mama yake aliyokuwa amekaa ameshika tama kuonesha kabisa uamuzi aliochukua umemchanganya sana na kumnyima raha.
Alipeleka macho yake kwenye simu yake iliyokuwa pembeni yake na kuichukua alitafuta namba ya Hans na kumpigia. Iliita kidogo na kupokelewa.
“Haloo ma adorable.”
“Vipi umeamka salama?” alimuuliza kwa sauti iliyopooza.
“Mmh! Naweza kusema nimezaliwa upya nimelala usingizi mtamu nilioukosa muda mrefu.”
“Nashukuru kama ni hivyo.”
“Mmh! Niambie moyo wangu?”
“Hans nilitaka kukujulisha kuwa sitakuwa hewani kwa siku mbili ila ya tatu nitarudi kama kawaida.”
“Kuna nini?”
“Utajua baadaye.”
“Upo wapi?”
“Nimetoka mara moja.”
“Sawa nimekuelewa mpenzi.”
“Basi nikutakie siku njema yenye furaha.”
“Na kwako pia.”
Mage alikata simu na kumpigia shoga yake Brenda, haikuchukua muda ilipokelewa upande wa pili.
“Vipi shoga?”
“Poa, za asubuhi?”
“Nzuri tu.”
“Nilitaka kukujulisha sitakuwa hewani kwa siku mbili.”
“Kwa nini shoga halafu mbona leo kama hujachangamka?”
“Aah! Nipo katika kipindi kigumu lakini nitakivuka tu japokuwa najua jasho la damu lazima litoke.”
“Bado unamsimamo uleule?”
“Utajua baada ya siku mbili.”
“Sasa upo wapi?”
“Nakwenda kwa Colin.”
“Loh! Afadhali shoga maana mimi mwenyewe nilikuwa sina amani moyoni mwangu.”
“Basi ndiyo hivyo tutawasiliana kesho kutwa.”
“Na kesho?”
“Sitakuwa hewani kwa siku mbili.”
“Mmh! Umeamua, safari njema msalimie sana shemu Colin mwambie nimemmisi.”
“Salamu zimefika.”
Baada ya Mage kukata simu shoga yake Brenda alitipa simu kwenye kochi na kushika kifua na kusema:
“Ooh! Afadhali Mage kabadili uamuzi sijui kama mama yake angenielewa.”
Mage baada ya kumaliza kuzungumza na Brenda aliweka simu pembeni na kuiweka mikono yote juu ya usukani na kukanyaka mafuta kuelekea nyumbani kwao Colin. Macho yake yalitulia kutazama mbele huku machozi yakijaa taratibu katika macho yake. Alijikuta akisema kwa sauti kama anazungumza na mtu.
“Mapenzi haya! Kwa nini Mungu uliumba mapenzi kwa nini yakuwa kila siku yanachukua furaha yangu badala ya kunifariji?”
Alichukua kitambaa pembeni yake alifuta machozi na kuendelea na safari. Alisimamisha gari mbele ya geti la nyumba ya kina Colin, geti lilifunguliwa na kuingia ndani. Aliliweka kwenye maegesho kabla ya kuteremka alivaa miwani ya jua ili kuficha macho yake na kuteremka
ITAENDELEA

WAKILI WA MOYO SEHEMU: 13

$
0
0

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
ILIPOISHIA:
Alichukua kitambaa pembeni yake alifuta machozi na kuendelea na safari. Alisimamisha gari mbele ya geti la nyumba ya kina Colin, geti lilifunguliwa na kuingia ndani. Aliliweka kwenye maegesho kabla ya kuteremka alivaa miwani ya jua ili kuficha macho yake na kuteremka.
SASA ENDELEA...
Wa kwanza kuonana naye alikuwa mama Colin ambaye alimkimbilia na kumpokea Mage.
“Wawaooo mkwe wangu.”
“Waawoo mama, Shikamoo.”
“Marahaba.”
“ Colin yupo wapi?”
“Yupo chumbani kwake, aliniambia utakuja.”
“Ndiyo mama.”
“Vipi unaendeleaje?”
“Namshukuru Mungu nipo sawa.”
“Haya mwanangu kamuone mwenzio maana alikuwa na kimuhemuhe hasa baada ya kusikia unaumwa.”
“Sawa mama.”
Mage alielekea chumbani kwa Colin, mlango ulikuwa umerudishwa aliusukuma bila hodi na kuingia ndani alimkuta Colin akibadika picha kubwa ya rangi ukutani wakiwa ufukweni wamelaliana chini ya picha ule kulikuwa na maneno ya rangi nyekundu yaliyokuwa yanasomeka, kwa juu yaliandikwa: ASANTE MUNGU KWA KUNIPA MKE MWEMA na chini kuliandikwa MAGRETH NAKUPENDA ZAIDI YA KUPENDA .
Mage aliposoma yale maneno na kuiona ile picha moyo ulimuuma na kuangua kilio cha sauti, Colin alishtuka kusikia sauti ya mchumba wake, alipogeuka alimuona Mage amesimama akiwa ameshika kifua chake. Aliteremka haraka kitandani alipokuwa amepanda kubandika picha ile kubwa na kumfuata alipokuwa amesimama na kumkumbatia kwa kumlazia kifuani.
“Vipi mpenzi kipi kinakuliza?”
“Najua nina mtihani mzito moyoni mwangu lakini Mungu atanipa nguvu na nitashinda.”
“Kuna nini mbona unanitisha?”
“Kawaida tu, Colin naomba ujiandae tuna safari.”
“Ya wapi?”
“Surprise.”
“Waawoo!” Colin alisema huku akimkumbatia Mage.
Kwa vile alikuwa ametoka kuoga alibadili nguo na kumweleza Mage.
“Nipo kamili mpenzi.”
“Chukua na nguo nyepesi za kupumzikia.”
“Tunaenda wapi?”
“Utajua tu.”
Walichukua begi dogo na kuongozana hadi sebuleni, walimkuta mama Colin akimuelekeza jambo msichana wa kazi alipowaona aliacha na kuwageukia.
“Jamani wapendanao safari ya wapi?”
“Tunatoka kidogo,” alijibu Mage.
“Haya mwende salama.”
“Asante mama, ila hatutakuwa hewani kwa siku mbili.”
“Kwa nini?”
“Utajua tu,” Mage alijibu
“Kwa hiyo leo hamrudi?”
“Ndiyo mama tutarudi kesho kutwa.”
“Mmh! Haya wanangu nawatakieni safari njema,” mama Colin aliwakumbatia wote na kuwabusu kisha aliwasindikiza nje hakuondoka mpaka walipotoka nje ya geti ndipo aliporudi ndani.
***
Baada ya gari kuingia barabarani Mage alimgeukia Colin aliyekuwa ametulia na kumwambia.
“Colin zima simu yako.”
“Kwa nini?”
“Sitaki uwasiliane na mtu yeyote zaidi yangu.”
“Sawa mpenzi,” Colin alizima simu yake.
“Zima na yangu.”
Colin alichukua simu ya Mage ni kuizima, safari iliendelea, gari lilielekea barabara ya Kawawa mpaka Mwenge na kukata mtaa wa viwanda mpaka njia panda ya Kawe. Mage hakukunja alinyoosha na kutokea Afrikana alikata kulia kuelekea Tegeta. Colin hakuhoji gari lilivuka Tegeta likaingia Boko likavuka Bunju na kuitafuta Bagamoyo
Ndani ya gari muziki laini uliendelea kuunguruma kila mtu akiwa kimya kutokana na mwendo wa kasi aliokuwa akienda nao Mage.
Alisimamisha gari mbele ya hoteli ya Oceanic Bay, baada ya kusimamisha gari alimgeukia Colin aliyekuwa ametulia akiuangalia umahiri wake kuendesha gari.
“Nina imani tuna siku mbili ya kila mmoja kumaliza hamu zake kwa mwenzie.”
“Mage mpenzi siku zote kitamu hakiishi hamu, penzi lako kwangu siwezi kulikinai.”
Mage hakuongeza neno alimshika mkono na kuongozana naye mpaka mapokezi na kukodi chumba kizuri kwa siku tatu.
“Mage si umesema tunarudi kesho kutwa.”
“Tatizo nini hata tukikaa mwaka kuna mtu anatudai?”
“Hakuna.”
Baada ya kupata chumba walikwenda chumbani kwao, chumba kilikuwa kizuri sana.
“Colin unakionaje chumba hiki?”
“Kizuri sana, unaonaje fungate yetu tuje tuifanye huku.”
“Tutaangalia muda ukifika.”
Baada ya kuoga kwa vile muda ulikuwa umekwenda walivaa nguo nyepesi na kwenda hotelini kupata chakula cha mchana. Kisha walihamia ufukweni kupata upepo wa bahari, muda mwingi Colin alikuwa mtu mwenye furaha kuwa karibu na mpenzi wake mchumba wake mkewe mtalajiwa.
Lakini Mage alionekana kulazimisha furaha kutokana na siri nzito iliyokuwemo moyoni mwake. Baada ya kutosheka na upepo wa bahari walirudi ndani na kujilaza kitandani mkao wa mahaba huku wakiangalia video. Colin muda mwingi alijiuliza kwa nini wamezima simu ilibidi amuulize Mage.
“Mpenzi kwa nini tusiwashe simu hata kwa muda?”
“Colin hizi ni siku zetu ambazo ni muhimu kwetu sitaki kusikia chochote masikioni kwangu zaidi ya sauti yako.”
“Nimekuelewa mpenzi wangu.”
“Colin,” Mage alimwita.
“Naam mpenzi.”
“Hivi mfano uwe nyumbani kwenu mara mama yangu anakupigia siku kukueleza nimefariki utafanyaje?”
“Mage hayo ni maneno gani, umesema tupo kwenye furaha sasa maneno ya kifo yanafuata nini?”
“Najua hapa siyo sehemu yake lakini naomba unijibu.”
“Kwa kweli nitachanganyikiwa naweza hata kufa.”
“Hivi umpendaye akifa kuna sababu ya kuchanganyikiwa ikiwa baada ya mazishi yake kuna wengine wapo pengine zaidi ya yule aliyeondoka?”
“Ni kweli, lakini kinachomtesa mtu ni mazoea si uzuri wa sura wala umbile la mtu.”
“Kwa mfano mi nikisema sikupendi utafanyaje?”
“Nitafanyaje nawe umeamua.”
“Hutaumia?”
“Nitaumia lakini nitafanya nini, lakini naamini mimi na wewe tunapendana hakiwezi kutokea kitu kama hicho.”
Mage alibadili mazungumzo kwa kumshika mkono Colin na kuelekea naye bafu kuoga, waliingia kwenye jakuzi na kuoshana kisha walirudi kitandani kuburudisha mioyo yao. Mage alimpa penzi Colin penzi shatashata ambalo lilimrusha akili naye alijibu mashambulizi kitu kilichomfanya Mage aangue kilio na kumshtua mpenzi wake.
“Vipi mpenzi mbona unalia?”
“Colin sina jinsi lazima iwe.”
“Iwe nini?”
“Utajua tu.”
Mage alimvamia Colin na kuendelea kustarehe bila kuliweka wazi lililikuwa likimliza, alijitahidi kurudi katika hali yake ya kawaida ya uchangamfu na kumfanya Colin asahau kitendawili chake.
Walikaa kwenye hoteli ile kwa siku mbili huku wakiongozana kama kumbikumbi huku kila mmoja alijua watu wale wanapenda mapenzi ya dhati. Siku iliyofuata majira ya mchana baada ya kupata chakula walipumzika kwa muda kabla ya kurudi mjini. Mage akiwa amejilaza pembeni ya Colin alijinyanyua na kumgeukia mpenzi wake na kumwita.
“Colin.”
“Naam mpenzi.”
“Hivi unajua kwa nini toka juzi sijakuita mpenzi?”
“Sijajua.”
Mage alitulia kwa muda akimtazama Colin usoni mara machozi yalianza kumtoka, Colin alizidi kumshangaa mpenzi wake kwani toka wamefika Bagamoyo ameshindwa kumwelewa.
“Colin, “ alimwita tena.”
“Naam.”
“Najua unanipenda.”
“Sana.”
“Najua kabisa nitakachokueleza kitakushtua na kukumiza moyo wako sawa na kuupasua bila ganzi kwa kisu butu. Lakini ukweli utabakia palepale sina jinsi, nina imani penzi la kweli huwa alitengenezwi na mtu bali mhusika mwenyewe.”
“Ni kweli kabisa.”
“Unajua penzi letu halikuwa la sisi kupendana bali kutengenezwa na wazazi wetu?”
“Najua lakini tulipoonana kila mtu alimpenda mwenzake.”
“Unajua hiyari yashinda utumwa?”
“Najua.”
“Nina imani nilikueleza jinsi mapenzi yalivyoniumiza.”
“Ndiyo.”
“Na aliyesababisha nilikueleza.”
“Ndiyo.”
“Basi napenda kukueleza hili ambalo moyo wangu unavuja damu kwa maumivu kwa vile sikupenda liwe kwa vile hiyari yashindwa utumwa, lazima niseme ukweli wa moyo wangu kuwa Colin nilikupenda lakini Hans nilimpenda zaidi. Hans baada ya kufiwa na mkewe amerudi kwangu na yupo tayari kutimiza ndoto yetu tuliiweka muda mrefu,” Mage alimeza mate huku akiendelea kutokwa machozi kisha aliendelea kuzungumza kwa sauti ya chini yenye mchanganyiko na kilio.
“Najua kauli yangu itakumiza lakini ndiyo ukweli wenyewe, Colin nimeamua kwa hiyari na mapenzi yangu nikiwa na akili timamu kuuvunja uchumba wetu kwa hiyo harusi yetu haitakuwepo tena, Penzi tamu tulilopeana ndilo la mwisho tukitoka hapa kila mtu ashike hamsini zake.”
“Mage,” Colin alimwita kwa sauti ya chini.
“Abee.”
“Unasema kweli au unatania?”
“Nasema kweli,” Mage alijibu huku akikaza macho.
“Hapana acha utani Mage unaweza kuniua kwa presha.”
“Huwezi Colin, wewe ni mwanaume umeubwa kukabiliana na matatizo, kumbuka amenikuta tayari nimeishaanza uhusiano na mtu ambaye ndiye aliyenionjesha dunia ya mapenzi na aliniahidi kunioa. Toka niachane naye sikuwahi kuwa na mwanaume mwingine zaidi yako kilichotokea ni kutoelewana lakini sasa hivi tumeelewana na mipango yetu lazima itimie.”
“Mage japo Hans ndiye alikuonjesha dunia ya mahaba lakini alikutenda, Mage nimekukosea nini mpaka uchukue uamuzi mzito na wa kikatili kama huo?” Colin aliuliza huku machozi yakimtoka.
“Hujanikosea kitu, hata mimi nilikupenda sana, lakini siwezi kuishi na wewe kwa kujilazimisha au kukufanya kama bodi lakini injini awe Hans. Colin, Hans nampenda sana aliniudhi na kuumiza moyo wangu lakini siku aliponiomba msamaha moyo wangu aliyeyuka kama bonge la mafuta kwenye kikaango cha moto. Siwezi kuwa nawe kimwili wakati mawazo yangu yote yapo kwa mwanaume mwingine.
“Narudia naomba ukubaliane na uamuzi wangu wa kuvunja uchumba tukiwa na mioyo safi, kuachana kwetu kusijenge uadui tuendelee kuwa marafiki kwenye harusi yangu uje ya kwako nije.”
“Mage uamuzi uliochukua ni kuupasua moyo wangu bila ganzi, naomba urudishe moyo nyuma mpenzi wangu, bora ungeninyang'anya kila kitu katika mwili wangu na kuniachia moyo wako ni muhimu kuliko chochote duniani japo nipo nawe kwa muda mfupi lakini nimekuzoea sana.”
“Siwezi kuishi mapenzi ya kuigiza niache nimpende aliyechaguliwa na moyo wangu.”
"Mage siwezi kukubali kirahisi namna hiyo nasema sikubali, lolote na liwe nasema huondoki kama sio nitamwaga damu ya mtu," Colin alisema huku akisimama.
"Colin mapenzi si lazima usisababishe nikakasilika na kutoa maamuzi yatakayokuumiza mara mbili."
"Nasema sikubali...toa uamuzi wowote kumbuka nimekutoa kwenye mateso ya kutendwa , leo nikuache uondoke hivihivi sikubali," Colin alikuwa mkali.
"Colin nasema hivi kila usemalo ni kweli tupu na una haki yoyote ya kufanya lakini kumbuka penzi alilazimishwi nina imani umenielewa kuwa mstaarabu tuachane kwa usalama."
Mage alinyanyuka na kumsogelea Colin aliyekuwa ameinama akilia na kumpigapiga mgongoni.
"Sweet naomba usilie mwanaume kaumbwa kukabiliana na matatizo hili ni moja wapo.”
Colin alinyanyuka kama mbogo na kumsukuma Mage aliyeanguka chini huku akibwata.
"Muongo mkubwa mnafiki wewe unanipaka mafuta kwa mgongo wa chupa eti sweet!"
"Huwezi amini Colin nakupenda sana japo Hans nampenda zaidi, nipo yatari kulipa gharama zote za maandalizi ya harusi yetu, pia hata kulipa gharama zozote ili kuhakikisha nawe unakuwa na mke atakayeziba pengo langu."
Mage pamoja na kusukumwa hakukasirika akiamka pale chini alipoanguka Colin hakumjibu neno lolote zaidi ya kuinama huku akilia. Mage alimshika mkono na kunyanyua, alimtazama kwa macho yaliyojaa machozi na kusema kwa sauti ya chini.
“Colin nisamehe sana siwezi kuwa mnafiki mapenzi nayajua, nipe ruksa mpenzi wangu. Nilikuja huku ili tupate muda wa kulizumgumza hili, sikutaka tulizungumze juujuu. Nakupenda lakini sitaki nikutese kwa kukunyanyasa kimapenzi kwa vile mapenzi nayajua yanavyoumiza.”
Colin alitulia huku akimtazama Mage aliyekuwa akitia huruma, alijiona mjinga kulazimisha mapenzi. Alikohoa kidogo na kusema:
“Sawa nimekuelewa.”
“Nashukuru.”
“Kuna la zaidi?” Colin alimuuliza Mage.
“Hakuna.”
“Tunaweza kuondoka.”
Walichukua vitu vyao na kuelekea nje kwenye gari ili warudi mjini.
***
Cecy baada ya kutoka twisheni alisimama chini ya mti kuagana na shoga yake huku wakijikumbusha baadhi ya mada walizopewa wakasome nyumbani. Alikuwa amepiga hatua kubwa katika kusoma na kundika hata kuzungumza lugha ya kingereza baada ya kusoma kwa uchungu mkubwa.
Siku zote aliamini kumkosa Colin kulitokana na kukosa elimu, kwake umaskini hakuuona sababu kama ungekuwa na elimu yake ambayo hata mama Colin angeiheshimu. Toka aanze kusoma alionekana ndiye mwanafunzi aliyetaka kujua lugha kuisoma kuiandika na kuizungumza.
Japokuwa hakukijua sana lakini aliweza kumsikia mtu na kumwelewa hata kumjibu mawili matatu. Ile ilimpa kiburi cha kuzungumza muda wote hata alipokosea hakujisikia vibaya kwa vile alielekezwa. Baada ya kujadiliana na shoga yake alisogea mbele kuelekea njia ya kwao japo palikuwa mbali kidogo lakini hakujali umbali ule kutembea kwa miguu kwa vile alikuwa akitafuta kitu.
Siku zote aliingia darasa la mchana kwa vile asubuhi alikuwa akienda kwenye biashara zake. Ada ya mwanzo alitumia fedha aliyoachiwa na Colin siku aliyompeleka kwao na kuwaacha kwenye mataa kwa ahadi tamu ya kuyabadili maisha yao. Alikumbatia daftari lake na kutembea taratibu kukifuata kichochoro cha kuingilia njia ya mkato. Aliangalia saa yake ilimuonesha ni saa kumi na moja na nusu jioni.
Alishtushwa na sauti ya gari aina ya Prado jeupe new model lililosimama nyuma yake. Alipogeuka aliona msichana akiteremka kwenye gari huku akibwata kwa sauti kuonesha anazozana na mtu ndani ya gari. Alipomwangalia aligundua ni Mage mwanamke aliyezima ndoto zake za kuwa mke wa Colin. Alisimama nyuma ya mti kumwangalia, alimuona akisema kwa sauti:
“Wewe mtu gani unayelazimisha mapenzi nimekueleza ninaye ninayempenda hutaki kunielewa. Naomba uteremke kwenye gari langu, siwezi kutembea na mtu asiyeelewa. Sasa hiyo elimu uliyosoma inakusaidia nini ikiwa hutambui nini maana ya upendo?
Nasema teremka la sivyo nitakuachia gari niondoke zangu.”
Baada ya muda Cecy alishtuka umuona mwanaume aliyekuwa akiambiwa vile ni Colin, baada ya kuteremka kwenye gari kinyonge na alisogea pembeni na kusimama bila kujua nyuma yake yupo Cecy.
Cecy roho ilimuuma kuona mtu ampendaye akidhalilishwa vile, Colin alionekana machozi yakimtoka kitu kilichozidi kuumiza moyo wake na kushangaa watu ambao muda si mrefu walitegemea kufunga ndoa lakini ajabu mwanamke kutoa maneno makali kama yale ya kumdhalilisha mumewe mtalajiwa.
Alitulia aione sinema ile inaishaje kwa kujificha nyuma ya mti ili wasimjue, baada ya muda alisikia sauti ya Colin.
“Mage pamoja na hayo lakini kumbuka tumepanga nini mimi na wewe katika maisha yetu?”
“Hainihusu! Nimekwambia mapenzi siyo lazima, ninaye nimpendaye wewe nikuweke wapi?”
“Mage...Mage.”
“Jina langu, kwa heri.”
Mage alisema huku akielekea kwenye gari ili aondoke na kumuacha Colin aliyekuwa bado amesimama akilia. Kitendo kile kilimuumiza sana Cecy bila kujitambua alitoka nyuma ya mti na kwenda kumvamia Mage kwa nyuma na kuzivuta nywele zake na kuanza kumshushia kipigo.
Colin alishtuka kumuona Cecy eneo lile na kujiuliza ametokea wapi, ilibidi amuwahi kumtoa juu ya Mage aliyekuwa akipiga kelele za maumivu.
“Cecy muache.”
“Hawezi kukudhalilisha kiasi hicho kama umalaya wake apeleke mbele,” Cecy alisema huku akitweta kwa hasira akitaka kujitoa mikononi mwa Colin ili akamfunze adabu Mage.
“Colin have you sent this bastard to come and attack me?“ (Colin umemtuma chokoraa huyu aje anipige?) Mage alibadili lugha na kusema huku akisikilizia maumivu.
“No, baby, I’m also suprised as to where she came from.” (Hapana mpenzi hata mimi nashangaa sijui katokea wapi.) Colin alijitetea.
“Colin, what type of a man who forces to be loved, what’s wrong with you? Let her go!” (Colin wewe ni mwanaume gani unang’ang’aniza mapenzi una kasoro gani mwacha aende) Cecy safari hii naye alivunja yai na kufanya Colin abakie mdomo wazi.
“Colin thank you, stay with that bastard whom you sent to beat me.” (Colin asante, baki na huyo chokoraa uliyemtuma kunipiga) Mage alisema huku akielekea kwenye gari.
Colin aliyekuwa amemshika Cecy ili asiendelee kumuadhibu Mage, alimuachia na kumfuata Mage kumuomba msamaha.
“Please Maggie excuse me, do not be so cruel to me.” (Tafadhali Mage rudisha moyo nyuma usinifanyie ukatiri huo.)
Alipopiga hatua ili amfuate Mage kwenye gari, Cecy alimfuata na kumzuia kwenda kuomba msamaha.
“Colin...Colin... why do you cling to her, how good is her; do you love her for her riches or behaviour? (Colin... Colin... unamng’ang’ania ana sifa gani, unampendea utajiri au tabia?)
Colin alijitahidi kujitoa mikononi mwa Cecy lakini alikamatwa madhubuti, wakati huo Mage alikuwa ameingia kwenye gari na kutupa nje begi la Colin na kuondoa gari kwa kasi na kumuacha Colin akilisindikiza kwa macho. Baada ya gari kupotea machoni alitulia huku machozi yakiziba macho.
Cecy roho ilimuuma kuona mtu ampendaye akitokwa machozi kwa ajili ya kulilia penzi lisilokuwepo.
“Colin, mbegu ya penzi humea kwenye moyo wenye rutuba ya mapenzi, kwa nini unalazimisha kupanda mbegu yako kwenye mawe? Kwani nini unakuwa kenge asiyetaka kuelewa. Mshukuru Mungu msichana wa watu amekuwa mkweli mapema,” Cecy alisema kwa sauti ya kilio iliyomshtua Colin na kurudisha macho kwake.
Pamoja na yote yaliyomtokea alishangazwa na ujasiri wa Cecy msichana aliyeonesha kuumizwa na kitendo cha kudhalilishwa na Mage. Kingine na uwezo wa kuzungumza kingereza kwa ufasaha mkubwa pia kuonekana binti mwenye mvuto kutokana na mavazi na muonekano.
“Cecy,” alimwita kwa sauti ya upole.
“Abee.”
“Kwanza samahani.”
“Ya nini Colin?”

WAKILI WA MOYO SEHEMU: 14

$
0
0


MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’

ILIPOISHIA:
Pamoja na yote yaliyomtokea alishangazwa na ujasiri wa Cecy msichana aliyeonesha kuumizwa na kitendo cha kudhalilishwa na Mage. Kingine na uwezo wa kuzungumza kingereza kwa ufasaha mkubwa pia kuonekana binti mwenye mvuto kutokana na mavazi na muonekano.
“Cecy,” alimwita kwa sauti ya upole.
“Abee.”
“Kwanza samahani.”
“Ya nini Colin?”
SASA ENDELEA...
“Najua nimekudhalilisha kwa kitendo changu cha kumlilia Mage.”
“Colin siwezi kukulaumu kwa vile ile ni haki yako japo sijui sababu ya yeye kukudhalilisha kiasi kile ikiwa kila kitu kipo katika hatua za mwisho kilichobaki ni ndoa.”
“Mage amerudiana na bwana yake wa zamani na kuamua kuvunja uchumba wetu.”
“Kama amekueleza ukweli sasa unamng’anganiza wa nini?”
“Cecy ni ghafla sana heri kungekuwa na tatizo, kanifuata nyumbani juzi na kunipeleka Bagamoyo, niliamini ana mapenzi yake ya dhati kwangu lakini baada ya kukaa siku mbili za furaha siku ya tatu alinieleza kitu ambacho kimenichanganya sana.”
“Colin ulikuwa unampenda Mage mapenzi ya dhati au tamaa ya macho?” Cecy alimuuliza akiwa amemkazia macho.
“Mapenzi ya dhati.”
“Muongo! Umempenda kwa shinikizo la mama yako, kama amejitoa kwa hiyari yake huoni hii ni nafasi ya kuipanda mbegu yako sehemu sahihi ambayo utaotesha mti mwenye kivuli na matunda matamu?”
“Cecy kwanza unatoka wapi muda huu?”
“Shule.”
“Hongera.”
“Siwezi kusema asante.”
“Kwa nini?”
“Mpaka ufute machozi yangu.”
Colin alitoa kitambaa mfukoni ili amfute Cecy machozi, lakini alishikwa mkono na kumfanya aulize:
“Vipi Cecy mbona unanishika mkono?”
“Si machozi haya Colin.”
“Machozi gani Cecy?” Colin alishtuka.
“Ya moyoni, nimeumizwa sana pia nimedhalilishwa sana juu ya penzi lako, lakini Mungu si mnafiki leo amekudhihilishia mbele ya macho yangu kuwa mke uliyechaguliwa mara ya pili hakuwa mke sahihi bali lilikuwa penzi la kuingiza. Colin mimi ndiye mkeo uliyechaguliwa na Mungu. Nifute machozi yangu kwa kufunga ndoa na mimi si kwa kitambaa cha mkononi bali cha moyoni,” Cecy alisema kwa sauti iliyojaa hisia kali za mapenzi.
“Cecy nimekuelewa naomba unipe muda.”
“Muda wa nini wakati nafasi yangu imerudi tena nikiishuhudia si kwa kuhadithiwa na mtu.”
“Nimekuelewa, niache kwanza nifike nyumbani kwanza kumbuka toka juzi sipo nyumbani na ninarudi na taarifa hizo sijajua mama atazipokeaje?”
“Mmh! Sawa, ila pole kwa yote yaliyokukuta.”
“Nashukuru.”
“Colin naomba nikusindikize mpaka kwenu,” Cecy aimwambia Colin huku akiuchezea mkono wake.
“Hapana si unamjua mama atapata la kusema.”
”Nimekuelewa mpenzi.”
Colin alitoa hela mfukoni bila kuzihesabu na kumpatia Cecy, alizipokea na kushukuru kwa kupiga magoti kitu kilichomshtua Colin na kuona tofauti yake na Mage. Siku zote Cecy alikuwa msichana mtiifu ambaye mwanzo alikuwa chaguo la mama yake baadaye alimgeuka baada ya kumuona Mage. Waliagana kila mmoja kukodi gari mpaka kwao.
****
Mage baada ya kuachana Colin alijiendesha gari kwa kasi huku moyo ukimuuma kwa kitendo chake cha kikatili alichomfanyia mtu aliyeonesha mapenzi mazito kwake na aliyemkabidhi moyo wake mzimamzima kutokana na kumuamini. Aliyakumbuka maneno yaliyokuwa kwenye picha kubwa chumbani kwa Colin yaliyosema, moja lilisema: ASANTE MUNGU KWA KUNIPA MKE MWEMA na lingine MAGE NAKUPENZA ZAIDI YA KUPENDA.
Mage alijikuta akilia na kufanya machozi kuziba macho, alisimamisha gari pembeni ya kuendelea kulia kilio cha kwikwi. Aliisikia sauti ya Colin ikisema:
““Mage uamuzi uliochukua ni kuupasua moyo wangu bila ganzi, naomba urudishe moyo nyuma, mpenzi wangu bora ungeninyang'anya kila kitu katika mwili wangu na kuniachia moyo wako ni muhimu kuliko chochote duniani japo nipo nawe kwa muda mfupi lakini nimekuzoea sana.”
Sauti ile ilimfanya apaze sauti na kusema:
“Colin nisamehe sana, najua jinsi gani nilivyokuumiza najuayajua mapenzi yanavyo jeruhi moyo wa mtu. Colin nisamehe sina jinsi nilikupenda lakini Hans ni pumzi zangu siwezi kuiacha nafasi adimu aliyonirudishia.”
Mage aliongea kwa sauti kama anazungumza na Colin, alinamia usukani na kuendelea kulia. Uchungu ulimjaa moyoni kila alivyomfikilia Colin jinsi alivyokuwa akimbembeleza na kutokata tamaa ya kukubaliana na ukweli kwamba penzi limekwisha.
Aliamini asingeweza kuendesha gari kwa hali aliyokuwa nayo kwani hata nguvu zilikuwa zimemuisha kwa ajili ya uchungu uliomjaa moyoni. Aliwaza kumpigia Brenda ili aje amchukue. Wazo lile hakukubaliana nalo kwa vile siku ile alitaka kwanza kuonana na Hans ili amweleze kilichojili ndipo aende nyumbani.
Aliamua kumpigia Hans, alichukua simu ili ampigie ilibidi afute machozi kwanza kuziona ‘kiipadi’ .
Alitafuta jina la Hans na kupiga, hakuita mara mbili ilipokewa upande wa pili.
“Haloo.”
“Hans,” Mage aliita.
“Naam Mage vipi mpenzi?”
“Upo wapi?”
“Nipo Masaki.”
“Naomba uje haraka.”
“Nyumbani kwenu?”
“Hapana nipo njiani karibia na njia panda ya Masaki.”
“Mbona kama unalia?”
“Hans njoo kwanza.”
“Haya nakuja.”
“Kodi bodaboda.”
“Sawa.”
Baada ya kukata simu aliitupia kwenye kiti cha pili na kujilaza kwenye kiti baada ya kukiteremsha kwa nyuma ili kumsubiri Hans.
****
Cecy baada ya kuachana na alikwenda hadi nyumbani kwao, baada ya kusalimiana na mama yake aliingia chumbani kwake na kujifungia chumbani kwake. Baada ya kuvua nguo zote alijifunga upande wa kanga na kujilaza chali kitandani na kuweka mikono nyuma ya kichwa na kutazama kwenye dali. Alitulia kwa muda na kuanza kuyakumbuka matukio yalitokea muda mfupi.
Alijikuta akijilaumu kuingilia mambo yasiyo muhusu, kwani ule ulikuwa ugomvi wa wapendao, lakini kwa upande mwingine aliona kufanya vile ni kulipigania penzi lake. Aliamini ndoa ya Mage na Colin haitakupo na ile ndiyo ilikuwa nafasi yake kukipata alichokipoteza.
Alijiuliza kama ndoa ile itavunjika nani atakuwa mke wa Colin, kwake aliona ana nafasi ndogo hasa baada ya mama Colin kumdharau kutokana na umaskini wake lazima angemtafuta mwanamke mwingine kutoka familia yenye uwezo. Bado alitaka kujua sababu ya Mage kuuvunja uchumba ambao ulibakia siku chache kufunga ndoa kanisani
Moyoni alijiapiza kama ndoa ya Colin na Mage itavunjika basi ataipigania nafasi yake kwa nguvu zake zote. Mama yake alishangaa kumuona mwanaye yumo ndani muda mrefu, alipomfuata alikuta umefungwa. Aligonga mlango huku akiita.
“Cecy mbona umeingia ndani mwaka mzima kuna usalama?”
“Ndiyo mama.”
“Hebu toka basi.”
Cecy alitoka nje, mama yake macho yake hakucheza mbali na uso wa mwanaye na kugundua mabadiliko.
“Cecy upo sawa?”
“Ndiyo.”
“Hapana kuna kitu kimekutokea, si kawaida yako kuingia ndani moja kwa moja bila kunitania na kizungu chako cha kuombea maji.”
“Ni kweli mama kuna kitu kimenitoka kumenichanganya sana.”
“Kitu gani?”
Cecy alimweleza mama yake yote yaliyotokea wakati akitoka twisheni, mama yake alishtuka kusikia kampiga mchumba wa Colin.
“Cecy kwa nini unatafuta balaa, unakumbuka mama Colin alituambia nini?”
“Mama mimi sijavunja ndoa yao bali wenyewe mimi kiichoniudhi ni kashfa aliyokuwa akiitoa yule mwanamke.”
“Colin kasemaje?”
“Amesema amechanganyikiwa kwani maamuzi yalikuwa ya ghafla ila alisema atanitafuta.”
“Mmh! Sawa, basi kaoge ule.”
“Sawa mama.”
Cecy alipitia ndoo ya maji na kuelekea bafuni kuoga na kumuacha mama yake akimtazama mwanaye na kutikisa kichwa aliamini vita ya mapenzi ni nzito kuliko ya kumsaka gaidi mapangoni.
***
Colin baada ya kuachana na Cecy na kukodi gari lililompeleka hadi kwao, aliteremkia nje ya geti na kuingia ndani kwa miguu. Mama yake alikuwa wa kwanza kumuona akiingia sebuleni, lakini uso wa mwanaye haukuonesha furaha kitu kilichomshtua na kuhoji.
“Colin, baba vipi kwema utokapo?”
“Kwema si kwema.”
“Una maanisha nini?”
“Nitakwambia naomba kwa sasa niache nikapumzike kwanza.”
“Kuna nini? Mbona unanitisha?”
“Mama naomba uniache kwanza.”
“Mage yupo wapi?”
“Sijui.”
“Colin ni majibu gani hayo?” mama alishtuka majibu ya mwanaye.
“Mama yangu nipo chini ya miguu yako naomba uniache kwanza.”
“Mmh! Sawa.”
Mama Colin aliachana na mwanaye aliyeelekea chumbani kwake, moyo wake ulimsukasuka alichukua simu kumpigia mama Mage kutaka kujua kuna nini kimetokea. Baadaya simu kuita kwa muda ilipokelewa upande wa pili.
“Haloo dada.”
“Za saa hizi?”
“Nzuri, lete habari.”
“Mage yupo hapo?”
“Mmh! Toka atoke juzi sijamuona kwani vipi?”
“Nimemuona Colin akirudi peke yake huku uso wake ukionesha kuna kitu si cha kawaida, nimemuuliza kuhusu Mage amesema hajui.”
“Mmh! Lazima watakuwa wametibuana, sasa Mage yupo wapi?”
“Hapo ndipo pananichanganya, nilipotaka kumchimba sana Colin ameniomba nimuache kwanza apumzike.”
“Mmh! Lazima watakuwa wametibuana tu.”
“Kwa hiyo hajafika?”
“Bado, akifika atanieleza tatizo, nitakujuza kila kitu.”
“Sawa dada.”
Mama Colin alikata simu, alipogeuka alimuona mwanaye amebeba vitu akitoka navyo nje, hakujua amebeba nini. Alisubiri muda ili akaone mwanaye amechukua nini na anapeleka wapi. Colin baada ya kuachana na mama yake alikwenda chumbani kwake, baada ya kufungua mlango wa chumba chake macho yake yalikutana na picha kubwa aliyoibandika muda mfupi kabla ya kuelekea Bagamoyo akiwa na Mage katika pozi zito la mahaba.
Picha kubwa aliyoibandika ukutani ambayo mwanzo aliiona ni sehemu ya kuongeza furaha ya moyo wake. Lakini siku ile ilikuwa chukizo la moyo wake, alipanda kitandani bila kuvua viatu na kuibandua na kuitupa chini huku akiitemea mate. Alifungua kabati na kutoka picha zote alizopiga na baadhi ya nguo za Mage alizikusanya na kutoka nazo nje kwenda kujichoma moto.
Alipofika nje alizikusanya sehemu moja na kuzimwagia mafuta ya taa na kuzitia moto, mama yake alitokea kwa nyuma yake. Alipotupa jicho aliona moja ya picha ya Mage ikiteketea na moto pia nguo za mkwewe mtarajiwa.
“Colin! Unafanya nini?” alimuuliza kwa sauti mwanaye.
Colin hakujibu kitu aligeuka kumtazama mama yake aliyekuwa ameshangaa mkono kiunoni.
“Colin mwanangu una nini mbona unachoma picha na nguo za mchumba wako?”
“Mama uliponichagulia mchumba ulifanya uchunguzi kwanza.”
“Wa nini?”
“Kama ana mpenzi anayempenda kuliko mimi.”
“Mage hakuna na mpenzi, kwani nini unaniuliza hivyo?”
“Ndiyo maana nikakuuliza ulifanya uchunguzi kabla ya kumchagua kuwa mkweo?”
“Ndiyo, kwani vipi?”
“Tulitaka kujenga nyumba kwenye kiwanja cha watu.”
“Una maana gani?”
“Mage ni mchumba wa mtu.”
“Una maanisha nini kusema hivyo?” mama Colin alishtuka kusikia habari ile.
Colin alimweleza yote yaliyojili Bagamoyo walipokaa siku tatu mpaka kumteremsha njiani na kumtupia mfuko wake. Lakini hakumweleza jinsi Cecy alivyo ingilia ugomvi ule na kipondo alichompa Mage.
Mama yake alibakia macho yamemtoka kama kaona meli ikitembea barabarani. Alishusha pumzi nzito na kubakia akimuangalia mwanaye asipate la kusema.
***
Hans alifika na bodaboda sehemu aliloelekezwa na Mage, aliliona gari limepaki pembeni. Alimuomba dereva wa bodaboda amshushe, aliteremka na kumlipa hela yake na kuchepua mwendo hadi kwenye gari alilolikuta limefungwa vioo vyote. Aligonga kwenye kioo na kumfanya Mage anyanyue kichwa kuangalia, alimuona Hans alifungua mlango.
Hans alishangaa kumkuta Mage macho yamemuiva kwa kulia.
“Vipi mpenzi?” alishtuka kuiona hali ile.
“Hans mpenzi umekuja?”
“Ndiyo mpenzi wangu mbona unalia?”
“Hans nimekaza moyo ili niumeze mfupa nisikupoteze mpenzi wangu.”
“Una maanisha nini?”
“Hii si sehemu sahihi ya mazungumzo, endesha gari tuondoke,” Mage alisema huku akihama kwenye usukani kumpisha Hans.
“Mmh! Safari ya wapi, nyumbani?” alimuuliza huku akimtazama usoni.
“Nyumbani siendi sasa hivi mpaka tumalizane na wewe.”
“Sasa twende wapi?”
“Sea Cliff hoteli.”
“Hakuna tatizo.”
Hans aligeuza gari na kuelekea Masaki, muda wote Mage alikuwa amejilaza kwenye siti baada ya kuilaza kwa nyuma. Hans alisimamisha gari kwenye maegesho ya Sea Cliff hoteli.
ITAENDELEA

HADITHI: WAKILI WA MOYO SEHEMU: 15

$
0
0

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’

ILIPOISHIA:
“Hakuna tatizo.”
Hans aligeuza gari na kuelekea Masaki, muda wote Mage alikuwa amejilaza kwenye siti baada ya kuilaza kwa nyuma. Hans alisimamisha gari kwenye maegesho ya Sea Cliff hoteli.
SASA ENDELEA...
“Bebi tumefika,” alimshtua Mage aliyekuwa amefumba macho.
“Kachukua chumba kabisa,” Mage alijibu bila kufumbua macho.
“Sawa.”
Hans aliteremka na kwenda kulipia chumba kisha alirudi kumweleza Mage.
“Tayari.”
Aliteremka na kufunga gari lao kisha waliongozana hadi ndani ya chumba walichokikodi. Mage alipofika alijilaza kitandani macho alitazama juu mikono alilalia kwa nyuma. Pembeni ya macho yake michirizi ya machozi iliendelea kuteremka na kulowesha shuka.
“Vipi bebi?” Hans alizidi alishtuka.
“Hans sijui nikueleze nini uelewe najua jamii itanitenga kwa ajili ya uamuzi wangu wa kuvunja uchumba, wapo watakao niona sina akili lakini anayejua mapenzi ataniunga mkono. Nimekubali kubeba lawama zote za wanadamu lakini niufurahishe moyo wako. Sijui nitakaporudi nyumbani mama atanipokeaje naweza kutengwa na familia kwa uamuzi wangu huu.”
“Kwani huyo jamaa umeisha mwambia ukweli?”
“Siku tatu zilizokuwa naye Bagamoyo nilizitenga mahususi kwa ajili ya kumweleza taratibu kuuvunja uchumba wetu rasmi. Ningeweza kumwambia tu, lakini naheshimu mapenzi yake kwangu.”
“Amepokeaje?”
“Ilikuwa kazi kwelikweli jamaa alichachamaa mpaka kutishia kutoa mtu roho, siyo siri alikuwa amekufa kaoza nina wasiwasi akawa mwendawazimu au kuchukua uamuzi wa kujinyonga.”
“Mi nafikiri mshale umerudi porini haujapotea, Mage nakuapia kwa Mungu kutoujutia uamuzi wako. Kama ulivyojitoa kwangu nami nitazishia mapenzi mara mia ya mwanzo. Nina amani ulikubali kuolewa kwa shinikizo, lakini moyo wako bado ulikuwa kwangu nami unaamini hivyo.
“Hii ni nafasi nyingine ya kuidhihilishia dunia kuwa mimi na wewe tulizaliwa ili tuwe mwili mmoja. Mage nashukuru kuuponya moyo wangu uliokuwa na maumivu ya muda mrefu kulishwa nisicho kitaka, lakini kwa sasa nakula ninachokitaka.”
“Hans naamini unanipenda zaidi ya kunipenda ndiyo sababu ya mimi kukubali kurudi kwako, wasiwasi wangu mkubwa ni familia yako. Hans nitakufa na mtu kila atakayetia mkono katika penzi letu sijali ni nani,” Mage alitoa mkwala mzito.
“Mage nitalipigania penzi letu nakuahidi hakuna atakayeingilia penzi letu, nakuahidi mapenzi ya peponi. Nitayafuta machozi yako kwa kitambaa cha upendo,” Hans alisema huku akimfuta machozi kwa kiganja cha mkono.
“Hans nimejilipua ukinitenda umenimaliza,” Mage alisema kwa sauti ya kilio huku akijitupia kifuani kwa Hans.
“Nakuhakikishi na harusi yetu haitachukua muda mrefu.”
“Kweli Hans?” alimuuliza huku akiyatoa macho yake yaliyojaa machozi kumtazama Hans.
“Toka uliponitamkia matumaini ya kurudi kwangu nilikwenda mbali zaidi ya maandalizi ya ndoa yetu. Nilikuwa nasubiri kauli yako ili nikueleze hili.”
“Wazazi wako je?”
“Niliwaeleza wakasema hawawezi kunichagulia tena.”
“Huoni kama ule wasiwasi wao juu ya kifo cha mkeo utazidi na mimi kuonekana ndiye muhusika?” Mage aliingiwa wasiwasi.
“Nilijua hilo litatokea lakini nimewaeleza mimi ndiye niliyekufuata japokuwa wewe haukuwa tayari kurudiana na mimi hasa baada ya kukutosa kukuoa pia familia yangu kukuingiza kwenye matatizo. Nashukuru walinielewa.”
“Mmh! Sawa, kwako umemaliza sijui kwangu mama atapokeaje.”
“Atakuelewa kwa vile anajua penzi letu lilivyokuwa naamini moyo wake utafurahi kumpata mkwe sahihi.”
“Mmh! Tutaona.”
Walikwenda kuoga kisha walipata vinywaji na kufurahisha nafsi zao walipanga kuondoka pale saa sita usiku.
****
Muda ulizidi kukatika bila Mage kuonekana kitu kilichozidi kumtia wasiwasi mama yake na kujiuliza atakuwa amepitia wapi. Mawazo yake yalimpeleka labda yupo kwa shoga yake Brenda. Lakini aliamini kama aliondoka nyumbani siku tatu zilizopita alitakiwa afike nyumbani kwanza ndipo aende kwa shoga yake.
Alipiga simu ya Mage haikuwa hewani kitu kilichofanya azidi kuingiwa wasiwasi, aliamua kumpigia simu Brenda. Simu iliita kwa muda mrefu bila kupokelewa na kushindwa kuelewa kuna nini ikiwa simu ya Mage haipatikani na simu ya shoga yake haipokelewi.
Akiwa katika ya mawazo simu iliita aliichukua haraka na kupokea ilikuwa inatoka kwa Brenda.
“Haloo mama.”
“Brenda, kwema?’
“Kwema mama, samahani simu ilikuwa mbali kidogo nimekuta umepiga, unasemaje mama?”
“Mage amefika huko?”
“Sijamuona, kwani amerudi?”
“Nasikia amerudi toka saa kumi na moja lakini mpaka sasa sijamuona na simu yake haipatikani.”
“Umemuulizia shemeji Colin si ndiye aliyekuwa naye?”
“Mmh! Ipo kazi.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Basi ngoja nimpigie Colin alinieleze Mage kaenda wapi.”
“Itakuwa vizuri.”
Baada ya kukata simu, alimpigia Colin nayo haikuwa hewani kitu kilichozidi kumweka njia panda asijue nini kinaendelea aliamua kumpigia mama Colin simu iliyopokelewa.
“Haloo shoga kuna habari gani maana mimi mwenyewe moyo hauna raha, toka Colin kafika kajifungua ndani kuna habari gani huko?” mama Colin alipokea na kuanza kumwaga maneno.
“Dada mbona umezungumza mengi, huku mpaka muda huu Mage sijamuona wala simu yake haipatikani. Nimemuulizia kwa shoga yake hajafika, simu ya Colin haipatikani kuna nini katikati mbona sielewi, Colin yupo?”
“Ndiyo.”
“Naomba kuzungumza naye.”
“Sawa.”
Mama Colin alimpelekea simu Colin aliyekuwa amejilaza akitafakari kilichotokea. Mpaka muda ule alikuwa akiona kama ndoto yenye ukweli. Alijiuliza maandalizi yote na matangazo ya sherehe ya kukata na shoka atafanya nini atawaeleza nini jamaa zake aliojitolea kusimamia sherehe ya harusi yao kwa gharama zao.
Rafiki zake wa nje ya nchi aliosoma nao Ulaya nao alijiuliza atawaambia nini ikiwa tayari walikuwa wameshona suti kwa ajili ya sherehe ile na walikuwa tayari kuja nchini ikiwa pamoja na kukodi vyumba kwenye hoteli za nyota tano na malipo yalikuwa tayari.
Kila alivyofikiria alikosa jibu, alitamani hata kumshawishi Mage akubali amuoe hata kwa mkataba wa mwezi mmoja ili jamaa zake wakiondoka waachane lakini wakiwa wamedhudhulia sherehe yake iliyopangwa kutekekeza mamilioni ya fedha. Pamoja na kuujua msimamo wa Mage bado aliamini kupitia wazazi wao anaweza kukubaliana nao.
Lakini wazo la kuendelea kumbembeleza aliona kama kujidhalilisha, alikumbuka kitu. Alinyanyuka kitandani na kwenda kwenye kabati, kabla hajashika mlango uligongwa alipaza sauti ukuuliza.
“Nani?”
“Mimi,” ilikuwa sauti ya mama yake.
“Naam mama, unasemaje?”
”Hebu fungua mlango.”
Alirudi hadi mlangoni na kufungua mlango, alionekana amechoka sana kitu kilichozidi kumuumiza mama yake.
“Mama Mage anataka kuzungumza na wewe.”
“Kuhusu nini?”
“Inasemekana toka ulipoachana naye hajarudi nyumbani na simu yake haipatikani, Colin mwanangu usiwe umemuacha wewe mtoto wa watu akaenda kujinyonga?”
“Mama mimi na wewe tunataniana hasa katika jambo zito kama hili? Inaonekana tukiwa ndani ya uchumba Mage alikuwa na mpenzi wake. Ni wazi lilikuwa shinikizo toka kwa mama yake ili nimuoe lakini ukweli umejidhihili maji hayachanganyikani na mafuta.”
“Hebu kwanza zungumza na mama Mage.”
“Mama nitaongea naye nini?”
“Ulichonieleza.”
Colin alichukua simu ya mama yake ambayo ilikuwa wakati huo imekata na kupiga, baada ya muda ilipokelewa upande wa pili.
“Haloo dada.”
“Hapana ni mimi Colin.”
“Ooh! Baba za siku mbili?”
“Nzuri, shikamoo.”
“Marahaba.”
“Naam mama.”
“Eti baba, mwenzio yupo wapi?”
“Sijui,” alijibu kwa mkato.
“Kwa nini unasema hujui wakati mlikuwa wote siku tatu.”
“Mama, nimeachana na Mage baada ya kunifukuza ndani ya gari lake kama mbwa.”
“Wee! Kwa sababu gani?” mama Mage alishtuka.
“Ana mtu ambaye ndiye aliyemuingiza dunia ya mapenzi na kwa kunitamkia kuwa amevunja uchumba wetu. Kumbembeleza kwangu kumekuwa kero kwake na kuamua kuniteremsha njiani kisha kunitupia mzigo wangu huku akinitolea maneno ya dharau kuwa yupo mwanaume wa ndoto yake.”
“Yupo wapi baba, yule mwanaume alimtenda.”
“Basi ameamua kurudi huko.”
“Sasa atakuwa amekwenda wapi?”
“Si kwa mpenzi wake,”Colin alijibu kwa kifupi.
“Lakini baba linazungumzika, mimi ndiye mzazi wake.”
“Ni kweli wewe ndiye mzazi wake lakini moyo wa uamuzi ampende nani unabakia kwa Mage.”
“Basi baba, niachie kazi hiyo.”
“Wala usisumbuke mwachie uamuzi wake, mapenzi hayalazimishwi japo kaniweka katika wakati mgumu maishani mwangu.”
“Baba…baba..naomba usifike huko nimekueleza niachie mimi naomba kuzungumza na mama yako.”
Colin alimpa simu mama yake aliyekuwa amesimama pembeni yake akiwa amepigwa na bumbuwazi kutokana na kauli za mwanaye.
“Haloo dada.”
“Dada kwanza nisamehe sana kama kweli asemayo Colin ni kweli, yaani nilidhania utani kumbe kweli. Dada naomba uniachie suala hilo.”
“Sawa, nikutakie usiku mwema.”
***
Majira ya saa sita usiku Mage aliingia ndani ya sebule ya nyumbani kwao, alishangaa kumkuta mama yake yupo kwenye sofa akiwa amepitiwa usingizi. Alimsogelea na kumbusu shavuni kitu kilichomfanya mama yake ashtuke. Mbele yake alikuwa amesimama mwanaye Mage.
Kabla ya kusema lolote aliangalia saa kubwa ya ukutani iliyomuonesha ni saa saba kasoro usiku. Hakuiamini aliangalia ya mkononi iliyokuwa sawa na ya ukutani, alimwangalia mwanaye kuanzia juu mpaka chini kama ndiyo siku yake ya kwanza kumuona kitu kilichomshtua Mage.
“Vipi mama?”
“Unatoka wapi?” mama yake alimuuliza kwa sauti kali huku akinyanyuka kwenye kochi.
“Kwani vipi?” Mage alijifanya kushangaa.
“Nijibu unatoka wapi muda huu?”
“Niliporudi nilipita kwa shoga yangu.”
“Nani?’
“Debora, humjui.”
“Kufanya nini?”
“Mama mbona maswali mengi?”
“Kwa nini unanitia aibu, Colin umemfanya nini?”
“Kama alivyokuambia kwa vile alichokueleza niliisha kueleza muda mrefu si kigeni kwako.”
“Kwa hiyo umerudiana na Hans?”
“Ndiyo mama ndiye chaguo la moyo wangu.”
“Wewe si ulikuwa unasema humpendi tena na mapenzi yako yote kwa Colin?”
“Mama ningempenda Colin kama Hans asingekuwepo, kama matatizo yangemtokea nimo ndani ya ndoa nisingeweza kutoka. Lakini amerudi kabla ya ndoa sina budi kumpokea, mama Hans nampenda zaidi ya kupenda nipo tayari kunioa bila mahari.”
“Mage mwanangu nitaweka wapi sura yangu?”
“Ukiwaogopa walimwengu huwezi kufanya jambo la kimaendeleo, watasema mwanzo lakini watanyamaza na kusahau.”
“Mage mwanangu naomba ukalale ili kesho tuzungumze vizuri.”
“Sawa mama.”
Mage alikwenda kulala na kumuacha mama yake akiwa bado yupo sebuleni.
***
Mama Colin usiku ulikuwa mkubwa kwake kila alivyojitahidi kulala usingizi ulikataa, aliamini kabisa Mage hana tatizo bali mwanaye ndiye aliyevunja uchumba na kusingizia Mage ana mwanaume mwingine anayempenda. Akili yake ilimpeleka kwa Cecy tu msichana aliyemuona ndiye tatizo kwa vile tokea awali aliona dalili mbaya.
Alipanga kesho asubuhi kwenda kwa kina Mage ili aweze kuzungumza naye na akimwambia Colin ndiye aliyevunja uchumba basi bleki yake ya kwanza kwa Cecy na kukitia moto kibanda chao na kumfanyia kitu kibaya ambacho hata kisahau mpaka kufa kwake.
Asubuhi alikuwa wa kwanza kufika mbele ya nyumba ya kina Mage na kipiga honi mbele ya geti. Baada ya kufunguliwa geti aliliingiza gari ndani na kwenda kupaki kwenye maegesho. Aliteremka na kuelekea ndani ambako ilionesha bado wamelala baada ya kumkuta msichana wa kazi akifanya usafi, alipomuona alimkaribisha:
“Karibu mama.”
“Asante, mama yupo wapi?”
“Bado yupo chumbani kwake.”
“Kamwite.”
Msichana wa kazi alikwenda kumuamsha mama Mage, baada ya muda alitokea na kushtuka kumuona mzazi mwenzie asubuhi ile.
“Karibu dada.”
“Asante, mmeamkaje?”
“Mmh! Tunamshukuru Mungu.”
“Mage yupo?”
“Yupo chumbani kwake.”
“Ndiye kanileta asubuhi yote hii.”
“Ngoja nikamwamshe.”
“Sawa.”
Mama Mage alikwenda chumbani kwa mwanaye na kumuamsha.
“Vipi mama mbona asubuhi sana?”
“Mama Colin anataka kuzungumza na wewe.”
“Ha! Mbona asubuhi sana?” Mage alishtuka.
“Kwani uliyofanya madogo?”
“Mmh! Haya twende nikamuone.”
Walitoka pamoja hadi sebuleni alipokuwa amekaa mama Colin.
“Shikamoo mama,” Mage alimsalimia mama Colin.
“Marahaba mwanangu, samahani kwa kukurupusha asubuhi.”
“Bila samahani mama.”
“Naomba tuzungumze kidogo.”
“Hakuna tatizo.”
“Na mimi niwepo?” mama Mage aliuliza.
“Kwanza naomba tuzungumze wawili kisha tutazungumza wote.”
Mama Mage aliondoka na kuwaacha mtu na mkwewe, baada ya kubaki wawili mama Colin alimuuliza Mage.
“Mage mwanangu, kuna tatizo gani kati yako na mwenzako?”
“Hakuna tatizo lolote.”
“Mbona anasema kuwa eti wewe umevunja ndoa yenu, ni kweli?”
“Ni kweli.”
“Kama ni hivyo sasa mbona unasema hakuna tatizo?”
“Ndiyo mama hakuna tatizo, ila ni kweli alichokisema Colin.”
“Wewe na yeye nani kavunja uchumba wenu?”
“Mimi.”
“Kwa nini?”
“Mama kabla ya kuwa na Colin nilikuwa na mchumba wangu ambaye kipindi hicho akuwa ameoa. Lakini kabla ya ndoa, alipata matatizo ya kufiwa na mkewe na kurudi kwangu. Kwa vile ndiye aliyekuwa chaguo la moyo wangu aliporudi kuniomba niwe naye wala sikuhitaji ushauri nilimkubalia na ndiye nategemea ufunga naye ndoa na si Colin,” Mage alisema kwa kujiamini.
“Mage, hebu kuwa mkweli naomba usinifiche, Colin amekufanya nini kilichopelekea kuchukua uamuzi huo?”
“Kwa haki ya Mungu hajanifanya lolote baya.”
“Hujamfumania na mwanamke?”
“Walaa.”
“Kwa nini unavunja ndoa yako? Mage nakuahidi kukupa chochote ukitakacho ili tu ukubali kufunga ndoa na Colin.”
“Mama naomba kuwa mkweli wa moyo wangu, japokuwa bado mdogo mapenzi nayajua kwa vile yalinijeruhi. Ningeweza kuolewa na Colin jina lakini mapenzi yangu yangekuwa kwa Hans. Lakini siwezi kufanya kitu kama hicho sitaki kumtesa Colin bila sababu.”
“Hans ndiye nani?”
“Mwanaume wa ndoto yangu.”
“Mmh! Nimekuelewa, basi Mage naomba ubadili uamuzi ili uolewe na Colin.”
“Siwezi kuulazimisha moyo wangu, najua nawavunjia heshima, lakini nayaogopa maumivu ya moyo, niliumia sana wakati Hans ameoa. Kurudi kwake kwangu ni kutibu majeraha ya moyo wangu siwezi…siwezi kubadilika kwa vile nampenda sana Hans,” Mage alisema kwa sauti ya hisia kali.
“Mmh!” mama Colin alishusha pumzi ndefu na kusema:
“Nimekuelewa.”
“Una la ziada?” Mage alimuuliza.
“Mpaka hapo sina, nikuache upumzike.”

HADITHI: WAKILI WA MOYO SEHEMU: 16

$
0
0

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’

ILIPOISHIA:
“Mmh!” mama Colin alishusha pumzi ndefu na kusema:
“Nimekuelewa.”
“Una la ziada?” Mage alimuuliza.
“Mpaka hapo sina, nikuache upumzike.”
SASA ENDELEA...
“Sawa mama msalimie Colin, naendelea kumuombea naye apate mke mwenye mapenzi naye ya kweli.”
“Amen.”
Mama Colin alimwita mama Mage amuage, baada ya kuja alimweleza:
“Dada nikukimbie.”
“Jamani, mbona haraka mmeelewana na mwanao?”
“Tumeelewana na nimemuelewa vizuri sana.”
“Basi nikutoe.”
Waliongozana kutoka nje walipofika nje mama Mage alitaka kujua kama mwanaye amebadili uamuzi.
“Vipi amesemaje?”
“Amesimamia msimamo wake, nami naheshimu alichokisema kwa vile amekuwa mkweli. Japo inauma lakini ndiyo ukweli wenyewe.”
“Bado hatujakata tamaa nitazungumza naye.”
“Muache tu, kwa aliyo zungumza hata kwa mtutu wa bunduki habadili uamuzi wake.”
“Mmh! Sawa, lakini Mage ni mtoto bado nina nafasi kama mzazi,” mama Mage alisema kwa sauti ya kukata tamaa.
Waliagana na mama Colini aliingia kwenye gari lake kurudi kwake akipata uhakika wa ndoa ya mwanaye kuvunjika.
***
Siku ya pili Mage alimuamsha mama yake aliyekuwa bado amelala, baada ya kuamka alimuaga.
“Mama nasafiri kidogo.”
“Unakwenda wapi?”
“South.”
“Una maanisha Afrika ya kusini?”
“Ndiyo mama.”
“Na nani?”
“Na mchumba wangu.”
“Nani, Colin?’
“Hapana mama, ya Colin yameishafutika moyoni mwangu itabaki kama historia.”
“Unakwenda na Hans?”
“Mama kuna mwingine? huyo ndiye aliyeshikilia maisha yangu.”
“Mmh! Sawa.”
“Bai mama,” Mage alimsogelea mama yake na kumbusu shavuni.
“Mage mwanangu ndiyo umeamua kunivua nguo mbele za watu?” mama yake bado hakuamini.
“Mama nakuahidi nikitoka South barua ya posa inakuja na ndoa itakuwa ya haraka sana. Najua utasahau yote.”
“Mage mwanangu unamuamini vipi Hans mwanaume alikuacha katika wakati mbaya?”
“Lile lilikuwa shinikizo la wazazi wake si uamuzi wake najua kabisa Hans ananipenda sana hata mimi kama ningeolewa na Colin lilikuwa shinikizo letu.”
“Mage mwanangu nani alikulazimisha, si ulikubali kwa hiyari yako?”
“Nilikubali ili kufunika kombe mwanaharamu apite.”
“Mmh! Sawa, safari njema,” mama alisema kwa sauti ya unyonge ambayo haikumshitua Mage.
Mage alitoka hadi nje na kuchukua gari la nyumbani ambalo alikwenda kuliacha uwanja wa ndege. Aliungana na mpenzi wake kwenda Afrika ya kusini kupumzika kwa wiki moja kabla ya kurudi kwa ajili ya maandalizi ya harusi kabambe.
Wakati Mage na zilipendwa wake wakienda kutuliza mawazo Colin naye aliamini kuendelea kuwepo Tanzania kwa muda ule akili yake haitakuwa sawa.
Alipanga siku inayofuata aende Afrika ya Kusini kwa wiki moja ili arudi na mawazo mapya. Kwa vile ndege ilikuwa ikiondoka saa sita mchana Colin alipanga kuondoka saa nne asubuhi ili awahi saa moja kabla ndege haijaondoka baada ya taratibu zote alijiandaa kwa siku ya pili.
Siku ya pili Colin akiwa amejilaza kitandani alikumbuka kitu na kunyanyuka kwenda kwenye kabati na kutoa picha alizompiga Cecy siku ya birth day yake. Alizichukua na kuziweka juu ya kitanda, katika zile picha aliikuta picha moja ya Mage. Alipitia picha mojamoja, aliona kitu cha ajabu mbele ya macho yake Cecy alikuwa msichana mrembo kuliko Mage na kujiuliza kipi kinachomfanya amng’ng’anie Mage wakati kuna almasi juu ya mchanga.
Alitulia akiitazama picha ya Cecy na Mage, mara simu yake iliita, alipoangalia ilikuwa ya rafiki yake Lukonge.
“Niambie Musoti,” alimwita kwa jina alilokuwa akipenda kumtania kutokana na kufanana na umbile la mchezaji wa timu ya Simba, Donald Musoti raia wa Kenya.
“Mzee vipi?”
“Poa za siku?”
“Nzuri naona namba ya South, lini tena huko?”
“Na wiki sasa.”
“Naona mzee umenikumbuka?”
“Kawaida tu, Colin kuna kitu kinanitatiza sina uhakika nacho?”
“Kitu gani?”
“Ngoja nitume picha kwenye WhatsApp kisha utanipa jibu.”
“Poa tuma.”
Baada ya sekunde chache picha iliingia kwenye simu kupitia WhatsApp, aliifungua na kukutana na picha tofauti za Mage akiwa na mwanaume wakiwa katika mkao wa mahaba mazito. Alituliza macho na kushindwa kuelewa picha ile imepigwa lini na Mage yupo wapi. Baada ya muda Lukonge alipiga simu na kuuliza:
“Umeelewa?”
“Ndiyo, hii picha umetoa wapi?”
“Nimezipiga muda si mrefu, huyu si shemeji Mage?”
“Kwani wewe upo wapi kwa sasa?”
“Nipo Hilton hotel hapa Daban.”
“Musoti ni historia ndefu niache kwa muda nitakupigia.”
“Poa.”
Baada ya Lukonge kukata simu, Colin aliziangalia upya zile picha jinsi Mage alivyojiachia na mwanaume Afrika ya kusini. Akiwa katikati ya lindi la mawazo na kumuangalia Mage ambaye aliamini kabisa hakuwa na mapenzi naye na ukweli ilizidi kudhihirika. Mlango uligongwa, aliweka simu pembeni na kunyanyua uso wake kuangali mlangoni bila kusema kitu.
Alijua ni mama yake amerudi baada ya asubuhi kuondoka kwenda kwa mama Mage kutaka kutafuta muafaka. Aliamini picha zile ndizo zitapunguza presha ya mama yake aliyeng’ang’ania kuokoa ndoa yake na Mage ambayo iliisha kufa. Alikumbuka ameacha simu alirudi kitandani na kuichukua ili amuoneshe mama yake zile picha za Mage akiwa na mwanaume nchini Afrika ya kusini.
Baada ya kuichukua simu alirudi hadi mlangoni na kufungua, alishtuka kumuona mwanamke mgeni kwake akitabasamu aliyekuwa na miwani ndogo nyeupe. Aliwekewa kidole mdomoni na kumsukuma kumrudisha ndani, naye hakuwa mbishi alirudi hadi kitandani na kukalishwa. Msichana yule mrembo alifunga mlango na komeo na kugeuka huku akitoa miwani ndogo na kutabasamu.
Colin alikuwa kama anaota baada ya kumuona aliyekuwa amesimama mbele yake ni Cecy hakika alikuwa amependeza sana.
“Ha! Cecy?”
“Ndiyo mimi,” Cecy alijibu kwa madaha.
“Siamini…Siamini Cecy wewe ni mwanamke mzuri sana tena sana.”
“Simshindi Mage.”
“Cecy naomba uachane na kile kichefuchefu.”
“Colin leo unamuona Mage kichefuchefu kwa vile amekukataa?”
“Ilikuwa shinikizo la mama tu lakini ukweli sikuwa na mapenzi naye kama ninavyokupenda,” Colin alijitetea.
“Colin napita nilitaka kujua kama upo,” Cecy baada ya kusema vile aligeuka na kutoka nje.
“Cecy hebu nisikilize.”
“Ungekuwa na shida na mimi ungenifuata nyumbani kwetu.”
Colin aliamini kabisa Cecy alikuwa amechukizwa na kitendo cha kumterekeza na ahadi za uongo. Alitoka mbio kumuwahi Cecy nje, alimkuta amekaribia getini alimfuata na kumshika mkono asiondoke.
“Cecy najua nimekukosea naomba unisamehe.”
“Colin najua hunipendi bali mimi najipendekeza kwako, endelea na Mage wako.”
“Hapana Cecy nakuapia haki ya Mungu wewe ndiye moyo wangu,” Colin alipiga magoti mbele ya Cecy ambaye siku ile alionekana mrembo mara dufu.
“Colin wewe ndiyo wa unifanya hivi au kwa vile mimi ni maskini mbumbumbu sijui lolote, asante,” Cecy alisema kwa sauti ya kilio.
“Ha..ha..Si..si…” Colin alinyamaza baada ya kusikia honi lakini alishindwa kunyanyuka kwa vile alikuwa bado kamshika mkono Cecy akimuomba msamaha.
Geti lilifunguliwa na gari la mama Colin liliingia na kushangaa kumuona mwanaye amepiga magoti mbele ya binti mrembo.
Cecy alipomuona mama Colin akiteremka kwenye gari alimsukuma Colin na kutimua mbio kwenda nje.
“Cecy…Cecy rudi na..na..”
Cecy hakugeuka alitoka hadi nje ya geti, bahati nzuri aliona bajaj inapita aliisimamisha na kupanda kisha alimweleza dereva ampeleke nyumbani kwao. Colin alipotoka nje alikuta ameisha ondoka. Alirudi ndani mbio na kumwambia mlinzi afungue geti, alipanda kwenye gari alilokujanalo mama yake na kumfukuzia Cecy kwa kuamini hasira za Cecy hazikuhitaji kupewa muda zaidi ya kutulizwa haraka la sivyo atakosa bara na pwani.
Mama Colin toka afike alikuwa akijionea vihoja asijue kumetokea nini na yule binti mrembo ni Cecy gani. Alimsogelea mlinzi na kumuuliza.
“Eti yule msichana ni nani?”
“Hata sijui, alikuja na kukuuliza kama upo nikamwambia haupo, akaniuliza Colin nikamwambia yumo ndani. Basi aliingia ndani hata hajakaa niliona akitoka mara nikamuona Colin akimkimbilia na kumshika yule msichana akawa mkali. Nilishangaa kumuona akipiga magoti kumuomba msamaha.”
“Nimesikia anamwita Cecy, ni Cecy yupi?”
“Mmh! Ndiyo leo namuona.”
“Mmh! Sasa atakuwa amekwenda wapi?”
“Hata najua! Labda atakuwa amemfuata huyo msichana.”
Colin aliendesha gari kwa kasi kuitafuta bajaj ambayo ilikuwa imeishapotea kuonesha Cecy alimwambia dereva aikimbize. Aliakanyaga mafuta kuitafuta bajaj kuifuata njia ya kuelekea nyumbani kwao Cecy. Alipokaribia nyumbani kwao alimuona akiteremka kwenye bajaj na kuingia ndani.
Colin alisimamisha gari mbele ya nyumba ya kina Cecy na kuteremka, hakufunga mlango alikimbilia ndani, Cecy alishangaa kumuona Colin pale alimuuliza kwa sauti ya juu.
“Colin umefuata nini hapa kwa masikini?”
“Cecy mpenzi naomba unisikilize.”
“Nikusikilize nini, ni wazi nalazimisha mapenzi nenda kwa Mage mwanamke mwenye uwezo na elimu, niache mimi maskini nisiye na elimu.”
“Ukifanya hivyo utakuwa ukinifunga mikono na kunipiga sitaweza kujitetea, naomba unipe nafasi.”
“Umetudhalilisha vya kutosha kwa kutudanganya kuishi maisha ya peponi leo yapo wapi, najua una chaguo lako naomba uondoke utuache na umaskini wetu.”
“Cecy najua nimewakosea lakini nami ni mwanadamu ninayehitaji kusamehewa kwa vile si mkamilifu.”
Mama Cecy aliyekuwa nyumba ya pili akichota maji aliporudi alishangaa kumkuta Colin kampigia magoti Cecy.
“Kuna nini?” aliuliza kwa mshangao.
“Mama huyu si alikuja hapa kusema nini na alifanya nini?” Cecy aliuliza kwa sauti hasira.
“Mama najua sikuwa mkweli lakini mpango wangu upo palepale.”
“Baada ya kukataliwa na Mage eeh?” Cecy alimuuliza huku amemshikia kiuno.
“Hapana majukumu yalinibana, mama naahidi nikitoka hapa kila nilichoahidi nakitimiza nisipofanya hivyo chukue uamuzi wowote.”
“Tuchukue uamuzi gani ikiwa hatukudai ni hitari yako si lazima,” mama Cecy alisema.
“Mama nilikuwa katika kipindi kibaya ambacho naamini ningelezimisha ningeweza kuwatia kwenye matatizo.”
“Colin, maisha yetu ndiyo haya hatuhitaji msaada wako, hatujaja kwenu kuomba msaada, hata masikini ana nafasi kwa muumba,” Cecy alisema huku machozi ya uchungu yakimtoka.
“Cecy usifike huko, najua unanipenda,nakuhakikishia kulipa upendo mara mbili.”
“Sihitaji,” Cecy alijibu kwa nyodo japo moyo wake wote ulikuwa kwa Colin alitaka kutikisa kibiriti kuona kama kimejaa.
“Cecy najua nimekukosea lakini amini huu ni wakati wako wa kuponya maumivu ya moyo wako.”
“Cecy msamehe mwenzako,” mama Cecy aliingilia kati.
“Basi amka,” Cecy alinyanyua Colin ambaye alikuwa bado amepiga magoti kama muumini aliyekuwa akiungama kanisani.
Colin alinyanyuka na kukumbatiana na Cecy ambaye alijilaza kifuani kwa mpenzi wake, mama yake alikuwa pembeni alitabasamu huku akiomba dua Colin amuoe Cecy ili kutimiza ndoto ya mwanaye.
“Cecy nataka kukuhakikishia mbele ya Mungu, mama yako na mchana wa jua kuwa wewe ndiye mke wangu wa maisha.”
“Muongo Colin unanidanganya,” Cecy alisema kwa sauti ya kudeka.
“Unataka nifanye nini ili uamini ninayosema.”
“Nioe niwe mkeo.”
“Nakuhakikishia kukuoa uwe mke wangu na mimi niwe mumeo.”
“Asante.”
“Naomba sasa hivi twende nyumbani nikamueleze mama mbele yangu.”
“Akikataa?”
“Hawezi, hii ni nafasi yangu ambayo hakuna wa kuiingilia, naomba uniamini.”
“Mmh! Sawa wacha nikaoge ili tuondoke.”
Colin alipewa kiti ili amsubiri Cecy aliyekwenda ndani kubadili nguo, alitoka amejifunga upande wa khanga na kutoka kuelekea bafuni kuoga.
Colin alimsindikiza kwa macho baada ya kupata nafasi ya kuliona umbile la Cecy katika vazi la kanga rangi adimu ya isiyochanganywa madawa ya ngozi.
Aliamini chaguo la kwanza la mama yake lilikuwa sahihi, alijua ni wakati wa mama yake kuamini chaguo la pili halikuwa sahihi bali tamaa ya macho ndiyo iliyompoteza. Cecy baada ya kumaliza kuoga alirudi ndani na kubadili nguo kwa kujipamba kwa vazi la kitenge lililompendeza alionekana mwanamke wa Kiafrika hasa. Alisimama mbele ya Colin na kutabasamu.
“Colin tunaweza kwenda.”
“Duh!” Colin alisema akiwa haamini.
“Ndiye mimi Cecy, mwafrika asilimia ninayejivunia rangi yangu nyeusi.”
“Basi mama inatosha, “Colin alisema huku akinyanyuka na kumshika mkono.
“Mama tunaomba tukukimbie,” Colin alimuaga mama Cecy.
“Haya baba Mungu awatangulie mfike salama.”
“Amina.”
Walishikana mikono na kutoka nje kuelekea kwenye gari, mama Cecy aliwasindikiza kwa macho na kunyanyua mikono juu na kurudi kuomba dua yake ya Colin kumuoa mwanaye ili roho itulie. Hakuteremsha jicho mpaka gari lilipopotea machoni mwake.
Ndani ya gari Cecy moyo wake ulikuwa na furaha nusu kwa vile aliamini lazima Colin atumie nguvu nyingi bila hivyo hakuna mapenzi kwa vile mama yake aliishajenga uadui mapema. Alionekana mtu mwenye mawazo mengi kitu kilichomfanya Colin amshtue.
”Vipi mpenzi?”
“Colin bado moyo wangu una wasiwasi.”
“Wa nini?”
“Jinsi mama yako atakavyonipokea.”
“Ondoa wasi kila kitu niachie mimi.”
Colin alisimamisha gari mbele ya geti na kupiga honi, mlango ulifunguliwa na kuliingiza gari ndani. Alizunguka upande wa pili na kumfungulia Cecy na kumshika mkono kuteremka kwenye gari kwa heshima kisha alielekea naye ndani. Walitembea taratibu kama mtu na mkewe angetokea mtu na kuwaona angejua ni wapenzi wa muda mrefu wanaopendana sana.
Walipofika mlango wa kuingia sebuleni Colin alisema kwa sauti ya unyenyekevu:
“Karibu malkia wangu.”
“Asante mfalme wangu,” Cecy naye alijibu kwa unyenyekevu.
Sauti zile zilimfanya mama Colin aliyekuwa ameinama akisoma biblia kunyanyua macho na kumuona mwanaye na msichana mrembo ambaye aliamini ndiye aliyeondoka muda mfupi uliopita.
“Shikamoo mamkwe!” Cecy alimsalimia mama Colin kwa unyenyekevu huku akipiga magoti ya heshima.
“Marahaba mama, karibu.”
“Asante,” Cecy alijibu huku akinyanyuka na kumfuata Colin aliyekuwa amesimama pembeni yake na kumshika mkono.
Colin alimuongoza Cecy mpaka kwenye sofa na kumkaribisha tena:
“Karibu.”
“Asante,” Cecy alijibu huku akikaa.
“Unatumia kinywaji gani?”
“Chochote utakachonichagulia mfalme wangu.”
“Colin si ungemwita dada wa kazi awahudumie,” mama Colin aliingilia kati.
“Hapana huyu ni mgeni wangu, kila kitu chake nitafanya mimi.”
“Mmh! Haya.”
Muda wote mama Colin alikuwa bado hajaipata picha ya yule msichana mrembo, alituliza macho kwa wizi ndipo alipomgundua kuwa ni Cecy msichana muuza ndizi. Alikunja uso kwa hasira na kuamini kabisa lile si chaguo sahihi kwa mwanaye bali ni papara ya kuachwa na Mage.
Alinyanyuka na kuelekea chumbani kwake, alipotoka eneo la sebule alimwita Colin.
“Colin.”
“Naam mama.”
“Njoo mara moja.”
“Nakuja,” Colin alisema huku akimwekea juisi kwenye glasi na kunywa kidogo kisha alimkaribisha.
“Karibu malkia wangu.”
“Asante mfalme wangu.”
“Samahani namsikiliza mama mara moja.”
“Nenda mpenzi kamsikilize mama.”
Colin alimfuata mama yake kwenye korido alipokuwa amesimama, alimsogelea karibu na kumuuliza:
“Unasemaje maana umenitoka kama kuna kitu?”
“Yule nani?” aliuliza huku akinyoosha kidole sebuleni.
“Mke wangu mtarajiwa chaguo sahihi la moyo wangu.”
“Colin… Colin una tatizo gani wanawake wote wameisha mpaka umfuate huyu maskini mbumbumbu asiyejua kitu. Mwanangu tuna fedha tunaweza kumuona msichana yeyote mzuri mwenye elimu yake kwa fedha yoyote na popote duniani.”

WAKILI WA MOYO SEHEMU: 17

$
0
0

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’

ILIPOISHIA:
“Yule nani?” aliuliza huku akinyoosha kidole sebuleni.
“Mke wangu mtarajiwa chaguo sahihi la moyo wangu.”
“Colin… Colin una tatizo gani wanawake wote wameisha mpaka umfuate huyu maskini mbumbumbu asiyejua kitu. Mwanangu tuna fedha tunaweza kumuona msichana yeyote mzuri mwenye elimu yake kwa fedha yoyote na popote duniani.”
SASA ENDELEA...
“Mama naomba kwa hili usizungumze chochote uniache kabisa, umetafuta mwanamke ambaye leo katuvua nguo kwa vile ulimfuata msomi mwenye uwezo.”
“Lakini suala la Mage bado tulikuwa tunalishughulikia bado lilikuwa halijafika mwisho. Hivi leo Mage aje na mama yake wakikute kinyago hiki kuna ndoa kweli?”
“Penzi langu na Mage liliishia Bagamoyo, lilikufa tukalizika halitafufuka tena.”
“Lakini bado wazazi hatajabariki uamuzi wenu.”
“Mama si uamuzi wetu bali wa Mage, kasema ukweli ana mtu anayempenda tatizo lipo wapi?”
“Basi Cecy si chaguo langu.”
“Mama, mimi ni mwanao umenizaa na kunilea na kunifundisha kila kitu, lakini suala la nimpende nani ni matakwa ya moyo wangu. Nilikukubalia kwa Mage kwa vile ni mzazi wangu zoezi lako limefeli sasa huu ni muda wangu.”
“Lakini siyo kwa Cecy.”
“Mama Cecy ni zaidi ya mwanamke ndiye mwenye nafasi moyoni mwangu zaidi ya hapo sitakuwa na mwanamke mwingine.”
“Colin, Cecy umemjulia wapi kama siyo mimi?”
“Basi hili ndilo chaguo lako lililokuwa sahihi hujui tu.”
“Nilikuwa namtania tu lakini si kwa ajili ya kuwa mkeo.”
“Basi imekuwa hivyo bila kutegemea.”
“ Basi mimi simtaki.”
“Kwa hiyo unatafuta aibu nyingine?” Colin alisema huku akifungua simu upande wa picha na kumuonesha mama yake.
“Umeona unayempenda?”
Aliangalia picha za Mage na kuuliza:
“Hizi picha za nani?”
“Mage na mpenzi wake,” Colin alimjibu huku akimtazama usoni.
“Picha hii imepigwa lini?”
“Leo.”
“Wapi?”
“Wapo Afrika ya kusini wanakula raha katika hoteli ya Hilton jijini Durban, sasa naomba uniache na Cecy wangu.”
“Colin bado hujanieleza kitu, tafuta msichana mwingine lakini kwa Cecy sipo radhi kuingiza uchafu katika familia yangu.”
“Mama nakupenda na kukuheshimu sana naomba kuhusu Cecy usiniingilie kabisa zaidi ya hapo nitaondoka na kukuacha na fedha zako.”
“Colin mwanangu mbona umefika mbali,” mama alishtuka.
“Kwa sababu umeingilia haki ya moyo wangu, wewe ni mzazi gani usiye na huruma nimeumizwa badala ya kunihurumia bado unataka kuniongezea maumivu,” Colin alisema kwa uchungu.
“Lakini kumbuka wewe ni msomi unawezaje kuoa mwanamke mbumbumbu?”
“Mama mapenzi si cheo, elimu wala fedha, Cecy ni zaidi ya vyote hivyo kwangu.”
“Sawa, lakini utakuja kunikumbuka na uamuzi wako hata nikifa.”
“Ni kweli mama nitakukumbuka kwa kunitafutia mchumba aliye bora kuliko Mage. Cecy ni lulu iliyokuwa imejificha kwenye matope.”
“Nimekuelewa mwanangu, naomba unisamehe kwa kukukwaza.”
“Nilikusamehe kabla hujatenda.”
“Basi naomba ya huku yaache hukuhuku.”
“Sawa mama.”
Baada ya makubaliano Colin alirudi kwa Cecy na mama yake kwenda chumbani, alipofika alimpigia simu mama Mage kutaka kupata ukweli wa kauli ya mwanaye.
Baada ya simu kuita ilipokelewa upande wa pili:
“Haloo, dada vipi?”
“Mmh! Yaani bado nachanganyikiwa ulisema Mage kaenda wapi?”
“Nilikuambia amekwenda kwa shoga yake.”
“Wapi?”
“Aliniaga anakwenda Kibaha,” mama Mage alidanganya.
“Mmh! Mbona Colin anasema katumiwa picha za Mage akiwa na mwanaume Afrika ya kusini wakila raha kwenye ufukwe wa Hilton Hotel?”
“Mmh! Labda maana ametoka toka jana, dada wee hebu tuachane na Mage tufanye mambo zingine.”
“Sawa dada nimekuelewa.”
Baada ya kukata simu alitulia kwa muda akiwaza, alijikuta akimchukia Cecy na kuuapia moyo wake hatakuwa tayari kuona mwanaye akioa mwanamke asiye na hadhi. Alipanga kuhakikisha anauvunja uhusiano ule kwa hali na mali ili Colin aoe mwanamke mwingine mwenye elimu na kutoka familia yenye uwezo.
Alitoka chumbani na kujifanya kujichekeza kwa Cecy huku akimtania.
“Jamaniii mmependezaje wapenzi!”
“Asante mkwe,” alijibu Cecy kwa furaha huku Colin aliuona unafiki wa mama yake uliojificha moyoni ambao mpenzi wake hakuujua.
Kwa vile mama Colin hakupenda Cecy kuwa pale aliondoka na kwenda chumbani kwake na siri yake nzito moyoni.
JIJINI DURBAN AFRIKA KUSINI
Katika ufukwe wa hoteli ya Hiltoni wapenzi wa wawili walikuwa wakila raha, Mage alikuwa amelala kifuani kwa Hans huku akichezea kidevu chenye ndevu chache.
“Hans nikuambie kitu?”
“Niambie mpenzi.”
“Ningebugi vibaya kuolewa na mrugaruga kama yule(Colin).”
“Si haraka zako, nilikueleza piga ua lazima mke wangu utakuwa wewe pamoja na wazazi kunilazimisha kumuoa yule mwanamke.”
“Nilichanganyikiwa baada ya kuona umepata mtoto.”
“Ilikuwa lazima iwe vile ili wasijue nimepanga nini mbeleni.”
“Asante Hans kwa kuponya majeraha ya moyo wangu.”
“Nami nashukuru kukubali kurudi mikononi mwangu.”
“Kwa hiyo ndoa lini?”
“Tukirudi tu nyumbani mipango inaanza mara moja.”
“Nitafurahije mpenzi wangu.”
“Usijali nipo kwa ajili yako.”
“Basi naomba turudi nyumbani ili tukalisema hili mbele ya wazazi wetu wote.”
“Hakuna tatizo nakusikiliza wewe.”
“Nataka kesho jioni tuwe mbele ya wazazi wako ukiwaeleza kwa mdomo wako kuwa mimi ndiye mkeo baada ya hapo twende kwetu nikamweleze mama kuwa wewe ndiye mume wangu.”
“Hakuna tatizo mpenzi wangu.”
Walikubaliana kuondoa Afrika ya kusini siku ya pili mchana warudi Tanzania ili kwenda mbele ya wazazi wao kuthibitisha mapenzi yao ya dhati.
***
Colin na Cecy baada ya kutoka nyumbani walikwenda Bagamoyo katika hoteli ya Malaika ambako alipanga kukaa kwa siku moja. Majira ya jioni wakiwa wamejilaza mchangani huku wakipepewa na upepo mwanana wa bahari Colin aliyaangalia mawimbi ya bahari na mitumbwi ya wavuvi aliokuwa wakivua samaki.
Baada ya kugandisha macho baharini alijikuta akitokwa na machozi baada ya kukumbuka sehemu kama ile ndiyo iliyotumika kuvunja uchumba wake na Mage japokuwa ilikuwa hoteli tofauti lakini ni Bagamoyo ileile.
Machozi yalimdondoka bila kujua na kuangukia kwenye paji la uso la Cecy aliyekuwa amejilaza mapajani kwa mpenzi wake na kumfanya anyanyue macho kumwangalia. Alishtuka kumuona akibubujikwa machozi kitu kilichomfanya amuulize.
“Vipi mpenzi wangu mbona unalia?”
“Nimekumbuka kitu ambacho kimesababisha nitokwe machozi.”
“Kitu gani mpenzi wangu?” Cecy alimuuliza huku akimfuta machozi kwa upande wa mtandio aliojifunga.
“Ni juzi tu maeneo hayahaya yaliujerudi moyo wangu lakini, leo hii maeneo yaleyale yameujenga upya na kujiona kama nimezaliwa upya.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Juzi tulikuja huku na Mage kuvunja uchumba wetu ambao ulinishtua sana na kuumiza moyo wangu japokuwa haikuwa hoteli hii, lakini ni hukuhuku Bagamoyo. Lakini leo nimezaliwa upya kwa kulipata penzi la kweli ambalo naamini nilitaka kulipoteza haya ni machozi ya uchungu na furaha.”
“Nifurahi kusikia hivyo, lakini moyo wangu bado haujaamini kama tayari wewe ni wangu.”
“Kwa nini Cecy?”
“Naogopa Mage anaweza kurudi na wewe kunitosa, nitaumia mara mbili kwa vile nimeonja utamu wa mapenzi naweza kufa kwa presha kama utafanya hivyo,” Cecy alisema kwa sauti ya kulalamika.
“Cecy unataka kuamini vipi wakati penzi langu lilikuwa wazi mbele ya mama yangu.”
“Mama yako alikuitia nini pembeni?”
“Tulikuwa na yetu wala haikuhusiana na sisi,” Colin alitengeneza uongo ili kuendeleza furaha ya siku ile.
“Mmh! Nilikuwa na wasi labda chokoraa nilimeingia kwenye nyumba ya malkia,” Cecy alitania utani wenye ukweli.
“Hapana wewe ndiye malkia wangu.”
“Nashukuru kusikia hivyo,” Cecy alimkumbatia mpenzi wake kwa furaha bila kujua palichimbika mpaka yeye kuwa pamoja muda ule.
***
Mage na Hans waliwasili katika aridhi ya Tanzania katika jiji la Dar na ndege ya shirika la Afrika ya Kusini. Nje ya uwanja wa ndege walisubiriwa na gari la kifahari Land Cruiser V8 nyeusi. Baada ya ndege kutua waliteremka na kwenda moja kwa moja ndani ya gari lililokuwa likiwasubiri na kuingia.
Gari liliondoka kuelekea Mikocheni anapoishi Hans, njiani Mage alikuwa na furaha ya ajabu kurudi mikononi kwa mpenzi wake mwanaume wa maisha yake. Baada gari kuingizwa ndani na kusimama Hans alizunguka upande wa pili na kumfungulia Mage mlango na kumkaribisha.”
“Karibu utamu wangu.”
“Asante raha zangu.”
Walishikana mikono na kuingia ndani, mapokezi ya familia ya Hans yalikuwa tofauti na siku za nyuma waliufurahia ugeni wa Mage huku wadogo zake wakimwita wifi na shemeji na wazazi wakimwita mkwe. Ilikuwa ni faraja kubwa moyoni kwa Mage aliona sawa na ngamia kupita katika tundu la sindano kukubalika katika familia ile.
Moyoni alijilaumu kukubali kuolewa na Colin kumbe ahadi ya kuvumilia ili ndoto yao ya muda mrefu waliyoahidiana kutenganishwa na kifo ilikuwa njiani. Familia haikuwa na tatizo tena kuingilia uamuzi wa mtoto wao kwa vile chaguo lao Mungu alilichukua hawakuwa na jinsi.
Baada ya mapokezi mazuri katika familia ya mpenzi wake Mage na Hans walielekea Kigamboni nyumbani kwao Mage ili kujitambulisha rasmi kwa mzazi wake. Walipofika Kigamboni Mage alimkaribisha Hans nyumbani kwao.
“Karibu mume wangu.”
“Asante mke wangu.”
Walishikana mikono na kuingia ndani kwa mwendo wa mahaba, sebuleni walimkuta mama Mage. Mage alimuachia mkono Hans na kumkimbilia mama yake na kumkumbatia.
“Waaawoo mama.”
“Mage mwanangu karibu mama.”
“Asante mama.”
Mage alichukua nafasi ile kumtambulisha Hans.
“Mama leo nimemleta mume wangu chaguo la moyo wangu.”
“Nimemuona, karibu baba,” mama Mage alisema kwa sauti ya unyonge.
“Asante mama, shikamoo.”
“Marahaba.”
“Mama mbona mnyonge unaumwa?” Mage alimuuliza mama yake.
“Walaa, mwili umechoka tu.”
Mama Mage alinyanyuka na kuelekea chumbani kuwapisha alipoondoka eneo la sebule alimwita mwanaye.
“Mage mama njoo mara moja.”
“Nakuja mama,” kabla ya kuondoka alimuaga mpenzi wake.
“Mpenzi nakuja.”
“Hakuna tatizo msikilize mama.”
Mage alimbusu shavuni Hans na kuchepua mwendo kwenda kumsikiliza mama yake.
“Abee mama.”
“Njoo chumbani.”
Waliongozana hadi chumbani, walipofika mama yake alisimama na kumwambia Mage akae kwenye kochi, baada ya kukaa alimgeukia na kumwita.
“Mage.”
“Abee mama.”
“Hivi ndiyo umeamua kunivua nguo?”
“Kukuvua nguo! Kivipi mama.”
“Kwa hiyo hutaki kuolewa na Colin?”
“Mamaaa! Mbona hilo tuliisha limaliza, si nimekueleza ukweli wangu na Colin anajua kila kitu. Sasa swali kama hilo linatoka wapi?”
“Mage kwa nini unalamba matapishi yako?”
“Mama Hans si matapishi ni chakula kilichowekwa kwenye Hot port nimekipakuwa bado kina moto. Unajua jinsi gani nilivyoteseka baada ya Hans kulazimishwa kuona mwanamke mwingine. Ni wewe uliniambia niwe na subira sasa leo karudi mikononi mwangu unaniuliza hivyo?”
“Kama ungekuwa huna mchumba nisingekuuliza lakini wewe tayari umeishakuwa mchumba wa mtu tena upo kwenye hatua za mwisho za ndoa.”
“Mama wewe ndiye unayekuza mambo Colin tumeisha malizana na sasa hivi tunatoka nyumbani kwao Hans ambako sikuamini kama wangenipokea kama malkia. Yaani mama nimefurahi kukubalika katika familia ya mpenzi wangu.”
“Mwanangu siku zote mkataa pema pabaya panamwita.”
“Mamaa maombi gani hayo?”
“Nakuambia utamkumbuka Colin, ipo siku Hans atakukimbia na kurudi kwa Colin utambembeleza ukitembea kwa magoti, kibaya ukute ameoa mwanangu utakuja jutia uamuzi wako,” mama alitoa taadhali.
“Mama kuwa na Hans sitajuta katika maisha yangu ni chaguo sahihi la moyo wangu.”
“Mmh! Sawa.”
“Kuonesha Hans hataki kunichezea wiki ijayo barua inakuja na baada ya majibu maandalizi yanaanza mara moja. Kinachotakiwa vikao vya harusi visogezwe mbele ili michango ya harusi yangu na Colin iwe yangu na Hans. Hapo nina imani hakuna kitakacho haribika.”
“Sawa, siwezi kukuingilia kwa vile umeamua mwenyewe, ila kila aliyae ushika kichwa chake.”
“Mama hiyo misemo, ninacho shukuru nimepata tiba ya moyo wangu, kuna lingine?”
“Hakuna.”
“Basi mama yangu naomba unipe baraka zako kinyongo chake kinaweza kuvuruga ndoto zangu.”
“Siwezi kuna na kinyongo kwa vile nipo kwa ajili ya kuyaona maisha yako yanakuwa mazuri na salama.”
“Asante mama,” Mage alimshukuru mama yake kwa kumkumbatia.
Mage baada ya kuachana na mama yake alikwenda sebuleni alipokuwa amemuacha mpenzi wake.
Alirudi sebuleni na kumvamia Hans kwa mahaba motomoto bila kujali yupo sehemu gani. Mama yake hakutoka ndani alijikuta moyo ukimuuma na kuanza kulia peke yake huku akilaumu mapenzi ya mumewe kumuharibu mtoto.
****
Siku ya pili Colin na Cecy alirudi nyumbani, alimpitisha nyumbani kwa kisha yeye alirudi nyumbani kwa vile kulikuwa na mambo ya kufuatilia kuhusiana na shughuli zake alizoanza ikiwemo kupata kibari cha kuanzisha kampuni ya mitindo na mavazi ambayo alipanga kumtumia Cecy kwa ajili ya maonesha ya mitindo ya nguo.
Walipofika kabla ya kuondoka Colin alimwambia Cecy:
“Mpenzi pumzika ila jioni nitakufuata tutakuwa na mazungumzo marefu ila utarudi kulala nyumbani najua bi mkubwa amekumisi.”
“Hakuna tatizo msalimie mkwe.”
“Kuanzia wiki ijayo nategemea kutimiza ile ahadi.”
“Ahadi gani?”
“Ya ujenzi wa nyumba yenu, leo nitamtuma mtu awatafutie nyumba ili kesho muhame ili kupisha ujenzi.”
“Kama ni kweli tutashukuru.”
Colin alimwita mama Cecy na kumpa laki mbili.
“Mama utakunywa soda.”
“Asante baba.”
“Hakuna tatizo.”
Colin aliaga na kuondoka kuwahi nyumbani ili awahi mjini kwenye mipango yake na kumuacha Cecy akikumbatiana na mama yake kwa furaha. Kwa vile alikuwa na haraka alifika nyumbani hakukaa alibadili nguo na kuvaa suti ili kwenda kwenye miadi yake. Wakati anatoka alikutana na mama yake sebuleni.
“He! Baba umerudi saa ngapi?”
”Sasa hivi mama, Leo namiadi ya jamaa wale wa kampuni ya matangazo.”
“Na mwenzio yupo wapi?”
“Nimemuacha kwao.”
“Sawa baba baadaye.”
“Sawa mama baadaye.’
Colini aliagana na mama yake na kutoka nje ambako alichukua gari kuwahi Posta mpya katika Jengo la Benjamini Mkapa ghorofa ya kimi na nne. Baada Colin kuondoka mama yake aliamini ile ndiyo nafasi ya kwenda nyumbani kwao Cecy ili kuhakikisha ndoa na mwanaye haifungwi.
Alioga harakaharaka na kutoka kwenda nyumbani kwao Cecy, aliendesha gari kwa kasi kidogo ili kuwahi kabla mwanaye hajarudi. Aliamini kutumia fedha zake ataweza kuisambaratisha ile ndoa. Alisimamisha gari mbele ya nyumba ya kina Cecy na kuteremka.
Alimkuta mama Cecy amekaa kwenye kibalaza cha nyumba, alipomuona alimkaribisha kwa furaha na bashasha.
“Ooh! Karibu dada.”
“Asante, za hapa?”
“Nzuri, karibu japo maisha yetu ya kuungaunga.”
“Aah! Kawaida tu wala msijali.”
Alipotaka kumkaribisha ndani alikataa alisimama mbele ya nyumba, aliyatazama mazingira wanayoishi Cecy na mama yake moyo wake ulichefuka kwa kuona jinsi gani mwanaye alivyopotea maboya kutaka kumuona mwanamke fukara kama yule ambaye halingani na sifa na hadhi ya familia yao.

WAKILI WA MOYO SEHEMU: 18

$
0
0

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’

ILIPOISHIA:
Cecy alizipokea na kumfanya mama Colin kutabasamu kwa kuamini fedha ni sabuni ya roho. Alizitazama zile fedha kwa uchungu huku machozi yakimtoka na kuona jinsi gani umaskini wao ulivyotumiwa kama kisu butu cha kuupasua moyo wake bila ganzi. Alitulia akilia huku machozi yakidondokea kwenye zile fedha.
SASA ENDELEA...
Kwa hasira alizinyanyua na kumpiga nazo usoni mama Colin na kutoka ndani ya gari, kitu kilichomuacha mdomo wazi mama Colin. Mama yake alishangaa kumuona mwanaye akitoka ndani ya gari akilia.
“Cecy kuna nini?”
“Mama niache kwanza, huyu mama ni mchawi.”
“Mchawi! Kafanya nini?” mama yake alishtuka.
Wakati huo mama Colin kwa aibu aliwasha gari lake na kuondoka bila kuaga. Aliushangaa ujasiri wa Cecy msichana maskini lakini mwenye kujiamini kupita kiasi kwa kukataa fedha zile na ofa ya kuyabadili maisha yao. Hakuamini binti muuza ndizi kukataa fedha zile wakati maisha yao ya kubahatisha. Lakini alijiapiza kwa nguvu kwa hiyari kwa fedha kwa damu lazima Cecy ataachana na Colin.
Mama Cecy alimfuata mwanaye aliyeingia chumbani huku akilia na kushindwa kuelewa mazungumzo ya ndani ya gari yalikuwa ya nini. Alikumta akiendelea kulia kitu kilichomfanya ajiulize kipi kikubwa walichokizungumza ndani ya gari.
Alimkuta amelala kifudifudi akilia kwa sauti ya kwikwi, wasiwasi wake labda Colin amepata tatizo.
“Cecy mwanangu kuna tatizo gani tena?”
“Mama inaumiza sana.”
“Kuna nini mpenzi wako kapata tatizo?”
“Mama mtu anaweza kuununua moyo wangu hata kuuchukua bure nikiwa nimekufa, lakini nikiwa hai siuuzi kwa gharama yoyote kwa vile furaha ya mtu hainunuliwi dukani.”
“Una maana gani?” mama yake alikuwa bado njia panda.
Cecy alimweleza mama yote aliyozungumza na mama Colin, mama yake macho yalimtoka pima kusikia taarifa ile baada ya kuamini kila kitu kilikuwa vizuri kilichobakia ni ndoa ya mwanaye na Colin.
“Mmh! Mbona makubwa madogo yana nafuu,” mama Cecy alisema akiwa amechoka na maneno yale.
“Mama mimi na Colin basi,” Cecy alisema kwa hasira.
“Huo ni uamuzi wa hasira lazima umsikilize mwenzako si amesema atakupitia jioni basi msubiri umsikilize naye anasemaje kama lao moja na mama yake una haki ya uamuzi wako.”
“Mama kosa langu nini? Yaani anatumia fedha zake kuinunua furaha yangu?” Cecy alisema kwa uchungu.
“Mwanangu kama Colin si chaguo la Mungu basi hamtaoana lakini kama ni chaguo la Mungu hakuna kitakachozuia.”
“Yule mwanamke ni mnafikia akiwa na mwanaye ananichekea kicheko cha mamba lakini kumbe ananitamani kunimeza.”
“Wee yaache tusubiri jioni.”
“Sawa, lakini nina amini hakuna ndoa yangu na Colin labda mapenzi ya sisi wenyewe lakini mama yake hanipendi na yupo radhi kutumia njia yoyote kukwamisha mapenzi yetu.”
”Ngoja tumsubiri Colin anasemaje.”
“Namsubiri kwa ajili yako lakini ningekuwa peke yangu asingekanyaga hapa.”
****
Majira ya jioni Colin alimpitia Cecy kama alivyomweleza, aliposimamisha gari alishangaa kutomuona mpenzi wake kama kawaida, kwani aliisha mzoesha vibaya kumpokea kwa kumrukia kwa mahaba motomoto. Baada ya kusimamisha gari aliteremka na kwenda ndani huku akiita jina la Cecy mkononi alikuwa amebeba zawadi za mpenzi wake.
“Beeeebi.”
Hakuwa na jibu zaidi ya kusikia sauti ya kilio toka ndani kitu kilichomshtua na kufanya akimbilie ndani kwa kuamini mpenzi wake yupo kwenye matatizo. Alimkuta Cecy amelala kifudifudi akilia kilio cha sauti.
“Cecy mpenzi una nini?”
“Colin unaweza kununua kila kitu chini ya jua lakini si furaha ya mtu,” Cecy alisema bila kugeuka.
“Kuna nini mpenzi wangu?” Colin alishangaa.
“Umenikuta maskini hata siku moja sikuja kwenu kuomba pesa ya kula, nimeishi kwa kuuza ndizi nitaendelea kuuza ndizi lakini hamuwezi kuutumia umaskini wetu kama siraha ya kununua haki ya moyo wangu.”
“Cecy hebu geuka mpenzi wangu, kipi nimekukosea mpaka useme maneno makali hivyo?”
“Najua hunipenda lakini usitumie gharama kubwa kuniacha, tamko lako ni tosha kuliko gharama na nguvu mnayotaka kuitumia. Ni kweli nakupenda jambo ambalo lipo wazi mbele ya muumba. Lakini ni vigumu kulazimisha mapenzi ni sawa na kumvuta punda mtoni lakini huwezi kumlazimisha kunywa maji.”
“Cecy mpenzi wangu mbona toka jana tumekuwa na siku nzuri ambayo nilitegemea kuimalizia leo. Kipi nilichokufanyia ikiwa nimekuaga nimekwenda kwenye mipango ya maisha yetu ya mbeleni. Nimekuja na furaha ili kukujulisha nimekupatia chuo cha mambo ya urembo ambacho utasoma miezi sita na ukitoka hapo utakuta nimeisha kukufungulia kampuni yako ya urembo.
“Kwa nini wanawake mnapenda kuumiza moyo wangu, Cecy kabla hatujaanza mapenzi ulionesha kunijali lakini kuanza kwa ukaribu wetu hata mwezi bado unataka kuupasua moyo wangu bila ganzi. Cecy niliamini wewe ndiye tiba ya moyo wangu, lakini unataka kuongeza msumali wa moto kwenye kidonda. Naomba basi mnihurumie nami binadamu ninayehitaji upendo. Mapenzi yangu yamekuwa kama mtu anayemwaga maji baharini yasiyoonekana.
“Kwa nini hukuniambia mapema Cecy umeacha nijirushe juu ya ghorofa ya mapenzi nikiamini utanidaka, lakini najiona naangukia pabaya nawe umekataa kunidaka nitakufa kifo kibaya. Cecy utajiri wetu hauingiliani na mapenzi yetu, fedha inaweza kununua kila kitu lakini si penzi la kweli bali upendo wa dhati toka chini ya uvungu wa moyo wa mtu mwenye mapenzi ya kweli asiyeangalia kitu bali mtu mwenyewe alivyo.
“Ni kosa gani nililokufanyia mpaka kufikia kusema maneno mazito yaliyoushtua moyo wangu, kama moyo ungekuwa ukitoka nje naamini ungekuwa unavuja damu kutokana na mshtuko na maumivu ya kuona unatolewa sehemu salama na kutupwa kwenye miba.”
Maneno ya Colin ambaye alionekana hajui kilichokuwa kikiendelea kilimfanya Cecy aongeze sauti ya kilio na kujinyanyua alipokuwa amejilaza na kwenda kujitupa kifuani kwa Colin kitu kilichomshangaza mpenzi wake.
“Cecy mpenzi wangu hebu kuwa mkweli tatizo nini mpaka kusema maneno makali? Nipo radhi kujitoa muhanga ili kuliokoa penzi letu.”
“Colin najua unanipenda lakini mama yako hanipendi,” Cecy alisema kwa sauti ya kilio.
“Bebi, maneno gani hayo ikiwa jana uliona alivyokufurahi, yasahau yote yaliyopita.”
“Colin, mama yako mnafiki, ana tabia ya unafiki wa mamba anakuchekea machoni lakini moyo anakuchukia.”
“Kwa nini unasema hivyo?” Colin alishtuka kusikia vile.
“Mama yako hataki tuwe pamoja yupo radhi kutumia gharama yoyote kuhakikisha anatutenganisha.”
“Lakini mbona yaliisha.”
Cecy aliamua kumweleza ukweli, ujio wa mama yake na ahadi na fedha aliyotoa kwa ajili kulivunja penzi lao. Colin alibakia macho yamemtoka pima asiamini maneno ya Cecy.
“Cecy unayosema ni kweli?”
“Nimzulie uongo mama yako ambaye kama tungeoana angekuwa mama mkwe wangu.”
“Kama kafikia hatua hiyo naomba kwanza unisamehe sana, najua nitafanya nini. Ila nakuahidi kwa kuonesha msimamo umezisha upendo moyoni mwangu, pia hela aliyotaka kukupa nitakupa mara kumi yake na kutimiza ahadi yangu kwa kulijenga penzi letu.”
“Colin, narudi huwezi kuununua moyo wangu.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Sihitaji pesa zako kwa ajili yakuonesha kuwa unanipenda bali mapenzi ya dhati toka kwako. Pendo langu halina gharama japo ni ghali kwa vile nilikubali kukupenda kama ulivyo wala si kwa ajili ya gari, majumba au fedha zenu.”
“Asante kufahamu hivyo, basi naomba ukaoge ili twende nilipokueleza jana.”
“Sawa mpenzi wangu.”
“Pia, kesho mtahama ili kupisha ujenzi wa nyumba yenu kwa muda, nimewatafutie nyumba nzima ambayo nimelipia kwa mwaka mzima.”
“Kwani hiyo nyumba unachukua muda gani kujengwa?”
“Nitaka ijengwe vizuri hata miezi miwili au mitatu.”
“Basi si ungechukua miezi mitatu?”
“Msiwe na wasi, niliwaambia wakakataa wakataka mwaka mzima.”
“Ipo wapi?”
“Kimara Baruti.”
“Asante mpenzi wangu,” Cecy alimkumbatia Colin kwa furaha na kuyasahau maumivu yote.
Cecy alikwenda kuoga akimuacha Colin ambaye alihisi kichwa kinataka kupasuka kwa mawazo kutokana na alichokifanya mama yake aliyeamini ndiyo muongozo wake na kuitengeneza furaha lakini kwake ilikuwa kinyume. Alipanga akitoka pale kwenda na Cecy nyumbani kwao ili mama yake akayasema yale mbele yake.
Baada ya Cecy kumaliza kuoga na kubadili nguo ambazo zilizidi kumpandisha chati na kumfanya aonekane binti mrembo kuliko wanawake wote duniani mbele Colin. Walishikana mikono na kuelekea ndani ya gari na kuelekea moja kwa moja nyumbani kwao Colin.
“Colin unanipeleka wapi?” Cecy alishtuka.
“Usihofu naomba unifuate na mimi.”
“Mmh! Sawa.”
Gari lilipiga hodi na geti lilifunguliwa na Colin kuliingiza ndani, kama kawaida alizunguka na kumfungulia mlango kisha alimshika mkono na kuingia naye ndani. Sebuleni alikuwa mama Colin akizungumza na msichana wa kazi alipomuona Colin alinyanyua macho na kumuona ameongoza na hasimu wake.
Alijikuta akiponyokwa na glasi ya juisi aliyokuwa ameshikilia. Cecy alisogea hadi karibu na mama Colin na kumsalimia.
“Shikamoo ma mkwe,” kama kawaida alipiga goti la heshima mpaka chini.
Mama Colin alinyanyuka alipokuwa amekaa na kumfuata Cecy na kumnyanyua alipokuwa bado amepiga magoti na kumkumbatia kwa muda huku machozi yakimtoka.
Colin alishangazwa na mama yake kufanya vile aliamini alifanya vile kujitakasa mbele ya macho ya mwanaye lakini moyoni alikuwa na nia mbaya kuliko bomu la kutegwa. Alijiuliza mama yake atamwambia nini kwa kitendo cha kigaidi alichokifanya cha kusambalatisha penzi lake.
“Cecy,” alimwita huku akimshika mabegani na kumtazama usoni kwa macho yaliyojaa machozi.
“Abee ma’ mkwe,” Cecy aliitikia huku naye machozi yakimtoka.
“Najua siku ya leo huenda hutanielewa, unaweza kuwa msichana wa kwanza kunionesha kitu si cha kawaida. Lakini nilichokifanya leo ni mtihani wangu wa mwisho kwako, nakili kwa moyo wangu katika wasichana niliowapenda ulikuwa wewe namba moja.
“Lakini sikumaanisha kuwa utakuwa mke wa mwanangu kwa vile nilikuwa na Malengo makubwa kwa mwanangu baada ya kutumia kiasi kikubwa kumsomesha.
Niliamini mwanamke atakayemfaa ni mwenye elimu kama yake pia anayetoka katika familia yenye uwezo ambaye atakuwa na mapenzi ya kweli na hatafuata mali aliyonayo mwanaume.
“ Niliamini chaguo langu lilikuwa sahihi la kumchagua Mage kwa vile ni msomi tena anatoka katika familia yenye uwezo pia mama yake ni shoga yangu. Lakini kumbe siyo, nakiri toka moyoni mwangu mapenzi niliyokuwa nikimpenda Cecy yaligeuka na kumuona ni adui namba moja anayetaka kuvuruga ndoto zangu.
“Mwanzo nilidhani utani lakini siku ya birthday ya Colin nilivyokuona ulivyopendeza mpaka kukusahau na picha nilizomkuta nazo Colin niliona ndoa hakuna. Moyo wangu ulikosa amani mpaka mipango ya harusi kwenda vizuri huku nikiwa sisikii taarifa yako.
“Kwa kweli niliumia sana kwa kitendo cha Mage kuuvunja uchumba tukiwa katika hatua za mwisho. Siku zote nilikosa usingizi nimekuwa nikipungua siku hadi siku. Kitendo cha kuibuka wewe kwa kweli kilinichanganya sana, sikuamini kama una mapenzi ya kweli na mwanangu zaidi ya kufuata mali zetu.
“ Mtihani niliokupa leo umenipa sababu sahihi ya mwanangu kukuchagua wewe kuwa mkewe. Cecy kitendo cha leo kilifukua mapenzi yote ya nyuma na kukiri mapenzi si elimu wala mali bali upendo wa dhati toka moyoni mwa mtu. Umenionesha jinsi gani unavyo mpenda mwanangu mapenzi ya dhati si kwa ulichonacho.
“ Napenda kuwaomba radhi wote kwa kuwakwaza kwa namna moja ana nyingine.
Colin mwanangu nataka kukutamkia hili mbele ya mpenzi wako na Mungu shahidi yangu kama nitakwenda kinyume naomba anifanye kitu chochote kibaya. Kuanzia leo namtambua rasmi Cecy kama mkwe wangu na mipango ya harusi itaanza mara moja. “Cecy mkwe wangu kuna zawadi nitakupa kwa kuonesha msimamo na mapenzi ya dhati kwa mwanangu naamini wewe ndiye mke aliyechaguliwa na Mungu.”
Mama Colin alisema huku machozi yakimtoka, kila mmoja alitokwa na machozi, yalikuwa maneno yenye kuumiza moyo yaliyotaka moyo wa chuma kukufanya usidondoshe chozi.
Colin hakuwa na la kumuuliza mama yake baada ya kila kitu kuwekwa wazi. Mama yao aliwakusanya na kuwakumbatia wote kisha aliwaachia na kutaka kupiga magoti kuwaomba msamaha lakini walimuwahi mama yao kabla hajapiga.
“Hapana mama huna kosa, bali sisi ndiyo tulikwenda tofauti na mawazo yako, tunaomba utusamehe sana. Ombi letu utupe idhini toka moyoni mwako ili tufunge ndoa yenye baraka,” Colin alimwambia mama yake.
“Mungu ananisikia nimeibariki ndoa yenu duniani na mbinguni.”
“Ma’ mkwe, naomba usinipe zawadi yenye gharama kubwa bali kunipa mume wa ndoto yangu, inawezekana uliponiita mkwe na kunieleza nitaolewa na mwanao anayesoma Ulaya ulidhani utani. Na siku nilipomuona nilichanganyikiwa zaidi, moyoni niliamini nimeokota dhahabu katikati ya soko.
“Lakini niliumia siku nilipojua kumbe kuna chagua sahihi la Colin, kuanguka kwangu si ungonjwa bali presha ilipanda na kushindwa kujizua. Niliamua kujitoa na kukaa pembeni huku nikiwa nimejikatia tamaa. Niliumia zaidi siku Mage alipomshusha Colin kwenye gari na kumdhalilisha kwa kweli japo nilikuwa sipendwi niliingilia ugomvi kwa vile chenye thamani kwenye moyo wangu nikikiona kikidhalilishwa.
“Mpaka leo mama unasema maneno matamu kama haya si kwa urahisi bali nimetoka jasho la damu. Nashukuru mama mkwe, nakuahidi kuwa mke bora na kufurahia chaguo lako la awali.”
Ilikuwa furaha siku hiyo iliagizwa shampeni na kufurahi kutambulika rasmi kwa Cecy katika nyumba ya kina Colin.
****
Mipango ya harusi ya Hans na Mage ilikwenda vizuri, mama Mage hakuwa na haja ya kukusanya tena michango ya sherehe zaidi ya kugawa kadi za send of ya harusi ya mwanaye. Katika watu waliopelekewa kadi ya send of ya Mage ni familia ya mama Colin, tena Mage alisisitiza Colin ahudhulie send of yake.
Taarifa zilifika Colin alikubali kuhudhulia kwa kujua hataumia kwani Cecy alikuwepo.
Siku ya sherehe ya send of Colin na Cecy waliingia wakiwa watu wa mwisho, ilikuwa siku ambayo Cecy aliitafuta kwa udi na uvumba kuwaonesha walimwengu kuwa kila mguu hutulia kwenye kiatu saizi yake wala si kuvaa kikubwa kikakupwaya au kidogo kikakubana lakini kwake kilikuwa kimetulia.
Wakiwa wamependeza Colin katika vazi la shati refu la kitambaa cha maua laini na suruali nyeusi na viatu vyeusi vilivyo chongoka kidogo mbele. Cecy alivaa gauni refu jekundu la mikanda mabegani la kitambaa chepesi na viatu virefu vilivyoongeza mzuri wake.
Waliingia taratibu huku Cecy akiuweka mkono wa Colin kwapani kwake na kuushika kwa mbele. Waliingia taratibu na kufanya watu wote wageuze shingo kuwatazama wapenzi wawili walionekana kama ndiyo wamepata shahada ya mapenzi muda si mrefu.
Mage alishtuka kumwona Colin akiwa amependeza sana akiwa na msichana mrembo ambaye alimsahau kama ndiye aliyempa kipigo siku alipomdhalilisha Colin. Moyo ulimlipuka na kujikuta akiingia wivu, Colin alikuwa na tofauti kubwa na Hans kimuonekana alikuwa ana mvuto kwa mwanamke yoyote.
Lakini mapenzi yake Hans yakuwa makubwa kuliko kitu chochote chini ya jua. Colin pamoja na umbile na sura nzuri lakini kwake moyoni kwake alikuwa na nafasi ndogo.
Naye mke matarajiwa alipendeza katika gauni la kitenge alililoshonwa kwa ustadi mkubwa na kumwongezea urembo wake. Aliamini kabisa msichana aliyechukua nafasi yake alikuwa kama maji ya bahari na yeye, kuvunja uchumba na Colin ilikuwa sawa na kuchota maji kwa kikombe ndani yake na kufanya pengo lake lisionekane kabisa.
Sherehe ilienda vizuri kila mtu aliyekuwepo aliisifia jinsi ilivyofana kwa burudani iliyoandaliwa ilifanya wageni wasichoke kuwepo ukumbuni pale.Katika watu walikuwa na furaha siku ile alikuwa mama Colin baada ya kumwona mwanaye alivyopendeza akiwa na Cecy msichana aliyekuwa kama dhahabu iliyokuwa imechafuliwa na tope lakini mwanaye aliisafisha na thamani yake kuonekana mbele ya macho ya watu.
Itaendelea Jumatatu

Tanzia: Aliyekuwa Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam , Willson Kabwe Afariki Dunia

$
0
0

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Wilson Kabwe ambaye April 19 mwaka huu alisimamishwa kazi na Rais Magufuli amefariki dunia usiku wa kuamkia leo.

Taarifa za kifo chake zimethibitishwa na  Meya wa Jiji la Dar  es Salaam, Isaya Mwita
Kabweamefikwa na mauti  akiwa nchini Indiakwa matibabu. Mungu ailaze mahala pema peponi roho ya marehemu. Amina

Jokate na siri ya mwanaume anayemtesa

$
0
0

Jokate Mwegelo ‘Kidoti’
Stori: Boniphace Ngumije
DIVA anayefanya vizuri kwenye tasnia ya urembo na mitindo Bongo, Jokate Mwegelo amefunguka kuwa ‘drama’ zinazoendelea kuhusu uhusiano wake wa kimapenzi nyingi hazina ukweli na ukweli anao moyoni.
Akipiga stori ‘direct’ na gazeti hili hivi karibuni, Jokate alikiri kuwa ana mpenzi ambaye anampenda sana lakini kwa bahati mbaya mpenzi huyohuyo anamuumiza sana lakini akakataa kumtaja jina alipobanwa na mwanahabari wetu.
“Kiukweli mtu niliyenaye ni sahihi kwangu, ninampenda sana japo na yeye kuna namna fulani ananitesa lakini kiukweli kwake nimefika na Mungu akipenda si muda mrefu watu watamfahamu,” alisema Jokate.
Hata hivyo, miezi ya hivi karibuni Jokate alikuwa akibanjuka kimalovee na Ali Saleh Kiba ‘King Kiba’ ambaye inasemekana wameshamwagana.

TFF YAAMUA KUWEKA MGUU WAKE SUALA LA VURUGU WALIZOFANYIWA YANGA ANGOLA

$
0
0


Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limesema litafanyia uchunguzi tuhuma za Yanga kufanyiwa vurugu nchini Angola ilipokuwa ikicheza na Sagrada Esperanca mechi ya kufuzu hatua ya makundi Kombe la Shirikisho.

Yanga imelalamika kufanyiwa vurugu hizo tangu ilipotua nchini humo katika Jiji la Luanda hadi ilipokuwa mjini Dundo, ambapo walihangaishwa katika usafiri na kuibiwa baadhi ya vifaa vyao.

Pia maofisa wa Esperanca waliwazuia waandishi wa habari wa Tanzania kufanya kazi zao ipasavyo ikiwemo kuwakataza kupiga picha na kuketi sehemu zisizostahili kwa kazi zao.


Hata hivyo, Yanga ilifungwa bao 1-0 na kufanikiwa kutinga hatua ya makundi Kombe la Shirikisho kwani katika mchezo wa awali jijini Dar es Salaam ilishinda mabao 2-0. Imefuzu kwa mabao 2-1.

Katibu Mkuu wa TFF, Selestine Mwesigwa, amesema watakaa na kujadili kile kilichotokea Angola kisha watafanya uchunguzi na kuchukua hatua.

“Kama shirikisho hatukufurahishwa na vitendo walivyofanyiwa Yanga, pia nichukue nafasi hii kuwapongeza kufuatia hatua waliyoifikia,” alisema Mwesigwa.


“Tutakaa na kufanya uchunguzi wa kina juu ya walichofanyiwa Yanga, tukibaini tatizo tutajua tuchukue uamuzi gani juu ya hilo.”

BOBAN, KASEJA MGUU NDANI, MGUU NJE MBEYA CITY, WATASUBIRI UAMUZI WA PHIRI

$
0
0


Kocha wa Mbeya City, Kinnah Phiri, amesema msimu huu amelazimika kuwa na lundo la wachezaji wakongwe kwani aliipokea timu hiyo katikati ya msimu, lakini msimu ujao anataka ‘mafaza’ wasiozidi watatu tu.

Phiri, raia wa Malawi, amesema anataka kujaza wachezaji vijana kikosini mwake msimu ujao akiamini wanaweza kumletea mafanikio.

Kocha huyo wa zamani wa Free States ya Afrika Kusini, amekwenda mbali kwa kusema anataka robo tatu ya kikosi kizima kiwe ni vijana, tofauti na sasa ilivyo na wakongwe hawatazidi watatu.

Mbeya City inayoshika nafasi ya nane katika Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi 34, ina wakongwe kama Juma Kaseja, Them Felix, Hassan Mwasapili, Anthony Kalyesubira, Ramadhan Chombo ‘Redondo’, Haruna Moshi ‘Boban’ na Steven Mazanda.

“Msimu huu nimekuta timu imeshasajili, lakini msimu ujao lazima nisimamie falsafa yangu. Ninataka robo tatu ya kikosi changu kiwe na wachezaji vijana. 

“Nitabaki na wakongwe watatu tu, ila siwezi kuwataja sasa kwa kuwa ligi bado inaendelea, nataka kuwatumia vijana kwani naamini nitafanikiwa nao,” alisema Phiri.

Wakati Phiri akisema hayo, taarifa zinasema Mbeya City ipo katika harakati za kumsajili straika wa Ndanda FC, Atupele Green. Mbeya City kesho Jumapili inamaliza ligi kuu kwa kucheza na Ndanda kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya.

SOURCE: CHAMPIONI

Busu la Penny lazua utata

$
0
0
Busu ambalo mtangazaji Peniel Mungilwa ‘Penny’ amempiga mwigizaji Shamsa Ford limezua utata kufuatia watu kumhusisha na tabia isiyofaa.
Hayo yalijiri hivi karibuni baada ya mtangazaji huyo kutupia picha kwenye Mtandao wa Kijamii wa Instagram ndipo wafuasi wa mtandao huo walipoanza kumsema vibaya wakidai anajiabisha kwa vitendo visivyofaa.
Alipoulizwa kuhusiana na jambo hilo, Penny alisema: “Hayo ni maneno tu huwa hayani sumbui, lile ni busu la kawaida. Nimembusu kama rafiki lakini nawashangaa hao wanaozua mambo yao na kuzungumza tofauti.”


Majina Ya Wanafunzi 1500 Kidato Cha 6 Waliochaguliwa JKT Kambi ya Rwamkoma - Mara

$
0
0
1 NYANKUMBU SECONDARY SCHOOL F ABIGAEL G KISAKA
2 MWANZA SECONDARY SCHOOL F ABIGAEL NICOLOUS GELVAS
3 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F ABIGAEL R SUNGI
4 TINDE GIRLS HIGH SCHOOL F ABIGAEL V KWAI
5 DODOMA SECONDARY SCHOOL F ABIGAELI JOSHUA MAGERE
6 DAKAWA HIGH SCHOOL F ABIJAI MOHAMED ABDALLAH
7 PATRICK MISSION SECONDARY SCHOOL F ABIJEL S MASANIKA
8 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ABIJELI AMOSI LWALI
9 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ABINES ATILIO TOSSI
10 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F ABISHEGI E KYANDO
11 LUSANGA SECONDARY SCHOOL F ABISINA SALIMU
12 UDZUNGWA SECONDARY SCHOOL F ACHESTA GREGORY KIVIKE
13 ST.CHRISTINA GIRL'S SCHOOL F ACHSAH NYAMAGANDA MAGANDA
14 ROSMINI SECONDARY SCHOOL F ACQUINA HIGGINS MASSAWE
15 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F ACQUINAS GEORGE KAZINGO
16 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL F ACRALA ABDALLAH BLANKET
17 MAWENI SECONDARY SCHOOL F ACRINA NGODA
18 MAJENGO SECONDARY SCHOOL F ADABETH CHRISANT KIMWERI
19 KIWELE SECONDARY SCHOOL F ADANI ATHUMAN FUNDI
20 JIKOMBOE SECONDARY SCHOOL F ADELA MASAMAKI
21 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAHATI RASHID
22 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL F BAHATI RICHARD
23 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAHATI SALUMU
24 KIDUGALA LUTHERAN SEMINARY F BAHATI SENGO
25 TUKUYU SECONDARY SCHOOL F BAHATI A MWAMBUNGU
26 TUKUYU SECONDARY SCHOOL F BAHATI ADAMU NGOMALE
27 MAWENI SECONDARY SCHOOL F BAHATI AMANI KASONGWA
28 KIBOSHO GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAHATI AUGUST SHAYO
29 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F BAHATI C MGANGA
30 GREEN BIRD GIRLS' SECONDARY SCHOOL F BAHATI C SIMBA
31 AIRWING SECONDARY SCHOOL F BAHATI CHURCHIL KATWAZA
32 RUVU SECONDARY SCHOOL F BAHATI ELIAS NGALIMOTO
33 COASTAL SECONDARY SCHOOL F BAHATI ERNEST ONESMO
34 KILAKALA SECONDARY SCHOOL F BAHATI FALUHENGA MSAUGE
35 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAHATI H MUSSA
36 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F BAHATI I JUMA
37 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAHATI JAPHET MWANSASU
38 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F BAHATI M KIRABUKO
39 RUVU SECONDARY SCHOOL F BAHATI M KIYEYEU
40 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAHATI M MAKARANGA
41 JIKOMBOE SECONDARY SCHOOL F CAREEN MAMUNONYA MALANDA
42 CANOSSA SECONDARY SCHOOL F CAREEN O MULILO
43 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F CAREEN SEPHANIA SANGA
44 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F CAREEN V VISTUSSI
45 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F CAREEN W MOLLEL
46 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F CAREENMERCY RICHARD KIRIA
47 TAQWA SECONDARY SCHOOL F CAREN JAPHET MALINA
48 ROSMINI SECONDARY SCHOOL F CARENSARAH ROBERT MZOO
49 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL F CARESMA C KILEO
50 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL F CARINE R MAGERE
51 MAKAMBAKO SECONDARY SCHOOL F CARINI CHRISTOPHER MNG'ONG'O
52 MKUU SECONDARY SCHOOL F CARITAS KEMIBALA
53 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL F CARITAS PROSPER
54 MWANZA SECONDARY SCHOOL F CARITAS D KAJUNA
55 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F CARLEN MUKWENDA
56 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL F CARLENE J OPIYO
57 VWAWA SECONDARY SCHOOL F CARLYNE A YOTHAM
58 ANNAGAMAZO SECONDARY SCHOOL F CARMELA C ISDORI
59 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F CAROLA J SWAI
60 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F CAROLINA CHARLES
61 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL F DAINA S KASISI
62 RUGAMBWA SECONDARY SCHOOL F DAINES DIDACE
63 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F DAINES BAHARIA KALINGA
64 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F DAINES LAUREAN MUHIMBA
65 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F DAINES LUDWIKO SANGA
66 LUFILYO SECONDARY SCHOOL F DAINES M MWALYEGO
67 MAHIWA SECONDARY SCHOOL F DAINES MSAFIRI YONAZANWA
68 MRINGA SECONDARY SCHOOL F DAINES P MATU
69 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL F DAINES YONA MWINUKA
70 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F DAINESI DAMASI
71 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL F DAINESS GAUDENCE
72 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F DAINESS D KATTO
73 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F DAINESS EDWARD MMARY
74 SUMVE SECONDARY SCHOOL F DAINESS ELIAS LEMNA
75 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F DAINESS EMMANUEL MOSHI
76 PANDAHILL SECONDARY SCHOOL F DAINESS FESTO CHAULA
77 RUVU SECONDARY SCHOOL F DAINESS KOKUTONA KAIZILEGE
78 URAMBO DAY SECONDARY SCHOOL F DAINESS M MUGETA
79 KAWAWA SECONDARY SCHOOL F DAINESS MANFRED HAULE
80 OSHARA SECONDARY SCHOOL F DAINESS MILKEL MALISA
81 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F EDDAH L MWAISUMBE
82 AHMES SECONDARY SCHOOL F EDDAH MOSES MWANKENJA
83 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F EDDAH S ASWILE
84 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL F EDEFRIDA EMMANUEL
85 TABORA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDELMARIA LONGINO
86 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F EDES M MWAIPOLA
87 PALLOTI GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDIBERATHA ONESMO
88 UDZUNGWA SECONDARY SCHOOL F EDILITRUDA DOMINICK TESHA
89 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F EDILITRUDA NESTORY NYAKI
90 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F EDIMA G TIJE
91 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F EDINA ALOYCE
92 MRINGA SECONDARY SCHOOL F EDINA ELIAS
93 NYANKUMBU SECONDARY SCHOOL F EDINA FRANCIS
94 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F EDINA FRANK
95 NANGWA SECONDARY SCHOOL F EDINA GABRIEL
96 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDINA GEORGE
97 RUVU SECONDARY SCHOOL F EDINA JUSTUS
98 SWILLA SECONDARY SCHOOL F EDINA KANGELE
99 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL F EDINA KANJALE
100 RUHUWIKO SECONDARY SCHOOL F EDINA KAPOMA
101 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F FADHILA FADHILI MSHANA
102 NGANZA SECONDARY SCHOOL F FADHILA HASSAN MTOI
103 BUKOBA SECONDARY SCHOOL F FADHILA HUSSEIN MAPUNDA
104 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL F FADHILA JUMANNE AHMAD
105 ZOGOWALE SECONDARY SCHOOL F FADHILA M BAKARI
106 RUVU SECONDARY SCHOOL F FADHILA M KILANGAZI
107 MWANZA SECONDARY SCHOOL F FADHILA M KILLO
108 NANGWANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F FADHILA M SAIDI
109 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F FADHILA MUSSA ISSA
110 RUVU SECONDARY SCHOOL F FADHILA R MANENTO
111 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F FADHILA RASULI HASSAN
112 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F FADHILA S ALLY
113 NANGWANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F FADHILA S MAULANA
114 CHAMAZI ISLAMIC SEMINARY F FADHILA SAID MSUYA
115 KIFARU SECONDARY SCHOOL F FADHILA Y EMMANUEL
116 LUGALO SECONDARY SCHOOL F FADHILA Z SAID
117 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL F FADHILINA MOHAMEDI
118 BENDEL MEMORIAL SECONDARY SCHOOL F FADHILUNI M MSUYA
119 LONDONI SECONDARY SCHOOL F FADHIRA NELSON SHUKIA
120 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL F FADYA S ALLY
121 LUGOBA SECONDARY SCHOOL F GAUDENSIA M MWALUNGWE
122 LUFILYO SECONDARY SCHOOL F GAUDENSIA RICHARD NGONYANI
123 FARAJA SIHA SEMINARY F GAUDIA AMADEUS KAMAGENGE
124 MRINGA SECONDARY SCHOOL F GAUDIOZA YODOS
125 NGANZA SECONDARY SCHOOL F GAYA MOSHI
126 TLAWI SECONDARY SCHOOL F GEAY T HILONGA
127 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F GELINA MAJILA BUKUKU
128 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F GELWINA LUCIAN
129 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F GEMA BAGUMA
130 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F GEMA SILVANUS
131 KAZIMA SECONDARY SCHOOL F GEMA AGUSTINI MROSSO
132 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F GEMA BERNARD KASONGO
133 KABANGA SECONDARY SCHOOL F GEMA COSMAS JOSEPH
134 NATTA SECONDARY SCHOOL F GEMA E SHAYO
135 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F GEMA ESANJU MUNENDE
136 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F GEMA G SWAI
137 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F GEMA HAMIS MODEST
138 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F GEMA I KIRIA
139 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F GEMA KIMARIO THEODORY
140 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F GEMA L MKUMBATA
141 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F HABIBA RASHID DAUDI
142 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F HABIBA RODE MWOMBEKI
143 MWENDAKULIMA SECONDARY SCHOOL F HABIBA SAID OMARY
144 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F HABIBA SELEMANI MAULIDI
145 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F HABIBA SHABANI SIMA
146 MUDIO ISLAMIC SEMINARY F HABIBA Y MAGANGA
147 LOMWE SECONDARY SCHOOL F HADIA AFUANI MGAYA
148 RUVU SECONDARY SCHOOL F HADIA JOSEPH MSUYA
149 LUGALO SECONDARY SCHOOL F HADIA M SALIM
150 SANGITI SECONDARY SCHOOL F HADIA OMARY ABTWALB
151 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F HADIJA ABDALLAH
152 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F HADIJA ABDALLAH
153 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F HADIJA ABDALRAHMAN
154 UWEMBA SECONDARY SCHOOL F HADIJA ALLY
155 TABORA GIRLS SECONDARY SCHOOL F HADIJA ALLY
156 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F HADIJA ASHIBAE
157 MAWENI SECONDARY SCHOOL F HADIJA AYUBU
158 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F HADIJA BAKARI
159 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F HADIJA FAKI
160 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F HADIJA HALFANI
161 AL-MUNTAZIR ISLAMIC SEMINARY F IFRAH HASSAN NOOR
162 TAQWA SECONDARY SCHOOL F IFTIKAAR MOHAMED AHMED
163 KIZWITE SECONDARY SCHOOL F IGGANILE ROBSON MWAIPAJA
164 MASASI GIRLS SECONDARY SCHOOL F IGNASIA DEUS
165 KIKODI SECONDARY SCHOOL F IGNASIA ABEL NDUNGURU
166 REGINAMUNDI GIRLS' SECONDARY SCHOOL F IGNASIA M MAKUNGANYA
167 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F IGNASIA VALERIAN LYAMUYA
168 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F IKLIMA O ABDALLAH
169 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F IKRA BIKIZO
170 OVERLAND SECONDARY SCHOOL F IKUNDA A MURO
171 NANGWA SECONDARY SCHOOL F IKUNDA JOSEPH SOI
172 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F IKUNDA SALVASTORY MRINA
173 AGAPE LUTHERAN J SEMINARY F IKUNDA WILLIAM SANDI
174 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F IKUPA B OBEL
175 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F IKUPA M NOAH
176 VWAWA SECONDARY SCHOOL F IKUTUSWA L KASHILILIKA
177 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F ILHAM AHMED
178 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F ILHAM M ABASS
179 BONDENI SECONDARY SCHOOL F ILHAM YAHYA HASSAN
180 NYASAKA ISLAMIC SECONDARY SCHOOL F ILHAM YUSUPH WALONGOLE
181 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKLINE BRYSON
182 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F JACKLINE CHARLES
183 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F JACKLINE CHILALA
184 ST.CHRISTINA GIRL'S SCHOOL F JACKLINE CHRISTOPHER
185 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE COPRIANO
186 KAJUMULO ALEXANDER GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKLINE DEUSDEDITH
187 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE DISHON
188 ANNE MARIE SECONDARY SCHOOL F JACKLINE DISMAS
189 KIWELE SECONDARY SCHOOL F JACKLINE DOMINICK
190 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKLINE ELIAS
191 ZOGOWALE SECONDARY SCHOOL F JACKLINE ELIUD
192 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL F JACKLINE ENOCK
193 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F JACKLINE FISSOO
194 TAQWA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE GODFREY
195 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE GODLIZEN
196 RUGAMBWA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE GOZBERTH
197 BARBRO-JOHANSSON SECONDARY SCHOOL F JACKLINE HAMISI
198 SONGE SECONDARY SCHOOL F JACKLINE JACKSON
199 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F JACKLINE JACOB
200 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKLINE JAPHET
201 UDZUNGWA SECONDARY SCHOOL F KALISTA E HENRY
202 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F KALISTA METHOD URIO
203 KAWAWA SECONDARY SCHOOL F KALMELA J MDEMU
204 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F KALUNDE DAUD
205 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F KALUNDE SHABANI
206 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F KALUNDE A MSANGI
207 KABANGA SECONDARY SCHOOL F KALUNDE SADIKI MIRAJ
208 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F KAMALJIT S LUBANA
209 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F KAMBE MARIA KITOSI
210 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F KAMIKAZI MARIUS
211 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL F KAMIRA SAID
212 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F KAMUNDE I HALIFA
213 KAZIMA SECONDARY SCHOOL F KAMWA M MAHOYOGO
214 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL F KANA CHARLES MWABULAMBO
215 MRINGA SECONDARY SCHOOL F KANDIDA NISETASI MARESI
216 NANGWA SECONDARY SCHOOL F KANG''WA WASHIMA
217 KIFARU SECONDARY SCHOOL F KANTI GASPER MEENA
218 BONICONSILI MABAMBA GIRLS SEC.SCHOOL F KANUBHO C BALOKOLA
219 RUGAMBWA SECONDARY SCHOOL F KANYORO J MWARA
220 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F KAPEMBA IDDI KALANDAMYA
221 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL F LAILATH MAYOYOLA
222 BABATI DAY SECONDARY SCHOOL F LAILATU YUSUPH
223 KABANGA SECONDARY SCHOOL F LAINA PHILIPO RAZARY
224 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F LAINES GEORGE KAMBO
225 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL F LAINETH MICHAEL KALENGELA
226 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL F LAIZA HIZA
227 MWANZA SECONDARY SCHOOL F LAMLATH AMRANI MUSSA
228 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL F LANINA H MUNISI
229 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F LARISSA L MAGAMBO
230 ILEJE SECONDARY SCHOOL F LAST JOHNFORD FUNGO
231 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F LATIFA ABDALLAH
232 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F LATIFA ALLI
233 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F LATIFA ALLY
234 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F LATIFA ATHUMAN
235 KIBASILA SECONDARY SCHOOL F LATIFA DILUNGA
236 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F LATIFA HAMISI
237 DAKAWA HIGH SCHOOL F LATIFA HAMZA
238 MSANGENI SECONDARY SCHOOL F LATIFA JUMA
239 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F LATIFA JUMA
240 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F LATIFA MAWAZO
241 VWAWA SECONDARY SCHOOL F MADOVENA RICHARD KATALE
242 BUGENE SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA ALEX
243 RUVU SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA ALEX
244 SUMVE SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA AMON
245 RUGAMBWA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA BONIPHACE
246 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA CHAPANGA
247 HURUMA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA CHARLES
248 BARBRO-JOHANSSON SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA CLEOFACE
249 AILANGA LUTHERAN JUNIOR SEMINARY F MAGDALENA DAVID
250 LORETO GIRLS SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA DEOGRATIUS
251 DAKAWA HIGH SCHOOL F MAGDALENA EDMUND
252 JOHN PAUL II KAHAMA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA EMMANUEL
253 KIZWITE SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA GEORGE
254 JOHN PAUL II KAHAMA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA IZENGO
255 NANGWANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA KAMBARANGWE
256 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F MAGDALENA KOSANA
257 UWEMBA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA LWENJE
258 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA MADALE
259 NGANZA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA MAGAFU
260 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA MAGEMBE
261 KIFUNGILO GIRLS SECONDARY SCHOOL F NADIA SALEH STAMBULI
262 RUVU SECONDARY SCHOOL F NADRA KHAMIS KATIMBA
263 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F NADYA A IBRAHIM
264 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F NADYA B MPANGALA
265 KINONDONI SECONDARY SCHOOL F NADYA S HAMIS
266 WAJA GIRLS SECONDARY SCHOOL F NADYA S SAIDY
267 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAEKU BENJAMIN KIVUYO
268 MARANGU SECONDARY SCHOOL F NAELIJWA ELISA TIMOTHEO
269 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F NAELIJWA F MDUMA
270 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F NAELIJWA WETENGERE KITOJO
271 KIBASILA SECONDARY SCHOOL F NAELY A MBOKA
272 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F NAENDAEL EMMANUEL NIKOMBOLWE
273 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F NAESHERY B MSUYA
274 COASTAL SECONDARY SCHOOL F NAETWE HAMISI
275 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL F NAFISA ALLY ISSA
276 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F NAFSA IDD
277 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAFSA ALLY MCHOME
278 MRINGA SECONDARY SCHOOL F NAGHENJWA JOSEPH MNGARA
279 KIWELE SECONDARY SCHOOL F NAGHENJWA LEONARD MGONJA
280 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAHAMI A MWILENGA
281 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ODILIA KOKWEMAGE MJANDWA
282 MSANGENI SECONDARY SCHOOL F ODILIA MARK HIGILO
283 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F ODINA JACKSON
284 DODOMA SECONDARY SCHOOL F OFRIDA BATHROMEO NDANZI
285 ILEJE SECONDARY SCHOOL F OKOLEWA F KANDONGA
286 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F OKULI ISRAEL SWAI
287 SONGE SECONDARY SCHOOL F OKULI OMBENI JONATHAN
288 MAJENGO SECONDARY SCHOOL F OLDA ELIAS
289 KIZWITE SECONDARY SCHOOL F OLEN ENOCK KIKUNGWE
290 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F OLETH I MADENGE
291 NANGWANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F OLGA LUDGER
292 UWEMBA SECONDARY SCHOOL F OLIDA PETER MGOWOLE
293 KABANGA SECONDARY SCHOOL F OLIETH AGANYIRA BENGESI
294 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F OLIGA ONESMO
295 KIWELE SECONDARY SCHOOL F OLIMPYA ALPHONCE
296 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F OLIPA YUSUPH
297 LUGALO SECONDARY SCHOOL F OLIPA A LWINGA
298 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F OLIPA YOHANA SANGA
299 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F OLIPA Z NYANJE
300 TINDE GIRLS HIGH SCHOOL F OLIPHA ASAPH JONATHAN
301 RUVU SECONDARY SCHOOL F PASCALINA BENY MSIGWA
302 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F PASCALINA H MWAISAKA
303 CHANG'OMBE SECONDARY SCHOOL F PASCALINA J TANGAWIZI
304 DAKAWA HIGH SCHOOL F PASCALINA LUSIMIKO MSUVA
305 SERENGETI DAY SECONDARY SCHOOL F PASCALINA S SARAKIKYA
306 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F PASCARIA ATHANAS CHOROHA
307 ST.CHRISTINA GIRL'S SCHOOL F PASCAZIA J NIBOYE
308 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASCHALIA BONUS MATEKELE
309 LORETO GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASCHALINA CHARLES MUNG'ONYA
310 MWANZA SECONDARY SCHOOL F PASCHALINA CHRISTOPHER BARADIGE
311 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F PASCHALINA CLEMENTINI QAMARA
312 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F PASCHALINA COSTANTIN MALLYA
313 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASCHALINA JOACHIM GWANDU
314 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASCHALINA MICHAEL AMMI
315 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F PASCHALINA P HANGALI
316 DAREDA SECONDARY SCHOOL F PASCHALINA QAFI HOSEA
317 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASCHALINE J NIIMA
318 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASCHAZIA AMOS
319 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL F PASCHAZIA DOMINICK
320 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F PASCHAZIA LEONIDAS
321 KIWELE SECONDARY SCHOOL F QUEEN FELISIAN MALIWA
322 DODOMA SECONDARY SCHOOL F QUEEN FRED MARIKI
323 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F QUEEN GERALD KIMAMBO
324 ARUSHA GIRLS SECONDARY SCHOOL F QUEEN GODWIN MUSHI
325 LONDONI SECONDARY SCHOOL F QUEEN HAMIDU MTEA
326 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F QUEEN IDD MPONDA
327 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F QUEEN JAMES KISOSO
328 JUDE SECONDARY SCHOOL F QUEEN JAPHET KIVUYO
329 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F QUEEN JOHN LAIZER
330 MAWENI SECONDARY SCHOOL F QUEEN JONATHAN LYIMO
331 SANGITI SECONDARY SCHOOL F QUEEN JOSEPH DANIEL
332 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL F QUEEN KAISAL LULAMBO
333 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F QUEEN L MALIWANGA
334 LANGASANI SECONDARY SCHOOL F QUEEN M MATAJIRI
335 TINDE GIRLS HIGH SCHOOL F QUEEN MASSABO KAPONGO
336 CHIEF KIDULILE SECONDARY SCHOOL F QUEEN N MBAWA
337 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F QUEEN OMARY HAULE
338 MASONYA SECONDARY SCHOOL F QUEEN P JOHN
339 CANOSSA SECONDARY SCHOOL F QUEEN S TEMBA
340 JAMHURI SECONDARY SCHOOL F QUEEN SIMON WILLIAM
341 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F RACHEL ESKIA
342 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F RACHEL GIBSON
343 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F RACHEL HALIFA
344 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F RACHEL IKUSA
345 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F RACHEL ITUMBI
346 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F RACHEL JAMES
347 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F RACHEL JOSEPH
348 UCHILE SECONDARY SCHOOL F RACHEL JOSEPH
349 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL F RACHEL KALUNGUBALA
350 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F RACHEL KIMWERI
351 LUFILYO SECONDARY SCHOOL F RACHEL LEORNAD
352 ST.JOSEPH NGARENARO SEC. SCHOOL F RACHEL LUCAS
353 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F RACHEL MASEBO
354 MSALATO SECONDARY SCHOOL F RACHEL MBUNDA
355 MKUGWA SECONDARY SCHOOL F RACHEL MSINGI
356 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F RACHEL MWAMBENE
357 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F RACHEL MWANGOMO
358 MWANZA SECONDARY SCHOOL F RACHEL NJAMAZI
359 SWILLA SECONDARY SCHOOL F RACHEL REGINALD
360 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F RACHEL RENATUS
361 CHANG'OMBE SECONDARY SCHOOL F SABHISMA ATHUMAN
362 MWANZA SECONDARY SCHOOL F SABINA ANDREW
363 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F SABINA ISULULU
364 DODOMA SECONDARY SCHOOL F SABINA JOHN
365 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F SABINA JUMA
366 DAKAWA HIGH SCHOOL F SABINA JUMA
367 LUFILYO SECONDARY SCHOOL F SABINA LAZARO
368 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL F SABINA LEONARD
369 MWENDAKULIMA SECONDARY SCHOOL F SABINA NYAMWEMBE
370 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL F SABINA PHOTUNATUS
371 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F SABINA ZABRON
372 MASASI GIRLS SECONDARY SCHOOL F SABINA ADOLF LANDULILA
373 LUKOLE SECONDARY SCHOOL F SABINA AUGUSTINE MASANJA
374 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL F SABINA CHREANCH MBORO
375 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F SABINA E NADA
376 SONGE SECONDARY SCHOOL F SABINA ISACK LYIMO
377 LORETO GIRLS SECONDARY SCHOOL F SABINA J MASANJA
378 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F SABINA JOHN MALALE
379 DONBOSCO-DIDIA SECONDARY SCHOOL F SABINA K NKWABI
380 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL F SABINA LAURENT NKOSHI
381 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F TABU EDWARD
382 LANGASANI SECONDARY SCHOOL F TABU ELIYA
383 KIWELE SECONDARY SCHOOL F TABU JUMA
384 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F TABU SAIMON
385 MWAMASHIMBA SECONDARY SCHOOL F TABU SHIGELA
386 MANYUNYU SECONDARY SCHOOL F TABU A ALLY
387 LUSANGA SECONDARY SCHOOL F TABU J KAMATA
388 VWAWA SECONDARY SCHOOL F TABU J MSANGAWALE
389 USONGWE SECONDARY SCHOOL F TABU M ANGYELILE
390 SERENGETI DAY SECONDARY SCHOOL F TABU MALICK ALLY
391 NANGWA SECONDARY SCHOOL F TABU MRISHO SHABAN
392 MASASI GIRLS SECONDARY SCHOOL F TABU N NGAYAMA
393 KIWELE SECONDARY SCHOOL F TABU STEPHANO TWEVE
394 SANGU SECONDARY SCHOOL F TABU T MWASHIUYA
395 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F TABULINA D UMBE
396 LUGALO SECONDARY SCHOOL F TAFUTENI CHRISTIAN MAHENGE
397 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F TAHIYA HASHIM MANENO
398 VWAWA SECONDARY SCHOOL F TAINESI A KASEKWA
399 PALLOTI GIRLS SECONDARY SCHOOL F TAJI DAVID HAJI
400 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F TAJI WILE KADEGE
401 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F UMRIKHELI JUMA
402 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F UMUKURUTHUMU MTORO
403 LUSANGA SECONDARY SCHOOL F UNIQUE D MFALAMAGOHA
404 WENDA HIGH SCHOOL F UPENDI S JUMA
405 SWILLA SECONDARY SCHOOL F UPENDO ALEX
406 LUTHERAN JUNIOR SEMINARY F UPENDO DICKSON
407 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F UPENDO EBERT
408 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F UPENDO EDWARD
409 LUSANGA SECONDARY SCHOOL F UPENDO ELSAIMON
410 DAKAWA HIGH SCHOOL F UPENDO HAULE
411 MAWENI SECONDARY SCHOOL F UPENDO HENRY
412 TUKUYU SECONDARY SCHOOL F UPENDO ISSA
413 MAKAMBAKO SECONDARY SCHOOL F UPENDO ISSAKWISA
414 TINDE GIRLS HIGH SCHOOL F UPENDO KIPAIWA
415 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F UPENDO KOPE
416 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL F UPENDO LWINGA
417 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL F UPENDO MACHA
418 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F UPENDO MASENGWA
419 ISIMILA SECONDARY SCHOOL F UPENDO MBUGHI
420 MASASI GIRLS SECONDARY SCHOOL F UPENDO MBWANA
421 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL F VAILETH SAMSON
422 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F VAILETH VALEN
423 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL F VAILETH VEDASTO
424 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F VAILETH ALLEN MLELWA
425 LUBALA SECONDARY SCHOOL F VAILETH ALTEMYUS ALMAS
426 MUYOVOZI SECONDARY SCHOOL F VAILETH B MWAISABILA
427 UDZUNGWA SECONDARY SCHOOL F VAILETH B TWEVE
428 NKASI SECONDARY SCHOOL F VAILETH BAHATI DAUDI
429 IVUMWE SECONDARY SCHOOL F VAILETH BENNY POLEPOLE
430 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F VAILETH BONIFASI SANGA
431 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F VAILETH C KIMOLA
432 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F VAILETH C MROSSO
433 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL F VAILETH C NTINDA
434 KAREMA SECONDARY SCHOOL F VAILETH CLEMENCE LUGONGO
435 LUPALILO SECONDARY SCHOOL F VAILETH FRANCIS HAULE
436 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL F VAILETH FRANK MOSHY
437 VWAWA SECONDARY SCHOOL F VAILETH G ACHIMPOTA
438 KIWELE SECONDARY SCHOOL F VAILETH G DEMBE
439 KIDUGALA LUTHERAN SEMINARY F VAILETH G MSIMINYUNGU
440 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F VAILETH G SIMBA
441 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F WANKEMBETA TIMOTHY
442 SUMVE SECONDARY SCHOOL F WANSEO E SHIUGA
443 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F WANSOLA PAULO
444 IKUNGI SECONDARY SCHOOL F WANSWEKULA LEONARD LYANGA
445 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL F WANZITA GIDAI MLASI
446 TUKUYU SECONDARY SCHOOL F WANZITA JAPHET MSENGI
447 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F WARDA ABDUL
448 MRINGA SECONDARY SCHOOL F WARDA ALLY
449 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F WARDA DACHI
450 KIRINJIKO ISLAMIC SEMINARY F WARDA MOHAMED
451 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F WARDA MUSA
452 RUVU SECONDARY SCHOOL F WARDA SULEIMANI
453 NANGWA SECONDARY SCHOOL F WARDA A KAONEKA
454 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F WARDA A MOHAMED
455 MWIKA SECONDARY SCHOOL F WARDA AYUB IMAM
456 NANGWA SECONDARY SCHOOL F WARDA F MAFTAHA
457 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F WARDA FARAJ ISLAM
458 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL F WARDA H NASSOR
459 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL F WARDA L SWAI
460 ANNAGAMAZO SECONDARY SCHOOL F WARDA MUSTAPHA SANGAWE
461 LONDONI SECONDARY SCHOOL F YASINTA EDWARD PEMBA
462 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F YASINTA ERNEST NGOWI
463 RUVU SECONDARY SCHOOL F YASINTA F ALAY
464 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F YASINTA F RICHARD
465 MBEZI SECONDARY SCHOOL F YASINTA GERVAS GERAZIUS
466 TUKUYU SECONDARY SCHOOL F YASINTA JOSEPH NKYA
467 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F YASINTA K GERVAS
468 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F YASINTA L MAROBO
469 RORYA SECONDARY SCHOOL F YASINTA LAURENCE KISHA
470 LUGALO SECONDARY SCHOOL F YASINTA LAURENT KAVILWA
471 TABORA GIRLS SECONDARY SCHOOL F YASINTA LUDANI MSUYA
472 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F YASINTA MATHIAS BUKWAYA
473 PALLOTI GIRLS SECONDARY SCHOOL F YASINTA MAXIMILLIAN DAMIAN
474 RUVU SECONDARY SCHOOL F YASINTA N PASCHAL
475 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F YASINTA NICODEMAS KENGWA
476 LUGALO SECONDARY SCHOOL F YASINTA OSMUND KUMBURU
477 LUFILYO SECONDARY SCHOOL F YASINTA PASTORY MAHOO
478 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F YASINTA PAUL KIBALI
479 KALIUA SECONDARY SCHOOL F YASINTA PHILIMON MYAMA
480 NKASI SECONDARY SCHOOL F YASINTA S KITAZI
481 RUGAMBWA SECONDARY SCHOOL F ZAIFATH SILAJI
482 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F ZAIFATH ABDULSWAMAD RAMADHAN
483 DAKAWA HIGH SCHOOL F ZAINA HASSAN
484 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA HATIBU
485 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA KAHEMA
486 MASASI GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA RAJABU
487 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA SAID
488 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F ZAINA SAIDI
489 USANGI DAY SECONDARY SCHOOL F ZAINA ABDALAH SHEMWETA
490 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA ATHUMANI MPUME
491 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA B MBELWA
492 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA BASHIRI MCHOME
493 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA DALIKO MLYUKA
494 BUNDA SECONDARY SCHOOL F ZAINA FADHILI ISSA
495 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F ZAINA M MASOUD
496 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA MALIKI ALLY
497 LOMWE SECONDARY SCHOOL F ZAINA MUHUDHARI ALLY
498 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA RASHIDI RAMADHANI
499 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINA YAHAYA RAMADHANI
500 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F ZAINAB AHMED
501 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL M ABDALAH MAFULUKA JUMA
502 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M ABDALAH MAULIDI KUSAHAU
503 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M ABDALAH OMARI KHALIFA
504 KIUMA SECONDARY SCHOOL M ABDALAH S TIKA
505 OCEAN SECONDARY SCHOOL M ABDALAH SAIDI MACHUNJA
506 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M ABDALLA SAID
507 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M ABDALLA SEIF
508 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M ABDALLA HAMISI OMARY
509 CHANG'OMBE SECONDARY SCHOOL M ABDALLA S MPATU
510 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH ABBASI
511 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH AHMED
512 LINDI SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH ASHRAFU
513 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH CHRISTOPHER
514 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH EKENGA
515 KIBITI SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH HAMADI
516 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH HASSAN
517 KIFARU SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH HASSANI
518 MUDIO ISLAMIC SEMINARY M ABDALLAH HILALY
519 AL-HARAMAIN ISLAMIC SEMINARY M ABDALLAH IBRAHIM
520 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH JUMA
521 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH JUMANNE
522 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH KASSIM
523 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH KASSIMU
524 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH MAJIDI
525 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH MBWANA
526 PUGU SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH MKINGIE
527 KIFARU SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH MKOMBOZI
528 EFATHA SEMINARY M ABDALLAH NAJIM
529 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH NASSORO
530 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH NG''ANZI
531 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH OMARY
532 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH RAJAB
533 AZANIA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH RAJABU
534 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M ABDALLAH RASHID
535 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH SAID
536 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH SAIDI
537 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M ABDALLAH SEIFU
538 NDANDA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH SELEMANI
539 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH SHABANI
540 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH SHADRACK
541 PIUS SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH SHOMARY
542 PAMBA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH YUSUPH
543 LINDI SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH A ABDALLAH
544 KWIRO SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH A BANE
545 LINDI SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH A HAMISI
546 NDANDA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH A HEMEDI
547 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH A JUMA
548 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH A KAMBOMBO
549 KIWANJA SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH A SALEH
550 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH ABRAHMAN HUNGU
551 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH ABRAHMANI ALLY
552 IVUMWE SECONDARY SCHOOL M BAHATI MWAMBAKALE
553 OSWARD MANG'OMBE S S M BAHATI PAUL
554 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M BAHATI PETER
555 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M BAHATI SAMSON
556 UMBWE SECONDARY SCHOOL M BAHATI SEURI
557 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M BAHATI TATILA
558 MINAKI SECONDARY SCHOOL M BAHATI VEDASTUS
559 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M BAHATI VICENT
560 DODOMA SECONDARY SCHOOL M BAHATI ANATORY JACOB
561 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M BAHATI B FAUSTINE
562 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M BAHATI B KIDESELA
563 BOGWE SECONDARY SCHOOL M BAHATI B MWENDESHA
564 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M BAHATI BENNY MWANDESILE
565 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M BAHATI C MWASENGA
566 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M BAHATI E MANG'ATI
567 CHOME SECONDARY SCHOOL M BAHATI E VICENT
568 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M BAHATI ELIA SAMWELI
569 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M BAHATI EUSTACK NYAMBO
570 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M BAHATI G KIDUMBA
571 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL M BAHATI HUMFREY DENYA
572 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M BAHATI ISDORI CHIWANGU
573 KIBITI SECONDARY SCHOOL M BAHATI JAMES MWAIJENGO
574 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M BAHATI JOEL CHATANDA
575 IWAWA SECONDARY SCHOOL M BAHATI JOHN KOMBA
576 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M BAHATI M BUGONDO
577 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M BAHATI M BUJIKU
578 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M BAHATI M LILANGA
579 KIGONIGONI SECONDARY SCHOOL M BAHATI M MIANO
580 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M BAHATI M SALUM
581 KIWANJA SECONDARY SCHOOL M BAHATI M TULEMBUKE
582 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M BAHATI M YOMBO
583 TARIME SECONDARY SCHOOL M BAHATI MARWA THOMAS
584 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M BAHATI N KYANDO
585 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M BAHATI N LIGWA
586 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M BAHATI N TWINZI
587 META SECONDARY SCHOOL M BAHATI PHILIMON MTELEKE
588 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M BAHATI R MWEMBE
589 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M BAHATI RASHIDI NOELY
590 MZUMBE SECONDARY SCHOOL M BAHATI S GAMAYA
591 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL M BAHATI S MZOPOLA
592 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M BAHATI SAMWEL CHACHA
593 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M BAHATI SAMWEL MBUKO
594 MADABA SECONDARY SCHOOL M BAHATI SEDY SANGA
595 KIDUGALA LUTHERAN SEMINARY M BAHATI STEPHANO MFUGALE
596 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M BAHATI T BUSANUKA
597 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M BAHATI THOMAS SEBASTIAN
598 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M BAHATI TUNGU KABULI
599 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M BAHATI W MALIMOJA
600 BONDENI SECONDARY SCHOOL M BAHATI Y SELEMANI
601 OSWARD MANG'OMBE S S M BAHATI Z BADILI
602 MKOLANI SECONDARY SCHOOL M BAHINGAI IDD
603 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M BAHINI SENI
604 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M BAHTI H MWALEMBE
605 BIHARAMULO SECONDARY SCHOOL M BAILON M ANACLET
606 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M BAIRES NAFTARY MCHAPE
607 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M BAKARI ABDALA
608 NYERERE SECONDARY SCHOOL M CAROLI ROBERT
609 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M CASBERT CHALE
610 MZUMBE SECONDARY SCHOOL M CASIAN NORMAN MTULUWA
611 MBALIZI SECONDARY SCHOOL M CASMIR JACOB LUPEKE
612 MARANGU SECONDARY SCHOOL M CASMIR VALERIAN MBORE
613 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CASMIRY BENEDICT CASMIRY
614 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CASSIAN G MHUZA
615 TARIME SECONDARY SCHOOL M CAST ONESPHORY
616 SWILLA SECONDARY SCHOOL M CASTO MALYONGA
617 SWILLA SECONDARY SCHOOL M CASTO TIGER
618 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M CASTOR AMAN
619 MOSHI SECONDARY SCHOOL M CASTOR BONIFACE
620 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M CASTOR MAGNUS
621 ILBORU SECONDARY SCHOOL M CASTOR CASPAR UHAHULA
622 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M CASTOR F MUSHUMBUSI
623 ILULA SECONDARY SCHOOL M CASTOR JOACHIM MOYO
624 KWIRO SECONDARY SCHOOL M CASTOR JOHN MSAGE
625 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M CASTOR LEOPOLD NGAILO
626 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M CASTORY ELIASI
627 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CASTORY LAURENT
628 MZUMBE SECONDARY SCHOOL M CASTORY LUOGA
629 TAQWA SECONDARY SCHOOL M CASTORY MAGANGA
630 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M CASTORY B SOSOMA
631 TARIME SECONDARY SCHOOL M CASTORY C MTEGA
632 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M CASTORY EVARISTO KITWE
633 MZUMBE SECONDARY SCHOOL M CASTORY G MUNISHI
634 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M CASTORY M ANDREW
635 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M CASTORY M LAURENT
636 KASITA SEMINARY M CASTORY VENANCE LIKOMO
637 HUMURA SECONDARY SCHOOL M CASTROL EZEKIEL
638 MOSHI SECONDARY SCHOOL M CATHBERT MASHAURI
639 ALPHA SECONDARY SCHOOL M CATHBERT FREDRICK KISAKA
640 KYELA SECONDARY SCHOOL M CATHBERT J NDWANGA
641 ILBORU SECONDARY SCHOOL M CATHBERT L MUGISA
642 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M CATHBERTH CHIKOKO ATHANAS
643 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M CATHBET O SAMILA
644 MOSHI SECONDARY SCHOOL M CATHBETH ELIAMANI KIMARO
645 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M CATHBETH SOLOMON HAULE
646 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M CATHIBERT MUJUNI GEORGE
647 KATE SECONDARY SCHOOL M CATUS FRUGENCE
648 AHMES SECONDARY SCHOOL M CAVIN COMFORT
649 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CECIL G MSONDE
650 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M CEDRICK A NYENZI
651 MINAKI SECONDARY SCHOOL M CELESTIN KAMUGISHA
652 MINAKI SECONDARY SCHOOL M CELESTINE LUNYILIJA
653 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M CELESTINE MICHAELI
654 NYEGEZI SEMINARY M CELESTINE MAYUNGA NYAKAMO
655 SWILLA SECONDARY SCHOOL M CELIS GENES KIMARIO
656 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M CERLIVIN C PALLANGYO
657 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M CHACHA ATTORNEY
658 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M CHACHA CHACHA
659 MOSHI SECONDARY SCHOOL M CHACHA ISAYA
660 IKIZU SECONDARY SCHOOL M CHACHA ISSACK
661 MAGU SECONDARY SCHOOL M CHACHA JOHN
662 NKASI SECONDARY SCHOOL M CHACHA JOSEPH
663 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M CHACHA JULIUS
664 MOSHI SECONDARY SCHOOL M CHACHA JUMA
665 BIHARAMULO SECONDARY SCHOOL M DAMIAN PAUL
666 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M DAMIAN SAID
667 KIWANJA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN A NDOINE
668 SALESIAN SEMINARY M DAMIAN ALCKADO MTANDUZI
669 NTUNDURU SECONDARY SCHOOL M DAMIAN ALEX CORNEL
670 MWANZA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN C MDALAMLA
671 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M DAMIAN CALIST SWAI
672 SAME SECONDARY SCHOOL M DAMIAN DICKSON MLONGWA
673 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN E MSOKWA
674 UWATA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN EVARIST NDASI
675 ILEJE SECONDARY SCHOOL M DAMIAN FESTUS KINOGAMUNI
676 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M DAMIAN IKO MAJUVA
677 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M DAMIAN J KAHAMBA
678 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M DAMIAN JOSEPH MACHA
679 ILBORU SECONDARY SCHOOL M DAMIAN MOHAMED MARARE
680 KONGWA SECONDARY SCHOOL M DAMIANO CHRISTOPHER
681 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M DAMIANO RAPHAEL
682 MAWENI SECONDARY SCHOOL M DAMIANO SAFARI
683 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M DAMIANO DEONATH GIDARBU
684 SAME SECONDARY SCHOOL M DAMIANO E NOGA
685 MOSHI SECONDARY SCHOOL M DAMIANO KASTULI PETER
686 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M DAMIANO NESPHOT FRANCIS
687 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M DAMIANO NOEL CHRIZOSTOM
688 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M DAMIANO P AMMA
689 KARATU SECONDARY SCHOOL M DAMIANO P KIRWAY
690 KIBITI SECONDARY SCHOOL M DAMIANO S NG''AYDA
691 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M DAMIANO SELEJIO DAMIANO
692 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M DAMIANO TARMO AMMO
693 CHATO SECONDARY SCHOOL M DAMITIRIUS BARNABAS
694 SUMBAWANGA SECONDARY SCHOOL M DAMSON BAHATI
695 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M DAN E GWAMAKA
696 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M DANCAN SHEM
697 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M DANCAN ANACLET LUCIAN
698 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M DANFORD ELIABU
699 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M DANFORD JOSEPH
700 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M DANFORD ATHANAS CHING'OLE
701 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M DANFORD BALINZIGO JONAS
702 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M DANFORD DOUGLAS SULEIMAN
703 KAWAWA SECONDARY SCHOOL M DANFORD EDWARD MWINUKA
704 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M DANFORD ERNEST NG''UMBI
705 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M DANFORD LAURENCE MAKUNDI
706 PUGU SECONDARY SCHOOL M DANFORD M ALLY
707 MWANGA SECONDARY SCHOOL M DANFOS YOAZA SADIKIEL
708 EFATHA SEMINARY M DANGALIRA PATRICK ALMAS
709 SAME SECONDARY SCHOOL M DANI A NGAYONGA
710 META SECONDARY SCHOOL M DANI DANIEL MWANSAMALE
711 KIFARU SECONDARY SCHOOL M DANI ERASTO KITUNDA
712 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M DANI J SIMKONDA
713 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL M DANI WILLIAM ELIONA
714 RUTABO SECONDARY SCHOOL M DANICE MHOJA JOHN
715 NDANDA SECONDARY SCHOOL M DANIEL ALBETUS
716 UWATA SECONDARY SCHOOL M DANIEL ALOIS
717 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M DANIEL AMANYISYE
718 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M DANIEL AWESTONE
719 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M DANIEL AYOUB
720 NDANDA SECONDARY SCHOOL M EDGAR SAIDI
721 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M EDGAR SIMBA
722 WENDA HIGH SCHOOL M EDGAR A MWAMPOMA
723 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M EDGAR ANTON RWAMUHURU
724 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M EDGAR B MLOWE
725 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL M EDGAR BOSCO MISSINGO
726 ILBORU SECONDARY SCHOOL M EDGAR D MPANGILE
727 MINAKI SECONDARY SCHOOL M EDGAR E MALYA
728 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M EDGAR E MASHAGA
729 MALECELA SECONDARY SCHOOL M EDGAR EGID NGAGA
730 MLIMA MBEYA HIGH SCHOOL M EDGAR F TEMIGUNGA
731 KAWAWA SECONDARY SCHOOL M EDGAR FEDRICK SANGA
732 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M EDGAR HELBERT ALFRED
733 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M EDGAR K ALLY
734 IMBORU SECONDARY SCHOOL M EDGAR LEONARD LEKULE
735 LUBALA SECONDARY SCHOOL M EDGAR LUGANO PWELE
736 KASULU SECONDARY SCHOOL M EDGAR MISIGARO ANDREA
737 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M EDGAR O MTEMANYONGO
738 META SECONDARY SCHOOL M EDGAR OMARY SALEHE
739 UMBWE SECONDARY SCHOOL M EDGAR RICHARD PETER
740 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EDGAR SIMON MWASILE
741 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M EDGAR VINTAN HAULE
742 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M EDGAR ZACHARIA SANJA
743 RUTABO SECONDARY SCHOOL M EDGER BUGANGA
744 UWATA SECONDARY SCHOOL M EDGER ELIAS
745 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M EDGER GUDULE
746 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M EDGER KAMWELA
747 META SECONDARY SCHOOL M EDGER A PONERA
748 NDANDA SECONDARY SCHOOL M EDGER ALOYCE KISUSANGE
749 MINAKI SECONDARY SCHOOL M EDGER ALOYCE NG'UMBI
750 IWAWA SECONDARY SCHOOL M EDGER GODWIN SANGA
751 LUBALA SECONDARY SCHOOL M EDGER LAURENT MWAMBINGAMA
752 SAME SECONDARY SCHOOL M EDGER P MASIGE
753 MWINYI SECONDARY SCHOOL M EDGER PETRO COSMAS
754 IMBORU SECONDARY SCHOOL M EDIBERTH A MISQU
755 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M EDIBIL JORAM
756 TAQWA SECONDARY SCHOOL M EDIBIL DAMAS KINAMA
757 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M EDIBILI EMMANUEL SHUMBU
758 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M EDIBILI K EDWIN
759 PIUS SECONDARY SCHOOL M EDIBILY EGBERT KABYAZI
760 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M EDIBILY LIVINGSTONE STANSLAUS
761 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EDICKO STANLEY NGUVILA
762 BOGWE SECONDARY SCHOOL M EDIEL EXAVERY BULINTYO
763 IWAWA SECONDARY SCHOOL M EDIFASTA ALBERTO MDETELE
764 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M EDIFORCE SIMON BIRUSHA
765 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M EDIGA JAMES
766 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M EDIGA BENISON KAMINYOGE
767 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M EDIGA KAWISHE JASTINE
768 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M FADHIL BENEDICTO
769 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M FADHIL MASOSI
770 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M FADHIL MOHAMED
771 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M FADHIL SALUM
772 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M FADHIL SHILELEMA
773 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M FADHIL AWADHI MSAGATI
774 KISIWANI SECONDARY SCHOOL M FADHIL J MWAMI
775 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M FADHIL KAZUMARI NANYAMBE
776 META SECONDARY SCHOOL M FADHIL M ADAMSON
777 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M FADHIL M MUSSA
778 KIRINJIKO ISLAMIC SEMINARY M FADHIL OMAR BAKARI
779 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M FADHIL S JOHN
780 CHIEF KIDULILE SECONDARY SCHOOL M FADHIL S MWALINDU
781 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M FADHIL S NAMWAMBE
782 MASJID QUBAH MUSLIM SEMINARY M FADHIL SAIDI JUMA
783 MBEYA SECONDARY SCHOOL M FADHILI AUGUSTINO
784 KIGWE SECONDARY SCHOOL M FADHILI BINAMU
785 MWINYI SECONDARY SCHOOL M FADHILI DANIEL
786 SADANI SECONDARY SCHOOL M FADHILI DAVID
787 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M FADHILI DISHON
788 GEITA SECONDARY SCHOOL M FADHILI EDWARD
789 META SECONDARY SCHOOL M FADHILI ELIAS
790 MTWARA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M FADHILI FABIAN
791 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M FADHILI FREDRICK
792 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL M FADHILI IBRAHIM
793 AZANIA SECONDARY SCHOOL M FADHILI ISMAIL
794 LUBALA SECONDARY SCHOOL M FADHILI JULIUS
795 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M FADHILI MOHAMED
796 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M FADHILI MUSA
797 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M FADHILI MWAMINI
798 LINDI SECONDARY SCHOOL M FADHILI NAMADENGWA
799 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M FADHILI NZUNDA
800 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M FADHILI OSSEA
801 SANGU SECONDARY SCHOOL M FADHILI RAMADHANI
802 TAQWA SECONDARY SCHOOL M FADHILI RAMADHANI
803 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M FADHILI SANGA
804 OCEAN SECONDARY SCHOOL M FADHILI SELEMANI
805 MKUU SECONDARY SCHOOL M FADHILI SHAO
806 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M FADHILI STUWART
807 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M FADHILI WAZIRI
808 LUBALA SECONDARY SCHOOL M FADHILI WILLIAM
809 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M FADHILI YUSUPH
810 UWATA SECONDARY SCHOOL M FADHILI A CHOMO
811 KIWANJA SECONDARY SCHOOL M FADHILI A URIO
812 KIDUGALA LUTHERAN SEMINARY M FADHILI ADACK ELIOTH
813 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M FADHILI AMOSI SEKIETE
814 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M FADHILI B MWANGUO
815 NORTHERN HIGHLANDS SECONDARY SCHOOL M GABRIEL JOSEPH NGERO
816 KIBITI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL JOSHUA GESOGWE
817 KWIRO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL K LUBAZU
818 SAME SECONDARY SCHOOL M GABRIEL KOMBE VENANCE
819 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M GABRIEL L MWAITELEKE
820 MKUU SECONDARY SCHOOL M GABRIEL LEKEY CHARLES
821 IMBORU SECONDARY SCHOOL M GABRIEL M ADAA
822 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL M DAGNO
823 NDANDA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL M MWITA
824 NYERERE SECONDARY SCHOOL M GABRIEL M RYOBA
825 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL MACXENSIUS MAGOGWA
826 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL MAKOYE BULUBA
827 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL MANDAGO MASHAURI
828 KIRINJIKO ISLAMIC SEMINARY M GABRIEL MARISA SALIM
829 SHAURITANGA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL MOSHIRO COLMAN
830 NDANDA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL N KITOMARI
831 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M GABRIEL N SANGA
832 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL NDUMINIFOO ANAUFO
833 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M GABRIEL PATRICK LWESYA
834 ST. MARY'S DULUTI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL PAUL LYIMO
835 MAFINGA SEMINARY M GABRIEL PHILIBERT MAYOYA
836 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL POUL MYUGUYE
837 MBEZI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL R SILUNGWE
838 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL RICHARD MTAFYA
839 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL S NASHON
840 AIRWING SECONDARY SCHOOL M GABRIEL U MELKIORY
841 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL V TARIMO
842 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M GABRIEL WILLIAM KIDAVA
843 LINDI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL Z LULANDALA
844 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL ZACHARIA COSMAS
845 SUJI SECONDARY SCHOOL M GABRIELI ELIAMINI MSHIGHENI
846 MBEZI SECONDARY SCHOOL M GABRIELY FREDY
847 NGUDU SECONDARY SCHOOL M GABRIELY J DWASI
848 KIGURUNYEMBE SECONDARY SCHOOL M GABRIELY NICHOLAUS NKANULIYE
849 OCEAN SECONDARY SCHOOL M GADAFI ATHUMANI
850 ILULA SECONDARY SCHOOL M GADI P GADI
851 KARATU SECONDARY SCHOOL M GADIEL EPHRAIM
852 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M GADIEL MAWA
853 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M GADIEL MSAFIRI
854 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M GADIEL P MHANDAGANI
855 UMBWE SECONDARY SCHOOL M GADIEL RAPHAEL MGHASE
856 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M GADSON AMON
857 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M GADSON BUHILI
858 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M GAFRID PATRICK MWENDA
859 TARIME SECONDARY SCHOOL M GAGA NINDWA GAGA
860 IWAWA SECONDARY SCHOOL M GAIN T GABRIEL
861 MIONO SECONDARY SCHOOL M GAITAN PIUS NGUNDA
862 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL M GALIYAYA NG'HUMBI
863 KABANGA SECONDARY SCHOOL M GALUMA SAYI CHARLES
864 TARIME SECONDARY SCHOOL M GALUS ALFRED
865 MINAKI SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI S OMARY
866 LINDI SECONDARY SCHOOL M HAFIDHU H MKUMBI
867 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M HAFIDHU MAYANJA RAMADHAN
868 MWANZA SECONDARY SCHOOL M HAGAI ANANIA
869 USEVYA SECONDARY SCHOOL M HAGAI CHRISTOPHER
870 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M HAGAI ESKAKA
871 SANGU SECONDARY SCHOOL M HAGAI ASEGELILE MWANDAMPAPA
872 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M HAGAI E KULANGA
873 MORINGE SOKOINE SECONDARY SCHOOL M HAGAI EMANUEL MASSAWE
874 SANGU SECONDARY SCHOOL M HAGAI J MUNNA
875 ILEJE SECONDARY SCHOOL M HAGAI J MWAKIPOSA
876 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M HAGAI S SWILLA
877 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL M HAGGAI EMMANUEL MBOGO
878 VUDOI SECONDARY SCHOOL M HAIDALLY YASSIN MUSTAPHA
879 NDANDA SECONDARY SCHOOL M HAIDARI ATHUMANI
880 KIFARU SECONDARY SCHOOL M HAIDARY ABUBAKARI
881 EAGLES SECONDARY SCHOOL M HAIDERY W SHANGO
882 TAQWA SECONDARY SCHOOL M HAIDIDI H JUMA
883 NYASAKA ISLAMIC SECONDARY SCHOOL M HAIKAR A MOHAMED
884 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M HAJI ABDALLAH
885 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M HAJI ABDI
886 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M HAJI BAKARI
887 KIBITI SECONDARY SCHOOL M HAJI ISSA
888 AZANIA SECONDARY SCHOOL M HAJI KATUNDU
889 GOLDEN RIDGE SECONDARY SCHOOL M HAJI MASOUD
890 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M HAJI MRUGA
891 NGUDU SECONDARY SCHOOL M HAJI SALIMU
892 UWATA SECONDARY SCHOOL M HAJI SHEMHILU
893 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M HAJI SULEIMAN
894 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M HAJI A CHINYAPI
895 AZANIA SECONDARY SCHOOL M HAJI A KAWEME
896 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M HAJI ALLY KILASI
897 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M HAJI DAMSON MHESI
898 IVUMWE SECONDARY SCHOOL M HAJI H KOMUNGOMA
899 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M HAJI H KUBYO
900 NDANDA SECONDARY SCHOOL M HAJI H NACHUNDU
901 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M HAJI H SAID
902 MAWENI SECONDARY SCHOOL M HAJI HAMADI HAJI
903 OCEAN SECONDARY SCHOOL M HAJI HASSAN SULEIMAN
904 SINGE SECONDARY SCHOOL M HAJI I OMARY
905 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M HAJI IDDI PIRU
906 KISIWANI SECONDARY SCHOOL M HAJI ISSA TWAHIRI
907 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M HAJI J MAVIRO
908 BENDEL MEMORIAL SECONDARY SCHOOL M HAJI JAMES TASINGA
909 EAGLES SECONDARY SCHOOL M HAJI JUMA MANKA
910 SANGU SECONDARY SCHOOL M HAJI M MALEMA
911 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M HAJI MIRAR HAJI
912 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M HAJI MUSA NYANGWA
913 PUGU SECONDARY SCHOOL M HAJI NYIRENDA YUSUFU
914 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M HAJI OMARY MHANGA
915 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MWINYIMKUU
916 KAWAWA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MYOVELLA
917 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM NCHAGWA
918 NDANDA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM SHABANI
919 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M IBRAHIM YUSSUF
920 AZANIA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM A IDRISA
921 EFATHA SEMINARY M IBRAHIM A MAGOGO
922 MBEYA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM A MBONDE
923 MBEZI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM A MOHAMED
924 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ABBAS DUMA
925 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ABDULKARIM HASSAN
926 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ABDULLAHI MKOJERA
927 GEITA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM AHMAD ABDALLAH
928 KIRINJIKO ISLAMIC SEMINARY M IBRAHIM ALLY MWINGE
929 LILIAN KIBO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ALOYCE MATEMU
930 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM AZIZI KIWANGA
931 FOREST HILL SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM B MATANJI
932 MINAKI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM BAKARI JUMA
933 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM C ANDREA
934 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM C MADINDA
935 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM D SABAYAYA
936 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM DITRICK MWINUKA
937 KISARIKA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM E MMARY
938 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ELIBARIKI MCHARO
939 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM F MPAHARE
940 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM F NDELWA
941 ST.PETER'S SEMINARY M IBRAHIM F TEMBO
942 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM G KAISI
943 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM G MWAKASOLA
944 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM GERSON NGULWA
945 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM GERVAS MAHALI
946 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM H MNYINGA
947 GEITA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM H NGAMIKO
948 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM H NGELO
949 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM HAFIDH CHAMBUSO
950 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM HAMIS LEKULE
951 SWILLA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM HAMIS PONERA
952 PUGU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM HAMZA IBRAHIM
953 AL-HARAMAIN ISLAMIC SEMINARY M IBRAHIM HAMZA RAMADHANI
954 LOYOLA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM I MGONZA
955 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM I MKUVALWA
956 KAWAWA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM IBRAHIM NDELWA
957 KIBITI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM IDDI JUKU
958 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ILIYASA NGWADA
959 ILBORU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM IRENEUS MAUKI
960 RIDHWAA SEMINARY M IBRAHIM ISMAIL MOHAMED
961 CHANGARAWE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ISMAIL RAJABU
962 MUYOVOZI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM J CHENZA
963 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M IBRAHIM J MSHIHIRI
964 UJIJI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM J MWAPINA
965 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM J PETER
966 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM J YUSUPH
967 BENDEL MEMORIAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON KENETH
968 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M JACKSON KIPETA
969 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON KITEGE
970 NKASI SECONDARY SCHOOL M JACKSON LEOPORD
971 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON LUFUNDISHA
972 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M JACKSON LUGATA
973 PUGU SECONDARY SCHOOL M JACKSON MAGOBE
974 KISIWANI SECONDARY SCHOOL M JACKSON MAGUNDULA
975 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M JACKSON MAHUVE
976 KABANGA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MAKARIUS
977 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON MANHE
978 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MARCO
979 PUGU SECONDARY SCHOOL M JACKSON MATINDE
980 LINDI SECONDARY SCHOOL M JACKSON MATITU
981 ST.MAURUS CHEMCHEMI SECONDARY SCHOOL M JACKSON MATOSHA
982 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MAYUNGA
983 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M JACKSON MBONEA
984 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MBUNI
985 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MILLES
986 USEVYA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MUSSA
987 SUMBAWANGA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MWANAKULYA
988 NKASI SECONDARY SCHOOL M JACKSON MWOPOLE
989 OCEAN SECONDARY SCHOOL M JACKSON NGOCHELO
990 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M JACKSON NIKUMWITIKA
991 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M JACKSON OBULA
992 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON PASCHAL
993 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M JACKSON PATRICK
994 NDANDA SECONDARY SCHOOL M JACKSON PAUL
995 MAWENI SECONDARY SCHOOL M JACKSON PHARES
996 KABANGA SECONDARY SCHOOL M JACKSON PROJESTUS
997 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M JACKSON RICHARD
998 ALPHA SECONDARY SCHOOL M JACKSON RICHARD
999 OSWARD MANG'OMBE S S M JACKSON RICHARD
1000 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M JACKSON ROGASIAN
1001 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M JACKSON SALUSTIAN
1002 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M JACKSON SANINGA
1003 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M JACKSON SEBASTIAN
1004 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M JACKSON SIMITI
1005 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M JACKSON SIMKOKO
1006 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M JACKSON VALENCE
1007 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M JACKSON WARYOBA
1008 GREEN BIRD BOYS SECONDARY SCHOOL M JACKSON WILLIUM
1009 MWIKA SECONDARY SCHOOL M JACKSON YOHANA
1010 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON A KIHUNDWA
1011 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M JACKSON A KISWESWE
1012 NYERERE SECONDARY SCHOOL M JACKSON A MALEKO
1013 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M JACKSON ADAM KWEBA
1014 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL M JACKSON AGUST KILAWE
1015 MINAKI SECONDARY SCHOOL M JACKSON ALLY MKUBWA
1016 MIONO SECONDARY SCHOOL M JACKSON ALOIS MGALILWA
1017 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M JACKSON ALPHONCE JACKSON
1018 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M JACKSON AMINI SWAI
1019 MAHENJE SEC SCHOOL M JACKSON ANJELIKA MLULA
1020 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M JACKSON ANTHON KAYANDA
1021 NGUDU SECONDARY SCHOOL M KAJANJA MBWANA
1022 UMBWE SECONDARY SCHOOL M KAJELI DEUSDEDITH MAGAFU
1023 KARATU SECONDARY SCHOOL M KAJENTAN TARIMO MJEURI
1024 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M KAJIVO AIDAN
1025 LUGUFU BOYS SECONDARY M KAJUNA B MAYANJA
1026 OSWARD MANG'OMBE S S M KAJURA ISRAEL MAFURU
1027 NDANDA SECONDARY SCHOOL M KAKULU CLEOPHACE KAJUJU
1028 MARIADO SECONDARY SCHOOL M KAKWAYA JOHN
1029 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M KALAGALA KAPUNDA
1030 NDANDA SECONDARY SCHOOL M KALEB CLEMENT
1031 PARANE SECONDARY SCHOOL M KALEB EXAUD
1032 MAMBWE SECONDARY SCHOOL M KALEB SIMON
1033 FARAJA SIHA SEMINARY M KALEB N AMBAKISYE
1034 META SECONDARY SCHOOL M KALEBU MADEUS
1035 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M KALEBU SAIDI
1036 CHANGARAWE SECONDARY SCHOOL M KALEBU CHELESTINO MTATE
1037 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M KALEBU DANIEL KISOSO
1038 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M KALEBU GODBLESS NDEMWELI
1039 MUYOVOZI SECONDARY SCHOOL M KALEBU JUSTINE CHUWA
1040 ILEJE SECONDARY SCHOOL M KALEBU VENANCE PILLA
1041 CHATO SECONDARY SCHOOL M KALEKWA MAMBO MASUD
1042 NYAMPULUKANO SECONDARY SCHOOL M KALEMELA KWILASA
1043 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M KALERO MAGOTI
1044 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M KALIKUMTIMA KAHITIRA MAGANYA
1045 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M KALIMANZIRA ARAMU
1046 MINAKI SECONDARY SCHOOL M KALOLO CLEOPHAS
1047 NDANDA SECONDARY SCHOOL M KALOLO G KISANGA
1048 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M KALSON KAISARY KIDENYA
1049 BUNDA SECONDARY SCHOOL M KALUMBILO THOMAS
1050 LAKE SECONDARY SCHOOL M KALUMBILO ANATORY KASUMBI
1051 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M KALUNGURU GODIANI MLULA
1052 MWANGA SECONDARY SCHOOL M KALUSE GADIEL LUKIO
1053 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M KAMAL M SLIM
1054 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M KAMALI NUNI ISSA
1055 UMBWE SECONDARY SCHOOL M KAMARA RICHARD
1056 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M KAMARUDIN TWALIB
1057 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M KAMBA LUBINZA
1058 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M KAMBAULAYA NKANDA
1059 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M KAMBONA V KAMBONA
1060 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M KAMBONESA PETER
1061 BUNDA SECONDARY SCHOOL M KAMEJA MAGANGA
1062 KYELA SECONDARY SCHOOL M KAMGISHA ANATORY
1063 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M KAMIL PROSPER MLINGI
1064 MKUU SECONDARY SCHOOL M KAMILI ALOYCE NYAKI
1065 MAUA SEMINARY M KAMILI T ASSEY
1066 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M KAMILIUS CHAWAKA
1067 SWILLA SECONDARY SCHOOL M KAMILO AUGUSTINE KAMATARE
1068 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M KAMKA M BUKELEBE
1069 TAQWA SECONDARY SCHOOL M KAMUGISHA RWAKIBIBI
1070 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M KAMULI DOMINICK
1071 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M KAMULI LUCAS
1072 MAGU SECONDARY SCHOOL M KAMULI SHIJA
1073 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M KAMULI SHINDIKA
1074 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M LAMECK JUSTO
1075 MOSHI SECONDARY SCHOOL M LAMECK KIJA
1076 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M LAMECK LIHWEULI
1077 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M LAMECK LUCHAGULA
1078 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M LAMECK LUDOVICK
1079 BIHARAMULO SECONDARY SCHOOL M LAMECK MADATA
1080 MBEZI SECONDARY SCHOOL M LAMECK MALEKELA
1081 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M LAMECK MILEKA
1082 CHATO SECONDARY SCHOOL M LAMECK MOI
1083 HIGHLANDS SECONDARY SCHOOL M LAMECK MWENDELE
1084 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL M LAMECK OKEYO
1085 OSWARD MANG'OMBE S S M LAMECK ONESMO
1086 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M LAMECK POTENTINE
1087 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M LAMECK RESPICIUS
1088 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M LAMECK RUGAIMUKAMU
1089 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M LAMECK SHABAN
1090 RUTABO SECONDARY SCHOOL M LAMECK SOSTENESS
1091 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M LAMECK STEPHEN
1092 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M LAMECK TABONWA
1093 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M LAMECK YUSUPH
1094 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M LAMECK A TEMBA
1095 ILEJE SECONDARY SCHOOL M LAMECK BALANKALIE ALEX
1096 NGUDU SECONDARY SCHOOL M LAMECK ELIAKIMU KAMULI
1097 MAGOTO SECONDARY SCHOOL M LAMECK GERSON NAONAWELU
1098 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M LAMECK GODFREY KIMARO
1099 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M LAMECK GREGORY MTONO
1100 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M LAMECK ISSAYA MLONGWA
1101 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M LAMECK J MANZI
1102 KIWANJA SECONDARY SCHOOL M LAMECK JOHN BUNDALA
1103 BOGWE SECONDARY SCHOOL M LAMECK K EWARD
1104 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M LAMECK K PAULO
1105 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M LAMECK L LAWRENCE
1106 TWIHULUMILE SECONDARY SCHOOL M LAMECK L LAWRENCE
1107 SANGU SECONDARY SCHOOL M LAMECK LAZARO KIDAVA
1108 CHATO SECONDARY SCHOOL M LAMECK M DAUDI
1109 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M LAMECK M MILASWA
1110 MWINYI SECONDARY SCHOOL M LAMECK M MWINTANGO
1111 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M LAMECK M SABASABA
1112 NDANDA SECONDARY SCHOOL M LAMECK MASUNGA PAUL
1113 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M LAMECK NDALAHWA BULAYA
1114 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M LAMECK OSWARD SANGA
1115 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M LAMECK P MACHIYA
1116 SCOLASTICA SECONDARY SCHOOL M LAMECK R MONYO
1117 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M LAMECK R SINGU
1118 MOSHI SECONDARY SCHOOL M LAMECK SIMON KONGO
1119 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M LAMECK W MGASHA
1120 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M LAMECK Y OGANGA
1121 CHANGARAWE SECONDARY SCHOOL M LAMON LEZILE LUOGA
1122 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M LAMSON LAMSON KIBONA
1123 SCOLASTICA SECONDARY SCHOOL M LANCY F KINABO
1124 UNGWASI SECONDARY SCHOOL M MACKDONALD P JOSEPH
1125 MKUU SECONDARY SCHOOL M MACKENZI T MSEMO
1126 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M MACKLEAN A JIMM
1127 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M MACKLINE EPHURAHIM MWALWEMBE
1128 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M MACKLINE MAXIMILLIAN RWAMUGIRA
1129 VUDOI SECONDARY SCHOOL M MACKSON AGREY
1130 MIONO SECONDARY SCHOOL M MACKSON HENERICO KAGENZI
1131 KIBITI SECONDARY SCHOOL M MACMILLAN GASPER MSIMBE
1132 KARATU SECONDARY SCHOOL M MACRINE A MGALLA
1133 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M MACRO W MASANJA
1134 MAWENI SECONDARY SCHOOL M MADADI M NGALALA
1135 GEITA SECONDARY SCHOOL M MADAHA LUHENDE
1136 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M MADAHA N MBULI
1137 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M MADARAKA JUMA
1138 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M MADARAKA M SANGA
1139 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M MADARAKA YONA MUHAMA
1140 POMERINI SECONDARY SCHOOL M MADAWA BENITHO MOFUGA
1141 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M MADAWA ERASTO MNYUKA
1142 KWIRO SECONDARY SCHOOL M MADEGE IDDY
1143 MATAI SECONDARY SCHOOL M MADILISHA M MITINJE
1144 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M MADOLA ABDALAH MGOA
1145 SWILLA SECONDARY SCHOOL M MADONA NYANGA KAMLY
1146 SADANI SECONDARY SCHOOL M MADOSHI DANIEL
1147 CHATO SECONDARY SCHOOL M MADSON VICENT
1148 SAME SECONDARY SCHOOL M MADUHU KICHIBA
1149 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M MADUHU KIDESHENI
1150 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M MADUHU MALEGI
1151 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M MADUHU MASANJA
1152 RUTABO SECONDARY SCHOOL M MADUHU NDILANHA
1153 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M MADUHU SHIWA
1154 UMBWE SECONDARY SCHOOL M MADUHU SOSPETER
1155 MOSHI SECONDARY SCHOOL M MADUHU JOEL SHOSHA
1156 NDANDA SECONDARY SCHOOL M MADUHU KICHENGA KILINGA
1157 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M MADUHU M MPYUPYU
1158 KIWANJA SECONDARY SCHOOL M MADUHU M YAGALUKA
1159 NTUNDURU SECONDARY SCHOOL M MADUKA STEPHANO KAZIMILI
1160 KARATU SECONDARY SCHOOL M MADULU DABASU
1161 MWANZA SECONDARY SCHOOL M MADULU M BULARO
1162 MWANZA SECONDARY SCHOOL M MADUMA JOAB
1163 MATAI SECONDARY SCHOOL M MAENDE CHACHA
1164 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M MAFANO JUMA
1165 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M MAFTAA JAMAL AHMED
1166 KARATU SECONDARY SCHOOL M MAFTAHA S TAMIMU
1167 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M MAFURU BONIPHACE
1168 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M MAFURU JOHN
1169 NDANDA SECONDARY SCHOOL M MAFURU MABUBA
1170 LUGUFU BOYS SECONDARY M MAFURU MANYAMA
1171 AIRWING SECONDARY SCHOOL M MAFURU C MWIZARUBI
1172 MUDIO ISLAMIC SEMINARY M MAFUTA IDRISA MAFUTA
1173 UWATA SECONDARY SCHOOL M MAGA D MAGA
1174 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M MAGABE BARU
1175 MWEMBENI SECONDARY SCHOOL M MAGABIRO ELIAS
1176 MWEMBENI SECONDARY SCHOOL M NASIBU SAID
1177 IWAWA SECONDARY SCHOOL M NASIBU A SAID
1178 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M NASIBU ABDALAH MSHANA
1179 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M NASIBU AJUD MAKOMBE
1180 AIRWING SECONDARY SCHOOL M NASIBU ATHUMANI MWINSHAHA
1181 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M NASIBU C NAKAMO
1182 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M NASIBU EZROMU MATHIAS
1183 BONDENI SECONDARY SCHOOL M NASIBU H ATHUMANI
1184 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M NASIBU HABIBU NGORA
1185 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M NASIBU K PANTALEO
1186 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M NASIBU NASORO BWILE
1187 MASJID QUBAH MUSLIM SEMINARY M NASIBU OMARY ABDALLAH
1188 MBEKENYERA SECONDARY SCHOOL M NASIBU R WEMBA
1189 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M NASIBU UWESU KABATA
1190 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M NASIR ABUBAKARI
1191 TAQWA SECONDARY SCHOOL M NASIR ABDULLA HEMED
1192 MORINGE SOKOINE SECONDARY SCHOOL M NASIRA NGAPUTI
1193 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M NASOLWA D KIZENGA
1194 KIBITI SECONDARY SCHOOL M NASON N ALLY
1195 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M NASON NASON MKITI
1196 MWINYI SECONDARY SCHOOL M NASORO BAKARI
1197 SANGU SECONDARY SCHOOL M NASORO NJELIKUS NGUKULA
1198 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M NASORO O SEIF
1199 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL M NASRI A ABDILLAH
1200 MBEZI SECONDARY SCHOOL M NASRI A ATHUMANI
1201 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M NASRI ATHUMANI SADICK
1202 AHMES SECONDARY SCHOOL M NASRI R ISSA
1203 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M NASRI RASHIDI KIMARIO
1204 KIGURUNYEMBE SECONDARY SCHOOL M NASRI SHABAN ALLY
1205 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M NASRI YAHAYA IDDI
1206 KIBITI SECONDARY SCHOOL M NASSA R ABDUL
1207 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M NASSAN PONTIAN
1208 TANDAHIMBA SECONDARY SCHOOL M NASSANA MADAI
1209 UMBWE SECONDARY SCHOOL M NASSER RAYMOND
1210 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M NASSER ABDALLAH ALGHME
1211 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M NASSIB H NYIKA
1212 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M NASSIBU SULEMAN MKALI
1213 IGAWILO SECONDARY SCHOOL M NASSIMU JULIUS
1214 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M NASSIR MWENEMZI
1215 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL M NASSIR A MARWILLO
1216 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M NASSIR HAMZA SEMNGOYA
1217 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M NASSIR MASSOUD OMAR
1218 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M NASSIR S MBUNDA
1219 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M NASSOR SAID
1220 SWILLA SECONDARY SCHOOL M NASSOR AHMAD NGORISA
1221 AL-MUNTAZIR ISLAMIC SEMINARY M NASSOR MORSADY HASSAN
1222 LOYOLA SECONDARY SCHOOL M NASSOR R RAMADHANI
1223 YEMEN SECONDARY SCHOOL M NASSOR S HABIBU
1224 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M NASSORO HAMADI
1225 RUTABO SECONDARY SCHOOL M OBUGO CHACHA
1226 NDANDA SECONDARY SCHOOL M OCHOODO OTIENO
1227 SANGU SECONDARY SCHOOL M OCKLINE MEDICO MSUNGU
1228 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN AUDAX
1229 KILOSA SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN BUBERWA
1230 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN CHARLES
1231 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN CYPRIAN
1232 MWANZA SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN HOSEA
1233 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN LUOGA
1234 WIZA SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN LWILA
1235 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN PASTORY
1236 MAGOTO SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN BRUNO MBUYA
1237 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN CLAVIUS LUAMBANO
1238 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN M PASCHAL
1239 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN MARCO JOHN
1240 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN MARSEL OSWALD
1241 ALPHA SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN PIUS DELEKU
1242 MINAKI SECONDARY SCHOOL M OCTAVIAN RAPHAEL KABASHI
1243 CONSOLATA SEMINARY M OCTAVIAN RWEGELELA MUJWAHUZI
1244 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M OCTAVIUS JONATHAN
1245 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M OCTAVIUS V RUGEMWA
1246 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M OCTOR PHILEMON
1247 MWINYI SECONDARY SCHOOL M ODAX J LUKONGE
1248 MZUMBE SECONDARY SCHOOL M ODDO ADELHELM NDUNGURU
1249 NDANDA SECONDARY SCHOOL M ODDO M MBALANGU
1250 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M ODEN M MOGHA
1251 MAHENJE SEC SCHOOL M ODENI BUKUKU
1252 ZACHARIA SECONDARY SCHOOL M ODERA B MCHONGWE
1253 UMBWE SECONDARY SCHOOL M ODHIAMBO MILONGO
1254 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M ODILO ALPHONCE
1255 ALDERSGATE SECONDARY SCHOOL M ODILO LEONARDI
1256 PEACE SECONDARY SCHOOL M ODILO SEVELINI
1257 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M ODRICK ALEX KINUNDA
1258 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M ODRICK YORAM NTETEMA
1259 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M OFILI BONIFACE HUNGU
1260 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M OGARE OTETE
1261 BUNDA SECONDARY SCHOOL M OGGU T NANYARO
1262 TARIME SECONDARY SCHOOL M OGINGA SUSA
1263 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M OJUNG'U ERNEST SIRIKWA
1264 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M OKAMAN OSIA
1265 PANDAHILL SECONDARY SCHOOL M OKEA PILLY MHANGA
1266 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M OKELLO PETER
1267 SWILLA SECONDARY SCHOOL M OKEN A MWANGOMALE
1268 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M OKEY F FANUEL
1269 SCOLASTICA SECONDARY SCHOOL M OLAIS LOMAYAN LAISSER
1270 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M OLAIS REUBEN MOLLEL
1271 BISHOP DURNING HIGH SCHOOL M OLAIS S LAIZER
1272 CHANGARAWE SECONDARY SCHOOL M OLAIS SAIMON NGELATA
1273 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M OLAPH O MSINDO
1274 JUDE SECONDARY SCHOOL M OLARIP ELIATOSHA TOMITO
1275 HUMURA SECONDARY SCHOOL M OLEN LONGINO
1276 SANGU SECONDARY SCHOOL M OLEN L MZUMBWE
1277 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M OLESTUS MWALIVALILA
1278 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M OLIVERY F MATATA
1279 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M OLORO A MANALI
1280 SANU SEMINARY M PASCAL P MADAWE
1281 KIDUGALA LUTHERAN SEMINARY M PASCAL PASCAL KILLE
1282 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M PASCAL PAULO MBOYA
1283 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M PASCAL PETER LUHEJA
1284 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M PASCAL RICHARD CHATANDA
1285 SAME SECONDARY SCHOOL M PASCAL S GWAMAKOMBE
1286 PIUS SECONDARY SCHOOL M PASCAL S KATOKE
1287 KISIMIRI SECONDARY SCHOOL M PASCHAL ALEXANDER
1288 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL ALOYCE
1289 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M PASCHAL ANDERSON
1290 PAMBA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL ANTHONY
1291 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M PASCHAL BENEDICT
1292 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M PASCHAL BONIPHACE
1293 CHATO SECONDARY SCHOOL M PASCHAL CHARLES
1294 MATAI SECONDARY SCHOOL M PASCHAL CHARLES
1295 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL DAUD
1296 GEITA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL DICKSON
1297 TAQWA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL DICKSON
1298 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL EMMANUEL
1299 TARIME SECONDARY SCHOOL M PASCHAL FRANCISCO
1300 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M PASCHAL GERVAS
1301 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL JOHN
1302 TAQWA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL JOHN
1303 MTWARA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M PASCHAL JULIUS
1304 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M PASCHAL KAGUNDA
1305 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M PASCHAL KATITO
1306 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M PASCHAL LAMECK
1307 TAQWA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL LAZARO
1308 KWIRO SECONDARY SCHOOL M PASCHAL LUHENDE
1309 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M PASCHAL MAKENGE
1310 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M PASCHAL MALIYATABU
1311 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M PASCHAL MARCO
1312 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL MARWA
1313 MARA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL MEZA
1314 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M PASCHAL MISOBI
1315 ILEJE SECONDARY SCHOOL M PASCHAL MOSES
1316 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M PASCHAL MOTERA
1317 CHATO SECONDARY SCHOOL M PASCHAL NCHAMBI
1318 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M PASCHAL NDOHELE
1319 RUTABO SECONDARY SCHOOL M PASCHAL NGASSA
1320 NTUNDURU SECONDARY SCHOOL M PASCHAL NICOLOUS
1321 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M PASCHAL NKOLOLO
1322 PAMBA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL NORBERT
1323 NKASI SECONDARY SCHOOL M PASCHAL NSALANGA
1324 NYEGEZI SEMINARY M PASCHAL NTUNGULU
1325 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL PAUL
1326 LUGUFU BOYS SECONDARY M PASCHAL PETER
1327 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL PHILIBERT
1328 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL RICHARD
1329 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M PASCHAL SAMSON
1330 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M PASCHAL SAMWEL
1331 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL M RAINEL J MLOWE
1332 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M RAINER PASCAL LIHEKA
1333 ST.MARY'S SEMINARY MBALIZI M RAINERY EVENT NCHIMBI
1334 ULAYASI SECONDARY SCHOOL M RAINERY FRANCE MGIMBA
1335 RUTABO SECONDARY SCHOOL M RAINUS FELECIAN TURAHI
1336 UWATA SECONDARY SCHOOL M RAISON MUSSA
1337 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M RAITON MESHACK BAKINA
1338 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M RAJAB LEONARD
1339 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M RAJAB RASHID
1340 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M RAJAB SAID
1341 META SECONDARY SCHOOL M RAJAB SAID
1342 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M RAJAB SWALEH
1343 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M RAJAB ZEWE
1344 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M RAJAB A KONDO
1345 MOSHI SECONDARY SCHOOL M RAJAB ABEID SINGO
1346 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M RAJAB E SHIGANZA
1347 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M RAJAB H MKALLA
1348 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M RAJAB HAFIDH MSOFE
1349 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M RAJAB HEMED LESSOH
1350 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M RAJAB ISIHAKA MBUGI
1351 KIBITI SECONDARY SCHOOL M RAJAB JUMA MPANDA
1352 AL-HARAMAIN ISLAMIC SEMINARY M RAJAB MALUMBO RAJAB
1353 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M RAJAB O JUMA
1354 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M RAJAB OMARY KIJANGWA
1355 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M RAJAB R AWAMI
1356 KWIRO SECONDARY SCHOOL M RAJAB R NYATUKA
1357 MWIKA SECONDARY SCHOOL M RAJAB S BAIDU
1358 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M RAJAB SULTAN MZIRAY
1359 META SECONDARY SCHOOL M RAJAB W MWAIGAGA
1360 ALPHA SECONDARY SCHOOL M RAJAB Y JUMA
1361 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M RAJABU ABBASI
1362 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M RAJABU BAKARI
1363 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M RAJABU HAMIDU
1364 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M RAJABU HASSANI
1365 TARIME SECONDARY SCHOOL M RAJABU IDRISA
1366 NKASI SECONDARY SCHOOL M RAJABU IRIGO
1367 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M RAJABU JUMA
1368 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M RAJABU JUMA
1369 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M RAJABU MAULIDI
1370 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M RAJABU MLOWE
1371 NDANDA SECONDARY SCHOOL M RAJABU MOHAMED
1372 ZACHARIA SECONDARY SCHOOL M RAJABU MOHAMEDI
1373 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M RAJABU MOSHI
1374 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M RAJABU MUSSA
1375 MWANZA SECONDARY SCHOOL M RAJABU MUSSA
1376 IWAWA SECONDARY SCHOOL M RAJABU OMARY
1377 PUGU SECONDARY SCHOOL M RAJABU SELEMANI
1378 LINDI SECONDARY SCHOOL M RAJABU SUDI
1379 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M RAJABU SUFIAN
1380 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M RAJABU TWAHA
1381 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M RAJABU WILLIAM
1382 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M RAJABU YAHYA
1383 LINDI SECONDARY SCHOOL M RAJABU A DIHYENGA
1384 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M SADEC MICHAEL LUTEGO
1385 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M SADI ATHUMAN
1386 AL-FAROUQ SEMINARY M SADI RASHIDI
1387 AL-MUNTAZIR ISLAMIC SEMINARY M SADI SWAIBU
1388 SADANI SECONDARY SCHOOL M SADI T JUMA
1389 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M SADICK ABEID
1390 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M SADICK HUSSEIN
1391 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M SADICK MWAISAKA
1392 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M SADICK SAMWELY
1393 TARIME SECONDARY SCHOOL M SADICK SELEMANI
1394 MWANZA SECONDARY SCHOOL M SADICK SELEMANI
1395 RUTABO SECONDARY SCHOOL M SADICK ALLY MNYANYI
1396 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M SADICK ANYANDIKILE KAYANGE
1397 ARUSHA SECONDARY SCHOOL M SADICK B SHEKIMWERI
1398 AZANIA SECONDARY SCHOOL M SADICK F SADICK
1399 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M SADICK J MASHARUBU
1400 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M SADICK M MWALUKIMBA
1401 MSOLWA SECONDARY SCHOOL M SADICK O CHAMWAKA
1402 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M SADICK OMARY KIZINU
1403 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M SADICK SAID SADICK
1404 KYELA SECONDARY SCHOOL M SADICK ZERA FRANK
1405 TARIME SECONDARY SCHOOL M SADIEL ELIDADI BHONDO
1406 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M SADIK P RASHID
1407 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M SADIKI ALLY
1408 SAME SECONDARY SCHOOL M SADIKI JOHN
1409 VUDOI SECONDARY SCHOOL M SADIKI KASSIMU
1410 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M SADIKI MASOUD
1411 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M SADIKI MUSSA
1412 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M SADIKI SAID
1413 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M SADIKI SELEMANI
1414 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M SADIKI A MWAKASUSA
1415 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M SADIKI A ZAWADI
1416 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M SADIKI IBRAHIMU KINYAGA
1417 LAKE SECONDARY SCHOOL M SADIKI J MSESE
1418 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M SADIKI J ULOMI
1419 ULAYASI SECONDARY SCHOOL M SADIKI L NJASYE
1420 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M SADIKI N MBOKELE
1421 MKUU SECONDARY SCHOOL M SADIKI S MIKIDADI
1422 DAREDA SECONDARY SCHOOL M SADIKIA P BASSO
1423 KIWANJA SECONDARY SCHOOL M SADIKIEL ELISANTE PALLANGYO
1424 KARATU SECONDARY SCHOOL M SADIKIEL S MANANGI
1425 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M SADIKIELI PETRO QALLO
1426 KARATU SECONDARY SCHOOL M SADIKIELY YOSIA DALLEY
1427 KATOKE LWERU SECONDARY SCHOOL M SADOCK SYLIVAND
1428 GEITA SECONDARY SCHOOL M SADOCK COSMAS DAMAS
1429 MVUMI SECONDARY SCHOOL M SADOCK EZRA NDAYANSE
1430 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M SADOCK GEORGE JOHN
1431 KIDUGALA LUTHERAN SEMINARY M SADOCK GODFREY MSIGWA
1432 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M SADOCK N MATHIAS
1433 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M SADOCK VINIUS GACHUNDA
1434 NDANDA SECONDARY SCHOOL M TARIKI M AZIZI
1435 BUNDA SECONDARY SCHOOL M TARIKI MOHAMEDI MKONGE
1436 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M TARIMO ANJAWE KAHEMELA
1437 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M TARIQ ABDALLAH SEIF
1438 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M TARIQ MOHAMEDI MTAHU
1439 LORD BADEN POWELL MEMORIAL SEC. SCHOOL M TARIQUE A MMINGWA
1440 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M TARISIS GOTADO KINONGO
1441 UMBWE SECONDARY SCHOOL M TARO EVANS KASALLA
1442 MIONO SECONDARY SCHOOL M TASHRIF MOHAMEDI
1443 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M TASLO ROSTA MAPUNDA
1444 BOGWE SECONDARY SCHOOL M TATANAI MVUMBAGU
1445 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M TATIANUS SEBASTIAN
1446 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M TATIZO W WINGA
1447 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M TATTI MWININGA
1448 SADANI SECONDARY SCHOOL M TAUDOSY MARIO NGWALE
1449 NYASAKA ISLAMIC SECONDARY SCHOOL M TAUFIQ MIKIDADI
1450 BONDENI SECONDARY SCHOOL M TAUFIQ N MSANGI
1451 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M TAULINI N PAULO
1452 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M TAWAKKAL MOHAMED AYUBU
1453 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M TAWALA JOSEPHAT MHIGIRA
1454 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M TAWFIQ ABDUL
1455 KONGWA SECONDARY SCHOOL M TAWFIQ HAMIS
1456 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M TAZAN B MBAJUKA
1457 MBALIZI SECONDARY SCHOOL M TEDDY LUWOLE
1458 FARAJA SIHA SEMINARY M TEDDY GOLDEN KIGOLA
1459 KILOSA SECONDARY SCHOOL M TEDDY YUSTINI NGANYAGWA
1460 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M TEDISTOKLAS THEONEST
1461 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M TEDIUS JUMA
1462 HIGHLANDS SECONDARY SCHOOL M TEDY MDEMU
1463 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M TEDY A ARONI
1464 KWIRO SECONDARY SCHOOL M TEDY CHEDY KAFYULILO
1465 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M TEDY DAMIAN MYAMBA
1466 KWIRO SECONDARY SCHOOL M TEDY SIMON MSIGWA
1467 ST. AMEDEUS SECONDARY SCHOOL M TEGEMEA WILLFRED
1468 KYELA SECONDARY SCHOOL M TEGEMEO GADIELY
1469 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M TEGEMEO JOIN
1470 MUYOVOZI SECONDARY SCHOOL M TEGEMEO JONAS
1471 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL M TEGEMEO ZAKARIA
1472 ILASI SEC SCHOOL M TEGEMEO J NDOSTE
1473 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M TEGEYE KASIANO NYANZARA
1474 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M TEGEYEKO PAUL LUGEZI
1475 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M TELENT DEUS
1476 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M TELESPHORY MADEMBWE
1477 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M TELESPHORY LUSSIAN MLELWA
1478 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M TELVIN P JAMES
1479 SADANI SECONDARY SCHOOL M TEMA BARACK LUFUNGA
1480 ALPHA SECONDARY SCHOOL M TEMAEL GEOFREY TEMAEL
1481 MVUMI SECONDARY SCHOOL M TEMI LAZARO MHECHELA
1482 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M TEMU JACKSON RIZIKI
1483 USEVYA SECONDARY SCHOOL M TENDE MASUNGA
1484 MAFINGA SEMINARY M TEONEST TEOBARD KINDOLE
1485 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M TERDIUS JAMES WANGALLAH
1486 SANGU SECONDARY SCHOOL M TERESIO COSMAS
1487 AZANIA SECONDARY SCHOOL M TERRY M HEZRON
1488 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M TETUS S MBUZI
1489 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M TEVIN VICTAR MAKANGE
1490 ALPHA SECONDARY SCHOOL M TEVIN W AMLUNGI
1491 HIGHLANDS SECONDARY SCHOOL M VASCO SABIUSI MLIMAKIFI
1492 SANGU SECONDARY SCHOOL M VASCO SYLVESTER KAPINGA
1493 META SECONDARY SCHOOL M VASCO ZALA MWAUTENGA
1494 KARAGWE SECONDARY SCHOOL M VASIUS EVARISTER
1495 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M VECTOR PHILIPO
1496 SANGU SECONDARY SCHOOL M VEDASCO GERODY SANGA
1497 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M VEDASTO MALIMI
1498 AZANIA SECONDARY SCHOOL M VEDASTO SHEYO
1499 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M VEDASTO D FUKO
1500 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M VEDASTO LEON MALLYA

Majina Ya Wanafunzi 1700 Kidato Cha 6 Waliochaguliwa JKT Kambi ya Bulombora-Kigoma

$
0
0



   

            1  DAR ES SALAAM S0298 FEZA GIRLS' SECONDARY SCHOOL F AALIYAH A ABDULRAHMAN
2 MBEYA S4193 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F ABBIA MICHAEL
3 MOROGORO S0729 MSOLWA SECONDARY SCHOOL F ABBY T SEMBUCHE
4 RUKWA S0610 NKASI SECONDARY SCHOOL F ABELA NGEMERA
5 TANGA S0209 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F ABELA RICHARD
6 KIGOMA S0230 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F ABELA JAPHET BENJAMIN
7 MWANZA S1051 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F ABELA O MUTIGANZI
8 MWANZA S0202 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F ABELLA FRANCIS MAINGU
9 IRINGA S0580 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F ABELLA S LUTHER
10 IRINGA S0325 LUGALO SECONDARY SCHOOL F ABGERA M BATUEL
11 SINGIDA S0348 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F ABIA EMILE
12 KAGERA S0218 RUGAMBWA SECONDARY SCHOOL F ABIA JOSEPH
13 MARA S0600 BUNDA SECONDARY SCHOOL F ABIA LAWI
14 MANYARA S0673 NANGWA SECONDARY SCHOOL F ABIA PAULO
15 MWANZA S0216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F ABIA SAMSON
16 IRINGA S0639 UDZUNGWA SECONDARY SCHOOL F ABIA JOHN SANGA
17 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F ABIBA MUHSEN KISOMA
18 MWANZA S0216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F ABIGAEL MAGESA
19 IRINGA S0639 UDZUNGWA SECONDARY SCHOOL F ABIGAEL NYIMBI
20 IRINGA S0203 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ABIGAEL A LYAMUNDA
21 DODOMA S0229 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F BABY ASENGA
22 TANGA S1174 COASTAL SECONDARY SCHOOL F BABY LAYTON
23 KIGOMA S0230 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F BABY SAID
24 DAR ES SALAAM S0938 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL F BABY D KASSIMU
25 PWANI S0549 LUGOBA SECONDARY SCHOOL F BABY J KIBODOGO
26 MWANZA S0249 LORETO GIRLS SECONDARY SCHOOL F BABY J MGAWE
27 MOROGORO S0332 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F BABY KATEMBO SOLIS
28 DAR ES SALAAM S2325 CANOSSA SECONDARY SCHOOL F BABYMARY RAPHAEL SANZEH
29 SINGIDA S0348 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F BABYTUNU ABASI UPETE
30 MWANZA S0202 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F BADRIA ALLY HAMISI
31 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F BADRIYA M KHAMIS
32 KILIMANJARO S0201 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F BAHAT P MAURICE
33 IRINGA S0203 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAHATH LENARD KIDUKO
34 MARA S0601 SERENGETI DAY SECONDARY SCHOOL F BAHATI CHRISTOPHER
35 MWANZA S0202 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAHATI KWEKA
36 KATAVI S0228 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAHATI MSOKWA
37 KILIMANJARO S0201 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F BAHATI MWAMBUNGU
38 IRINGA S0325 LUGALO SECONDARY SCHOOL F BAHATI MWANYESYA
39 KILIMANJARO S0328 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F BAHATI NDAHANI
40 RUKWA S0610 NKASI SECONDARY SCHOOL F BAHATI PAULO
41 SIMIYU S0227 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F CAFREN MPINGWA
42 KIGOMA S0725 NEWMAN SECONDARY SCHOOL F CALEN MICHAEL JANUARY
43 KILIMANJARO S0782 MWIKA SECONDARY SCHOOL F CALISTA MARTIN TSAXARA
44 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL F CALISTA YUDATHADE MREMA
45 MBEYA S0211 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F CALISTER ANATHOLY MASSAWE
46 PWANI S0369 RUVU SECONDARY SCHOOL F CALISTER F MKOLO
47 KILIMANJARO S0201 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F CALISTER PAUL SWAI
48 MBEYA S0211 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F CALISTER STEVEN KATTO
49 IRINGA S0445 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL F CALORINE MODESTUS MASINGA
50 SINGIDA S0245 PALLOTI GIRLS SECONDARY SCHOOL F CANDIDA MICHAEL MTUTUI
51 MBEYA S0341 SANGU SECONDARY SCHOOL F CANISIA A MKINGA
52 KILIMANJARO S0207 KIRAENI GIRLS SECONDARY SCHOOL F CAREEN EUSTAD
53 MWANZA S0333 MWANZA SECONDARY SCHOOL F CAREEN MUKANDALA
54 KILIMANJARO S1187 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F CAREEN A LYIMO
55 KILIMANJARO S2315 KANDOTO SAYANSI SECONDARY SCHOOL F CAREEN BONIFACE NGOWI
56 TANGA S0233 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F CAREEN DANIEL MOLLEL
57 KILIMANJARO S1187 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F CAREEN F NJOGORO
58 KIGOMA S0299 MKUGWA SECONDARY SCHOOL F CAREEN GEORGE MPHURU
59 KILIMANJARO S0212 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F CAREEN JOMO MOSHI
60 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F CAREEN K MUSHI
61 MWANZA S1107 MWAMASHIMBA SECONDARY SCHOOL F DADAA MELITA LESSEYO
62 MWANZA S0202 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F DAFRODHA ELIAS MWANANDOTA
63 DODOMA S0229 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F DAFROSA DEODATUS
64 DODOMA S0306 DODOMA SECONDARY SCHOOL F DAFROSA SOSPETER
65 MANYARA S0673 NANGWA SECONDARY SCHOOL F DAFROSA BLASTUS MAKANZA
66 IRINGA S0203 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F DAFROSA ROBERT KAPERA
67 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL F DAFROSA U MALAI
68 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL F DAFROZA ARON
69 MBEYA S0211 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F DAFROZA LUSAMBO
70 SIMIYU S0227 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F DAFROZA PHILIPO
71 TANGA S0224 KIFUNGILO GIRLS SECONDARY SCHOOL F DAFROZA ASTERI MROSSO
72 GEITA S1164 MISSUNGWI SECONDARY SCHOOL F DAFROZA COSMAS MAYUNGA
73 MWANZA S1107 MWAMASHIMBA SECONDARY SCHOOL F DAFROZA DAMIAN MAYUNGA
74 KIGOMA S0769 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL F DAFROZA NESTORY NZILUHILE
75 KIGOMA S0769 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL F DAFROZA PETRO SONGOYE
76 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F DAILAS DAUDI
77 MBEYA S0417 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL F DAIMA ABONIKE KALINGA
78 IRINGA S1770 IMAGE SECONDARY SCHOOL F DAINA KILASI
79 NJOMBE S0430 UWEMBA SECONDARY SCHOOL F DAINA ABRAHAM MWAKALINGA
80 DAR ES SALAAM S3536 LILIAN KIBO SECONDARY SCHOOL F DAINA GANO NSAJIGWA
81 KAGERA S0218 RUGAMBWA SECONDARY SCHOOL F EARLINESS KARONDO
82 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL F EASTER HAULE
83 KAGERA S0218 RUGAMBWA SECONDARY SCHOOL F EASTER RWEMANYIRA
84 RUVUMA S0234 ST.LUISE MBINGA GIRLS SEC. SCHOOL F EASTER EBERHARD MOYO
85 MBEYA S0330 MBEYA SECONDARY SCHOOL F EASTER M JAPHET
86 GEITA S1498 LUGEYE SECONDARY SCHOOL F EASTERNEEMA GABRIEL YUNGE
87 MBEYA S0538 VWAWA SECONDARY SCHOOL F EBIA A MBUGHI
88 TABORA S0936 KALIUA SECONDARY SCHOOL F EBIA HENRY MLOLWA
89 MBEYA S0913 USONGWE SECONDARY SCHOOL F EBIANA P MBILINYI
90 MBEYA S0581 ILEJE SECONDARY SCHOOL F ECHIKAELI MROSO SEVERINI
91 DODOMA S0229 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDA DANIEL LUMAZI
92 MOROGORO S0617 LUSANGA SECONDARY SCHOOL F EDA DAVID SINDA
93 RUVUMA S0219 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDA S MTOKOMA
94 RUVUMA S1454 LONDONI SECONDARY SCHOOL F EDAH M KISWIGU
95 KATAVI S1637 MILUNDIKWA SECONDARY SCHOOL F EDBERTHA JELOS CHATANDA
96 MWANZA S0539 MAGU SECONDARY SCHOOL F EDDA F MATANDA
97 IRINGA S0580 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F EDDA M HUBERT
98 ARUSHA S1268 KISIMIRI SECONDARY SCHOOL F EDDA MICHAEL YOHANA
99 DAR ES SALAAM S0222 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F EDDAH CHARLES
100 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL F EDDAH MOHAMED
101 DAR ES SALAAM S2325 CANOSSA SECONDARY SCHOOL F FABIOLA CYPRIAN
102 DAR ES SALAAM S0222 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F FABIOLA MICHAEL
103 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F FABIOLA TIMOTHY
104 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F FABIOLA A AMMA
105 PWANI S0369 RUVU SECONDARY SCHOOL F FABIOLA ALLY MSHANA
106 KILIMANJARO S0544 MKUU SECONDARY SCHOOL F FABIOLA FAUSTINE TESHA
107 SINGIDA S0348 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F FABIOLA FELIX MATHEW
108 DODOMA S4207 MARIA DE MATTIAS SECONDARY SCHOOL F FABIOLA FREDRICK GABRIEL
109 MARA S0601 SERENGETI DAY SECONDARY SCHOOL F FABIOLA KIMARIO EDES
110 KAGERA S0611 KABANGA SECONDARY SCHOOL F FABIOLA MATHIAS MAKUMBANO
111 MWANZA S0539 MAGU SECONDARY SCHOOL F FABIOLA TEODORI JOSEPH
112 KILIMANJARO S0221 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F FABIOLA VENANCE MOSHI
113 MWANZA S0216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F FADHILA HARUNA
114 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F FADHILA KASSIM
115 DAR ES SALAAM S0222 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F FADHILA OMARY
116 MWANZA S0216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F FADHILA SHABAN
117 MOROGORO S0668 DAKAWA HIGH SCHOOL F FADHILA SHABANI
118 PWANI S0549 LUGOBA SECONDARY SCHOOL F FADHILA ABDUL-LATIF KIBOKELA
119 TANGA S0209 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F FADHILA AZIZI KETTO
120 GEITA S1164 MISSUNGWI SECONDARY SCHOOL F FADHILA F LIKOKA
121 KILIMANJARO S0328 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F GABRIELA GERMANUS MHEPELA
122 KILIMANJARO S0635 MSUFINI SECONDARY SCHOOL F GABRIELA VENOST MASSAWE
123 TANGA S0692 ROSMINI SECONDARY SCHOOL F GABRIELLA G IDSERT
124 PWANI S0248 MARIAN GIRLS SECONDARY SCHOOL F GABRIELLA R TEMBA
125 KATAVI S0228 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F GAINA JUMA MWAKABANA
126 IRINGA S0325 LUGALO SECONDARY SCHOOL F GAITANA VALENTINO MBALINGA
127 IRINGA S0748 KAWAWA SECONDARY SCHOOL F GAITANA WILLIUM MLAMKA
128 PWANI S0369 RUVU SECONDARY SCHOOL F GALUSIA LEMRUTU BARTALOME
129 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F GAMAR AHMED
130 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL F GAMAWISHI ERASTO
131 MWANZA S0202 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F GATH MARWA
132 IRINGA S0203 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F GATI GEORGE WAMBURA
133 KATAVI S1637 MILUNDIKWA SECONDARY SCHOOL F GAUDENCIA SAMWEL
134 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL F GAUDENCIA H NYARIGO
135 NJOMBE S0427 MAKAMBAKO SECONDARY SCHOOL F GAUDENCIA L TUMBEZA
136 IRINGA S0276 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F GAUDENSIA JOSEPH
137 MOROGORO S0617 LUSANGA SECONDARY SCHOOL F GAUDENSIA MPEPO
138 MBEYA S0538 VWAWA SECONDARY SCHOOL F GAUDENSIA GODFREY MWAKALUKWA
139 TABORA S0314 KAZIMA SECONDARY SCHOOL F GAUDENSIA GOTIFRID TARIMO
140 MOROGORO S0332 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F GAUDENSIA KOLMANI LEONI
141 MARA S0281 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F HABBY JACOB
142 MOROGORO S0668 DAKAWA HIGH SCHOOL F HABIBA ABDALLAH
143 PWANI S3464 ZOGOWALE SECONDARY SCHOOL F HABIBA HAMISI
144 DAR ES SALAAM S0437 AL-MUNTAZIR ISLAMIC SEMINARY F HABIBA HANIU
145 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F HABIBA IMAMU
146 DODOMA S0214 MSALATO SECONDARY SCHOOL F HABIBA KULWA
147 DAR ES SALAAM S1434 PIUS SECONDARY SCHOOL F HABIBA SALUM
148 IRINGA S0580 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F HABIBA SHABANI
149 KAGERA S0360 KISHOJU SECONDARY SCHOOL F HABIBA SHAFII
150 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F HABIBA A HUSSEIN
151 DAR ES SALAAM S0493 AL-HARAMAIN ISLAMIC SEMINARY F HABIBA H ISSA
152 IRINGA S0203 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F HABIBA H RAJABU
153 KATAVI S2385 KAREMA SECONDARY SCHOOL F HABIBA HUSSEIN MASUDI
154 KILIMANJARO S0787 MSANGENI SECONDARY SCHOOL F HABIBA IBRAHIMU MAKAMBA
155 MBEYA S4193 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F HABIBA ISSA NASSORO
156 TABORA S0936 KALIUA SECONDARY SCHOOL F HABIBA M MBELA
157 PWANI S5145 MIONO SECONDARY SCHOOL F HABIBA MHIDINI NYUMBA
158 KILIMANJARO S4922 WATU SECONDARY SCHOOL F HABIBA NUHU MZIRAY
159 IRINGA S1668 KIWELE SECONDARY SCHOOL F HABIBA O MUSSA
160 MWANZA S0216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F HABIBA R NACHIWA
161 PWANI S0549 LUGOBA SECONDARY SCHOOL F ICHIKAEL GODFREY MBOYA
162 PWANI S3464 ZOGOWALE SECONDARY SCHOOL F IDA AJUNA THEOPHIL
163 PWANI S0248 MARIAN GIRLS SECONDARY SCHOOL F IDA JUSTIN KIMARIO
164 PWANI S0549 LUGOBA SECONDARY SCHOOL F IDA PRINCHIPIUS MUTAYOBA
165 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL F IDAYA EDSON ADAM
166 IRINGA S0203 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F IDAYA MPAPAYAI MLINDINDI
167 SINGIDA S0348 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F IDDA BAKUZA
168 DAR ES SALAAM S1278 MBEZI SECONDARY SCHOOL F IDDA THOMAS
169 KAGERA S4661 KAJUMULO ALEXANDER GIRLS SECONDARY SCHOOL F IDDA TRESPHORY
170 MBEYA S4193 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F IDDA ALFRED MOSHI
171 MBEYA S0341 SANGU SECONDARY SCHOOL F IDDA EDWARD KABUKA
172 MBEYA S0867 PANDAHILL SECONDARY SCHOOL F IDDA ERASMUS MATERU
173 KILIMANJARO S0782 MWIKA SECONDARY SCHOOL F IDDA FABIAN MUSHI
174 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F IDDA J PETER
175 SIMIYU S0227 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F IDDA MARANDU APOLINARY
176 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F IDDA S SILVEST
177 IRINGA S0276 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F IDDAH NASSORO SALUM
178 MBEYA S1645 LUBALA SECONDARY SCHOOL F IDERITHA ALEX NDWEWE
179 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F IELEEN DIDAS MUTABINGWA
180 DAR ES SALAAM S0437 AL-MUNTAZIR ISLAMIC SEMINARY F IFRAH A HERSI
181 MWANZA S0202 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKDEBORAH ZEPHANIAH LENDIMI
182 ARUSHA S0949 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F JACKILINA BARTALOME RAFAEL
183 KILIMANJARO S0544 MKUU SECONDARY SCHOOL F JACKILINA MROSSO CHARLES
184 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F JACKILINE BENEDICTO
185 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL F JACKILINE MAKUNDI
186 MARA S0281 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F JACKLINA JAPHES
187 RUKWA S3560 UCHILE SECONDARY SCHOOL F JACKLINA MACHELELA
188 MWANZA S1051 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F JACKLINA A KANSAPA
189 MANYARA S0673 NANGWA SECONDARY SCHOOL F JACKLINA KIMARIO FRANSI
190 KILIMANJARO S0212 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKLINA LASWAY EMILIAN
191 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F JACKLINA RICHARD CHAMI
192 NJOMBE S0427 MAKAMBAKO SECONDARY SCHOOL F JACKLINA RICHARD MOHELE
193 KILIMANJARO S0328 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F JACKLINA SAMALI REVOCATI
194 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL F JACKLINA SHAYO DONATH
195 MOROGORO S0370 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F JACKLINA TEMBA ALOYCE
196 KIGOMA S0230 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F JACKLINA YORAM SHEDRACK
197 IRINGA S1144 ISIMILA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE AKASI
198 DAR ES SALAAM S0620 TEGETA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE ALFRED
199 MWANZA S0216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE AMOS
200 TABORA S0314 KAZIMA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE BLASTO
201 KAGERA S0611 KABANGA SECONDARY SCHOOL F KABULA JOHN
202 GEITA S2178 GOLDEN RIDGE SECONDARY SCHOOL F KABULA KIFUNGO
203 GEITA S4535 JIKOMBOE SECONDARY SCHOOL F KABULA MHOJA
204 MWANZA S3794 NYANKUMBU SECONDARY SCHOOL F KABULA E LUKAMULA
205 MBEYA S4193 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F KABULA L KOMANYA
206 DAR ES SALAAM S0800 LOYOLA SECONDARY SCHOOL F KABULA P MWANGAMBO
207 KILIMANJARO S0201 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F KABULA S MBATTA
208 KILIMANJARO S0782 MWIKA SECONDARY SCHOOL F KABURA GISHANGA SELEMANI
209 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL F KADADA SAMUNGE LAIZER
210 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F KADHIYA SALUM MZEE
211 PWANI S0549 LUGOBA SECONDARY SCHOOL F KAFAYA HUSSEIN JUMA
212 MBEYA S1043 TUKUYU SECONDARY SCHOOL F KAGEMLO VENANCE LUSINDE
213 MOROGORO S0332 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F KAGEMULO BURHAN MUTAHYABARWA
214 KIGOMA S0230 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F KAGEMULO R RWIZA
215 MWANZA S0539 MAGU SECONDARY SCHOOL F KAHABI B SHINYANGA
216 MANYARA S0643 DAREDA SECONDARY SCHOOL F KAKANI E GIDARINYAU
217 TABORA S0314 KAZIMA SECONDARY SCHOOL F KALEKWA NICODEM
218 MBEYA S0640 MBALIZI SECONDARY SCHOOL F KALEKWA J RAMADHANI
219 MOROGORO S0729 MSOLWA SECONDARY SCHOOL F KALIMUNDA S MWAITELEKE
220 MOROGORO S0370 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F KALISTA ATHANAS LWIMBO
221 SHINYANGA S3503 MWENDAKULIMA SECONDARY SCHOOL F LABI GAPI
222 IRINGA S0325 LUGALO SECONDARY SCHOOL F LACKIAT KHANIF
223 MOROGORO S0206 KILAKALA SECONDARY SCHOOL F LADHIA S MDOBA
224 MOROGORO S0206 KILAKALA SECONDARY SCHOOL F LADINA REGINALD
225 KILIMANJARO S0927 LANGASANI SECONDARY SCHOOL F LADYNESS MALLE
226 MWANZA S0216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F LAHELI I GULILAGA
227 LINDI S0812 MAHIWA SECONDARY SCHOOL F LAHERY MALYUS NGONYANI
228 MOROGORO S0668 DAKAWA HIGH SCHOOL F LAILA KHAMIS
229 MTWARA S0139 MTWARA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F LAILA KHAMISI
230 MANYARA S0673 NANGWA SECONDARY SCHOOL F LAILA SELEMANI
231 PWANI S1599 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F LAILA A JUMA
232 MWANZA S0202 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F LAILA IDDY ROMBE
233 TABORA S0220 TABORA GIRLS SECONDARY SCHOOL F LAILA LATWIFU SAID
234 DAR ES SALAAM S0342 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL F LAILA MOHAMED ALLY
235 RUKWA S4785 KIRANDO SECONDARY SCHOOL F LAILA OMARI JUMA
236 IRINGA S0276 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F LAILA R HASSAN
237 DAR ES SALAAM S0204 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F LAILA V HASSAN
238 IRINGA S0203 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F LAILA Y KARAGIZA
239 MTWARA S0831 NANGWANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F LAILAT MARUNDA
240 MTWARA S1077 OCEAN SECONDARY SCHOOL F LAILAT MUSSA
241 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MAANDALIO SHEDRACK
242 NJOMBE S0427 MAKAMBAKO SECONDARY SCHOOL F MAASUMA A BUDAH
243 PWANI S1599 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F MACHENDE KAPWERA
244 MWANZA S0249 LORETO GIRLS SECONDARY SCHOOL F MACKLINA BYERA MATHEW
245 MWANZA S0333 MWANZA SECONDARY SCHOOL F MACKLINA M ALBOGAST
246 MBEYA S0538 VWAWA SECONDARY SCHOOL F MACKLINA MICHAEL SIAME
247 MOROGORO S0210 BIGWA SISTERS SEMINARY F MACKLINA N ANDELIA
248 TANGA S0255 ST.CHRISTINA GIRL'S SCHOOL F MACKLINE SINGANO
249 TANGA S0692 ROSMINI SECONDARY SCHOOL F MACKLINE JOSEPH PASTORY
250 IRINGA S0203 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MACKRINA E CHALAMILA
251 KILIMANJARO S0221 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F MACKRINA METHEW JERONIMO
252 MARA S0778 SONGE SECONDARY SCHOOL F MACLINA ANTONY
253 KILIMANJARO S1187 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F MACLINE MATHEW MOMBO
254 KAGERA S0611 KABANGA SECONDARY SCHOOL F MACRINA FORTUNATUS
255 MARA S1392 NATTA SECONDARY SCHOOL F MACRINA E LAPYA
256 PWANI S1071 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F MADELINE T MALLANDA
257 NJOMBE S0271 MANYUNYU SECONDARY SCHOOL F MADHAHABU AHMAD NDOWEKA
258 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL F MADINA HUSSEIN
259 DODOMA S0214 MSALATO SECONDARY SCHOOL F MADINA MUSSA
260 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F MADINA HUSSEIN NZENZELY
261 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MARY DAMIAN MWACHA
262 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F MARY E MBWAMBO
263 ARUSHA S0949 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F MARY FRANK MATHIAS
264 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F MARY J KATEMA
265 ARUSHA S0454 ST.JOSEPH NGARENARO SEC. SCHOOL F MARY J KINGAZI
266 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MARY J MALLEY
267 ARUSHA S0409 MORINGE SOKOINE SECONDARY SCHOOL F MARY JOHN KIRWAY
268 ARUSHA S3646 ST. MARY'S DULUTI SECONDARY SCHOOL F MARY JOSEPH FISSO
269 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F MARY P SHANA
270 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MARY PASKALI LOHAY
271 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL F MARY PETRO LYANGA
272 ARUSHA S5260 ARUSHA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MARY R MARIKI
273 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F MARY R MWANTYALA
274 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F MARY S SULLE
275 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F MARY S SULLE
276 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F MARYGLORY D MICHAEL
277 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F MARYGORETH L ROMAN
278 ARUSHA S5260 ARUSHA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MARYGORETH MAWALLA BRUNO
279 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MARYJUSTA ELIONA NYARI
280 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F MATRIDA H KIBUGA
281 ARUSHA S2421 STAR SECONDARY SCHOOL F MAUREEN A HANS
282 ARUSHA S0329 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL F MAUREEN ANORLD ULOMI
283 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F MAUREEN JOSEPH MURRAY
284 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL F MAURINE AYUBU MOLLEL
285 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL F MECKLINE C KIMBELE
286 ARUSHA S2421 STAR SECONDARY SCHOOL F MECKRINA JOSEPH NGURUWE
287 ARUSHA S1822 ANNAGAMAZO SECONDARY SCHOOL F MELANIA J NOYA
288 ARUSHA S1268 KISIMIRI SECONDARY SCHOOL F MERCY KIHOMO MPANGALA
289 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL F MERCY WILLBERD MBASHA
290 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F MERCYANA KINOMGAMBI KATUNDU
291 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F MERINA JAMES
292 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MERYICIANA WILIBROAD MILALA
293 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F MERYSIA HOSEA ABEL
294 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F MICKNESS NYONI MILLAN
295 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F MILEMBE S JOSEPH
296 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F MILLIAM EMMANUEL CHUKILIZO
297 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F MINAEL HOPSON FANUEL
298 ARUSHA S2421 STAR SECONDARY SCHOOL F MIRIAM BETHUEL MACHA
299 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F MIRIAM DANIEL KESSY
300 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL F MIRIAM KITOI PALLANGYO
301 ARUSHA S0409 MORINGE SOKOINE SECONDARY SCHOOL F MIRIUM O SARAKIKYA
302 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F MISHI IBRAHIM MALAN
303 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F MKUNDE ALLY BARUTI
304 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F MKWAYA ELIAS
305 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F MONALISA DAVID
306 ARUSHA S5260 ARUSHA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MONICA SIMON
307 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F MONICA A KAMOTA
308 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F MONICA D LYIMO
309 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MONICA M SHANGE
310 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F MONIKA FRANSIS
311 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MOSHI KASALENGE
312 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MOSHI A MKWABI
313 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F MOZA S MCHERECHETA
314 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL F MUNIRA M MIOMBO
315 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F MUTESI CHARLES
316 ARUSHA S4014 WINNING SPIRIT SECONDARY SCHOOL F MUZNA H LAIZER
317 ARUSHA S4746 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL F MWAIJA M GUZUYE
318 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MWAJUMA JUMA
319 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F MWAJUMA H KATEKA
320 ARUSHA S0949 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F MWANAHAWA RICHARD MBOGO
321 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F MWANAIDI RAJABU KASAMBULA
322 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F MWANAIDI S JABIRI
323 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F MWANAISHA MAKWILA
324 ARUSHA S4039 ST. THERESA OF THE CHILD JESUS F MWANAISHA OMARI KINYENGA
325 MARA S1392 NATTA SECONDARY SCHOOL F NAAMINI MWAMPULULE
326 IRINGA S0276 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAAMINI J KISIMBO
327 KILIMANJARO S0787 MSANGENI SECONDARY SCHOOL F NAAMINI NAIMUKIWA MABIRANGA
328 SHINYANGA S3503 MWENDAKULIMA SECONDARY SCHOOL F NAANJELA BERNAD MRINDOKO
329 ARUSHA S4746 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL F NAANJELA MOSES MCHOME
330 MOROGORO S0668 DAKAWA HIGH SCHOOL F NAANJELA T MNZAVA
331 KILIMANJARO S0212 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAATA T LAIZER
332 ARUSHA S0246 MAASAE GIRLS LUTHERAN SECONDARY SCH F NAATOSIM JONATHAN
333 PWANI S1071 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F NAAVA BEATRICE KAMPUNGA
334 DAR ES SALAAM S0437 AL-MUNTAZIR ISLAMIC SEMINARY F NABAITHA T SULEIMAN
335 MWANZA S1665 NYASAKA ISLAMIC SECONDARY SCHOOL F NABILA H RASHID
336 KILIMANJARO S0253 GREEN BIRD GIRLS' SECONDARY SCHOOL F NABILA JUMA SHAABAN
337 MBEYA S0341 SANGU SECONDARY SCHOOL F NABWIKE MWAKYEJA
338 RUVUMA S0540 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL F NACHA HONORIUS MGAYA
339 MOROGORO S0370 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F NACHARO BAKARI MGONJA
340 DAR ES SALAAM S0264 BARBRO-JOHANSSON SECONDARY SCHOOL F NADEZHDA O MAALIM
341 MOROGORO S0332 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F NADHIFA JUMA RAJABU
342 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F NADHIFA S SASILO
343 DAR ES SALAAM S1278 MBEZI SECONDARY SCHOOL F NADIA B ZAKARIA
344 DAR ES SALAAM S0671 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL F NADIA IDD KIMARO
345 ARUSHA S1198 TANZANIA ADVENTIST SECONDARY SCHOOL F NAOMI GEORGE MARIKA
346 ARUSHA S0949 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F NAPENDAELI OMBENI MMBAGA
347 ARUSHA S0949 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F NARISHWAHEDI YONNA MSAMBAA
348 ARUSHA S0246 MAASAE GIRLS LUTHERAN SECONDARY SCH F NASARU SAKAY
349 ARUSHA S0246 MAASAE GIRLS LUTHERAN SECONDARY SCH F NASERIAN D KAMBAINE
350 ARUSHA S0632 BONDENI SECONDARY SCHOOL F NASRA ABUU HAJI
351 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F NASRA HAMISI OMARI
352 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F NATHALIA L MRUTU
353 ARUSHA S0246 MAASAE GIRLS LUTHERAN SECONDARY SCH F NAUMU SILOMA
354 ARUSHA S1268 KISIMIRI SECONDARY SCHOOL F NAVINA JASTIN MUTABAZI
355 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL F NAVONEIWA JOEL MVAMBA
356 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F NAYLAH A MOHAMED
357 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F NDAPUKAY K LENGARE
358 ARUSHA S4514 ORKEESWA SECONDARY SCHOOL F NDEERAY PUSINDAWA
359 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F NDIHOLEYE Z SHABAN
360 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F NDUDULA ABDULRAHMANI MWALUKO
361 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F NEEMA ABELY
362 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F NEEMA CHRISTOPHER
363 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F NEEMA DAUD
364 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F NEEMA EPIMACK
365 ARUSHA S4746 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL F NEEMA ERASTO
366 ARUSHA S4514 ORKEESWA SECONDARY SCHOOL F NEEMA EZEKIEL
367 ARUSHA S0454 ST.JOSEPH NGARENARO SEC. SCHOOL F NEEMA JEREMIAH
368 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F NEEMA KELLYA
369 ARUSHA S0409 MORINGE SOKOINE SECONDARY SCHOOL F NEEMA SAIBULU
370 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F NEEMA TEKSI
371 ARUSHA S0949 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F NEEMA VEDASTUS
372 ARUSHA S0454 ST.JOSEPH NGARENARO SEC. SCHOOL F NEEMA WILLIAM
373 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F NEEMA YUSUPH
374 ARUSHA S0329 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL F NEEMA AMINIRABI SWAI
375 ARUSHA S0949 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F NEEMA CHRISTOPHER MAGANGA
376 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL F NEEMA CHRISTOPHER ZEFRANCO
377 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F NEEMA DISMAS ABEID
378 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F NEEMA E SULLE
379 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL F NEEMA ELIREHEMA MUSHI
380 ARUSHA S1198 TANZANIA ADVENTIST SECONDARY SCHOOL F NEEMA F SINGO
381 ARUSHA S4039 ST. THERESA OF THE CHILD JESUS F NEEMA G KOROSO
382 ARUSHA S4039 ST. THERESA OF THE CHILD JESUS F NEEMA GOODLUCK NDESHIRIO
383 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F NEEMA GRAYSON SAFIELI
384 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F NEEMA J MMARY
385 ARUSHA S0329 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL F NEEMA LAURENTI TLEMU
386 ARUSHA S4746 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL F NEEMA MAIKO MASAGASI
387 ARUSHA S0409 MORINGE SOKOINE SECONDARY SCHOOL F NEEMA MARKO SIRIA
388 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F NEEMA NIMZIHIRWA K
389 ARUSHA S0632 BONDENI SECONDARY SCHOOL F NEEMA PAULO MAGIMBI
390 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F NEEMA S MHANDO
391 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F NEEMA S MSUYA
392 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F NEEMA T GODFREY
393 ARUSHA S4746 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL F NEEMA TIMOTHEO MBWILO
394 ARUSHA S4746 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL F NEMBUAN LOSERIAN MEPUKORI
395 ARUSHA S5260 ARUSHA GIRLS SECONDARY SCHOOL F NENGAI RIDAS
396 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F NENGAI SAMWELI WAPII
397 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F NEVIS URIO
398 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F NG'WAMBA MASANJA
399 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F NIRAM TWALIB DUMBA
400 ARUSHA S4746 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL F NISYA SILVANUS NNUNDUMA
401 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL F NJUMALI MERIKINOI KIVUYO
402 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F NOELA MARGWE MALLE
403 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F NOELA WILBARD SHIRIMA
404 ARUSHA S4039 ST. THERESA OF THE CHILD JESUS F NOELAMANKA DENIS MUSHI
405 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F NORA P BERNARD
406 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL F NORAH BATHOLOMEO RWAMISI
407 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F NORAH R KIMARO
408 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F NORINE MBINGA
409 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL F NOSIM STEPHANO SIMON
410 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F NOSSIM SIFAEL KIVUYO
411 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F NURIATH AMRI
412 ARUSHA S1549 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL F NURU EPHRAIM
413 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F NURU ISANDEKO
414 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL F NURU R ANDREW
415 ARUSHA S0949 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F NUSRATH MOHAMEDI IDDI
416 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F NUSURA IBRAHIMU MDACHI
417 ARUSHA S5260 ARUSHA GIRLS SECONDARY SCHOOL F NYANGETA S CHANGARA
418 ARUSHA S1159 EMBARWAY SECONDARY SCHOOL F NYANJALA K JOHN
419 GEITA S5122 WAJA GIRLS SECONDARY SCHOOL F OBINA OBADIA
420 MBEYA S0211 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F OCTAVIA DANFORD MAHENGE
421 TABORA S0754 URAMBO DAY SECONDARY SCHOOL F OCTAVIA JOHN LUSHINA
422 KILIMANJARO S1187 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F OCTAVIA LUCIANI MATERU
423 KILIMANJARO S1187 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F OCTAVIN T LUMBILLAH
424 KILIMANJARO S0201 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F OCTAVINA NGALANDA
425 MTWARA S0215 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ODDA BERNAD TEMBO
426 RUKWA S0853 KIZWITE SECONDARY SCHOOL F ODELIVA ODILLO
427 MWANZA S0216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F ODETHA BAHATI
428 IRINGA S0203 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ODETHA KALOLO
429 KILIMANJARO S0544 MKUU SECONDARY SCHOOL F ODETHA ONESMO
430 DODOMA S0306 DODOMA SECONDARY SCHOOL F ODETHA ONESPHORY
431 KATAVI S1637 MILUNDIKWA SECONDARY SCHOOL F ODETHA MUDUGU ONESMO
432 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F ODETHA SANGATI BUGUZI
433 MARA S1392 NATTA SECONDARY SCHOOL F ODIA MECKSON
434 PWANI S5145 MIONO SECONDARY SCHOOL F ODILA CHRISTOPHER MTEGA
435 DAR ES SALAAM S3535 DEBRABANT SECONDARY SCHOOL F ODILIA D ANDREW
436 KILIMANJARO S0212 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F ODILIA F GURTI
437 MWANZA S0202 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F ODILIA FRATERINE SWAI
438 TANGA S0209 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F ODILIA KIMARIO BLANCE
439 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL F PALMER A SHAYO
440 DAR ES SALAAM S1343 ANNE MARIE SECONDARY SCHOOL F PALVIS P KANAN
441 MBEYA S0581 ILEJE SECONDARY SCHOOL F PAMAIN W KALINGA
442 TANGA S0209 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F PAMELA JOHNSON
443 KILIMANJARO S1466 MAGADINI SECONDARY SCHOOL F PAMELA SIMON
444 KILIMANJARO S0663 SANGITI SECONDARY SCHOOL F PAMELA DONALD KIMARIO
445 DAR ES SALAAM S1343 ANNE MARIE SECONDARY SCHOOL F PAMELA ISAAC LYIMO
446 PWANI S1599 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F PAMELA JOSEPH TOWILO
447 KATAVI S1637 MILUNDIKWA SECONDARY SCHOOL F PAMELA NELSON KAMWAYA
448 IRINGA S0580 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F PAMELA RAPHAEL MKEMANGWA
449 KILIMANJARO S0223 MASAMA GIRLS SECONDARY SCHOOL F PAMELA SAMSON LEMA
450 KATAVI S0228 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F PAREEN N ALLY
451 MWANZA S0333 MWANZA SECONDARY SCHOOL F PARVIN HENRY JOVITHA
452 TANGA S0233 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F PASCALIA A NYONI
453 SIMIYU S0227 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASCALIA DAVID WANZAGI
454 PWANI S1599 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F PASCALIA H MWAISAKA
455 MWANZA S0216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F PASCALIA M KISSIKE
456 MBEYA S1043 TUKUYU SECONDARY SCHOOL F PASCALIA MALION KAMENDU
457 IRINGA S1610 CHIEF KIDULILE SECONDARY SCHOOL F PASCALINA SIMON
458 KILIMANJARO S0750 OSHARA SECONDARY SCHOOL F PASCALINA THADEUS
459 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F PENDO SAMWEL
460 ARUSHA S1600 BISHOP DURNING HIGH SCHOOL F PENDO GEOFREY AYO
461 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F PENDO LAZARO KAMANDO
462 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F PENDO N LIMBU
463 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F PENDO R POGWA
464 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F PENINA M SESE
465 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL F PENUELI ELIYUKO MMBAGA
466 ARUSHA S0454 ST.JOSEPH NGARENARO SEC. SCHOOL F PENUELY EZEKIEL
467 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F PERUSI S WAIGAMA
468 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F PETRONILA THOMAS ASSENGA
469 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F PHILIPINA FERDINAND MASSAWE
470 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F PHOEBE S PETER
471 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F PHOIBE A MASANGWA
472 ARUSHA S4039 ST. THERESA OF THE CHILD JESUS F PLONA MUSYANGI
473 ARUSHA S2421 STAR SECONDARY SCHOOL F PRICILAR PETER KAYUMBO
474 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F PRISCA MELAMI
475 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F PRISCA AMBOKILE SUMBI
476 ARUSHA S0198 AILANGA LUTHERAN JUNIOR SEMINARY F PRISCA AMRI MGOMBAWATU
477 ARUSHA S2421 STAR SECONDARY SCHOOL F PRISCA FULGENCE LEMNGE
478 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F PRISCA LUCAS MBOYA
479 ARUSHA S0526 MRINGA SECONDARY SCHOOL F PRISCA PROSPER MATEMBA
480 ARUSHA S1285 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F PRIVATULA ABEL HERMAN
481 ARUSHA S0329 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL F QUEEN DAVID
482 IRINGA S0618 LUPALILO SECONDARY SCHOOL F QUEEN EPHRAIM
483 KILIMANJARO S0221 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F QUEEN GISHI
484 MBEYA s1939 MAWENI SECONDARY SCHOOL F QUEEN ISSA
485 SHINYANGA S3503 MWENDAKULIMA SECONDARY SCHOOL F QUEEN JOHN
486 MOROGORO S0359 KIGURUNYEMBE SECONDARY SCHOOL F QUEEN KANGOZI
487 PWANI S0248 MARIAN GIRLS SECONDARY SCHOOL F QUEEN MASIKO
488 MBEYA S0330 MBEYA SECONDARY SCHOOL F QUEEN MWASONGWE
489 SINGIDA S0348 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F QUEEN NALWEYA
490 KAGERA S1689 PEACE SECONDARY SCHOOL F QUEEN SEIF
491 DAR ES SALAAM S0222 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F QUEEN STEPHEN
492 KILIMANJARO S0328 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F QUEEN WILLIAM
493 DAR ES SALAAM S0204 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F QUEEN ADAM MSHANA
494 RUKWA S0853 KIZWITE SECONDARY SCHOOL F QUEEN ANDREW KYUNGU
495 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F QUEEN B MBILIZI
496 MARA S0778 SONGE SECONDARY SCHOOL F QUEEN BRAYSON LYATUU
497 MWANZA S0333 MWANZA SECONDARY SCHOOL F QUEEN C ISAME
498 KILIMANJARO S0212 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F QUEEN CHARLES KIMAMBO
499 KILIMANJARO S0201 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F QUEEN EXAVERY AKARO
500 MARA S0778 SONGE SECONDARY SCHOOL F QUEEN F NNKO
701 MBEYA S3885 WENDA HIGH SCHOOL M AARON D LAUWO
702 KATAVI S2213 USEVYA SECONDARY SCHOOL M ABACHA CHARLES ADAM
703 KIGOMA S0320 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M ABACY GIDION
704 KAGERA S0473 KANYIGO SECONDARY SCHOOL M ABAD ABAS
705 MBEYA S1043 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M ABADALLAH LEONARD
706 RUKWA S1008 ST.MAURUS CHEMCHEMI SECONDARY SCHOOL M ABANI ANDREA
707 PWANI S2354 EAGLES SECONDARY SCHOOL M ABAS KAPINGA
708 NJOMBE S0653 MWAKAVUTA SECONDARY SCHOOL M ABAS KOGOTA
709 KIGOMA S1270 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M ABAS NUHU
710 MBEYA S1262 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M ABAS A LIWAGAYA
711 KAGERA S0488 RUTABO SECONDARY SCHOOL M ABAS C LIKALAFU
712 MWANZA S4856 TWIHULUMILE SECONDARY SCHOOL M ABAS JUMA SEBASTIAN
713 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M ABAS MICHAEL LUWONGO
714 MBEYA S0341 SANGU SECONDARY SCHOOL M ABASI HAMISI
715 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M ABASI MASHI
716 TANGA S2278 MACECHU SECONDARY SCHOOL M ABASI SAID
717 KILIMANJARO S0135 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M ABASI A AWAZI
718 SINGIDA S0715 ILONGERO SECONDARY SCHOOL M ABASI A KIYA
719 TANGA S2278 MACECHU SECONDARY SCHOOL M ABASI HAMADI MFAUME
720 ARUSHA S1549 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M ABASI JUMA SHABANI
721 MBEYA S1148 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M ABASI M KIBWANA
722 KILIMANJARO S0160 UMBWE SECONDARY SCHOOL M ABASI MASOUD IBRAHIM
723 MBEYA S1262 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M ABASI METHOD PELLA
724 LINDI S0726 MBEKENYERA SECONDARY SCHOOL M ABASI N AHMADI
725 DAR ES SALAAM S2549 ALPHA SECONDARY SCHOOL M ABASI S NYANGE
726 MBEYA S1344 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M ABASI ZIADI MAGWIZA
727 MBEYA S0581 ILEJE SECONDARY SCHOOL M ABASS KAIS KIHWELE
728 RUVUMA S0153 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M ABASS SKITU SANGALI
729 KILIMANJARO S0188 KIRINJIKO ISLAMIC SEMINARY M ABBAS HASSAN
730 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M ABBAS ABDUL KIZUA
731 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M ABBAS ALLY KAMWE
732 DAR ES SALAAM S1434 PIUS SECONDARY SCHOOL M ABBAS M ABBASI
733 DAR ES SALAAM S0671 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M ABBAS M MAGOMBA
734 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M ABBAS MIRAJI MWILENGA
735 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M ABBAS SHABANI NDEE
736 SINGIDA S0607 LULUMBA SECONDARY SCHOOL M ABBIS AKIMU
737 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M ABBU MOHAMED MAKEO
738 MOROGORO S0729 MSOLWA SECONDARY SCHOOL M ABBY-SEN ANDREW SWAI
739 RUVUMA S1430 KIUMA SECONDARY SCHOOL M ABDALA MAKUNGANA
740 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M ABDALA A JUMA
741 DODOMA S0465 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M ABDALA ABDI RAMADHANI
742 SIMIYU S0712 BARIADI SECONDARY SCHOOL M ABDALA JUMA SUDY
743 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M ABDALA LUCAS YUSUPH
744 TANGA S0516 MOMBO SECONDARY SCHOOL M ABDALA MIRAJI DANGA
745 DAR ES SALAAM S2426 CHAMAZI ISLAMIC SEMINARY M ABDALA O NGINGITE
746 MOROGORO S0123 KWIRO SECONDARY SCHOOL M ABDALA RAMADHANI SHAMWEPU
747 SIMIYU S1418 KISHAPU SECONDARY SCHOOL M ABDALA S NASSORO
748 LINDI S0726 MBEKENYERA SECONDARY SCHOOL M ABDALA Y AJALI
749 PWANI S0133 MINAKI SECONDARY SCHOOL M ABDALAH BURHANI
750 RUVUMA S4646 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M ABDALAH FAKI
751 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M ABDALAH HASHIMU
752 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M ABDALAH KOMBO
753 KILIMANJARO S0150 SAME SECONDARY SCHOOL M ABDALAH MGANGA
754 DAR ES SALAAM S0938 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M ABDALAH NURU
755 MARA S0129 MARA SECONDARY SCHOOL M ABDALAH RAMADHAN
756 MOROGORO S0332 MOROGORO SECONDARY SCHOOL M ABDALAH SALIMU
757 MWANZA S1051 MKOLANI SECONDARY SCHOOL M ABDALAH SALUM
758 TABORA S0314 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M ABDALAH ZINGA
759 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M ABDALAH ABUBAKAR OMARY
760 RUVUMA S0404 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M ABDALAH CHIKAMBO ABDALAH
761 LINDI S0324 LINDI SECONDARY SCHOOL M ABDALAH HAMISI ABDALAH
762 LINDI S0726 MBEKENYERA SECONDARY SCHOOL M ABDALAH M BAKARI
763 RUVUMA S0404 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M ABDALAH MAARUFU SAIDI
764 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M ABDULSHAKUR Y KASHANGWA
765 KAGERA S0473 KANYIGO SECONDARY SCHOOL M ABDULWAHABU IDDY
766 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M ABDULY R BRUNO
767 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M ABDUNI ATHMANI MLULA
768 ARUSHA S1549 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M ABDUR-RAUPH MOHAMMAD HUSSEIN
769 KAGERA S0488 RUTABO SECONDARY SCHOOL M ABDUTWALIB C MANYAMA
770 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M ABEDI MUHIDINI RASHIDI
771 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M ABEDNEGO PETER
772 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M ABEDNEGO JOB WAPALILA
773 DODOMA S1033 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M ABEID FAIDA
774 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M ABEID JUMA
775 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M ABEID MICHAEL
776 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M ABEID MSANGANZILA
777 GEITA S0752 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M ABEID MSWADIKU
778 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M ABEID WILLIAM
779 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M ABEID I SALUMU
780 ARUSHA S1098 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M ABEID M MWIHAJI
781 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M ABEID S KOBBA
782 IRINGA S0515 ILULA SECONDARY SCHOOL M ABEL EMANUEL
783 GEITA S4605 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M ABEL FILBERT
784 ARUSHA S0409 MORINGE SOKOINE SECONDARY SCHOOL M BABA KILUSU
785 ARUSHA S0409 MORINGE SOKOINE SECONDARY SCHOOL M BABA LOTUMIEKI
786 MARA S0136 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M BABA KUTANDAWA MOLLEL
787 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M BABEL G MVUNGI
788 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL M BABU LEKISHON
789 DAR ES SALAAM S0189 FEZA BOYS' SECONDARY SCHOOL M BABU I KIKULA
790 ARUSHA S1098 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M BABU L SEKEI
791 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M BABU LEVILAL MELEJAKI
792 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M BABU Z MKWAZU
793 KILIMANJARO S1284 NORTHERN HIGHLANDS SECONDARY SCHOOL M BABUELI PENIELI MALISA
794 PWANI S1071 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M BABUU M MPITA
795 PWANI S1071 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M BADDY BASHIR NYANGASA
796 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M BADILIKO MIDYANKO
797 MTWARA S1077 OCEAN SECONDARY SCHOOL M BADILU MAMLO
798 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL M BADREEN FRANCIS MGAMBA
799 MWANZA S0823 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M BADRU NASSIB
800 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M BADRU M FYAGIRA
801 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M BAENDAKI PAUL
802 KIGOMA S4862 GOMBE HIGH SCHOOL M BAGOMWA JULIUS BAGOMWA
803 RUVUMA S0153 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M BAHAMA LAWRENT
804 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M BAHAME GAMBUNA
805 MBEYA S1344 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M BAHARI MOHAMEDI
806 MOROGORO S0117 KASITA SEMINARY M BAHAT ERNEST
807 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M BAHATH SAMWEL
808 MBEYA S0341 SANGU SECONDARY SCHOOL M BAHATH JULIUS KIMBE
809 TABORA S0132 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M BAHATI AUGUSTINO
810 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M BAHATI BALEKELE
811 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M BAHATI BENJAMIN
812 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M BAHATI BRIGHTON
813 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M BAHATI BUDAGA
814 MOROGORO S0367 KILOSA SECONDARY SCHOOL M BAHATI BUKELEBE
815 MBEYA S1262 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M BAHATI BURTON
816 MARA S0136 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M BAHATI CHARLES
817 RUVUMA S1186 MAKITA SECONDARY SCHOOL M BAHATI DANIEL
818 KATAVI S2213 USEVYA SECONDARY SCHOOL M BAHATI DEUS
819 KILIMANJARO S0818 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M BAHATI ELIPOKEA
820 PWANI S0870 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M BAHATI ENOCK
821 SHINYANGA S0152 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M BAHATI GANGILA
822 GEITA S2178 GOLDEN RIDGE SECONDARY SCHOOL M BAHATI IDD
823 MWANZA S0151 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M BAHATI JAJI
824 GEITA S0706 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M BAHATI JUMA
825 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M BAHATI JUMA
826 MWANZA S0151 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M BAHATI JUMA
827 PWANI S0413 KIBITI SECONDARY SCHOOL M BAHATI KAMONGO
828 MBEYA S3905 UWATA SECONDARY SCHOOL M BAHATI KAMWEZI
829 MARA S0352 TARIME SECONDARY SCHOOL M BAHATI KAZUNGU
830 RUVUMA S0404 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M BAHATI KIYUMBI
831 KATAVI S2213 USEVYA SECONDARY SCHOOL M BAHATI KULWA
832 KIGOMA S1270 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M BAHATI KULWA
833 MWANZA S0104 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M BAHATI LAZARO
834 PWANI S0351 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M BAHATI LUCHAGULA
835 MARA S0352 TARIME SECONDARY SCHOOL M BAHATI LUSHINGE
836 TABORA S0314 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M BAHATI MAHOGOYO
837 SIMIYU S0710 BINZA SECONDARY SCHOOL M BAHATI MAKA
838 MBEYA S1148 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M BAHATI MANENO
839 TABORA S0346 UYUI SECONDARY SCHOOL M BAHATI MARANDO
840 MARA S2383 OSWARD MANG'OMBE S S M BAHATI MARCO
841 KIGOMA S1270 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M BAHATI MATEMELA
842 KAGERA S0612 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M BAHATI MATHIAS
843 MWANZA S0151 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M BAHATI MAZIKU
844 MARA S0136 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M BAHATI MSHINGWA
845 DAR ES SALAAM S1011 CHANG'OMBE SECONDARY SCHOOL M BAHATI MWAKILASA
846 MBEYA S1043 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M BAHATI MWAMASO
847 GEITA S0752 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M BARAKA HESRON MAUNDA
848 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M BARAKA HUMPHREY SHILLA
849 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M BARAKA HUSSEIN CHAVALA
850 DODOMA S0697 KIGWE SECONDARY SCHOOL M BARAKA ISACK NGOLLO
851 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M BARAKA J JOSEPHAT
852 ARUSHA S3646 ST. MARY'S DULUTI SECONDARY SCHOOL M BARAKA J MBISE
853 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M BARAKA J MCHUNDA
854 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M BARAKA J MJEMA
855 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M BARAKA JOHN MHAGAMA
856 KAGERA S0488 RUTABO SECONDARY SCHOOL M BARAKA JOSANI MABONDO
857 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M BARAKA JOSEPH HABARI
858 DAR ES SALAAM S0147 PUGU SECONDARY SCHOOL M BARAKA JOSEPH MBUMA
859 ARUSHA S1098 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M BARAKA K SULEMAN
860 IRINGA S0445 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M BARAKA KAJENI KIBIKIMUNU
861 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M BARAKA LAITON KAYENGILE
862 DODOMA S0904 KONGWA SECONDARY SCHOOL M BARAKA LAZARO MLAWA
863 DODOMA S0804 MVUMI SECONDARY SCHOOL M BARAKA LUKAS NDEJEPA
864 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M BARAKA M JOSEPH
865 DODOMA S0904 KONGWA SECONDARY SCHOOL M CAIN C CHUHIRA
866 MANYARA S0168 SANU SEMINARY M CALISTI ANTONI LAZARO
867 GEITA S2178 GOLDEN RIDGE SECONDARY SCHOOL M CALLOCELUS AUDAX
868 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M CALORIUS CLEMENCE
869 RUVUMA S4007 AGUSTIVO SECONDARY SCHOOL M CALTON L MOSHA
870 MBEYA S0890 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M CALVEN P MKWINDA
871 DAR ES SALAAM S0147 PUGU SECONDARY SCHOOL M CALVIN IBRAHIM
872 RUVUMA S0404 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M CALVIN AIDAN MWALYAMBWILE
873 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M CALVIN ANTHONY RICHARD
874 PWANI S0351 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M CALVIN ARNOLD MBASHA
875 RUKWA S0116 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M CALVIN B KONGA
876 MARA S0136 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M CALVIN B MJULE
877 NJOMBE S0653 MWAKAVUTA SECONDARY SCHOOL M CALVIN C MAYOMBA
878 KILIMANJARO S0184 AGAPE LUTHERAN J SEMINARY M CALVIN CATHBERT LEMA
879 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M CALVIN CHAMILL MALEKO
880 KILIMANJARO S1272 KISARIKA SECONDARY SCHOOL M CALVIN CHRISTOPHER MARO
881 TANGA S0516 MOMBO SECONDARY SCHOOL M CALVIN CLEMENT MGENI
882 MBEYA S2427 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M CALVIN D ANDREW
883 KILIMANJARO S0184 AGAPE LUTHERAN J SEMINARY M CALVIN DAMSON NGOWI
884 KILIMANJARO S0184 AGAPE LUTHERAN J SEMINARY M CALVIN E MBWAMBO
885 SHINYANGA S0152 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M CALVIN ELEUTERI LYARI
886 MBEYA S0112 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CALVIN ERASMO NGUNANGWA
887 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M CALVIN FREDRICK ULIKI
888 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M CALVIN G NAFTALI
889 GEITA S0386 GEITA SECONDARY SCHOOL M CALVIN GODFREY DUNIA
890 TANGA S0156 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CALVIN GODSON MOSHI
891 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M CALVIN GOODLUCK LYATUU
892 SHINYANGA S0152 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M CALVIN HELIHURUMA TAMILWAY
893 GEITA S0386 GEITA SECONDARY SCHOOL M CALVIN HENRY MREMA
894 KILIMANJARO S1272 KISARIKA SECONDARY SCHOOL M CALVIN HUBERT LYATUU
895 KILIMANJARO S0160 UMBWE SECONDARY SCHOOL M CALVIN I MALISA
896 KILIMANJARO S1272 KISARIKA SECONDARY SCHOOL M CALVIN JAMES BARAKA
897 KILIMANJARO S0514 UROKI SECONDARY SCHOOL M CALVIN JEREMIA KIMARO
898 KILIMANJARO S0906 VUDOI SECONDARY SCHOOL M CALVIN JOHN KATERA
899 PWANI S1450 EFATHA SEMINARY M CALVIN M TAWETE
900 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M CALVIN MELVIN SENGASU
901 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M CALVIN NDEKIRWA MBISE
902 PWANI S4213 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M CALVIN P BABU
903 TANGA S0142 GALANOS SECONDARY SCHOOL M CALVIN RAFAEL MALYA
904 DAR ES SALAAM S1434 PIUS SECONDARY SCHOOL M CALVIN SAMSON NDELWA
905 KILIMANJARO S0125 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M CALVIN STEVEN SHILEREYO
906 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M CALVIN SWATY MLAY
907 PWANI S0870 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M CALVIN TARAMAELI NDOSI
908 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M CALVIN VICTOR MASHAMBA
909 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M CAMILIUS KALOZA
910 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M CAMILLIUS ODEMARY MSOMA
911 IRINGA S0113 MAFINGA SEMINARY M CAMILLUS LEONCE MWAHESA
912 TANGA S0142 GALANOS SECONDARY SCHOOL M CANDIDUCE BEDA HYERA
913 KILIMANJARO S1757 BENDEL MEMORIAL SECONDARY SCHOOL M CANISIUS E CONSTANTIN
914 DAR ES SALAAM S1434 PIUS SECONDARY SCHOOL M CANISIUS FREDRICK PENDAWAZIMU
915 RUKWA S0609 MATAI SECONDARY SCHOOL M CARLMEN NTONJI
916 IRINGA S0445 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M CARLOS LUBIDA
917 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M CARLOS THOBIAS
918 RUVUMA S0153 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M CARLOS EDWARD MADALE
919 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M CARLOS EMMANUEL TCHAO
920 TANGA S0142 GALANOS SECONDARY SCHOOL M CARLOS MARTIN DHIMBI
921 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M CARLOS N KATEKELE
922 KAGERA S0841 HUMURA SECONDARY SCHOOL M CARLOS NDYETABULA FROLENCE
923 DAR ES SALAAM S0800 LOYOLA SECONDARY SCHOOL M CARLPSON MUNISI
924 SINGIDA S1032 ITIGI SECONDARY SCHOOL M CARLSON KASTULI BEY
925 MOROGORO S3914 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M CAROL JOSEPH
926 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M CAROL FURAHINI TARIMO
927 MBEYA S1043 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M CAROL Z MATTUNDA
928 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M CHIHIKA K CHIHIKA
929 ARUSHA S1549 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M CHIKOZE CLEMENT NKWAMBA
930 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M CHILAVI HAMISI CHILAVI
931 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M CHIPANDE C GEORGE
932 DODOMA S0465 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M CHIPEGWA ALEXANDER CHISAWILO
933 DAR ES SALAAM S0800 LOYOLA SECONDARY SCHOOL M CHIPEGWA DONALD CHIDOWU
934 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M CHOKENI NATHANAEL
935 KAGERA S0405 BIHARAMULO SECONDARY SCHOOL M CHRIAN BARAKA MODEST
936 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M CHRIS JOHN MOLLEL
937 IRINGA S4197 EFATHA SECONDARY SCHOOL M CHRISANT MHAVILE
938 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M CHRISPIN BWIRE
939 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M CHRISPIN MBUGA
940 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M CHRISPIN PESAMBILI
941 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CHRISPIN G KIYANGA
942 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M CHRISPIN GELARD MFUGALE
943 DAR ES SALAAM S0938 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M CHRISPIN JOHN HAULE
944 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M CHRISPINE AKATALYEBA
945 ARUSHA S0329 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL M CHRISPINE M BEJUMULA
946 KAGERA S0360 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M CHRISPINE M WANGOLE
947 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M CHRISPINE N GERALD
948 GEITA S0706 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M CHRISPO M MAGATI
949 DODOMA S0465 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M CHRISROPHER LUCAS KASAMBARA
950 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M CHRISTAD J MWAYONGA
951 LINDI S0596 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M DACHI MZEE
952 PWANI S0922 MWINYI SECONDARY SCHOOL M DADI ALLY SEIFU
953 LINDI S0596 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M DADI I JAGAWA
954 MOROGORO S0332 MOROGORO SECONDARY SCHOOL M DADI J NURDIN
955 RUVUMA S0751 RUHUWIKO SECONDARY SCHOOL M DADLEY MILLANZI
956 SIMIYU S0641 MEATU SECONDARY SCHOOL M DADU NDOGO
957 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M DADU MATANGA KAHANYA
958 PWANI S1450 EFATHA SEMINARY M DAFFA JULIUS KIBAJA
959 MANYARA S1093 ALDERSGATE SECONDARY SCHOOL M DAFFA SILASI KIMERA
960 KIGOMA S0585 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M DAGA KAGAGA MGOMELA
961 MOROGORO S3914 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M DAGLAS WIDON MICHAEL
962 NJOMBE S0444 ITAMBA SECONDARY SCHOOL M DAGOBERT EUFRASTUS HAULE
963 KIGOMA S1270 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M DAGRAS DAVID
964 LINDI S0596 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M DAHALANI ABDALLAH
965 DODOMA S1033 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M DAHAYE H BURA
966 MBEYA S2427 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M DAHAYE S ONNA
967 MWANZA S0151 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M DAIFORD BURTON
968 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M DAIMON MWANGAMILO
969 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M DAIMON JAMES LUCHAGULLA
970 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M DAIMONI K PATRICK
971 RUKWA S0610 NKASI SECONDARY SCHOOL M DAIMONI P MASAKO
972 MTWARA S0139 MTWARA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M DAISON NDIMILA
973 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M DAISON K SANGA
974 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M DALAHILE GASWA
975 MBEYA S1645 LUBALA SECONDARY SCHOOL M DALALI MASHIGULU
976 MOROGORO S0123 KWIRO SECONDARY SCHOOL M DALFONY AMON NTUNGIYE
977 PWANI S0133 MINAKI SECONDARY SCHOOL M DALLEN D YORONIMO
978 MBEYA S0112 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M DALTON JOHN MHOMISOLI
979 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL M DALTON ONESMO AYO
980 SINGIDA S0715 ILONGERO SECONDARY SCHOOL M DALTON ROLAND JAPHET
981 NJOMBE S1157 IWAWA SECONDARY SCHOOL M DALWESHI YASIN MBEJU
982 TANGA S0142 GALANOS SECONDARY SCHOOL M DAMAS CHARLES
983 KIGOMA S0385 UJIJI SECONDARY SCHOOL M DAMAS DAUDI
984 MBEYA S0890 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M DAMAS ESAU
985 SHINYANGA S0152 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M DAMAS GWESA
986 PWANI S1071 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M DAMAS JOHN
987 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M DAMAS MALIPESA
988 TABORA S0314 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M DAMAS MARCO
989 KILIMANJARO S0150 SAME SECONDARY SCHOOL M DAMAS MASANJA
990 MWANZA S0151 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M DAMAS MAYUYA
991 SINGIDA S1032 ITIGI SECONDARY SCHOOL M DAMAS MESHACK
992 RUVUMA S0120 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M DAMAS NYAMAKA
993 RUVUMA S4646 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M DAMAS ABEL MZENA
994 NJOMBE S0167 KIDUGALA LUTHERAN SEMINARY M DAMAS GEORGE KITINDI
995 KILIMANJARO S0165 URU SEMINARY M DAMAS JONHBOSCO MALLYA
996 SHINYANGA S0152 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M DAMAS JUMA SAGUDA
997 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M DAMAS KAMWAGA PATRICE
998 KAGERA S0360 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M DAMAS MATENDE LIMADYANSE
999 IRINGA S0448 SADANI SECONDARY SCHOOL M DAMAS MICHAEL MWAKISOLE
1000 TANGA S2278 MACECHU SECONDARY SCHOOL M DAMAS NYAKISA SANGA
1001 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M DAMAS P SHIRIMA
1002 IRINGA S1578 CHANGARAWE SECONDARY SCHOOL M DAMAS PROTAS MSEMWA
1003 KAGERA S0405 BIHARAMULO SECONDARY SCHOOL M DAMAS ZEPHLINI BISHANGA
1004 KIGOMA S1270 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M DAMASEN ALBERT
1005 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M DAMASI KIBONA
1006 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M DAMASI MICHAEL
1007 MOROGORO S3914 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M DAMIAN ALFREDY
1008 MWANZA S0333 MWANZA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN CLAUDIAN
1009 KIGOMA S1270 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN GASPARY
1010 RUVUMA S1199 MADABA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN JACKSONI
1011 KAGERA S1349 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN KALEBU
1012 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN MBOTWA
1013 RUVUMA S1186 MAKITA SECONDARY SCHOOL M DAMIAN MBWAGA
1014 GEITA S0752 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M DANIFORD K MUKWENDA
1015 KAGERA S0488 RUTABO SECONDARY SCHOOL M DANIPHORD LEONARD
1016 KAGERA S0397 RULENGE SECONDARY SCHOOL M DANKAN DADILY
1017 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M DANNI I MULAKI
1018 ARUSHA S0329 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL M DANSON HAPPYMARK SHOO
1019 IRINGA S0448 SADANI SECONDARY SCHOOL M DANSTAN MWAMBIKE
1020 KAGERA S0612 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M DASTAN ANDREW
1021 KAGERA S0360 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M DASTAN DAUSON
1022 IRINGA S0748 KAWAWA SECONDARY SCHOOL M DASTAN SEBASTIAN
1023 ARUSHA S1061 MAKIBA SECONDARY SCHOOL M DASTAN DAWSON NKULIKIYE
1024 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M DASTAN J SHEGE
1025 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M DASTAN JOEL MICHAEL
1026 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M DASTAN L KAYOMBO
1027 DAR ES SALAAM S1343 ANNE MARIE SECONDARY SCHOOL M DASTAN R KISIMBE
1028 KAGERA S0667 NYAISHOZI SECONDARY SCHOOL M DASTAN VUMILIA CLAVERY
1029 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M DASTANI LEONIDAS
1030 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M DASTANI MTAMA SEMAINDA
1031 KAGERA S0488 RUTABO SECONDARY SCHOOL M DATIUS ANATORY
1032 KAGERA S1689 PEACE SECONDARY SCHOOL M DATIUS DOMINICK
1033 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M DATIUS EMILIAN
1034 KAGERA S1349 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M DATIUS AUDAX SYLIVESTER
1035 DODOMA S2006 MSAKWALO SECONDARY SCHOOL M DATIUS COSTANTINE FRANCE
1036 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M DATIUS RUTASHUBANYUMA DEODATUS
1037 KATAVI S2213 USEVYA SECONDARY SCHOOL M DATIUS RWEGOSHORA RUGEMALIRA
1038 KAGERA S0455 TWEYAMBE SECONDARY SCHOOL M DATUS SEBASTIAN
1039 KAGERA S0612 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M DAUD AMOS
1040 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M EASTON DEOGRATIUS DANIEL
1041 MARA S1625 J.W.BUKANGA SECONDARY SCHOOL M EBAMBO NYAMBARYA
1042 MBEYA S0112 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EBBY ELYON SWALLO
1043 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M EBEN HEAVEN MAMUYA
1044 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M EBENERICK MSHANA WILLIAM
1045 KILIMANJARO S4797 FARAJA SIHA SEMINARY M EBENEZA RICHARDI RUME
1046 PWANI S0351 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M EBENEZER JOROJICK
1047 KILIMANJARO S0160 UMBWE SECONDARY SCHOOL M EBENEZER MARIKI
1048 KILIMANJARO S0906 VUDOI SECONDARY SCHOOL M EBENEZER MASALA
1049 KILIMANJARO S0614 NYERERE SECONDARY SCHOOL M EBENEZER AMAN MOSHI
1050 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL M EBENEZER CALIST MLAY
1051 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M EBENEZER D MINJA
1052 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M EBENEZER D MNANKALI
1053 KILIMANJARO S0356 VUNJO SECONDARY SCHOOL M EBENEZER ISRAEL NATSE
1054 MOROGORO S0140 MZUMBE SECONDARY SCHOOL M EBENEZER JOHNSON MONYO
1055 MARA S2383 OSWARD MANG'OMBE S S M EBENEZER R URIOH
1056 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M EBENEZER S RINGO
1057 TANGA S0142 GALANOS SECONDARY SCHOOL M EBENEZER SETH MACHA
1058 DAR ES SALAAM S0784 AIRWING SECONDARY SCHOOL M EBENEZER SOLOMON NGOWI
1059 GEITA S4605 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M EBENEZER WS SINDATO
1060 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M EBENEZERY JOPHREY
1061 ARUSHA S1198 TANZANIA ADVENTIST SECONDARY SCHOOL M EBENEZERY J IZUNGO
1062 MBEYA S0867 PANDAHILL SECONDARY SCHOOL M EBERHARD KIGODI
1063 MBEYA S0681 IVUMWE SECONDARY SCHOOL M EBIAT JOSPHAT NYONGOLE
1064 RUVUMA S0404 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M EBRANIA EMMANUEL MWASHAMBELA
1065 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M EBRON HAULE KELVIN
1066 MOROGORO S0107 LUTHERAN JUNIOR SEMINARY M EDBART JEREMIA
1067 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M EDBERT M NG'OMAITANGA
1068 MBEYA S3905 UWATA SECONDARY SCHOOL M EDDY MWAKYEMBE
1069 TABORA S0740 ALI HASSAN MWINYI ISL. SEC. SCHOOL M EDDY NEPO
1070 RUVUMA S0153 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M EDDY E MAHENGE
1071 TANGA S0142 GALANOS SECONDARY SCHOOL M EDDY EDWIN MBUNGU
1072 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M EDDY S SHEMBILU
1073 IRINGA S0448 SADANI SECONDARY SCHOOL M EDEGAR EDMOND STEPHAN0
1074 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M EDEN EMANUEL
1075 KILIMANJARO S0125 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M EDEN FRANK TEMU
1076 KILIMANJARO S0614 NYERERE SECONDARY SCHOOL M EDEN M MEELA
1077 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M EDEN SADIKI TEETE
1078 MBEYA S0341 SANGU SECONDARY SCHOOL M EDEN TANAL MWANTEPELE
1079 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M EDES PETER TARIMO
1080 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M EDESY A MOTESHA
1081 DAR ES SALAAM S0938 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M EDFONCE FRANCIS
1082 MBEYA S0112 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EDGA A MWANDA
1083 DAR ES SALAAM S1011 CHANG'OMBE SECONDARY SCHOOL M EDGA A NAAMANI
1084 IRINGA S0448 SADANI SECONDARY SCHOOL M EDGA B KONDO
1085 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M EDGA I LUOGA
1086 MBEYA S1148 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M EDGA PRIVA ATANAS
1087 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EDGA ROBINSON RUBUBURA
1088 MOROGORO S0154 ST.PETER'S SEMINARY M EDGALD C NKONDO
1089 DAR ES SALAAM S1011 CHANG'OMBE SECONDARY SCHOOL M EDGAR BRUCHARD
1090 DAR ES SALAAM S0189 FEZA BOYS' SECONDARY SCHOOL M EDGAR BUBERWA
1091 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M EDGAR DOMINICUS
1092 RUKWA S0116 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M EDGAR EDWARD
1093 MBEYA S1262 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M EDGAR ENDREW
1094 PWANI S1071 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M EDGAR FELICIAN
1095 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M EDGAR FURUMERICUS
1096 KILIMANJARO S0135 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EDGAR JUSTUS
1097 KAGERA S0387 KARAGWE SECONDARY SCHOOL M EDGAR KAFUBA
1098 PWANI S1071 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M EDGAR LUCAS
1099 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M EDGAR MBWILO
1100 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M EDGAR PALLANGYO
1101 RUVUMA S4646 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M EDGAR PIUS
1102 TANGA S3804 MUHEZA HIGH SCHOOL M EDGAR REVELIAN
1103 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M EFREM OMEGA MEGAMO
1104 DAR ES SALAAM S0800 LOYOLA SECONDARY SCHOOL M EFREM PROSPER ASSEY
1105 DAR ES SALAAM S0189 FEZA BOYS' SECONDARY SCHOOL M EGBERTUS BUSIGAZI
1106 IRINGA S1578 CHANGARAWE SECONDARY SCHOOL M EGID NASSON MATINYA
1107 KAGERA S0667 NYAISHOZI SECONDARY SCHOOL M EGIDIUS PROTASE
1108 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M EGLON S MATTO
1109 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M EIFFEL ARCHIMEDES CAESAR
1110 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M EINSTEIN E LYARUU
1111 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M EINSTEIN PETER MKANDA
1112 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M ELADI SWAY DONATH
1113 KAGERA S0360 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M ELADIUS KALOMBA
1114 IRINGA S0652 POMERINI SECONDARY SCHOOL M ELARIO D MAGE
1115 IRINGA S0445 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M ELASMO NGWAULANGA
1116 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M ELBERTUS THEOBARD
1117 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M EL-CID W MAREALLE
1118 KAGERA S1689 PEACE SECONDARY SCHOOL M ELENEUS ELIAS
1119 IRINGA S0445 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M ELENEUS ALPHONCE KAPELA
1120 DAR ES SALAAM S0182 AL-FAROUQ SEMINARY M ELENGERE K MOLLEL
1121 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M ELENZIAN JOHN
1122 SIMIYU S1531 OLD SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M FAADHI JUMANNE SAID
1123 TANGA S0142 GALANOS SECONDARY SCHOOL M FABIAN ALEX
1124 MOROGORO S0140 MZUMBE SECONDARY SCHOOL M FABIAN ALOYCE
1125 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M FABIAN ANICETH
1126 MWANZA S4856 TWIHULUMILE SECONDARY SCHOOL M FABIAN DAKTAR
1127 RUVUMA S0120 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M FABIAN DICKENS
1128 MWANZA S0578 TAQWA SECONDARY SCHOOL M FABIAN ELIAS
1129 TABORA S1375 NEW ERA SECONDARY SCHOOL M FABIAN EMMANUEL
1130 KAGERA S0397 RULENGE SECONDARY SCHOOL M FABIAN FAUSTINE
1131 RUVUMA S0153 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M FABIAN GODFREY
1132 KAGERA S0611 KABANGA SECONDARY SCHOOL M FABIAN JULIUS
1133 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M FABIAN KAISI
1134 MARA S0136 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M FABIAN LINUS
1135 MBEYA S1262 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M FABIAN LUKOMANO
1136 MWANZA S0554 NGUDU SECONDARY SCHOOL M FABIAN MACHELE
1137 MBEYA S0581 ILEJE SECONDARY SCHOOL M FABIAN MARCO
1138 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M FABIAN MARTINE
1139 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M FABIAN MATUKU
1140 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M FABIAN MEDARD
1141 MBEYA S0341 SANGU SECONDARY SCHOOL M FABIAN NGUBI
1142 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M FABIAN REUBEN
1143 LINDI S0596 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M FABIAN ROBERT
1144 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M FABIAN SANGA
1145 MWANZA S0823 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M FABIAN B MAPESA
1146 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M FABIAN B MASUMBUKO
1147 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M FABIAN B MINGA
1148 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M FABIAN B NTIGGA
1149 KATAVI S1232 KATE SECONDARY SCHOOL M FABIAN BARNABAS MWAKATUMA
1150 RUVUMA S4646 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M FABIAN BEATUS HAULE
1151 DAR ES SALAAM S0960 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M FABIAN D MWANSASU
1152 RUVUMA S0540 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL M FABIAN DEUS MDAKI
1153 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M FABIAN F MASHIMI
1154 KILIMANJARO S0818 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M FABIAN FAUSTINE MBISU
1155 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M FABIAN ILAMLA MAHONA
1156 KILIMANJARO S1522 SCOLASTICA SECONDARY SCHOOL M FABIAN J MAKUNE
1157 KILIMANJARO S0160 UMBWE SECONDARY SCHOOL M FABIAN J MWASHIUYA
1158 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M FABIAN J SILAS
1159 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M FABIAN JOHN KAMAMBA
1160 IRINGA S0448 SADANI SECONDARY SCHOOL M FABIAN K JOSEPH
1161 NJOMBE S0143 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M FABIAN LUCAS MARICHA
1162 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M FABIAN M STEVEN
1163 MBEYA S0417 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M FABIAN MABULA NZIGULA
1164 GEITA S0706 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M FABIAN MABULA PETER
1165 SINGIDA S0607 LULUMBA SECONDARY SCHOOL M FABIAN MJUMBO JOAKIM
1166 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M FABIAN N BESSANGO
1167 RUVUMA S0404 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M FABIAN N MWEMBE
1168 MBEYA S0581 ILEJE SECONDARY SCHOOL M FABIAN O CHAVALA
1169 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M FABIAN P NYANKORO
1170 TABORA S0713 IGUNGA SECONDARY SCHOOL M FABIAN PETRO MADUHU
1171 IRINGA S0515 ILULA SECONDARY SCHOOL M FABIAN S KASENSE
1172 TANGA S3804 MUHEZA HIGH SCHOOL M FABIAN T ISSAYA
1173 NJOMBE S0653 MWAKAVUTA SECONDARY SCHOOL M FABIANI MJAILI
1174 LINDI S0596 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M FABIANI ERNEST KILUGALA
1175 MARA S0136 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M FABIANO JAMES
1176 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M FABIANO MERINO
1177 SINGIDA S1032 ITIGI SECONDARY SCHOOL M FABIANO A GWAREHHI
1178 KILIMANJARO S0125 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M FABIANO ALBERTO MBONALIBA
1179 MBEYA S1043 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M FABIANO ANTONY MYINGA
1180 MBEYA S0890 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M FABIANO P DUGHA
1181 MBEYA S3601 ILASI SEC SCHOOL M FABIE F FABIAN
1182 TANGA S0142 GALANOS SECONDARY SCHOOL M FABIO K RAPHAEL
1183 SHINYANGA S0152 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M FABIUS FRED FRETHO
1184 KILIMANJARO S0818 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M FABRISIO CHRISTIAN KALENGA
1185 ARUSHA S1098 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M FEDRICK ATHUMANI MNYAGI
1186 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M FEDRICK L NTONGOLO
1187 DODOMA S1033 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M FEDRICK MAFIE LIVINGSTONE
1188 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M FEDRICK PETER KIKOTI
1189 IRINGA S0445 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M FEDRICK PIUS KINDOLE
1190 KAGERA S0360 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M FEDUKA GABELELA
1191 DAR ES SALAAM S0671 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M FEISAL AWADH
1192 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M FEKA E KANDORE
1193 DAR ES SALAAM S3535 DEBRABANT SECONDARY SCHOOL M FELICE TUMWESIGE FELICIAN
1194 DAR ES SALAAM S1434 PIUS SECONDARY SCHOOL M FELICIAN J MLOKOZI
1195 GEITA S5244 WAJA BOYS SECONDARY SCHOOL M FELICIAN M NDEGE
1196 DAR ES SALAAM S1343 ANNE MARIE SECONDARY SCHOOL M FELICK ELIA MWELELWA
1197 IRINGA S0448 SADANI SECONDARY SCHOOL M FELIN AUGUSTINO NG'UMBI
1198 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M FELIS CHAHE
1199 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M FELIX ANDREW
1200 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M FELIX DIDACUS
1201 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M FELIX EVARIST
1202 DAR ES SALAAM S1246 MIDLANDS SECONDARY SCHOOL M FELIX KAMBONA
1203 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M FELIX MREMI
1204 MBEYA S1344 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M GABLIELY P ANGETERILE
1205 NJOMBE S0143 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M GABRIEL EDWARD
1206 MWANZA S0104 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M GABRIEL GABINUS
1207 KILIMANJARO S0544 MKUU SECONDARY SCHOOL M GABRIEL GEOFREY
1208 MWANZA S0578 TAQWA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL GEORGE
1209 MBEYA S1344 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M GABRIEL HEZRON
1210 MBEYA S0417 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL JAMPION
1211 SHINYANGA S0152 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL JOHN
1212 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL JONAS
1213 MBEYA S0757 KYELA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL JOSEPH
1214 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL KANDURUM
1215 KILIMANJARO S0818 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL LEMBRIS
1216 MOROGORO S3914 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M GABRIEL MATHEW
1217 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M GABRIEL MBOGELA
1218 MBEYA S3905 UWATA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL MGAYA
1219 MBEYA S1584 KIWANJA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL MILTON
1220 MOROGORO S0123 KWIRO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL MPAGAMA
1221 MBEYA S2341 MLIMA MBEYA HIGH SCHOOL M GABRIEL MWASONGWE
1222 PWANI S0133 MINAKI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL RAPHAEL
1223 KILIMANJARO S0160 UMBWE SECONDARY SCHOOL M GABRIEL SEBASTIAN
1224 MBEYA S3885 WENDA HIGH SCHOOL M GABRIEL SUMBUKA
1225 TABORA S1375 NEW ERA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL THOMAS
1226 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL USWEGE
1227 KAGERA S0488 RUTABO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL A OPITA
1228 SIMIYU S0710 BINZA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL A PASTORY
1229 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL A SIMIME
1230 KILIMANJARO S4405 ST. AMEDEUS SECONDARY SCHOOL M GABRIEL ALOYCE MSELLE
1231 MARA S0352 TARIME SECONDARY SCHOOL M GABRIEL B MUGETA
1232 DAR ES SALAAM S3535 DEBRABANT SECONDARY SCHOOL M GABRIEL BADWIN MHENGA
1233 NJOMBE S1157 IWAWA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL BARIKI SENKORO
1234 RUVUMA S0120 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL BEDA NDAWEKA
1235 PWANI S0549 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL BERNARD LYIMO
1236 TANGA S2278 MACECHU SECONDARY SCHOOL M GABRIEL BONIFACE MWIGUNE
1237 KILIMANJARO S0135 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M GABRIEL C GWAJE
1238 PWANI S0413 KIBITI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL C KAVISHE
1239 MBEYA S2341 MLIMA MBEYA HIGH SCHOOL M GABRIEL D MAKUMI
1240 PWANI S0351 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL DAUD GABRIEL
1241 IRINGA S0174 CONSOLATA SEMINARY M GABRIEL DAUDI TEMU
1242 RUVUMA S0404 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M GABRIEL DAVID MWASAKIFWA
1243 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL DOMINICK LYIMO
1244 MOROGORO S3914 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M GABRIEL E MAOKOLA
1245 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M GABRIEL E SHAO
1246 SHINYANGA S0152 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL E TUNGU
1247 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M GABRIEL EMMANUEL LWESHA
1248 KILIMANJARO S1272 KISARIKA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL EZROM SHOO
1249 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL FIDELIS MYOVELLA
1250 NJOMBE S0143 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M GABRIEL FRANCIS MHAGAMA
1251 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL G DELLI
1252 MARA S0129 MARA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL G KIBOI
1253 KILIMANJARO S0160 UMBWE SECONDARY SCHOOL M GABRIEL G MAGAYU
1254 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M GABRIEL G MAYAYA
1255 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M GABRIEL GA SOLITA
1256 TANGA S0142 GALANOS SECONDARY SCHOOL M GABRIEL GASIANO SAIDI
1257 DAR ES SALAAM S0147 PUGU SECONDARY SCHOOL M GABRIEL GODFREY SWAI
1258 MANYARA S0168 SANU SEMINARY M GABRIEL H CLETI
1259 TABORA S0132 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL INKWAY BARBAYDU
1260 RUVUMA S0540 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL J EMMANUEL
1261 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL J MWABUPINA
1262 MARA S0129 MARA SECONDARY SCHOOL M GABRIEL J STEVEN
1263 MANYARA S0368 IMBORU SECONDARY SCHOOL M GABRIEL J THEOBALD
1264 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M GABRIEL JAMES TEMBA
1265 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M GABRIEL JEREMIA MWING'HOLENI
1266 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M GABRIEL JEROMIN MASSAWE
1267 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M GEORGE ROBERT
1268 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M GEORGE STEPHANO
1269 DAR ES SALAAM S1278 MBEZI SECONDARY SCHOOL M GEORGE STEVEN
1270 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M GEORGE A JUAKALI
1271 DAR ES SALAAM S0620 TEGETA SECONDARY SCHOOL M GEORGE A MATHEW
1272 DAR ES SALAAM S3535 DEBRABANT SECONDARY SCHOOL M GEORGE A MNUNGA
1273 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL M GEORGE ALLEN MANJIRA
1274 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M GEORGE B MBELWA
1275 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M GEORGE BERKMANS SARAPAHI
1276 KAGERA S0612 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M GEORGE C LUSATO
1277 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M GEORGE CHRISTIAN NGOLLY
1278 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M GEORGE E MATERU
1279 ARUSHA S1098 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M GEORGE E MGAYA
1280 DAR ES SALAAM S2549 ALPHA SECONDARY SCHOOL M GEORGE E SELENGIA
1281 IRINGA S0448 SADANI SECONDARY SCHOOL M GEORGE ELIAS MAKIWA
1282 ARUSHA S1098 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M GEORGE ELIAS NGOMBA
1283 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M GEORGE EMMANUEL NDOMBA
1284 IRINGA S1610 CHIEF KIDULILE SECONDARY SCHOOL M GEORGE G KASASA
1285 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M GEORGE GRAYSON ISHENGOMA
1286 KIGOMA S0769 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M HABAKUKI NAHAYO
1287 TABORA S0132 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M HABAKUKI S MGEZE
1288 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M HABBY N PHILIPO
1289 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M HABI SIMON
1290 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M HABIB N HABIB
1291 MBEYA S0341 SANGU SECONDARY SCHOOL M HABIBU ABDUL
1292 TANGA S1174 COASTAL SECONDARY SCHOOL M HABIBU ADAMU
1293 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M HABIBU AMIRI
1294 IRINGA S1578 CHANGARAWE SECONDARY SCHOOL M HABIBU FARAJI
1295 TABORA S0936 KALIUA SECONDARY SCHOOL M HABIBU MOHAMED
1296 RUVUMA S4646 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M HABIBU RAMADHAN
1297 PWANI S0351 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M HABIBU SAID
1298 DAR ES SALAAM S0960 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M HABIBU SAIDAN
1299 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M HABIBU SALIMU
1300 MBEYA S0417 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M HABIBU WASTON
1301 PWANI S0870 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M HABIBU A MBEGA
1302 IRINGA S1610 CHIEF KIDULILE SECONDARY SCHOOL M HABIBU ALLY YAGALA
1303 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M HABIBU B MHANDO
1304 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M HABIBU DAUDI MRINDOKO
1305 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M HABIBU HASSAN ATHMAN
1306 MWANZA S0144 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M HABIBU IDDI HABIBU
1307 SIMIYU S1531 OLD SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M HABIBU JUMA GWAE
1308 MBEYA S0581 ILEJE SECONDARY SCHOOL M HABIBU JUMANNE RASHIDI
1309 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M HABIBU M UMARU
1310 TANGA S0511 HANDENI SECONDARY SCHOOL M HABIBU MOHAMEDI MTENGETI
1311 MOROGORO S0123 KWIRO SECONDARY SCHOOL M HABIBU O MKINDU
1312 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M HABIBU S KIBONGO
1313 KILIMANJARO S0614 NYERERE SECONDARY SCHOOL M HABIBU SHABANI SIMA
1314 PWANI S0133 MINAKI SECONDARY SCHOOL M HABIL ATHUMAN
1315 PWANI S0413 KIBITI SECONDARY SCHOOL M HABIL WILLIAM
1316 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M HABIL TABLEY KAPYELA
1317 MBEYA S0330 MBEYA SECONDARY SCHOOL M HABILI MWAISANGO
1318 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M HABILI SYLVANUS
1319 KILIMANJARO S1183 SANYA JUU SECONDARY SCHOOL M HABILI MAHIZI MAPESA
1320 IRINGA S0448 SADANI SECONDARY SCHOOL M HABILI NUHU MBILINYI
1321 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M HABILI SAMSON HABILI
1322 RUVUMA S0120 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M HADJI JUMA
1323 MBEYA S1141 SWILLA SECONDARY SCHOOL M HADJI YUSUPH
1324 KAGERA S0455 TWEYAMBE SECONDARY SCHOOL M HADSON BEDNEGO
1325 RUKWA S0116 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M HADSON KAPELA
1326 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M HADSON PIUS
1327 DODOMA S0306 DODOMA SECONDARY SCHOOL M HADSON CHARLES MAFUNDA
1328 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M HAFIDH ALLY
1329 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M HAFIDH FADHIL
1330 RUVUMA S0404 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M HAFIDH NAMALECHA
1331 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M HAFIDH SEIF
1332 KILIMANJARO S0485 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M HAFIDH HUSSEIN KABESSELA
1333 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M HAFIDH JUMA BAITU
1334 PWANI S0870 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M HAFIDH S MIRAJI
1335 MBEYA S2427 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M HAFIDH SULEIMAN SAID
1336 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M HAFIDH SULEIMAN SELELE
1337 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M HAFIDHI ABDALLAH
1338 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI ABDALLAH
1339 DAR ES SALAAM S0738 RIDHWAA SEMINARY M HAFIDHI AMINI
1340 MTWARA S2153 AQUINAS SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI DAUDI
1341 MBEYA S0112 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI F MASOUD
1342 DAR ES SALAAM S0731 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI H HUSSEIN
1343 PWANI S1599 BAOBAB SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI H NTISSI
1344 MBEYA S0330 MBEYA SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI M HUSSEIN
1345 PWANI S0413 KIBITI SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI M KANDURU
1346 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI R NZALAWAHE
1347 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M HAFIDHI S MANJAMBWA
1348 RUVUMA S1199 MADABA SECONDARY SCHOOL M HAFIDHI S MITAMBO
1349 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M HAMISI S HAMISI
1350 DAR ES SALAAM S1278 MBEZI SECONDARY SCHOOL M HAMISI S LAY
1351 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M HAMISI S UHANGO
1352 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M HAMISI SADAN KIDABADABA
1353 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M HAMISI SAID MBONDE
1354 DAR ES SALAAM S0147 PUGU SECONDARY SCHOOL M HAMISI SALUMU NAMPOTO
1355 DAR ES SALAAM S0335 MZIZIMA SECONDARY SCHOOL M HAMZA ZUBERI
1356 DAR ES SALAAM S0671 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M HAMZA ABDALLA HAMAD
1357 DAR ES SALAAM S1278 MBEZI SECONDARY SCHOOL M HAMZA ABDELEMAN TWAHA
1358 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL M HAMZA H ABED
1359 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M HAMZA HALIDI MSUYA
1360 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M HAMZA I MWALIKO
1361 DAR ES SALAAM S0800 LOYOLA SECONDARY SCHOOL M IAN A KOMBA
1362 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M IAN B MEENA
1363 RUKWA S1008 ST.MAURUS CHEMCHEMI SECONDARY SCHOOL M IAN G CARLOS
1364 PWANI S0119 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M IAN GOODMAN CHACKY
1365 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M IAN JACKSON MOLLEL
1366 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M IAN KONDO MWAIMU
1367 MOROGORO S0729 MSOLWA SECONDARY SCHOOL M IAN L ISHENGOMA
1368 DAR ES SALAAM S1475 PERFECT-VISION SECONDARY SCHOOL M IAN L KILUNGU
1369 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M IAN MWANUZI RUGAIMUKAMU
1370 KILIMANJARO S1183 SANYA JUU SECONDARY SCHOOL M IAN O OBIRO
1371 MOROGORO S0140 MZUMBE SECONDARY SCHOOL M IAN P MAKIPONYA
1372 DAR ES SALAAM S2549 ALPHA SECONDARY SCHOOL M IAN R RWABUYONGO
1373 KILIMANJARO S0184 AGAPE LUTHERAN J SEMINARY M IAN RAY SHOO
1374 GEITA S0686 CHATO SECONDARY SCHOOL M IBADA MARTINE
1375 RUKWA S0116 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M IBADI MUSSA
1376 IRINGA S0448 SADANI SECONDARY SCHOOL M IBADI N HEMED
1377 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M IBADI RASHIDI WANJE
1378 PWANI S0549 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M IBAHATI JOHN
1379 TABORA S0155 TABORA BOYS SECONDARY SCHOOL M IBAHATI K ANDREA
1380 TANGA S0156 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M IBALAJA KIBELA
1381 DAR ES SALAAM S0784 AIRWING SECONDARY SCHOOL M IBIN SALEHE
1382 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M IBON HEMED
1383 DAR ES SALAAM S0147 PUGU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ABDALLAH
1384 DAR ES SALAAM S0438 MASJID QUBAH MUSLIM SEMINARY M IBRAHIM ABDI
1385 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM AFIKILE
1386 MWANZA S0333 MWANZA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM AHMAD
1387 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM AKILIMALI
1388 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ALLY
1389 PWANI S1599 BAOBAB SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM APOLINARY
1390 MBEYA S1645 LUBALA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ARON
1391 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ASWILE
1392 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM BAKARI
1393 MBEYA S0112 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM DANIEL
1394 SHINYANGA S0883 DONBOSCO-DIDIA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM EDWARD
1395 DAR ES SALAAM S1011 CHANG'OMBE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM FIDELIS
1396 DAR ES SALAAM S0731 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM HABSHI
1397 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM HAMIS
1398 PWANI S0133 MINAKI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM HUSSEIN
1399 KAGERA S0611 KABANGA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM JOHN
1400 MARA S0552 MAGOTO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM JOHN
1401 GEITA S0386 GEITA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM JOSEPH
1402 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM JUMA
1403 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM JUMANNE
1404 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM KAWAMBWA
1405 PWANI S5145 MIONO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM KITIKE
1406 KAGERA S0611 KABANGA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM KITINGA
1407 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM KYAMBA
1408 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM LAZARO
1409 MWANZA S0546 PAMBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MAKOYE
1410 NJOMBE S0167 KIDUGALA LUTHERAN SEMINARY M IBRAHIM MAMBA
1411 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MARANGO
1412 DAR ES SALAAM S0493 AL-HARAMAIN ISLAMIC SEMINARY M IBRAHIM MASHAKA
1413 GEITA S0386 GEITA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MBOCKU
1414 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MFAKI
1415 PWANI S0413 KIBITI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MKETO
1416 LINDI S0596 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MNDOLWA
1417 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MOHAMEDI
1418 PWANI S0549 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MOSHI
1419 DAR ES SALAAM S0731 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MSAFIRI
1420 PWANI S1071 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MSANGI
1421 PWANI S0133 MINAKI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MTENGA
1422 MWANZA S0144 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MUSTAPHA
1423 MBEYA S0341 SANGU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM MWAIGWISYA
1424 KAGERA S0611 KABANGA SECONDARY SCHOOL M ILENEUS EVODIUS
1425 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M IMANI CONSTANTINE
1426 DAR ES SALAAM S2549 ALPHA SECONDARY SCHOOL M IMANI KADIVA
1427 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL M IMANI MBULI
1428 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M IMANI REVELIAN
1429 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M IMANI TIBAIGANA
1430 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M IMANI A MWAMWEMBE
1431 DAR ES SALAAM S0731 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M IMANI ABSALUM SANGA
1432 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M IMANI E MTIGILE
1433 DODOMA S0465 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M IMANI GHARIBU ABDALLAH
1434 KAGERA S1349 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M IMANI GODWIN GEORGE
1435 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M IMANI L MABULA
1436 DODOMA S0904 KONGWA SECONDARY SCHOOL M IMANI SIMON BIDA
1437 KAGERA S0397 RULENGE SECONDARY SCHOOL M IMANI VEDASTO RUGANA
1438 MWANZA S0546 PAMBA SECONDARY SCHOOL M JABARY QASIM JAMES
1439 KILIMANJARO S0906 VUDOI SECONDARY SCHOOL M JABBIR KAZERI
1440 PWANI S0133 MINAKI SECONDARY SCHOOL M JABIL ABDUL
1441 KILIMANJARO S0818 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M JABIR RAMADHANI
1442 MBEYA S0443 META SECONDARY SCHOOL M JABIR HASSAN ALMASI
1443 PWANI S0351 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M JABIR I JABIRI
1444 MTWARA S0139 MTWARA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JABIRI ABDALLAH
1445 MBEYA S0443 META SECONDARY SCHOOL M JABIRI KILONGOLA
1446 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M JABIRI MOHAMED
1447 PWANI S0133 MINAKI SECONDARY SCHOOL M JABIRI ALLY JUMA
1448 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M JABIRI HASSAN SABOUR
1449 DODOMA S0465 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M JABIRI ISSA RASHIDI
1450 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M JABIRI JAMALI KIMARO
1451 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M JABIRI JANUARY LILUNGULU
1452 TABORA S0155 TABORA BOYS SECONDARY SCHOOL M JABIRI S LIWANJILO
1453 KILIMANJARO S0468 KIRIKI SECONDARY SCHOOL M JABIRI YAHAYA RAMADHANI
1454 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M JABIRY SELEMANI JABIRY
1455 DAR ES SALAAM S0496 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M JABNETH J NGARAMA
1456 MBEYA S1043 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M JACK J MBWILLAH
1457 MBEYA S2427 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M JACKLINO SILVESTA MWINUKA
1458 MWANZA S0144 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M JACKLINUS MULEGI
1459 PWANI S0351 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M JACKOB ALOISI CHAVALA
1460 MARA S0352 TARIME SECONDARY SCHOOL M JACKOB Y MAGERO
1461 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M JACKOBO A MBWAGA
1462 IRINGA S0128 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M JACKOMU FULGENZI KAKINGO
1463 SINGIDA S0662 MWANZI SECONDARY SCHOOL M JACKSON AMOS
1464 RUVUMA S0404 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M JACKSON ANJELO
1465 MBEYA S0443 META SECONDARY SCHOOL M JACKSON BWENDA
1466 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON CHESAGA
1467 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M JACKSON CHIBALE
1468 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M JACKSON CHIMOMOLA
1469 ARUSHA S0329 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL M JACKSON CHRISTOPHER
1470 RUKWA S0884 MAMBWE SECONDARY SCHOOL M JACKSON CHUZI
1471 LINDI S0596 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M JACKSON COLOMBA
1472 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M JACKSON DANIEL
1473 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M JACKSON DEOGRATIUS
1474 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M JACKSON DOUGLAS
1475 SHINYANGA S0152 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M JACKSON EMMANUEL
1476 NJOMBE S1157 IWAWA SECONDARY SCHOOL M JACKSON ERASTO
1477 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M JACKSON ERNEST
1478 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M JACKSON FRANK
1479 TABORA S0132 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M JACKSON FREDRICK
1480 MBEYA S3905 UWATA SECONDARY SCHOOL M JACKSON GEMUA
1481 DAR ES SALAAM S0316 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M JACKSON GEORGE
1482 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M JACKSON GEORGE
1483 KAGERA S0488 RUTABO SECONDARY SCHOOL M JACKSON HEZRON
1484 SINGIDA S1032 ITIGI SECONDARY SCHOOL M JACKSON HUMBA
1485 PWANI S0870 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M JACKSON ISHENGOMA
1486 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOEL
1487 DAR ES SALAAM S0960 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M JACKSON JOHN
1488 MARA S0352 TARIME SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOHN
1489 MBEYA S0757 KYELA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOHN
1490 NJOMBE S1157 IWAWA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOHN
1491 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOHN
1492 KAGERA S0473 KANYIGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSEPH
1493 KILIMANJARO S0782 MWIKA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSEPH
1494 LINDI S0726 MBEKENYERA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSEPH
1495 MWANZA S0333 MWANZA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSEPH
1496 TABORA S1375 NEW ERA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSEPH
1497 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JULIUS
1498 MOROGORO S3914 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M JACKSON JULIUS
1499 MARA S0136 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JUMA
1500 KAGERA S0397 RULENGE SECONDARY SCHOOL M JACKSON KAZIMOTO
1501 DAR ES SALAAM S0960 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M JAMAL AKIDA
1502 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M JAMAL HAJI
1503 DAR ES SALAAM S0800 LOYOLA SECONDARY SCHOOL M JAMAL NGARAWA
1504 GEITA S4605 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M JAMAL YASSIN
1505 DODOMA S0138 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL M JAMAL YUNUSU
1506 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M JAMAL H JENGO
1507 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M JAMAL RAMADHANI MWEZINGO
1508 KAGERA S0473 KANYIGO SECONDARY SCHOOL M JAMALI BASHIRU
1509 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M JAMALI GWELINO IBRAHIM
1510 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M JAMALI H RAMADHANI
1511 KAGERA S0611 KABANGA SECONDARY SCHOOL M JAMALI JUMA MARUSU
1512 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M JAMALI NYANGE MKHOMOI
1513 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M JAMALI RAJABU LOYI
1514 ARUSHA S4459 JUDE SECONDARY SCHOOL M JAMALY MUHIDINI VARISANGA
1515 KAGERA S4294 KATOKE LWERU SECONDARY SCHOOL M JAMARI YOHANA JANUARY
1516 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M JAMARY HARUNA
1517 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M JAMES ALEXANDER
1518 DAR ES SALAAM S0620 TEGETA SECONDARY SCHOOL M JAMES BERNARD
1519 GEITA S0752 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M JAMES CHACHA
1520 KAGERA S0488 RUTABO SECONDARY SCHOOL M JAMES DOMINICK
1521 KAGERA S1349 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M JAMES DOTTO
1522 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M JAMES GAMA
1523 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M JAMES GASPARY
1524 SIMIYU S1531 OLD SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M KAAMBWA HASAN DAUDI
1525 IRINGA S0108 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M KAANAELI I MBISE
1526 MARA S0136 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M KAAY NAYOKUTUK
1527 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M KABABI D MANYONYI
1528 KIGOMA S5353 LUGUFU BOYS SECONDARY M KABADI ELIAS
1529 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M KABALA IDDI KABALA
1530 MWANZA S0823 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M KABATE S KASSIM
1531 KILIMANJARO S0160 UMBWE SECONDARY SCHOOL M KABEA SAIDI KABEA
1532 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M KABEMBO OSCAR
1533 MARA S0129 MARA SECONDARY SCHOOL M KABETA MHOJA
1534 DODOMA S0103 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M KABISI J LISTONI
1535 KIGOMA S0585 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M KABISI TUNGU TUMAINI
1536 IRINGA S0748 KAWAWA SECONDARY SCHOOL M KABOLA B KALANGAHE
1537 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M KABOTE NINDWA
1538 DAR ES SALAAM S0347 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M KABURI A ZACHARIA
1539 DODOMA S1033 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M KABWE SHIJA NKONDWI
1540 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M KACHALE E KACHALE
1541 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M KACHELI S IREMBA
1542 DAR ES SALAAM S0784 AIRWING SECONDARY SCHOOL M KACHEUKA K RASHID
1543 MBEYA S1148 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M KADALA L LUHAYO
1544 KIGOMA S0585 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M KADAUS MARTIN BAKECHA
1545 ARUSHA S1198 TANZANIA ADVENTIST SECONDARY SCHOOL M KADEGHE KITOY KADEGHE
1546 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M KADEGHE RAMADHAN NZIMA
1547 MBEYA S0417 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M KADESHI L LWAGA
1548 KILIMANJARO S0135 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M KADIKILO PELEKA SHABANI
1549 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M KADIVA P MVUNGI
1550 DAR ES SALAAM S1278 MBEZI SECONDARY SCHOOL M KADOGOO E COSMAS
1551 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M KADOLE MALAWI
1552 KILIMANJARO S0134 MOSHI SECONDARY SCHOOL M KADUMA ALFRED
1553 TABORA S0936 KALIUA SECONDARY SCHOOL M KAFILA JONAS
1554 KIGOMA S1270 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M KAFUKU K MASALYUKA
1555 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M KAGABO PASCHAL
1556 TABORA S0314 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M KAGASHANI KWESIGA
1557 PWANI S0413 KIBITI SECONDARY SCHOOL M KAGOMBORA ROLANDIPAUL TIRUTANGWA
1558 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M KAGUNDA LUHAGA
1559 MARA S0925 KASOMA SECONDARY SCHOOL M KAGURI C KAGURI
1560 SIMIYU S3886 SIMBA WA YUDA M KAHABI GHARAMA
1561 KILIMANJARO S0150 SAME SECONDARY SCHOOL M KAHEMA NDEGELEKI
1562 MWANZA S0151 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M KAHIBI KAHIBI RAPHAEL
1563 TANGA S0548 SHAMBALAI SECONDARY SCHOOL M KAHLID ALLY
1564 KILIMANJARO S0125 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M KAHUMUZA DONATH MIHANDA
1565 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M KAIBU CHESCO NGWETA
1566 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M KAIMU MASOUD URASSA
1567 MBEYA S0581 ILEJE SECONDARY SCHOOL M KAIMU P MBUKWA
1568 KIGOMA S0769 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M KAIMUKILWA J TIBAZARWA
1569 RUVUMA S1220 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M KAIN A BOAZ
1570 MBEYA S4803 NDYUDA SECONDARY SCHOOL M KAIN NAKOLY NGIMBUCHI
1571 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M KAINDI SAMUEL
1572 KIGOMA S1270 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M KAINI ABDALA TOBOTOBO
1573 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M KAISI MUSSA
1574 LINDI S0324 LINDI SECONDARY SCHOOL M KAISI A MWASHA
1575 TABORA S0936 KALIUA SECONDARY SCHOOL M KAISY G CHARLES
1576 PWANI S1071 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M KAITAN C NZIKU
1577 KILIMANJARO S0544 MKUU SECONDARY SCHOOL M KAITAN YUDA MSUYA
1578 SINGIDA S0334 MWENGE SECONDARY SCHOOL M KAITIRA BENSON
1579 IRINGA S1578 CHANGARAWE SECONDARY SCHOOL M KAIZA ISRAEL KAGUO
1580 NJOMBE S1495 GENESIS HIGH SCHOOL M KAIZA JAJI MBILINYI
1581 IRINGA S1596 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M KAIZA LAWAMA NGAILE
1582 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M KAIZA R KAGANZI
1583 IRINGA S0748 KAWAWA SECONDARY SCHOOL M KAIZA VALENTINO LWIMBO
1584 MBEYA S1043 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M KAIZAL ELIAS MHAPA
1585 MBEYA S2427 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M KAIZARI MALEWA
1586 MTWARA S0338 NDANDA SECONDARY SCHOOL M KAIZER DAUDI
1587 KAGERA S0397 RULENGE SECONDARY SCHOOL M KELVIN KAGARUKI
1588 DAR ES SALAAM S1434 PIUS SECONDARY SCHOOL M KELVIN KASABILA
1589 DODOMA S0697 KIGWE SECONDARY SCHOOL M KELVIN KATABARO
1590 ARUSHA S1098 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M KELVIN LUGENGA
1591 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M KELVIN MABITI
1592 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M KELVIN MACHA
1593 KAGERA S1349 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M KELVIN MJUNI
1594 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M KELVIN MPANGALA
1595 DAR ES SALAAM S1246 MIDLANDS SECONDARY SCHOOL M KELVIN MSYANI
1596 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M KELVIN MTAO
1597 DAR ES SALAAM S0960 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M KELVIN MTEWELE
1598 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M KELVIN MUYUNGI
1599 DAR ES SALAAM S4692 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M KELVIN MWAKATUMBULA
1600 ARUSHA S0110 ILBORU SECONDARY SCHOOL M KELVIN MWANGOMO
1601 IRINGA S0652 POMERINI SECONDARY SCHOOL M KELVIN NGEWE
1602 DAR ES SALAAM S0534 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M KELVIN OSCAR
1603 GEITA S0386 GEITA SECONDARY SCHOOL M KELVIN PHARES
1604 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M KELVIN PRINCEPIUS
1605 KAGERA S4419 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M KELVIN PROJEST
1606 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M KELVIN SAMSON
1607 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M KELVIN SIMON
1608 DAR ES SALAAM S2499 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M KELVIN STEWART
1609 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M KELVIN VINCENT
1610 DODOMA S0175 SALESIAN SEMINARY M KELVIN A MLAWA
1611 MANYARA S0361 SINGE SECONDARY SCHOOL M LAANYU MEPUKORY
1612 GEITA S4605 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M LABAN GEORGE
1613 NJOMBE S0143 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M LABAN MESHACK NDONDOLE
1614 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M LABANI EZEKIEL
1615 MWANZA S0151 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M LABANI DARIUS MGONYA
1616 MWANZA S0539 MAGU SECONDARY SCHOOL M LABANI FRANK SOBAI
1617 GEITA S4605 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M LACKIUS ROBERT
1618 NJOMBE S1157 IWAWA SECONDARY SCHOOL M LACKSON SIKWESE
1619 MBEYA S0149 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M LACKSON K MGOLA
1620 MBEYA S0417 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M LACKSON SENGO MWANANDA
1621 TANGA S1257 ARAFAH ISLAMIC SEMINARY M LADINI I ALFANI
1622 KILIMANJARO S0160 UMBWE SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS AFRICANUS
1623 RUVUMA S4646 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS ISHENGOMA
1624 MWANZA S0146 NYEGEZI SEMINARY M LADISLAUS LUSATO
1625 KAGERA S0473 KANYIGO SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS MARTIN
1626 PWANI S0133 MINAKI SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS MUTAKUBWA
1627 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS YAMOLA
1628 RUVUMA S0540 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS A IKULA
1629 PWANI S0413 KIBITI SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS E MPELEMBWA
1630 DAR ES SALAAM S0189 FEZA BOYS' SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS L MWAMANGA
1631 ARUSHA S0302 ARUSHA SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS LAURINE MKENGA
1632 KAGERA S0109 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS M BARAKA
1633 DAR ES SALAAM S0960 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M LADISLAUS PROBY MASSY
1634 MOROGORO S0107 LUTHERAN JUNIOR SEMINARY M LADISLAUS R GIRAY
1635 DODOMA S0697 KIGWE SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS R SILVESTA
1636 MWANZA S0146 NYEGEZI SEMINARY M LADISLAUS RENOVATUS MWIZARUBI
1637 SINGIDA S0106 DUNG'UNYI SEMINARY M LADISLAUS REVOCATUS LUSSATO
1638 KILIMANJARO S0160 UMBWE SECONDARY SCHOOL M LADISLAUS VALERIAN TUMAINI
1639 MARA S0136 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M LADSLAUS YAMBI
1640 MOROGORO S3914 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M LADSLAUS BARNABASI MODEST
1641 ARUSHA S2421 STAR SECONDARY SCHOOL M LAIDAN BABU
1642 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M LAILEJILEJI N LINGAI
1643 ARUSHA S3646 ST. MARY'S DULUTI SECONDARY SCHOOL M LAIMERI SAITORE LAIZER
1644 MOROGORO S0367 KILOSA SECONDARY SCHOOL M LAIMONDI F MGALA
1645 ARUSHA S4514 ORKEESWA SECONDARY SCHOOL M LAIS JOSEPH
1646 ARUSHA S4514 ORKEESWA SECONDARY SCHOOL M LAIS LAZARO
1647 KILIMANJARO S0818 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M LAIS L MAYON
1648 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M LAIS M SEKEYAN
1649 KILIMANJARO S1183 SANYA JUU SECONDARY SCHOOL M LAIS NGONINA KURESOI
1650 TANGA S0345 USAGARA SECONDARY SCHOOL M LAIS OLTOBIKOY PUSINDAWA
1651 IRINGA S0445 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M LAISON LAISON FUTE
1652 NJOMBE S1157 IWAWA SECONDARY SCHOOL M LAITON LULANDALA
1653 SINGIDA S1032 ITIGI SECONDARY SCHOOL M LAITON MWAKIHABA
1654 MOROGORO S0123 KWIRO SECONDARY SCHOOL M LAITON NGOLE
1655 ARUSHA S1098 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M LAITON GODLISTEN MATEMBA
1656 IRINGA S0158 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M LAIZA E CHARLES
1657 MBEYA S1645 LUBALA SECONDARY SCHOOL M LAIZACK BISHAFU
1658 MBEYA S0757 KYELA SECONDARY SCHOOL M LALAHE M SINGOY
1659 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M LALAYOK N OLUBI
1660 MBEYA S1201 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M LAMAYAN PENETI PAULO
1661 DAR ES SALAAM S1434 PIUS SECONDARY SCHOOL M LAMBERT RAPHAEL MDOGO
1662 MWANZA S0104 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M LAMBERT RESPICIUS NICAS
1663 MBEYA S0890 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M LAMBERTUS ROBERTH MNYAMBO
1664 KIGOMA S0585 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M LAMBO SENI
1665 KIGOMA S1270 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M LAMECK AMOS
1666 KAGERA S0611 KABANGA SECONDARY SCHOOL M LAMECK ANACLETH
1667 KAGERA S1349 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M LAMECK ANG'ULO
1668 MWANZA S0578 TAQWA SECONDARY SCHOOL M LAMECK BARNABA
1669 GEITA S0386 GEITA SECONDARY SCHOOL M LAMECK BENEDICT
1670 KILIMANJARO S0125 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M LAMECK BENJAMIN
1671 KATAVI S2213 USEVYA SECONDARY SCHOOL M LAMECK CHARLES
1672 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M LAMECK GEORGE
1673 MTWARA S1077 OCEAN SECONDARY SCHOOL M LAMECK GIDEON
1674 ARUSHA S0857 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M LEONARD M LUFUNGA
1675 DODOMA S0904 KONGWA SECONDARY SCHOOL M LEONARD MNYETI MNYETI
1676 ARUSHA S0329 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL M LEONARD MPEMBENI MLEMBA
1677 ARUSHA S0629 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M LEONARD P MMARI
1678 DAR ES SALAAM S0147 PUGU SECONDARY SCHOOL M LEONARD S CHANDARUA
1679 DAR ES SALAAM S0800 LOYOLA SECONDARY SCHOOL M LEONARD THOBIAS BUYI
1680 DAR ES SALAAM S0342 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL M LEONARD TITUS LUGENDO
1681 ARUSHA S0409 MORINGE SOKOINE SECONDARY SCHOOL M LEONARD W SABAYA
1682 DODOMA S1033 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M LEONCE SPERATUS
1683 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M LEONCE LEANDRY DAHAYE
1684 IRINGA S0449 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M LEONCE LEONARD MBATA
1685 KAGERA S0488 RUTABO SECONDARY SCHOOL M LEONIDAS LINUS
1686 DAR ES SALAAM S0784 AIRWING SECONDARY SCHOOL M LEONIDAS K RWENYAGIRA
1687 IRINGA S1770 IMAGE SECONDARY SCHOOL M LEONS DAVID CHUNGULU
1688 KAGERA S0145 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M LEOPORD EMMANUEL
1689 GEITA S0752 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M LEOPORD EDWARD NYAMKECHA
1690 DAR ES SALAAM S0147 PUGU SECONDARY SCHOOL M LEPAAPA SOOMBE
1691 ARUSHA S0364 KARATU SECONDARY SCHOOL M LEPARAKWO PUSINDAWA
1692 ARUSHA S0329 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL M LETIAN P MORIJOI
1693 KAGERA S0405 BIHARAMULO SECONDARY SCHOOL M LETUS LAULIAN
1694 IRINGA S1610 CHIEF KIDULILE SECONDARY SCHOOL M LEVI LENSON NDAMBO
1695 DODOMA S0465 JAMHURI SECONDARY SCHOOL M LEVINE LUCIAN KOBELO
1696 ARUSHA S0308 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL M LEVINI PETER TSERE
1697 KAGERA S0115 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M LEVIS CHARLES
1698 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M LEVIS MWOMBEKI
1699 DAR ES SALAAM S0101 AZANIA SECONDARY SCHOOL M LEVIS G NYAKINA
1700 DAR ES SALAAM S3535 DEBRABANT SECONDARY SCHOOL M MAACHI A MAACHI

Majina Ya Kidato Cha Sita 2016 Wanaotakiwa Kujiunga Na JKT Kwa Mujibu Wa Sheria......Tarehe ya Kuripoti Kambini ni Tarehe 1 Hadi 5 Juni

$
0
0

Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), limechagua vijana waliohitimu elimu ya sekondari kidato cha sita kwa mwaka 2016, kutoka shule zote za Tanzania Bara kuhudhuria mafunzo ya JKT kwa Mujibu wa Sheria.

Sanjari na uchaguzi huo, JKT limewapangia makambi watakayokwenda kupatiwa mafunzo kwa muda wa miezi mitatu na wanatakiwa kuripoti makambini kuanzia tarehe 01 - 05 Juni 2016.

Vijana waliochaguliwa, wamepangiwa katika Kambi za JKT Rwamkoma – Mara, JKT Msange – Tabora, JKT Ruvu – Pwani, JKT Makutupora – Dodoma, JKT Mafinga – Iringa, JKT Mlale – Ruvuma, JKT Mgambo na JKT Maramba – Tanga, JKT Bulombora, JKT Kanembwa na JKT Mtabila – Kigoma.

Aidha, wahitimu wenye ulemavu wa kuonekana kwa macho (physical disabilities) wanatakiwa kuripoti Kambi ya JKT RUVU, iliyopo Mlandizi mkoani Pwani, ambayo ina miundombinu ya kuhudumia watu wa jamii hiyo.

JKT linawataka vijana hao kuripoti makambini wakiwa na nguo za michezo kama vile ‘track suit’, bukta, raba pamoja na nguo za kuzuia baridi kwa waliopangiwa kwenye makambi yenye baridi kama JKT Makutupora, JKT Mafinga, JKT Mlale, JKT Kanembwa na JKT Mtabila.

Mkuu wa JKT anawakaribisha vijana wote waliochanguliwa ili waweze kujiunga na vijana wenzao katika kujifunza uzalendo, umoja wa kitaifa, uhodari, stadi za kazi, stadi za maisha na utayari wa kulijenga na kulitumikia Taifa letu.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Habari na Uhusiano
Makao Makuu ya JKT

Tarehe 20 Mei 2016

Manchester United 2-1 Crystal Palace (AET): Jesse Lingard nets extra-time winner in FA Cup final to save Louis van Gaal's season

$
0
0
It may as well have been 1990 revisited. All it lacked was the replay. But the central themes, the broad narrative, were just as they were 26 years ago.
There was the South London hero coming off the bench to breathe life into Crystal Palace, so much so that they dared to hope a major trophy finally beckoned.
There was the Manchester United comeback, with eight minutes left, and the ache for Alan Pardew of a glorious opportunity missed. And then there was the beleaguered United boss parading the FA Cup as vindication of his regime.
Jesse Lingard strips off his shirt after scoring an extra-time winner to claim the FA Cup with a 2-1 defeat of Crystal Palace
Jesse Lingard strips off his shirt after scoring an extra-time winner to claim the FA Cup with a 2-1 defeat of Crystal Palace
Substitute Lingard netted the winner despite Manchester United being reduced to 10-men after Chris Smalling saw red in extra-time
The lid of the FA Cup lid goes flying as Wayne Rooney and Michael Carrick lift the famous trophy at Wembley
The lid of the FA Cup lid goes flying as Wayne Rooney and Michael Carrick lift the famous trophy at Wembley
Rooney (centre) leads the celebrations as the champagne sprays after Manchester United's FA Cup final victory
Rooney (centre) leads the celebrations as the champagne sprays after Manchester United's FA Cup final victory
Manager Louis van Gaal is applauded as he hoists the trophy after what may yet be his final game in charge of United
Manchester United players celebrate on the pitch after winning their first silverware since Sir Alex Ferguson retired
Manchester United responded to Palace's opening goal within minutes with Juan Mata netting the equaliser
Manchester United responded to Palace's opening goal within minutes with Juan Mata netting the equaliser
The Spain playmaker leaps at the corner flag to celebrate drawing Manchester United level in the FA Cup final
Substitute Jason Puncheon celebrates with team-mates after coming on to smash home the opening goal for Crystal Palace
Substitute Jason Puncheon celebrates with team-mates after coming on to smash home the opening goal for Crystal Palace
Manchester United keeper David de Gea is beaten by the sheer force of Puncheon's volley on 78 minutes
Manchester United keeper David de Gea is beaten by the sheer force of Puncheon's volley on 78 minutes
The United squad celebrate in their dressing room with the FA Cup, with experienced winger Antonio Valencia holding the famous trophy
The United squad celebrate in their dressing room with the FA Cup, with experienced winger Antonio Valencia holding the famous trophy

PLAYER RATINGS by Sami Mokbel 

Manchester United: De Gea 7, Valencia 7, Smalling 5, Blind 6, Rojo 6.5 (Darmian 6.5), Carrick 7.5, Mata 7.5 (Lingard 7.5), Fellaini 7, Rooney 8.5, Martial 7, Rashford 8 (Young 6.5)
Subs: Jones, Romero, Ander Herrera, Schneiderlin
Booked: Smalling, Rojo, Mata, Rooney, Fellaini
Scorer: Mata 81'
Crystal Palace: Hennessey 6.5, Ward 7.5, Dann 8 (Mariappa 6.5), Delaney 7.5, Souare 7, Jedinak 7, Cabaye 6 (Puncheon 7.5), Zaha 6.5, McArthur 6, Bolasie 6.5, Wickham 6.5 (Gayle 6.5) 
Subs: Speroni, Adebayor, Sako, Kelly
Booked: Dann, Delaney
Scorer: Puncheon 78' 
Referee: Mark Clattenburg
Attendance: 88,619
Louis van Gaal will not get another 23 years after this final, like Sir Alex Ferguson did, but at least when the Dutchman finally delivered a trophy it was in the manner we have come to expect.
Not gloriously, not with smooth, delightful football. It was ponderous at times and United teetered on the brink of a calamitous defeat more than once.
But they got there in the end. And one of Van Gaal’s fledglings, Jesse Lingard, delivered a stunning winning goal, 20 minutes into extra time, just as United seemed to be imploding with defender Chris Smalling having been sent off.
Lingard’s strike from Damien Delaney’s clearance was something quite glorious with which to cap Van Gaal’s reign.
As such it was hardly in keeping with the previous two years, but for sheer belligerence alone, he perhaps deserved this victory.
He certainly thought so, plonking the FA Cup in front of the press before launching into a justification of his time at United.
‘In spite of being down to 10 players, we showed the spirit that we have shown on the way to the final,’ he said.
‘We do fight to the end. When we proved that again in the final, you can be very proud as Manchester United manager and as a fan.’
That United made it was no thanks to Smalling. Extra time had been a scrappy, nervy affair and the chief drama in the first period came when Yannick Bolasie spun past Smalling, who fell, grappling, grabbing and finally pulling Bolasie back by a boot as he tried to dash away. A second yellow card was inevitable and Smalling was sent off.
Palace had 15 minutes to make the advantage count. They sensed their moment. Dwight Gayle was played in, had a second to shoot but found David de Gea equal to his strike.

Haya Hapa Majina Ya Wanafunzi 1500 Kidato Cha 6 Waliochaguliwa JKT Kambi ya Kanembwa- Kigoma

$
0
0


1 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F ADELAIDE ANDREHEM MLWILO

2 LUGALO SECONDARY SCHOOL F ADELAIDE AULELIANI MWALONGO

3 KIBOSHO GIRLS SECONDARY SCHOOL F ADELFINA LAZARI MOSHA

4 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F ADELHELMA EVARISTO MKINGA

5 NGANZA SECONDARY SCHOOL F ADELICK WILBROAD

6 MASONYA SECONDARY SCHOOL F ADELINA AKILI

7 FARAJA SIHA SEMINARY F ADELINA COSMAS

8 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ADELINA INOCENT

9 KAZIMA SECONDARY SCHOOL F ADELINA KASSIM

10 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F ADELINA KASUSA

11 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ADELINA MARANDO

12 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F ADELINA NSAJIGWA

13 ST.JOSEPH GIRLS SEMINARY F ADELINA PETER

14 MASONYA SECONDARY SCHOOL F ADELINA PHILEMON

15 MISSUNGWI SECONDARY SCHOOL F ADELINA SOSTENES

16 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ADELINA WENCESLAUS

17 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F ADELINA A BAYO

18 TABORA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ADELINA A MPANGENI

19 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F ADELINA ANTIPAS SHIRIMA

20 ZOGOWALE SECONDARY SCHOOL F ADELINA ASSENGA AMEDE

21 MISSUNGWI SECONDARY SCHOOL F BAITINA HARUNI MSUYA

22 BUNDA SECONDARY SCHOOL F BAITUNI S MAJANDILA

23 VWAWA SECONDARY SCHOOL F BALBINA MAHINYA

24 MASASI GIRLS SECONDARY SCHOOL F BALBINA ULEDI

25 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F BALBINA ANICETH KIWIA

26 NGANZA SECONDARY SCHOOL F BALBINA D LYIMO

27 MPITIMBI SECONDARY SCHOOL F BALBINA E MAPUNDA

28 ST.CHRISTINA GIRL'S SCHOOL F BALDWINA P MAHIMBO

29 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F BALIATU SHAFII ZANGA

30 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F BALICHENE SONDA

31 SUMVE SECONDARY SCHOOL F BALKE MAZIKU

32 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F BALKIS HAMIDU

33 FEZA GIRLS' SECONDARY SCHOOL F BALQEES S MOHAMED

34 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F BALQIS J SAID

35 KIBASILA SECONDARY SCHOOL F BALQUIS KATUNDU

36 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F BAMLANGE KALELA

37 BEROYA SECONDARY SCHOOL F BAPTISTA MILINGA

38 ST.LUISE MBINGA GIRLS SEC. SCHOOL F BARAKA C KOMBA

39 LUPALILO SECONDARY SCHOOL F BARAKA OTMARY MLOWE

40 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F BARBIERY BETRAM CHILIMA

41 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F CAROLINE C SEBASTIAN

42 LUKOLE SECONDARY SCHOOL F CAROLINE CHARLES MASAMU

43 BUPANDAGILA SECONDARY SCHOOL F CAROLINE CRODWARD KAMUGISHA

44 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F CAROLINE D KASONGOYO

45 MSALATO SECONDARY SCHOOL F CAROLINE DANIEL SHOIDE

46 UWEMBA SECONDARY SCHOOL F CAROLINE ELIAH MGHASE

47 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F CAROLINE EMANUEL MUYA

48 BUNDA SECONDARY SCHOOL F CAROLINE F MSUYA

49 SCOLASTICA SECONDARY SCHOOL F CAROLINE FELIX KIMARO

50 KIWELE SECONDARY SCHOOL F CAROLINE G MALEMA

51 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F CAROLINE H KABOGO

52 WAJA GIRLS SECONDARY SCHOOL F CAROLINE H SIGALLA

53 PIUS SECONDARY SCHOOL F CAROLINE ISAACK PAUL

54 KIBASILA SECONDARY SCHOOL F CAROLINE J KAIGI

55 KIBASILA SECONDARY SCHOOL F CAROLINE JEROME BYALUGABA

56 AIRWING SECONDARY SCHOOL F CAROLINE JEROME MTOROBO

57 MUHEZA HIGH SCHOOL F CAROLINE JOSEPH ANGAIYA

58 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F CAROLINE JULIUS BAMWEBUGA

59 TABORA GIRLS SECONDARY SCHOOL F CAROLINE K UISO

60 ANNAGAMAZO SECONDARY SCHOOL F CAROLINE L BRANGIS

61 NGANZA SECONDARY SCHOOL F DANIELA FRANK SEBAHENE

62 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F DAPHROSA LEONARD NGAWAIYA

63 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F DARIA NCHANILA

64 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F DARIA DANIEL NKYA

65 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F DARLIN KAKOZI

66 IGAWILO SECONDARY SCHOOL F DATIVA CHAMBANENJE

67 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL F DATIVA DEUS

68 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F DATIVA GEORGE

69 NGANZA SECONDARY SCHOOL F DATIVA MATUNGWA

70 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F DATIVA PAUL

71 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F DATIVA RWESHELWA

72 KABANGA SECONDARY SCHOOL F DATIVA SYLIVAND

73 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F DATIVA TIBESIGWA

74 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL F DATIVA VENANT

75 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F DATIVA A ERNEUS

76 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F DATIVA AMAN MTUI

77 MAJENGO SECONDARY SCHOOL F DATIVA AUGUST TEMU

78 CANOSSA SECONDARY SCHOOL F DATIVA CHARLES NYALUKE

79 CANOSSA SECONDARY SCHOOL F DATIVA D RWEYEMAMU

80 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL F DATIVA D SALUFU

81 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDINA D PASTORY

82 NANGWANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDINA DIDAS FLORIAN

83 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDINA DUNSTAN NYAGALU

84 LUGALO SECONDARY SCHOOL F EDINA E LUHWAGO

85 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F EDINA ELIAKIMU BALIAGATI

86 PAMBA SECONDARY SCHOOL F EDINA GWABO JOSEPH

87 TUKUYU SECONDARY SCHOOL F EDINA H MWAKAPALA

88 IVUMWE SECONDARY SCHOOL F EDINA INNOCENT SENGO

89 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDINA ISRAEL YATOSH

90 NYANKUMBU SECONDARY SCHOOL F EDINA J KAHAMBILO

91 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F EDINA J KAPUNGU

92 ISIMILA SECONDARY SCHOOL F EDINA JACOB CHAULA

93 LORETO GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDINA JENEROZA LEOPOLD

94 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F EDINA JOSEPH JACOB

95 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F EDINA K EDWARD

96 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDINA K OSHUMAA

97 RUVU SECONDARY SCHOOL F EDINA KOKWIJUKA ERNEST

98 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDINA L KIBASA

99 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F EDINA L SELEMAN

100 TABORA GIRLS SECONDARY SCHOOL F EDINA L SHIRIMA

101 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL F FAILUNA HUSSEIN KAMAU

102 IKUNGI SECONDARY SCHOOL F FAILUNA RAMADHANI TUTA

103 KALIUA SECONDARY SCHOOL F FAIMA ISIHAKA

104 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F FAINES KIZANYE

105 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F FAINES TOBIAS

106 LUGALO SECONDARY SCHOOL F FAINES ZEBEDAYO

107 LUPALILO SECONDARY SCHOOL F FAINES ATILIO MDAGE

108 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F FAINES M KAHOGO

109 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL F FAINES NOEL BROWN

110 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F FAINES SEPO STEVEN

111 KABANGA SECONDARY SCHOOL F FAINESS ELISON SAMWEL

112 JOHN PAUL II KAHAMA SECONDARY SCHOOL F FAINESS KASANDA RENATUS

113 RUVU SECONDARY SCHOOL F FAINESS M KYANDO

114 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F FAIR B GADAU

115 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL F FAITH ISSAWANGU

116 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F FAITH A MWAIPOPO

117 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F FAITH ABBA MSOFE

118 NANGWA SECONDARY SCHOOL F FAITH ASA MEENA

119 CANOSSA SECONDARY SCHOOL F FAITH CECILIA MDACHI

120 LUKOLE SECONDARY SCHOOL F FAITH CHARLES TIBIHIKA

121 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F GEORGIA RUKILIZA

122 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F GEORGIA MADANGI AWE

123 MBEYA SECONDARY SCHOOL F GEORGIA POTITUS ISHENGOMA

124 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F GEORGINA CHARLES KAVENGA

125 BARBRO-JOHANSSON SECONDARY SCHOOL F GEORGINA GEORGE MGOYELA

126 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F GEORGINA MICHAEL MDUDA

127 PREMIER GIRLS SECONDARY SCHOOL F GERALDA M KATEMBA

128 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F GERALDINA MUSHUMBUSI

129 KILAKALA SECONDARY SCHOOL F GERALDINA SEVERIN KOMBA

130 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F GERALDINA VENANSI KIMARIO

131 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F GERDA ARBOGAST

132 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F GEREMANA E BOTA

133 EFATHA SEMINARY F GERINE KOMANGO LUSINDE

134 MIONO SECONDARY SCHOOL F GERMANA CHELULA

135 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL F GERMANA JOHN

136 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F GERMANA EUGEN MARK

137 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F GERMANA G MKOKA

138 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F GERMANA GAUDENCE CHAMI

139 LUFILYO SECONDARY SCHOOL F GERMANA P NYENZA

140 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F GERODA REAGAN

141 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F HADIJA SELEMANI

142 BABATI DAY SECONDARY SCHOOL F HADIJA SHABANI

143 MPITIMBI SECONDARY SCHOOL F HADIJA SHABANI

144 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F HADIJA ZUBERY

145 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F HADIJA A ISSA

146 KIFARU SECONDARY SCHOOL F HADIJA A LUSONZO

147 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL F HADIJA A MOHAMED

148 JIKOMBOE SECONDARY SCHOOL F HADIJA A MOHAMEDI

149 MWENDAKULIMA SECONDARY SCHOOL F HADIJA A MSHANGAMA

150 ANNE MARIE SECONDARY SCHOOL F HADIJA A NGWALO

151 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F HADIJA ABDUL MSIMBE

152 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F HADIJA ADAM KARUNDA

153 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F HADIJA AHMAD MCHELU

154 KIRINJIKO ISLAMIC SEMINARY F HADIJA ALLY MSEMO

155 RUVU SECONDARY SCHOOL F HADIJA ATHUMANI ABEID

156 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F HADIJA FADHILI ATHUMANI

157 ARUSHA MODERN SECONDARY SCHOOL F HADIJA H BAYO

158 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL F HADIJA H DUA

159 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F HADIJA H MOHAMED

160 KALIUA SECONDARY SCHOOL F HADIJA H MOHAMEDI

161 SUMVE SECONDARY SCHOOL F IMANI EDWARD SILAS

162 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F IMANI FRANCE NZIKU

163 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F IMANI GAUDENCE LUPOGO

164 NANGWA SECONDARY SCHOOL F IMANI P MAO

165 LUGOBA SECONDARY SCHOOL F IMANI S KISSANDA

166 UCHILE SECONDARY SCHOOL F IMELDA GOODLUCK

167 KAREMA SECONDARY SCHOOL F IMELDA MICHAEL

168 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F IMELDA PELAGI

169 PEACE SECONDARY SCHOOL F IMELDA RUSERUKA

170 KARAGWE SECONDARY SCHOOL F IMELDA SAMSON

171 NGANZA SECONDARY SCHOOL F IMELDA WINCHISLAUS

172 ST.LUISE MBINGA GIRLS SEC. SCHOOL F IMELDA ALOIS CHALLE

173 ROSMINI SECONDARY SCHOOL F IMELDA DOMINICK ISSANGYA

174 UWEMBA SECONDARY SCHOOL F IMELDA ERICK NGOWO

175 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F IMELDA H KABEREGE

176 IVUMWE SECONDARY SCHOOL F IMELDA J KOMBA

177 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F IMELDA J MBUNDA

178 DAREDA SECONDARY SCHOOL F IMELDA JANE SAPALI

179 ISIMILA SECONDARY SCHOOL F IMELDA JOHN SANGA

180 LUKOLE SECONDARY SCHOOL F IMELTHA NOLASCO

181 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE MBYAZITA

182 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE MLIGO

183 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE MNGARA

184 IVUMWE SECONDARY SCHOOL F JACKLINE MOSES

185 PANDAHILL SECONDARY SCHOOL F JACKLINE MSWIMA

186 MARIAN GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKLINE MTUI

187 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F JACKLINE MWATUKA

188 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE NESTORY

189 DUTWA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE OBARE

190 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKLINE ONESMO

191 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKLINE PETER

192 MAKAMBAKO SECONDARY SCHOOL F JACKLINE PHAUSTINE

193 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F JACKLINE RICHARD

194 MBEYA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE RWEYEMAMU

195 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F JACKLINE SEVERINE

196 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL F JACKLINE SHITINDI

197 NGANZA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE SIMON

198 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F JACKLINE STEPHEN

199 ZOGOWALE SECONDARY SCHOOL F JACKLINE TEMU

200 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F JACKLINE A BWANA

201 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F KASSANA M MANYANDA

202 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F KATALINA LUCHAGULA DEUS

203 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL F KATARINA BAKARI ALLY

204 DAREDA SECONDARY SCHOOL F KATARINA EPHRAIM MOLLA

205 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F KATARINA MASSAWE WENSESLAUS

206 MARIAN GIRLS SECONDARY SCHOOL F KATRINA N MTINANGI

207 TAQWA SECONDARY SCHOOL F KAUMBYA AUGUSTINE FAUSTINE

208 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F KAUNDIME MUHINA ABDALLAH

209 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F KAUTHAR ALLY NYONI

210 KILAKALA SECONDARY SCHOOL F KAUYE K LWANGA

211 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F KAUYEROSE A BOTTO

212 MAJENGO SECONDARY SCHOOL F KAWTHAR MOHAMED ABDI

213 HURUMA GIRLS SECONDARY SCHOOL F KEFLEN BUNANI

214 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F KEFRENE P KISUSI

215 MARIAN GIRLS SECONDARY SCHOOL F KELLEN METTA

216 NGANZA SECONDARY SCHOOL F KELLEN MWAIJUMBA

217 CANOSSA SECONDARY SCHOOL F KELLY A MLEH

218 MAJENGO SECONDARY SCHOOL F KEMIGISHA JOANITA

219 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F KEMILEMBE MUGANYIZI

220 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL F KEMILEMBE C KATIKIRO

221 KIWELE SECONDARY SCHOOL F LATIFA I MOHAMED

222 LUPALILO SECONDARY SCHOOL F LATIFA I SELEMAN

223 USANGI DAY SECONDARY SCHOOL F LATIFA IDDI JUMA

224 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F LATIFA J MKENGA

225 PIUS SECONDARY SCHOOL F LATIFA JUMANNE DOTTO

226 LUGALO SECONDARY SCHOOL F LATIFA L MUNISI

227 MTWARA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F LATIFA M HASSAN

228 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F LATIFA MASHAKA NGWAYA

229 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F LATIFA MOHAMED OMARI

230 SANGU SECONDARY SCHOOL F LATIFA MOHAMEDI MUYA

231 LONDONI SECONDARY SCHOOL F LATIFA MROPE SELEMANI

232 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F LATIFA NASSORO YAHYA

233 AL-KHEIR ISLAMIC GIRLS SEMINARY F LATIFA OMARY MOHAMMEDI

234 MRINGA SECONDARY SCHOOL F LATIFA R ISSA

235 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F LATIFA R KIDULI

236 KIRINJIKO ISLAMIC SEMINARY F LATIFA R MCHANA

237 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F LATIFA S ALLY

238 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F LATIFA S MARUZUKU

239 PIUS SECONDARY SCHOOL F LATIFA S MOHAMEDI

240 RUVU SECONDARY SCHOOL F LATIFA S NJENGA

241 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA E SWAI

242 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA ELISANTE THOMAS

243 ZOGOWALE SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA EMANUEL MBILINYI

244 WAJA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA F MNENEY

245 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA FANUEL MLACHA

246 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA FRANCIS HAULE

247 DAREDA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA GABRIEL LAKWAY

248 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA GODLOVE KIULA

249 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA GREGORY KIGOSI

250 SCOLASTICA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA HUBERTH SENGA

251 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA J BURA

252 LUGEYE SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA J LAMECK

253 MBEYA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA J LUKONDO

254 DAKAWA HIGH SCHOOL F MAGDALENA JAMES KAPELELE

255 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA JOSEPH LESSERI

256 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F MAGDALENA JOSEPH TESHA

257 SWILLA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA K MBILINYI

258 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA K MUSHI

259 MBEZI SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA KABUNGA VICENT

260 VWAWA SECONDARY SCHOOL F MAGDALENA L MWADANGALA

261 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F NAIMA HARUNA ABDALLAH

262 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAIMA K MBOLELA

263 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F NAIMA M NASSOR

264 ST.CHRISTINA GIRL'S SCHOOL F NAIMA SALUM KASHORO

265 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F NAIMANA IBRAHIM

266 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F NAIMI PETER KILEO

267 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAIPHAT F MWAKISALE

268 AQUINAS SECONDARY SCHOOL F NAIRA RASHID MNUNDUMA

269 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAIRATH SHAKOOR

270 MUDIO ISLAMIC SEMINARY F NAIRO BAKARI MBWAMBO

271 KIFUNGILO GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAISHIKA JOHN MBWAMBO

272 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F NAISHIYE SAIGURAN

273 LOYOLA SECONDARY SCHOOL F NAISHOOKI WILBERT OLE-MBILLE

274 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F NAISHORWA LOIBANGUTI MERINYO

275 DODOMA SECONDARY SCHOOL F NAJA ABDUL MBWILO

276 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F NAJA ELIA MKONGWA

277 MASASI GIRLS SECONDARY SCHOOL F NAJENJWA GADI MBWAMBO

278 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F NAJJAT ALLY SINDO

279 DAKAWA HIGH SCHOOL F NAJMA SALUM

280 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F NAJMA SEMENI

281 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F OLIVA M GURTU

282 MAJENGO SECONDARY SCHOOL F OLIVA M LAGO

283 WAMA-NAKAYAMA SECONDARY SCHOOL F OLIVA MATHIAS KANANI

284 MANYUNYU SECONDARY SCHOOL F OLIVA SHIRIMA ERASTO

285 NGANZA SECONDARY SCHOOL F OLIVER GERALD

286 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F OLIVER HAMIS

287 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL F OLIVER NICODEMUS

288 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F OLIVER PASCHAL

289 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F OLIVER STEPHANO

290 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F OLIVER AMOS MDAMU

291 MAJENGO SECONDARY SCHOOL F OLIVER CHARLES MUNISI

292 MASAMA GIRLS SECONDARY SCHOOL F OLIVER E NDOSI

293 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL F OLIVER FIDELIS MERERE

294 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F OLIVER H KESSY

295 DODOMA SECONDARY SCHOOL F OLIVER JOHN ANATORY

296 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F OLIVER L KOROSO

297 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F OLIVER M GWAKISA

298 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F OLIVER M JOSEPH

299 MWANZA SECONDARY SCHOOL F OLIVER NYABAYANGO CHASSAMA

300 LUGALO SECONDARY SCHOOL F OLIVER ONESMO MKONGWA

301 DR. OLSEN SECONDARY SCHOOL F PASKALINA J SIKUKUU

302 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F PASKALINA JULIUS MAHEMBE

303 URAMBO DAY SECONDARY SCHOOL F PASKALINA MPUME HUSSEIN

304 RUVU SECONDARY SCHOOL F PASKALINA N HHANDO

305 IGOWOLE SECONDARY SCHOOL F PASKALINA OTUMARY MGENI

306 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL F PASKALINA PAUL HINYUYE

307 AHMES SECONDARY SCHOOL F PASKAZIA AUDAX

308 MWANZA SECONDARY SCHOOL F PASKAZIA BISEKO

309 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASKAZIA DAUSON

310 LORETO GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASKAZIA JACOB

311 MAKONGO SECONDARY SCHOOL F PASKAZIA MABULA

312 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL F PASKAZIA K PAUL

313 MARIAN GIRLS SECONDARY SCHOOL F PASQUITA ALMA SYLVESTER MAHUWI

314 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F PATISTA ADRIANO MWIRU

315 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL F PATMOS SENI

316 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F PATRA JONAS MLAKI

317 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F PATRESIA M MLOGI

318 DUTWA SECONDARY SCHOOL F PATRICIA ADEN

319 MWANZA SECONDARY SCHOOL F PATRICIA ANTONY

320 KASOMA SECONDARY SCHOOL F PATRICIA BARNABAS

321 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F PUDENSIANA EMMANUEL

322 JANGWANI SECONDARY SCHOOL F RACHEL FERDINAND MAHAVILE

323 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F RACHEL FRANCIS BASU

324 LUGALO SECONDARY SCHOOL F RACHEL GEHAZ MBEYELA

325 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F RACHEL GOODLUCK KENNY

326 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F RACHEL ISAYA MWAKIBETE

327 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F RACHEL J MABISA

328 KIFARU SECONDARY SCHOOL F RACHEL J MUSSA

329 MSOLWA SECONDARY SCHOOL F RACHEL J MWAKAMBINDA

330 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F RACHEL J STANFORD

331 MBEYA SECONDARY SCHOOL F RACHEL JAMES SIBALE

332 NORTHERN HIGHLANDS SECONDARY SCHOOL F RACHEL JOHN MSIGARA

333 URAMBO DAY SECONDARY SCHOOL F RACHEL JOSHUA MSAMBA

334 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL F RACHEL JULIAS MUBHANGA

335 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F RACHEL KULWA JAPAN

336 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F RACHEL L ALOYCE

337 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F RACHEL LUTENGANO MWAKIFWAMBA

338 MSANGENI SECONDARY SCHOOL F RACHEL M ELIAS

339 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F RACHEL M KAJELELO

340 TINDE GIRLS HIGH SCHOOL F RACHEL M LUBUNGA

341 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F RACHEL M MAKOBA

342 BONDENI SECONDARY SCHOOL F RAHMA A BAKARI

343 ST. THERESA OF THE CHILD JESUS F RAHMA ISSA NURU

344 ARUSHA GIRLS SECONDARY SCHOOL F REBECA ELISHA

345 MRINGA SECONDARY SCHOOL F REBECA MABULA

346 ARUSHA SECONDARY SCHOOL F REBECA J NELA

347 MAASAE GIRLS LUTHERAN SECONDARY SCH F REBECCA KORDUNI

348 ANNAGAMAZO SECONDARY SCHOOL F REDEMTHA SELESTINE MZOLA

349 MAASAE GIRLS LUTHERAN SECONDARY SCH F REGINA APATE

350 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL F REGINA E BENJA

351 MRINGA SECONDARY SCHOOL F REGINA EDWARD MWAMPINGE

352 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F REGINA HIRBA MANYA

353 MRINGA SECONDARY SCHOOL F REGINA J BUKULA

354 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL F REGINA L MOLLEL

355 BISHOP DURNING HIGH SCHOOL F REGINA P DAFFI

356 MRINGA SECONDARY SCHOOL F REGINA SAMWEL KITOSI

357 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL F REHEMA AKWILOMBE

358 ANNAGAMAZO SECONDARY SCHOOL F REHEMA ALOYCE

359 MAASAE GIRLS LUTHERAN SECONDARY SCH F REHEMA GRAYSON

360 MAASAE GIRLS LUTHERAN SECONDARY SCH F REHEMA JOSEPH

361 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F SABRINA ABDALLAH MWENDA

362 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL F SABRINA ALYSTIDIA LUKOSI

363 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F SABRINA B MNONJELA

364 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F SABRINA H SALUM

365 AL-HARAMAIN ISLAMIC SEMINARY F SABRINA I SULEIMAN

366 KAWAWA SECONDARY SCHOOL F SABRINA J SHEKIVULI

367 TUSIIME SECONDARY SCHOOL F SABRINA KHERI ALUTA

368 KIBOSHO GIRLS SECONDARY SCHOOL F SABRINA MOHAMED CHEMBERA

369 KIRAENI GIRLS SECONDARY SCHOOL F SABRINA RAMADHANI KAYANDA

370 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F SABRINA SAID HOTTY

371 MAKONGO SECONDARY SCHOOL F SABRINA TAHIL OMARY

372 OSHARA SECONDARY SCHOOL F SABRINAH H MAKANYAGA

373 MASASI GIRLS SECONDARY SCHOOL F SABUYI JOHN KATAMBI

374 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F SADA ALLY

375 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F SADA ATHUMAN

376 LUGALO SECONDARY SCHOOL F SADA BUDI

377 RUVU SECONDARY SCHOOL F SADA HALFANI

378 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F SADA MASUNGA

379 HIGHLANDS SECONDARY SCHOOL F SADA MPOSEWA

380 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F SADA SALUMU

381 AL-MUNTAZIR ISLAMIC SEMINARY F TATHEER SACHEDINA

382 UWEMBA SECONDARY SCHOOL F TATHNIMU N MEHRABI

383 LUPALILO SECONDARY SCHOOL F TATU ADAMU

384 IGUNGA SECONDARY SCHOOL F TATU AHAMADI

385 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F TATU ALLY

386 LUGEYE SECONDARY SCHOOL F TATU ALLY

387 NANGWANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F TATU ALLY

388 ZANAKI SECONDARY SCHOOL F TATU HABIBU

389 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F TATU HAMADI

390 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F TATU JUMA

391 RUVU SECONDARY SCHOOL F TATU KASSIM

392 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F TATU KASSIMU

393 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F TATU MANENO

394 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F TATU MOHAMED

395 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL F TATU MUHARAMI

396 MAKAMBAKO SECONDARY SCHOOL F TATU OMARY

397 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F TATU PHAUSTINE

398 RUVU SECONDARY SCHOOL F TATU RAMADHANI

399 MAKAMBAKO SECONDARY SCHOOL F TATU THABITI

400 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL F TATU TITUS

401 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F UPENDO D NYAKI

402 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL F UPENDO DAUDI MANYA

403 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F UPENDO DENICE KIMAMBO

404 KAREMA SECONDARY SCHOOL F UPENDO DONATUS MHENI

405 ANNAGAMAZO SECONDARY SCHOOL F UPENDO E ANDONGOLILE

406 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F UPENDO E LYIMO

407 PIUS SECONDARY SCHOOL F UPENDO E MMARI

408 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F UPENDO E MSELI

409 LUGOBA SECONDARY SCHOOL F UPENDO E MWAKIPOSA

410 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F UPENDO E URIO

411 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F UPENDO ELIJA MCHOMVU

412 JUDE SECONDARY SCHOOL F UPENDO EMANUEL KANUYA

413 BABATI DAY SECONDARY SCHOOL F UPENDO EMMANUEL RAMADHANI

414 IRKISONGO SECONDARY SCHOOL F UPENDO FILEX MMBANDO

415 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F UPENDO G ADAM

416 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL F UPENDO G MAKOKO

417 MBEZI SECONDARY SCHOOL F UPENDO G MDUMA

418 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F UPENDO G URONU

419 ST.MARY GORETI SECONDARY SCHOOL F UPENDO GAMALIELY MAFIE

420 MAWENZI SECONDARY SCHOOL F UPENDO GAUDENCE PETER

421 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL F VAILETH NICHOLAUS LUHWAVI

422 IRINGA GIRLS SECONDARY SCHOOL F VAILETH O MWANJALA

423 MWANZI SECONDARY SCHOOL F VAILETH ONESMO EZEKIEL

424 IVUMWE SECONDARY SCHOOL F VAILETH PETRO SANGA

425 MRINGA SECONDARY SCHOOL F VAILETH RICHARD CHAMI

426 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F VAILETH S MAYUGO

427 MAKAMBAKO SECONDARY SCHOOL F VAILETH S MWANGOLOMBE

428 SONGEA GIRLS SECONDARY SCHOOL F VAILETH SHOMORO NGULWA

429 KIFARU SECONDARY SCHOOL F VAILETH ULKWAY ISAYA

430 LONGIDO SECONDARY SCHOOL F VAILETH W ZACHARIA

431 FLORIAN SECONDARY SCHOOL F VAINES SIMON KINYOWA

432 LOLEZA SECONDARY SCHOOL F VAINESS EPHRAEM

433 MAGU SECONDARY SCHOOL F VAINESS LAURENCE

434 LUTHERAN JUNIOR SEMINARY F VAIRETI V MNGUTO

435 MZIZIMA SECONDARY SCHOOL F VAISHALI J SANGAR

436 UMOJA SECONDARY SCHOOL F VALDY ERICK KHAHIMA

437 KIUMA SECONDARY SCHOOL F VALELIA A MAHUNDI

438 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F VALENCEA M VENANCE

439 MWENDAKULIMA SECONDARY SCHOOL F VALENCIA DOMINICO

440 TABORA GIRLS SECONDARY SCHOOL F VALENTINA MORRIS

441 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F WEMA JOSEPH

442 KISHOJU SECONDARY SCHOOL F WEMA MAKOYE

443 WIZA SECONDARY SCHOOL F WEMA MBUKWA

444 LUFILYO SECONDARY SCHOOL F WEMA TIMOTH

445 TUMAINI SECONDARY SCHOOL F WEMA D KIGUMBE

446 VWAWA SECONDARY SCHOOL F WEMA E SHIMWELA

447 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F WEMA ENOS NTIBARUSIGA

448 KILAKALA SECONDARY SCHOOL F WEMA F MBOGONI

449 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F WEMA G ROBERT

450 CANOSSA SECONDARY SCHOOL F WEMA J KAJANGE

451 MBEYA SECONDARY SCHOOL F WEMA J KIBWEJA

452 NANGWA SECONDARY SCHOOL F WEMA JOHNSON NJAU

453 WENDA HIGH SCHOOL F WEMA MUSA STENES

454 TARAKEA SECONDARY SCHOOL F WEMA MWIGIRE DEO

455 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F WEMA NSANGARUFU MWAKIBETE

456 JUDE SECONDARY SCHOOL F WEMA OBED BETHUEL

457 HARRISON UWATA SECONDARY SCHOOL F WEMA Y NYUMILE

458 IFUNDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F WEMAELI JUMA

459 MANYUNYU SECONDARY SCHOOL F WEMAELI SIMON FURAHINI

460 MOROGORO SECONDARY SCHOOL F WENDE ISAACK NYATO

461 REGINAMUNDI GIRLS' SECONDARY SCHOOL F YOANA HERMAN THOMAS

462 WERUWERU SECONDARY SCHOOL F YOHANA A MBOYA

463 KONDOA GIRLS SECONDARY SCHOOL F YOHANA EFREM KESSY

464 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL F YOHANA I MAPHIE

465 NANGWA SECONDARY SCHOOL F YOHANA J GOJONJO

466 DAREDA SECONDARY SCHOOL F YOHANA J JOSEPHAT

467 MASWA GIRLS SECONDARY SCHOOL F YOHANA JOHN MOMBURI

468 RUVU SECONDARY SCHOOL F YOHANA SHAO GELAS

469 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F YOHANA T GIRAY

470 KIBONDO SECONDARY SCHOOL F YOKEBETH EMMANUEL NONI

471 SWILLA SECONDARY SCHOOL F YOKEBETH GERSON KONGA

472 ILEJE SECONDARY SCHOOL F YOKEBETH SAMWEL DHAHABU

473 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL F YOLANDA KOMBA

474 CHIEF IHUNYO SEC SCHOOL F YOLANDA ATANASI MWENDA

475 DAREDA SECONDARY SCHOOL F YOLANDA CHARLES TARIMO

476 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F YOLANDA FAUSTIN KIMARO

477 ITAMBA SECONDARY SCHOOL F YOLANDA N KIKOTI

478 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL F YOSEPHA CHESKO NYAKUNGA

479 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL F YOSEPHA MARTIN KOMBA

480 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL F YOSEPHA SAMWEL MAPUNDA

481 JAMHURI SECONDARY SCHOOL F ZAINAB M HAMIS

482 NGANZA SECONDARY SCHOOL F ZAINAB M HASSANI

483 NGANZA SECONDARY SCHOOL F ZAINAB M IBRAHIM

484 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINAB MIKIDADI JUMA

485 MACHAME GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINAB MKONDYA SAID

486 KOROGWE GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINAB MOHAMED LIMO

487 MPANDA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINAB MOHAMED SEIF

488 ST.MARY'S MAZINDE JUU SEC. SCHOOL F ZAINAB MUSSA MKWANDA

489 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL F ZAINAB S WAZIRI

490 KIBASILA SECONDARY SCHOOL F ZAINAB SAID ABBASI

491 KUNDUCHI GIRLS ISLAMIC HIGH SCHOOL F ZAINABU AHMAD

492 ASHIRA SECONDARY SCHOOL F ZAINABU ALLY

493 BWIRU GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINABU AUSI

494 MKOLANI SECONDARY SCHOOL F ZAINABU CHANDE

495 SONGE SECONDARY SCHOOL F ZAINABU EMMANUEL

496 NEW ERA SECONDARY SCHOOL F ZAINABU FERUZI

497 IFAKARA SECONDARY SCHOOL F ZAINABU HAMAD

498 FOREST HILL SECONDARY SCHOOL F ZAINABU IDDI

499 MTWARA GIRLS SECONDARY SCHOOL F ZAINABU KAMBONA

500 BAOBAB SECONDARY SCHOOL F ZAINABU KIMAYA

501 TARIME SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH U KAPOSO

502 MATAI SECONDARY SCHOOL M ABDALLAH YUSUPH OPPY

503 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M ABDARAH JUMA

504 KISIWANI SECONDARY SCHOOL M ABDARAHAMANI TWAHA MTAITA

505 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M ABDARAHMAN J KISOMA

506 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M ABDI CHAULA

507 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M ABDI HASSANI

508 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M ABDI JABU

509 ITIGI SECONDARY SCHOOL M ABDI MASIKU

510 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M ABDI SHABAN

511 LOMWE SECONDARY SCHOOL M ABDI YUSUPH

512 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M ABDI A HOSSENI

513 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M ABDI ALLY MBOGO

514 SAME SECONDARY SCHOOL M ABDI HAMISI SALIMU

515 PUGU SECONDARY SCHOOL M ABDI HATIBU SELEMANI

516 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M ABDI K DIMOSO

517 AL-HARAMAIN ISLAMIC SEMINARY M ABDI P HASSANI

518 MATAKA SECONDARY SCHOOL M ABDI RAMADHANI KHALIFA

519 NGUDU SECONDARY SCHOOL M ABDI RAMADHANI MOLELI

520 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M ABDIEL MATHIAS

521 SAME SECONDARY SCHOOL M ABDIEL MRISHO SIMBA

522 MINAKI SECONDARY SCHOOL M ABDILAH ALLY

523 MINAKI SECONDARY SCHOOL M ABDILAH ABEID MNYAGANE

524 AZANIA SECONDARY SCHOOL M ABDILAH S MAGILA

525 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M ABDILAH SAID SHIRIMA

526 KYELA SECONDARY SCHOOL M ABDILAHI HALIFA IBUMA

527 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M ABDILAHI J HAJI

528 LWANDAI SECONDARY SCHOOL M ABDILAHI R SAIDI

529 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M ABDILAHI S MBONDE

530 MWENGE SECONDARY SCHOOL M ABDILAHI SHABANI HUSSEIN

531 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M ABDILLAH AHMADI

532 KIBITI SECONDARY SCHOOL M ABDILLAH DADI NURDIN

533 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M ABDILLAH ISMAILY BAKARI

534 KIRINJIKO ISLAMIC SEMINARY M ABDILLAH M KASSIM

535 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M ABDILLAH MOHAMMED AMOUR

536 AL-HARAMAIN ISLAMIC SEMINARY M ABDILLAH S SELEMANI

537 GALANOS SECONDARY SCHOOL M ABDILLAHI HAMISI

538 LILIAN KIBO SECONDARY SCHOOL M ABDILLAHI R HAJI

539 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M ABDILLAHI R MANSOUL

540 MOROGORO SECONDARY SCHOOL M ABDIN HARUNA

541 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M ABDISALAN B OSMAN

542 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M ABDISHAKUR ABDUL

543 RULENGE SECONDARY SCHOOL M ABDON BUSEGA

544 KABANGA SECONDARY SCHOOL M ABDON DAUDI

545 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M ABDON MODEST

546 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M ABDON VENEDEUS

547 MAKITA SECONDARY SCHOOL M ABDON ABDON KAPINGA

548 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M ABDON EDWIN MBUNGU

549 NYERERE SECONDARY SCHOOL M ABDON FRUMENCE MSACKY

550 LULUMBA SECONDARY SCHOOL M ABDON J ABDON

551 KIBITI SECONDARY SCHOOL M ABDU ABDALLAH

552 NDANDA SECONDARY SCHOOL M ABDU MUHIDINI

553 BEROYA SECONDARY SCHOOL M ABDU KASSIM MLANGA

554 GALANOS SECONDARY SCHOOL M ABDU M SAMULI

555 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL M ABDU S MBIKU

556 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M ABDU Y MPANGAMAWE

557 KARATU SECONDARY SCHOOL M ABDUEL S MAEDA

558 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M ABDUKADIR ZAIDI MATUTU

559 PUGU SECONDARY SCHOOL M ABDUKADIRI SHUNGU MADARAKA

560 CORNERSTONE LEADERSHIP SECONDARY SCHOOL M ABDUL AHMADI

561 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M ABDUL ISAYA

562 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M ABDUL ISDORY

563 NYAMPULUKANO SECONDARY SCHOOL M ABDUL KALUNGA

564 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M ABDULATIFU ISMAIL

565 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M ABDULATIFU TAMIMU ZIDADU

566 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M ABDULAZACK HAMIS FARIJALA

567 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M ABDULAZACK S BAKARI

568 SHAMBALAI SECONDARY SCHOOL M ABDUL-AZIZ M MZIMBIRI

569 MATAKA SECONDARY SCHOOL M ABDUL-AZIZ S EL-MIYAKHY

570 LWANDAI SECONDARY SCHOOL M ABDULBASTI T ALLY

571 ROSMINI SECONDARY SCHOOL M ABDULHAMID KHALID BYANAKU

572 SHAMBALAI SECONDARY SCHOOL M ABDULI IBRAHIMU

573 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M ABDULIZAIDU ADAMU MADODO

574 MUHEZA HIGH SCHOOL M ABDULKADIRI MUHUDI

575 LORD BADEN POWELL MEMORIAL SEC. SCHOOL M ABDULKARIM HAMISI

576 GALANOS SECONDARY SCHOOL M ABDULKARIM SAIDI

577 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M ABDULKARIM SAADUN TEMBA

578 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M BAKARI O ALLY

579 GALANOS SECONDARY SCHOOL M BAKARI O ALLY

580 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M BAKARI OMARI BAKARI

581 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M BAKARI QWANTSAWE NINGA

582 SANGU SECONDARY SCHOOL M BAKARI R MAJUNGA

583 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M BAKARI RAJABU ROZO

584 NDANDA SECONDARY SCHOOL M BAKARI RASHIDI BAKARI

585 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M BAKARI RASHIDI KHOZZA

586 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M BAKARI S CHIWAULA

587 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M BAKARI S KALAMA

588 KIUMA SECONDARY SCHOOL M BAKARI S NAMBWINYA

589 TANDAHIMBA SECONDARY SCHOOL M BAKARI S RAJABU

590 MINAKI SECONDARY SCHOOL M BAKARI S SAID

591 SAME SECONDARY SCHOOL M BAKARI SAID NGWIJO

592 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M BAKARI SAID NTAKITUGU

593 MKUU SECONDARY SCHOOL M BAKARI SALIMU HUSSEIN

594 NDANDA SECONDARY SCHOOL M BAKARI SANDALI MUHAJI

595 PIUS SECONDARY SCHOOL M BAKARI SUZO NGONGI

596 ILONGERO SECONDARY SCHOOL M BAKARI TWAZIHIRWA HOYANGE

597 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M BAKARI W RAMADHANI

598 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M BAKARI Y SALIMU

599 MBEKENYERA SECONDARY SCHOOL M BAKARI YUSUFU AHMADI

600 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M BAKII IBRAHIM HAMZA

601 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M BAKIRI M CHANDE

602 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M BAKULILEHI THOMAS

603 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M BALA PUNGUJA

604 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M BALATI RAJABU

605 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M BALDWIN JOSEPH

606 GALANOS SECONDARY SCHOOL M BALEKELE W CHELEHANI

607 MWENGE SECONDARY SCHOOL M BALELE DALUSI

608 NYAMPULUKANO SECONDARY SCHOOL M BALELE FELECIAN

609 KIBITI SECONDARY SCHOOL M BALELE KAFUMU

610 NDANDA SECONDARY SCHOOL M BALELE NG'HABI

611 SHAMBALAI SECONDARY SCHOOL M BALELE A KIANGI

612 MAMBWE SECONDARY SCHOOL M BALENGA SAID BALENGA

613 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M BALIKAMA S POLIDORI

614 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M BALIO KALASHANI

615 NEWMAN SECONDARY SCHOOL M BALISESA HUME

616 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M BALOZI KARDUNI

617 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M BALTAZAL HELBERT BALANZIZE

618 KWIRO SECONDARY SCHOOL M BALTAZAR DEOGRATIUS

619 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M BALTAZAR L ARBOGAST

620 GEITA SECONDARY SCHOOL M BALTAZAR MICHAEL MSOMA

621 UMBWE SECONDARY SCHOOL M BALTAZAR N LEMA

622 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M BALTAZARI J MAPUNDA

623 AGAPE LUTHERAN J SEMINARY M BALTAZARI ROGASIAN MASSAWE

624 ST. VICENT SECONDARY SCHOOL M BALTAZARY METHOD

625 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M BALTAZARY MARK ASSENGA

626 KWIRO SECONDARY SCHOOL M BALTAZARY P MGINA

627 MWENGE SECONDARY SCHOOL M BALTHAZARY MASOLWA JAMES

628 BARIADI SECONDARY SCHOOL M BALUHYA DOMINIC

629 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M BALUHYA M PAUL

630 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M BAMBINO ALBERTO MGONZO

631 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M BANATH DANIEL

632 MWENGE SECONDARY SCHOOL M BANE ROBSON MATARI

633 IWAWA SECONDARY SCHOOL M BANGA M KARADENGA

634 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M BANGAYE POLYCARPO JEGWE

635 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M BANZI S KIKO

636 MOSHI SECONDARY SCHOOL M BAPTISON MOSES KITANGALALA

637 SAME SECONDARY SCHOOL M BAPTIST MAPUNDA

638 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M BAPTIST JOHN NDUNGURU

639 MATAKA SECONDARY SCHOOL M BARACK MKOMBA

640 RUTABO SECONDARY SCHOOL M BARAGETI ALFRED

641 ST.MAURUS CHEMCHEMI SECONDARY SCHOOL M BARAKA MICHAEL

642 NEW ERA SECONDARY SCHOOL M BARAKA MSIGALA

643 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M BARAKA MWAKYELU

644 MEATU SECONDARY SCHOOL M BARAKA MWANGUNDA

645 BUPANDAGILA SECONDARY SCHOOL M BARAKA MWIHAGANI

646 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M BARAKA NKYALE

647 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M BARAKA RAMADHANI

648 MATAKA SECONDARY SCHOOL M BARAKA REUBEN

649 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M BARAKA SELEMAN

650 MWENGE SECONDARY SCHOOL M BARAKA SHABAN

651 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M BARAKA SHIBANDA

652 KIBITI SECONDARY SCHOOL M BARAKA SIMON

653 SUMBAWANGA SECONDARY SCHOOL M BARAKA SIMON

654 MWENGE SECONDARY SCHOOL M BARAKA WILSON

655 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M BARAKA YUSUPH

656 MINAKI SECONDARY SCHOOL M BARAKA ZEPHANIA

657 MINAKI SECONDARY SCHOOL M BARAKA A MAZEMLE

658 MINAKI SECONDARY SCHOOL M BARAKA A MZAVA

659 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M BARAKA AFRAEL NANYARO

660 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M CHARLES CORNEL

661 MINAKI SECONDARY SCHOOL M CHARLES COSMAS

662 HUMURA SECONDARY SCHOOL M CHARLES DERICK

663 TARIME SECONDARY SCHOOL M CHARLES DIONISE

664 KARATU SECONDARY SCHOOL M CHARLES DODAY

665 TEGETA SECONDARY SCHOOL M CHARLES DONALD

666 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M CHARLES DONARD

667 SAME SECONDARY SCHOOL M CHARLES DONART

668 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M CHARLES EDWARD

669 KIBITI SECONDARY SCHOOL M CHARLES ELISHA

670 BOGWE SECONDARY SCHOOL M CHARLES EMMANUEL

671 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M CHARLES EZEKIEL

672 TAQWA SECONDARY SCHOOL M CHARLES GEORGE

673 TWIHULUMILE SECONDARY SCHOOL M CHARLES GERVAS

674 KARATU SECONDARY SCHOOL M CHARLES HARUNA

675 NGUDU SECONDARY SCHOOL M CHARLES HARUNA

676 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M CHARLES HERMAN

677 META SECONDARY SCHOOL M CHARLES JIDAI

678 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M CHARLES JILALA

679 MWENGE SECONDARY SCHOOL M CHARLES JISANGIYI

680 SANGU SECONDARY SCHOOL M CHARLES JOHN

681 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CHARLES JOHN

682 BARIADI SECONDARY SCHOOL M CHARLES JONATHAN

683 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CHARLES JOSEPH

684 VUDOI SECONDARY SCHOOL M CHARLES JOSEPH

685 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M CHARLES JUMA

686 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M CHARLES JUMA

687 MBEZI BEACH SECONDARY SCHOOL M CHARLES KANKILA

688 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M CHARLES KASSIM

689 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M CHARLES KIDALI

690 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M CHARLES KIDIMA

691 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M CHARLES KIMELA

692 MWENGE SECONDARY SCHOOL M CHARLES KWARA

693 ISONGOLE SECONDARY SCHOOL M CHARLES LUCAS

694 KONGWA SECONDARY SCHOOL M CHARLES LUNGWA

695 BUNDA SECONDARY SCHOOL M CHARLES MABAGALA

696 UYUI SECONDARY SCHOOL M CHARLES MAGESA

697 BARIADI SECONDARY SCHOOL M CHARLES MARCO

698 MWEMBENI SECONDARY SCHOOL M CHARLES MARWA

699 RUTABO SECONDARY SCHOOL M CHARLES MASATU

700 LINDI SECONDARY SCHOOL M CHARLES MASHAKA

701 TAQWA SECONDARY SCHOOL M CHARLES MASINDE

702 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M CHARLES MATHIAS

703 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M CHARLES MAYUNGA

704 ILULA SECONDARY SCHOOL M CHARLES MGANGAJI

705 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M CHARLES MHANDO

706 ST.MAURUS CHEMCHEMI SECONDARY SCHOOL M CHARLES MLOWEZI

707 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M CHARLES MNDOLWA

708 KALIUA SECONDARY SCHOOL M CHARLES MRISHO

709 MOSHI SECONDARY SCHOOL M CHARLES MSUKA

710 TARIME SECONDARY SCHOOL M CHARLES MSYANGI

711 SANGU SECONDARY SCHOOL M CHARLES MWAKISALU

712 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M CHARLES MWAMBA

713 ILBORU SECONDARY SCHOOL M CHARLES MWANGASA

714 ULAYASI SECONDARY SCHOOL M CHARLES MWANGU

715 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M CHARLES MWITA

716 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M CHARLES MWITA

717 KAGANGO SECONDARY SCHOOL M CHARLES MZAMBIA

718 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M CHARLES NDAMBO

719 ILULA SECONDARY SCHOOL M CHARLES NGOTORO

720 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M CHARLES NTEMI

721 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M CHARLES PASCAL

722 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M CHARLES PASCHAL

723 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M CHARLES EMMANUEL MAHEMBO

724 GALANOS SECONDARY SCHOOL M CHARLES EXAVIERRY MAPUNDA

725 IWAWA SECONDARY SCHOOL M CHARLES EZEKIEL ELTWAZA

726 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M CHARLES F MWANYANJE

727 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M CHARLES FULMENCE NACHAN

728 GALANOS SECONDARY SCHOOL M CHARLES G CHAMBO

729 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M CHARLES J ERENEST

730 MWENGE SECONDARY SCHOOL M CHARLES J KABIPI

731 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M CHARLES JOSEPH KAYOLO

732 AHMES SECONDARY SCHOOL M CHARLES K ODASI

733 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M CHARLES L MSIGWA

734 MINAKI SECONDARY SCHOOL M CHARLES LWANGA MAUNGILA

735 GALANOS SECONDARY SCHOOL M CHARLES M AUGUSTINO

736 MINAKI SECONDARY SCHOOL M CHARLES M BAHATI

737 ILONGERO SECONDARY SCHOOL M CHARLES M TALLA

738 MUHEZA HIGH SCHOOL M CHARLES MAGUZU TULI

739 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M CHARLES MARWA SYLVESTER

740 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M CHARLES MASALU BONIFACE

741 KARATU SECONDARY SCHOOL M DANIEL MWIKWABI

742 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M DANIEL MWINGIRA

743 MWANGA SECONDARY SCHOOL M DANIEL MWITA

744 GEITA SECONDARY SCHOOL M DANIEL NOAH

745 SUMBAWANGA SECONDARY SCHOOL M DANIEL NOAH

746 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL M DANIEL NTINDA

747 UMBWE SECONDARY SCHOOL M DANIEL OBADIA

748 BOGWE SECONDARY SCHOOL M DANIEL PASCHAL

749 NGUDU SECONDARY SCHOOL M DANIEL PAUL

750 SAME SECONDARY SCHOOL M DANIEL PETRO

751 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M DANIEL PHANUEL

752 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M DANIEL PROSPER

753 IGUNGA SECONDARY SCHOOL M DANIEL REUBEN

754 CHATO SECONDARY SCHOOL M DANIEL ROBERT

755 GOLDEN RIDGE SECONDARY SCHOOL M DANIEL ROBERT

756 MWENGE SECONDARY SCHOOL M DANIEL SADOCK

757 MOSHI SECONDARY SCHOOL M DANIEL SAID

758 VUDOI SECONDARY SCHOOL M DANIEL SAID

759 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M DANIEL SELEMAN

760 AZANIA SECONDARY SCHOOL M DANIEL SERYA

761 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M DANIEL SHADRACK

762 MBEYA SECONDARY SCHOOL M DANIEL SIMON

763 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M DANIEL SIMTOWE

764 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M DANIEL STEPHANO

765 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M DANIEL SUMBU

766 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M DANIEL THOBIAS

767 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M DANIEL UZIEL

768 TABORA BOYS SECONDARY SCHOOL M DANIEL VICENT

769 META SECONDARY SCHOOL M DANIEL WILLIAM

770 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M DANIEL WILLIAM

771 SAME SECONDARY SCHOOL M DANIEL YONA

772 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M DANIEL YUSTINE

773 KONGWA SECONDARY SCHOOL M DANIEL A KITINA

774 AZANIA SECONDARY SCHOOL M DANIEL A KONDO

775 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M DANIEL A MARSELI

776 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M DANIEL A MBELA

777 SANGU SECONDARY SCHOOL M DANIEL A MOGHA

778 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M DANIEL A MOLLEL

779 ILBORU SECONDARY SCHOOL M DANIEL A SHEKETO

780 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M DANIEL AKONAAY MATLE

781 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M DANIEL ALEX MWENDA

782 URU SEMINARY M DANIEL ALFRED AKARO

783 MINAKI SECONDARY SCHOOL M DANIEL AMOS MWAMLIMA

784 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M DANIEL ANDREA JULIUS

785 KIBITI SECONDARY SCHOOL M DANIEL ANTONI RAFAEL

786 MARA SECONDARY SCHOOL M DANIEL ARBOGAST MARAWITHI

787 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M DANIEL ASTERIO DANIEL

788 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M DANIEL ASUKILE MWAKALINGA

789 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M DANIEL AUGUSTINO MTUI

790 GEITA SECONDARY SCHOOL M DANIEL B MALUGU

791 DAREDA SECONDARY SCHOOL M DANIEL B MAYYO

792 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M DANIEL BALTAZARI NGOLI

793 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M DANIEL BARTHOLOMEO KYANDO

794 MAKIBA SECONDARY SCHOOL M DANIEL BENEDICT MASHIKU

795 MKUU SECONDARY SCHOOL M DANIEL BENJAMIN MILAO

796 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M DANIEL BILLULA MUSSA

797 BIHAWANA SECONDARY SCHOOL M DANIEL BOAY PETER

798 SWILLA SECONDARY SCHOOL M DANIEL BURTON NGANYULE

799 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M DANIEL C KAMBANGA

800 MINAKI SECONDARY SCHOOL M DANIEL C KITINJE

801 MSUFINI SECONDARY SCHOOL M DANIEL C NYAKEHE

802 AZANIA SECONDARY SCHOOL M DANIEL CALVIN LUSANDA

803 SIMBA WA YUDA M DANIEL CHACHA NYAGEKO

804 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M DANIEL J MGEYEKWA

805 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL M DANIEL J MGUNDA

806 BAOBAB SECONDARY SCHOOL M DANIEL JACOB SANGA

807 MWENGE SECONDARY SCHOOL M DANIEL JACOB WANYENJE

808 MATAKA SECONDARY SCHOOL M DANIEL JOHN NDIMBO

809 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M DANIEL JOHN NYENZA

810 MEATU SECONDARY SCHOOL M DANIEL K KIYUMBANI

811 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M DANIEL KASINDE MANG'WATA

812 GALANOS SECONDARY SCHOOL M DANIEL KIWANGO GEORGE

813 MWENGE SECONDARY SCHOOL M DANIEL L NCHUNGA

814 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M DANIEL LAWRENCE MKALAWA

815 MWENGE SECONDARY SCHOOL M DANIEL LEMA FRANK

816 KIBITI SECONDARY SCHOOL M DANIEL LIVINGSTONE KATANI

817 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M DANIEL LUCAS MTWEVE

818 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M DANIEL M BASAYA

819 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M DANIEL M BASESA

820 KISARAWE LUTHERAN JUNIOR SEMINARY M DANIEL M DANIEL

821 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M DANIEL M JOSEPH

822 MINAKI SECONDARY SCHOOL M DANIEL M MOLLEL

823 ILEJE SECONDARY SCHOOL M EDSON AHIMIDIWE MASSAWE

824 EAGLES SECONDARY SCHOOL M EDSON AMBILIKILE MWANKUSYE

825 KIBITI SECONDARY SCHOOL M EDSON BILLINGI FRANCISCO

826 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M EDSON D BULANDI

827 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EDSON D BWIRE

828 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EDSON E ERNEST

829 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M EDSON E KYARUZI

830 ILBORU SECONDARY SCHOOL M EDSON E MUVUNYI

831 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL M EDSON EDSON MBULLY

832 LWANGWA SECONDARY SCHOOL M EDSON EDSON MWAIHOJO

833 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M EDSON F KIBIKI

834 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EDSON F MPALASINGE

835 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M EDSON FRANK MWAMBASANGA

836 GREEN BIRD BOYS SECONDARY SCHOOL M EDSON GOODLUCK MASHAURI

837 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M EDSON GUSTAVO MALANDA

838 META SECONDARY SCHOOL M EDSON HUDSONI MSYANI

839 NDANDA SECONDARY SCHOOL M EDSON J TOGORO

840 TAQWA SECONDARY SCHOOL M EDSON JOSEPH TEMBA

841 TABORA BOYS SECONDARY SCHOOL M EDSON K NCHIMBI

842 ITENDE SECONDARY SCHOOL M EDSON KANISIUS MGIMBA

843 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M EDSON KOSTANTINO NYONI

844 MAGU SECONDARY SCHOOL M EDSON LEONARD GABRIEL

845 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M EDSON M MANENO

846 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M EDSON M SYLIVESTER

847 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M EDSON MURIMI LAWRENCE

848 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M EDSON N KEHA

849 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M EDSON N LAMECK

850 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M EDSON NYANZILA JOACHIM

851 LWANGWA SECONDARY SCHOOL M EDSON RAPHAEL KIKOTI

852 ILEJE SECONDARY SCHOOL M EDSON RICHARD MPONZI

853 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M EDSON ROBERT SANGA

854 GALANOS SECONDARY SCHOOL M EDSON S HARNAA

855 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M EDSON S LAIZER

856 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M EDSON S MOYO

857 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M EDSON SAMWEL MWAMBE

858 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M EDSON SETHI MBEMBATI

859 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M EDSON TITTUS NGANJI

860 ULAYASI SECONDARY SCHOOL M EDSON WILLIAM MWAKABUBA

861 KAWAWA SECONDARY SCHOOL M EDSON WISDOM MWAKYOMBE

862 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M EDSON Y MSANGI

863 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M EDSONI EDESIUS MBOGORO

864 SALESIAN SEMINARY M EDTRAUD EDDY HAULE

865 MOROGORO SECONDARY SCHOOL M EDWARD ADONGO

866 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M EDWARD ALOYCE

867 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M EDWARD DASTAN

868 UMBWE SECONDARY SCHOOL M EDWARD DISMAS

869 WENDA HIGH SCHOOL M EDWARD EMMANUEL

870 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M EDWARD FABIAN

871 KAHORORO SECONDARY SCHOOL M EDWARD FIDEL

872 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M EDWARD GASPER

873 OSWARD MANG'OMBE S S M EDWARD GEORGE

874 ILONGERO SECONDARY SCHOOL M EDWARD GIVISHON

875 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M EDWARD JAPHET

876 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M EDWARD JOKEYA

877 KISHOJU SECONDARY SCHOOL M EDWARD JOSEPH

878 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M EDWARD JOSEPH

879 MANGUANJUKI SECONDARY SCHOOL M EDWARD JOSEPH

880 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M EDWARD KADELYA

881 USA SEMINARY M EDWARD KENNEDY

882 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M EDWARD KIJAZI

883 MWANZA SECONDARY SCHOOL M EDWARD MAJALIWA

884 TARIME SECONDARY SCHOOL M EDWARD MANJANO

885 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M EDWARD MARTINE

886 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M EDWARD NICHOLAUS CHUNDWA

887 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M EDWARD PATRIC NDUNGURU

888 HANDENI SECONDARY SCHOOL M EDWARD S KISOTA

889 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M EDWARD STEVEN NGUMA

890 HANDENI SECONDARY SCHOOL M EDWARD W MUUGA

891 KIBITI SECONDARY SCHOOL M EDWARD Z KILELE

892 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M EDWIN MAGIRI

893 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M EDWIN MUGIZI

894 MINAKI SECONDARY SCHOOL M EDWIN RICHARD

895 KIBITI SECONDARY SCHOOL M EDWIN ROMANI

896 MOMBO SECONDARY SCHOOL M EDWIN WILFRED

897 RUHUWIKO SECONDARY SCHOOL M EDWIN BLASDUS KOWELO

898 ITULAHUMBA SECONDARY SCHOOL M EDWIN BOSCO FWENI

899 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL M EDWIN CHARLES LUPEMBE

900 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M EDWIN D MASOI

901 RUHUWIKO SECONDARY SCHOOL M EDWIN EDWIN HAULE

902 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M EDWIN EMMANUEL MWANDALIMA

903 GENESIS HIGH SCHOOL M EDWIN EPHRAYM MTOVANO

904 KISHAPU SECONDARY SCHOOL M FADHILI Y JUMA

905 MOSHI SECONDARY SCHOOL M FADHILI ZEBEDAYO MVENA

906 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M FADHILI ZEBEDAYO MWANGONELA

907 GALANOS SECONDARY SCHOOL M FADHILIANO Z NDANYOYE

908 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M FADHILY OMARY

909 LUKOLE SECONDARY SCHOOL M FADHIRI BIGAMBOBYABO KAROLI

910 MWINYI SECONDARY SCHOOL M FADHIRI JUMA CHAMBUA

911 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M FADI MAJORA

912 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M FADIGA HAMISI

913 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M FADO CHEYO

914 AZANIA SECONDARY SCHOOL M FAHAD A JUMA

915 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M FAHAD ABDUL-AZIZ BREIK

916 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M FAHAD I TWAHA

917 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M FAHAD S MWINYI

918 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M FAHADI ABDALAH MUSSA

919 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M FAHADI ZB JUMA

920 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M FAHAMI ABDALAH MUSSA

921 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M FAHAMU FIKENI GIDION

922 HIGHLANDS SECONDARY SCHOOL M FAHAMU MODESTUS KALENGA

923 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M FAHARUDIN ZUBERY

924 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M FAHD S NAMAHALA

925 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL M FAHIM SALUM ISMAIL

926 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M FAHIMU YAHAYA ALLY

927 AL-MUNTAZIR ISLAMIC SEMINARY M FAHMI ABDUL AME

928 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M FAHMI BAKAR SULEIMAN

929 NDANDA SECONDARY SCHOOL M FAHMI S YUSUPHU

930 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M FAI A MOGHA

931 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M FAIDA ANDREA

932 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M FAIDA BUNDALA

933 MATAKA SECONDARY SCHOOL M FAIDA EMMANUEL

934 KARATU SECONDARY SCHOOL M FAIDA MIBAKO

935 LULUMBA SECONDARY SCHOOL M FAIDA K EDWARD

936 NKASI SECONDARY SCHOOL M FAIDA LUSHOMI MASHIKU

937 OCEAN SECONDARY SCHOOL M FAIDHAKI RASHIDI

938 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M FAISAL I KANYANDEKWE

939 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M FAISAL M MOHAMED

940 AMANI ABEID KARUME SECONDARY SCHOOL M FAISAL M TUSA

941 EDMUND-RICE-SINON SECONDARY SCHOOL M FAISON FRANCO MARIKA

942 OSWARD MANG'OMBE S S M FAITH M ELIAKIMU

943 NDANDA SECONDARY SCHOOL M FAIZER ANAFI

944 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M FAKHI B MOHAMED

945 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M FAKII ATHUMANI MANJAULE

946 MWENGE SECONDARY SCHOOL M FALAULA PASTORY

947 MEATU SECONDARY SCHOOL M FALE NDEKELWA

948 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M FALESI WILLIAM NTUNUNGU

949 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M FALESY SANGA

950 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M FALIJI P SHITINDI

951 ANNE MARIE SECONDARY SCHOOL M FALMEN J FALMEN

952 MAGU SECONDARY SCHOOL M FAMBO KIDANHA

953 LULUMBA SECONDARY SCHOOL M FAMILY MOSES MILAMBI

954 MPWAPWA SECONDARY SCHOOL M FANAKA KAMWELA

955 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M FANIKIO KAMOJA FUNGO

956 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M FANIKIO R TOZO

957 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M FANIKIWA PETRO

958 IGAWILO SECONDARY SCHOOL M FANIKIWA WILLIAM MTAFYA

959 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M FANTASHIRU RWEHABURA MUSSA

960 LINDI SECONDARY SCHOOL M FANUEL BWIRE

961 CHIEF KIDULILE SECONDARY SCHOOL M FANUEL GASPER

962 MATAI SECONDARY SCHOOL M FANUEL JUMANNE

963 MBALIZI SECONDARY SCHOOL M FANUEL MWAISUMO

964 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M FANUEL MWAZEMBE

965 MVUMI SECONDARY SCHOOL M FANUEL A MICHAEL

966 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M FANUEL A MTAWA

967 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M FARAJAEL N TUMAIYO

968 MINAKI SECONDARY SCHOOL M FARAJI ALLY

969 KIUMA SECONDARY SCHOOL M FARAJI CHINGAMBE

970 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M FARAJI FADHILI

971 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M FARAJI MAHAMUDU

972 IWAWA SECONDARY SCHOOL M FARAJI MAHANJU

973 KIBITI SECONDARY SCHOOL M FARAJI A MPOSO

974 KIBITI SECONDARY SCHOOL M FARAJI A MSUMI

975 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M FARAJI H BURIANI

976 SUMBAWANGA SECONDARY SCHOOL M FARAJI I HABIBU

977 KIUMA SECONDARY SCHOOL M FARAJI MACHEMBA MTILA

978 GALANOS SECONDARY SCHOOL M FAREED YAHYA

979 BARIADI SECONDARY SCHOOL M FARES ALEX

980 SIMBA WA YUDA M FARES G DAUD

981 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M FARIAS B RUBUGA

982 OLD SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M FARID R ALLY

983 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M FARIDI RAMADHANI ABDI

984 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M FARIDI Y WANDU

985 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M FARIJALA HUDDY KIANGI

986 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M FARIJI JERRY KASIBA

987 SHAMBALAI SECONDARY SCHOOL M FARIJI RAMADHAN MBWAMBO

988 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M FASADI MOHAMEDI SALANGA

989 KIBITI SECONDARY SCHOOL M FATAEL ADOLF TILYA

990 NKASI SECONDARY SCHOOL M FAUSTIN BUNZALI

991 SUMBAWANGA SECONDARY SCHOOL M FAUSTIN DAMIAN

992 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M GASTO P SWAI

993 KARATU SECONDARY SCHOOL M GASTO PAUL ANDREA

994 USAGARA SECONDARY SCHOOL M GASTO R RENATUS

995 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M GASTO REGNALD MNG'ANYA

996 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M GASTO S SHIRIMA

997 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M GASTO SELESTINE ROBERT

998 GANAKO SECONDARY SCHOOL M GASTO SINEDI MGULA

999 VUNJO SECONDARY SCHOOL M GASTO USHAKI FREDERK

1000 RUHUWIKO SECONDARY SCHOOL M GASTON AUREUS MBUNDA

1001 COASTAL SECONDARY SCHOOL M GASTON B NGUVILA

1002 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M GASTON B SANGA

1003 GENESIS HIGH SCHOOL M GASTON BAILONY TWEVE

1004 SADANI SECONDARY SCHOOL M GASTON CORIBI MASHOKO

1005 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M GASTON GILBERT GABRIEL

1006 GALANOS SECONDARY SCHOOL M GASTON RWITANA RWEGASIRA

1007 ST.JOSEPH'S CATHEDRAL SECONDARY SCHOOL M GASTON W MAKISHE

1008 UMBWE SECONDARY SCHOOL M GASTON WILLIUM MTEI

1009 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M GASTONE MALEMBO

1010 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M GASTONY PETER NZASULE

1011 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M GATENGA J NYAMORONGA

1012 UWATA SECONDARY SCHOOL M GAUDANCE NSUBIRI

1013 META SECONDARY SCHOOL M GAUDANCE RAYNER NDOKOMA

1014 SANGU SECONDARY SCHOOL M GAUDENCE MWAKAJOKA

1015 UMBWE SECONDARY SCHOOL M GAUDENCE MWAKILATU

1016 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M GAUDENCE A MWAKIPESILE

1017 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M GAUDENCE ABRAHAM KESSY

1018 SADANI SECONDARY SCHOOL M GAUDENCE ANZAAMEN ULOMI

1019 MKUU SECONDARY SCHOOL M GAUDENCE BONIPHACE CHUWA

1020 GEITA SECONDARY SCHOOL M GAUDENCE C MOHELE

1021 USAGARA SECONDARY SCHOOL M GAUDENCE JOSHUA MWANGOMALE

1022 NYERERE SECONDARY SCHOOL M GAUDENCE KAVISHE DISMAS

1023 WENDA HIGH SCHOOL M GAUDENSI G SWAI

1024 ILONGERO SECONDARY SCHOOL M GAUDENSI L THOBIASI

1025 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M GAUDIN GEORGE

1026 KIUMA SECONDARY SCHOOL M GAVANA JUMA

1027 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M GAYO G MWANGOSI

1028 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M GAYYO DANIEL KINYAMAGOHA

1029 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M GEAZ AMAN KINYAMAGOHA

1030 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M GEAZ E MASILU

1031 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M GEAZI A GEORGE

1032 MWIKA SECONDARY SCHOOL M GEBRA MELKIORY MAGEUZI

1033 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M GEBRA SHAO CHRISPINI

1034 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M GEBRA WILBROD MOSHA

1035 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M GEBU NG'WIGULU

1036 VUDOI SECONDARY SCHOOL M GEHAZI GEOPHREY MAKOGA

1037 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M GELARD PROSPER JACKSON

1038 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M GELARD THOMPHSON NGUNYALI

1039 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M GELAS SEVERINE KANINII

1040 KANYIGO SECONDARY SCHOOL M GELEVAS M LEONS

1041 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M GELEWA EDWARD

1042 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M GELGORY PETRO

1043 TANZANIA ADVENTIST SECONDARY SCHOOL M GELIGA D MSHOLLA

1044 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M GELLY MWAMKAMBA

1045 MAFINGA SEMINARY M GELWIN JOHN NZIKU

1046 KANYIGO SECONDARY SCHOOL M GEMA B LAUREAN

1047 MWIKA SECONDARY SCHOOL M GEMINO B PETER

1048 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M GENES BENEDICT MUSHI

1049 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M GENES FRIMINI JASTINI

1050 MUHEZA HIGH SCHOOL M GENES SHAYO PETER

1051 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M GENYA ISANGULA

1052 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL M GEO CHARLES

1053 MWENGE SECONDARY SCHOOL M GEOFLEY DOTTO

1054 RUTABO SECONDARY SCHOOL M GEOFRED GABRIEL

1055 TABORA BOYS SECONDARY SCHOOL M GEOFREY HERMAN MAHUNDI

1056 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M GEOFREY HERMAN MSAMBULE

1057 GALANOS SECONDARY SCHOOL M GEOFREY J KANUYA

1058 KIBITI SECONDARY SCHOOL M GEOFREY J NTETELE

1059 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M GEOFREY JACKSON MDETE

1060 HAGAFILO SEC. SCHOOL M GEOFREY JOAS TOSSY

1061 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M GEOFREY JOEL SANGA

1062 MWAKAVUTA SECONDARY SCHOOL M GEOFREY JONAS MLIMA

1063 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M GEOFREY JOSEPHAT BALINDE

1064 GALANOS SECONDARY SCHOOL M GEOFREY M ALEX

1065 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M GEOFREY M MWEMI

1066 MINAKI SECONDARY SCHOOL M GEOFREY PETER MOLLEL

1067 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M GEOFREY S ITEMBE

1068 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M GEOFREY THOBIAS MDEDE

1069 COASTAL SECONDARY SCHOOL M GEOFREY V MKALANGA

1070 MWAKAVUTA SECONDARY SCHOOL M GEOGRE I MURO

1071 KIBITI SECONDARY SCHOOL M GEOPHREY GIDION

1072 MINAKI SECONDARY SCHOOL M GEOPHREY AYOUB KIHWELO

1073 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M GEORGE ALEDIWANI

1074 BINZA SECONDARY SCHOOL M GEORGE ALEXANDER

1075 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M GEORGE AMOS

1076 MWENGE SECONDARY SCHOOL M GEORGE ANDREW

1077 KWIRO SECONDARY SCHOOL M HALISONI N BIZOGE

1078 RUHUWIKO SECONDARY SCHOOL M HALPHAN OMARY GEHO

1079 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M HALSON NASEKILE

1080 KALIUA SECONDARY SCHOOL M HALUI M EDSON

1081 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M HALVIN SHAYO

1082 IKIZU SECONDARY SCHOOL M HAMAD MWITA

1083 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M HAMAD SAIDI

1084 TUKUYU SECONDARY SCHOOL M HAMAD A KIPONZA

1085 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M HAMAD ATHUMAN HUSSEIN

1086 MBEZI SECONDARY SCHOOL M HAMAD IBRAHIM SEMBELLAH

1087 KIRINJIKO ISLAMIC SEMINARY M HAMAD NURU SUYA

1088 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M HAMAD RAMADHAN ISSA

1089 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M HAMAD S MSANGI

1090 KYELA SECONDARY SCHOOL M HAMADI ALLY

1091 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M HAMADI ALLY

1092 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL M HAMADI DOTTO

1093 MBEZI SECONDARY SCHOOL M HAMADI HAMIS

1094 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M HAMADI MWASHIUYA

1095 KIZUKA SECONDARY SCHOOL M HAMADI ABRAHMANI SAIDI

1096 MWEMBETOGWA SECONDARY SCHOOL M HAMADI HAMIDU MTAMBO

1097 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M HAMADI IMRANI KINYOGOLI

1098 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M HAMADI JUMA JUMANNE

1099 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M HAMADI KENYATA MRISHO

1100 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M HAMADI M MAKAME

1101 KISARIKA SECONDARY SCHOOL M HAMADI MGAZA IBRAHIM

1102 ILEJE SECONDARY SCHOOL M HAMADI N HAMADI

1103 PUGU SECONDARY SCHOOL M HAMADI RAMADHANI NJIKU

1104 NYAMPULUKANO SECONDARY SCHOOL M HAMADI S JUMA

1105 MAKITA SECONDARY SCHOOL M HAMDANI AKIDA

1106 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M HAMED JOHN

1107 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M HAMED M SALIM

1108 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL M HAMENYANA LUCAS MPILIPILI

1109 BUGENE SECONDARY SCHOOL M HAMENYIMANA KASUMALI

1110 MATAKA SECONDARY SCHOOL M HAMFREY KENJEVALE KAPOLA

1111 ENABOISHU SECONDARY SCHOOL M HAMID HASSAN

1112 SHAABAN ROBERT SECONDARY SCHOOL M HAMID A MBAROUK

1113 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M HAMID SALIM MIKOLE

1114 MAMBWE SECONDARY SCHOOL M HAMIDU ATHUMANI

1115 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M HAMIDU D CHAMBO

1116 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M HAMIDU H SAIDI

1117 MATAKA SECONDARY SCHOOL M HAMIDU K KITICHO

1118 MATAKA SECONDARY SCHOOL M HAMIDU OLIVA HAMZA

1119 MAWENI SECONDARY SCHOOL M HAMIDU P WAZIRI

1120 MKUU SECONDARY SCHOOL M HAMIDU R SENZOKA

1121 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M HAMIDU R YUSUPH

1122 MWAKAVUTA SECONDARY SCHOOL M HAMIDU RAMADHANI SABU

1123 SAME SECONDARY SCHOOL M HAMIDU S MKINGA

1124 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M HAMIDU SAMAGWA BALIHUTA

1125 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M HAMIDY HASHIMU

1126 AGAPE LUTHERAN J SEMINARY M HAMILTON JUMA MRUMA

1127 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M HAMIM M KAPAMBWE

1128 MAGUFULI SECONDARY SCHOOL M HAMIMU IDDI ABDI

1129 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M HAMIMU KASIMU MKILINDI

1130 MALAGARASI SECONDARY SCHOOL M HAMIS ABBAKARY

1131 LINDI SECONDARY SCHOOL M HAMIS ABDALLAH

1132 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M HAMIS AJARI

1133 NORTHERN HIGHLANDS SECONDARY SCHOOL M HAMIS ALLAWI

1134 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M HAMIS ALPHONCE

1135 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M HAMIS ATHUMAN

1136 IGUNGA SECONDARY SCHOOL M HAMIS BILALI

1137 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M HAMIS CHACHA

1138 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M HAMIS CHELEWA

1139 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M HAMIS CHIPITA

1140 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M HAMIS M HAMIS

1141 BINZA SECONDARY SCHOOL M HAMIS M SHIJA

1142 MEATU SECONDARY SCHOOL M HAMIS PETER AIDAN

1143 BINZA SECONDARY SCHOOL M HAMIS RAMADHAN HAMIS

1144 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M HAMIS S AHMADI

1145 MAKITA SECONDARY SCHOOL M HAMIS YUSUPH NGAILO

1146 SHAMBALAI SECONDARY SCHOOL M HAMISI EDISON

1147 KIUMA SECONDARY SCHOOL M HAMISI HAMISI

1148 MWINYI SECONDARY SCHOOL M HAMISI HASSANI

1149 MAMBWE SECONDARY SCHOOL M HAMISI JUMANNE

1150 USAGARA SECONDARY SCHOOL M HAMISI JUMANNE

1151 KALIUA SECONDARY SCHOOL M HAMISI OMARY

1152 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M HAMISI SAIDI

1153 TANZANIA ADVENTIST SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM UNUKU NDEMBO

1154 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM W KANOTI

1155 TARIME SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM W MAKUBI

1156 AIRWING SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM YAHAYA HUSSEIN

1157 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM YAKUBU OMARY

1158 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM YUSUPH OPPY

1159 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIM ZABRON NYENYELI

1160 MWINYI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU ABDALLAH

1161 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU ATHUMANI

1162 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU HASSANI

1163 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU HASSANI

1164 MBEYA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU KALINGA

1165 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU KANG'ONG'O

1166 KATOKE LWERU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU KHATWIBU

1167 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU KYAMBA

1168 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU MALIKI

1169 SADANI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU MOSYA

1170 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU MSUMI

1171 TAQWA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU PHILIPO

1172 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU SALUMU

1173 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU SALUMU

1174 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU SEIF

1175 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU SINDWAN

1176 GALANOS SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU YUSUPH

1177 MACECHU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU A JUMANNE

1178 MAKITA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU A NGIGI

1179 ARUSHA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU ARESTARICK MUSHI

1180 ECKERNFORDE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU ATHUMANI IBRAHIMU

1181 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU B MASALA

1182 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU C PAUL

1183 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M IBRAHIMU E KAFUKO

1184 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU GITILO NANA

1185 SAME SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU GROSSARY MGINA

1186 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU H SALIMU

1187 KYELA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU HALIFA DEFU

1188 UBUNGO ISLAMIC HIGH SCHOOL M IBRAHIMU HASSANI KABANGE

1189 LUGOBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU I HEMEDI

1190 SAME SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU ISSA PETRO

1191 MUYOVOZI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU J LYANDA

1192 SAME SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU JUMA MANGU

1193 ILBORU SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU KASULE MALASE

1194 RIDHWAA SEMINARY M IBRAHIMU KHAMISI HAMADI

1195 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU M MASSANA

1196 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU M OMARI

1197 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU M OMARY

1198 MWINYI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU M RASHIDI

1199 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU MATATA KIBIRITI

1200 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU MAULID CHOBU

1201 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU MUSA IBRAHIM

1202 MWENGE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU MUSA IBRAHIMU

1203 ECKERNFORDE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU R KAJEMBE

1204 PARANE SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU S RAMADHANI

1205 MUHEZA HIGH SCHOOL M IBRAHIMU S SAGUTI

1206 SUJI SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU SAFIEL KINKORO

1207 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU SAIDI KALELA

1208 KALIUA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU SHABAN RINGI

1209 MUNANILA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU SWALEHE NCHASI

1210 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU THABITI IBRAHIMU

1211 KONGWA SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU TWAHA IBRAHIMU

1212 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M IBRAHIMU W SAID

1213 NDANDA SECONDARY SCHOOL M ICHITEGELEZA M CHINZEH

1214 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M IDAN N YADUNIA

1215 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M IDD ALLY

1216 MWINYI SECONDARY SCHOOL M IDDY HUSSEIN ISSA

1217 MWENGE SECONDARY SCHOOL M IDDY J JUMANNE

1218 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M IDDY RIDHAA SWALEHE

1219 NEW ERA SECONDARY SCHOOL M IDDY S MPAMILA

1220 MWINYI SECONDARY SCHOOL M IDDY S RAMADHANI

1221 USAGARA SECONDARY SCHOOL M IDDY SAIDI KIRIMA

1222 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M IDFONCE JUSTIN KILUMILE

1223 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M IDHAA H NDITI

1224 USAGARA SECONDARY SCHOOL M IDID M MBAYE

1225 KIBITI SECONDARY SCHOOL M IDRISA HASHIM

1226 BINZA SECONDARY SCHOOL M IDRISA HASHIMU

1227 MOMBO SECONDARY SCHOOL M IDRISA RAMADHANI

1228 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M IDRISA A MPONDA

1229 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M IDRISA ABTWAI MSHANA

1230 MAMBWE SECONDARY SCHOOL M IDRISA HAMZA MATARI

1231 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M IDRISA IBRAHIMU ABDALAH

1232 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M IDRISA M MKOPOKA

1233 KIBITI SECONDARY SCHOOL M IDRISA RAJABU MAULIDI

1234 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M IDRISA S KAMBI

1235 ILBORU SECONDARY SCHOOL M JACKSON I SHELUKINDO

1236 MWENGE SECONDARY SCHOOL M JACKSON I TLUWAY

1237 AZANIA SECONDARY SCHOOL M JACKSON J CHARLES

1238 BULUBA SECONDARY SCHOOL M JACKSON J LABACHA

1239 LORD BADEN POWELL MEMORIAL SEC. SCHOOL M JACKSON J MAHOMELA

1240 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON J MAHUNDI

1241 LUFILYO SECONDARY SCHOOL M JACKSON J MBISE

1242 LOYOLA SECONDARY SCHOOL M JACKSON J MGOYO

1243 KARATU SECONDARY SCHOOL M JACKSON J MWANJELA

1244 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON J MZIMBE

1245 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON J NTIGIZU

1246 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON J NYEOJA

1247 MOSHI SECONDARY SCHOOL M JACKSON J PANGA

1248 KAWAWA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JAPHET EZEKIEL

1249 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JAPHETH MWAIPAJA

1250 MTWARA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON JERAD LUSINGO

1251 USA SEMINARY M JACKSON JEROME KIRIA

1252 GALANOS SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOHN MESHACK

1253 MUYOVOZI SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOHN THOMASY

1254 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSEPH BAZILIKANYE

1255 ST. AMEDEUS SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSEPH KULANGWA

1256 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSEPH MWANDIA

1257 KYELA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSEPH SAIDI

1258 NDANDA SECONDARY SCHOOL M JACKSON JOSSE NKYA

1259 GALANOS SECONDARY SCHOOL M JACKSON JULIUS MADEBE

1260 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M JACKSON K MTATIRO

1261 LUTENGANO SECONDARY SCHOOL M JACKSON KAISTONI MTAVANGU

1262 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M JACKSON KAIZILEGE ALEX

1263 MOMBO SECONDARY SCHOOL M JACKSON KALISTO CHATANDA

1264 MOSHI TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON L LESANIA

1265 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON L MALILA

1266 MKUU SECONDARY SCHOOL M JACKSON L MARIUS

1267 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M JACKSON L MWAIPUNGU

1268 MVUMI SECONDARY SCHOOL M JACKSON LAMECK SUNGURA

1269 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M JACKSON LAURENCE NZIKU

1270 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON LINUS NDINDE

1271 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON LUCAS KIBISA

1272 RUTABO SECONDARY SCHOOL M JACKSON M CHACHA

1273 PEACE SECONDARY SCHOOL M JACKSON M KATABARO

1274 MAGU SECONDARY SCHOOL M JACKSON M MAKUNJA

1275 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON M YOTHAM

1276 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MAGENI NG'HWAGILA

1277 NDANDA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MAKARIUS SIMWINGA

1278 MARA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MARCO PANGA

1279 NDANDA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MARTIN GOI

1280 MADABA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MATHEW SHECHAMBO

1281 CONSOLATA SEMINARY M JACKSON MATHIAS MUNGO

1282 KIFARU SECONDARY SCHOOL M JACKSON MELKIORY TARIMO

1283 MAGU SECONDARY SCHOOL M JACKSON MHOJA WILLIAM

1284 SWILLA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MICHAEL SANGA

1285 BARIADI SECONDARY SCHOOL M JACKSON MIHAYO SELEMAN

1286 MIONO SECONDARY SCHOOL M JACKSON MUHOZA JOHN

1287 CHATO SECONDARY SCHOOL M JACKSON MUSA MAGUNILA

1288 LWANGWA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MWAMINI NOAH

1289 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M JACKSON MWIKWABI MBANGO

1290 BAGAMOYO SECONDARY SCHOOL M JACKSON MWIMBA COSMAS

1291 NGUDU SECONDARY SCHOOL M JACKSON N EDWARD

1292 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M JACKSON NESTORY CHARLES

1293 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACKSON NOLASKO MDUGO

1294 NYARUBANDA SECONDARY SCHOOL M JACKSON NYAMVUGWA FALES

1295 BAOBAB SECONDARY SCHOOL M JACKSON O MICHAEL

1296 MAKUMIRA SECONDARY SCHOOL M JACKSON O NCHAGASI

1297 LILIAN KIBO SECONDARY SCHOOL M JACKSON OLIVARY SHAYO

1298 MAKITA SECONDARY SCHOOL M JACOB E MWAINE

1299 ITIGI SECONDARY SCHOOL M JACOB FEDRICK MBIJIMA

1300 MEATU SECONDARY SCHOOL M JACOB JOSEPH MAREGESI

1301 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M JACOB JOSEPH SAKRI

1302 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M JACOB M MSETI

1303 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M JACOB NICHOLAUS CHAWALA

1304 MAKITA SECONDARY SCHOOL M JACOB NICOLAUS NYALUSI

1305 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M JACOB ONANI LUVANDA

1306 NAMABENGO SECONDARY SCHOOL M JACOB R SUMUNI

1307 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M JACOB RAPHAEL KILAGA

1308 MINAKI SECONDARY SCHOOL M JACOB T OCTAVIAN

1309 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M JACOB WILLIAM MHAGAMA

1310 ITAMBA SECONDARY SCHOOL M JACOBO ANYAWILE NKINDA

1311 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M JACOBO YOHANA MTATURU

1312 KIDUGALA LUTHERAN SEMINARY M JACTAN ELIEZA NZIKU

1313 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M JADI MTESIGWA

1314 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M JADI JUMANNE KALINGA

1315 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M JAFAR JUMA MWAMBUSI

1316 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M JAFARI JUMA

1317 UYUI SECONDARY SCHOOL M JAFARI RAMADHANI

1318 KIUMA SECONDARY SCHOOL M JAFARI A ABEID

1319 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M KARIM SHABAN NASSORO

1320 GALANOS SECONDARY SCHOOL M KARIM Y HUSSEIN

1321 TARAKEA SECONDARY SCHOOL M KARIMU ABDALLAH

1322 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M KARIMU AHMADI

1323 TANDAHIMBA SECONDARY SCHOOL M KARIMU AMRI

1324 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M KARIMU HAMISI

1325 MAKONGO SECONDARY SCHOOL M KARIMU HARUNA

1326 RUHUWIKO SECONDARY SCHOOL M KARIMU HASSANI

1327 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M KARIMU MANYORI

1328 AZANIA SECONDARY SCHOOL M KARIMU MIRAJI

1329 NDANDA SECONDARY SCHOOL M KARIMU MOHAMEDI

1330 OCEAN SECONDARY SCHOOL M KARIMU MOHAMEDI

1331 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M KARIMU A KIGOGORO

1332 KWIRO SECONDARY SCHOOL M KARIMU A MASHINGA

1333 KALANGALALA SECONDARY SCHOOL M KARIMU ADAM HATIBU

1334 GALANOS SECONDARY SCHOOL M KARIMU B HAMISI

1335 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M KARIMU K KARIMU

1336 LIWALE DAY SECONDARY SCHOOL M KARIMU M ABDALA

1337 VUNJO SECONDARY SCHOOL M KARIMU M ISIMAIL

1338 ULAYASI SECONDARY SCHOOL M KARIMU M LUHINDI

1339 TUSIIME SECONDARY SCHOOL M KARIMU MTIMBO MIJOMBO

1340 MAJI YA CHAI SECONDARY SCHOOL M KARIMU MUSTAFA CHUNGWA

1341 LINDI SECONDARY SCHOOL M KARIMU R NASIBU

1342 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M KARIMU S KIPOZI

1343 MAPOSENI SECONDARY SCHOOL M KARIMU S MUSSA

1344 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M KARIMU S NANKUNA

1345 LOMWE SECONDARY SCHOOL M KARIMU SAIDI MSHANA

1346 MADABA SECONDARY SCHOOL M KARIMU W SENKELE

1347 KWIRO SECONDARY SCHOOL M KARIMU YAHYA HARUNA

1348 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M KARINDOGO M ZAKAYO

1349 J.J.MUNGAI SECONDARY SCHOOL M KARISIO FELIO SEVEYAGE

1350 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M KARISTO PHILIPO MWINUKA

1351 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M KARISTO RICHARD LIHAWA

1352 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M KARLMAX PAUL

1353 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M KAROL M NDUNGURU

1354 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M KAROLI KHAMIS

1355 TARIME SECONDARY SCHOOL M KAROLI MATHAYO

1356 BULUBA SECONDARY SCHOOL M KARONDA B JULIUS

1357 IKIZU SECONDARY SCHOOL M KARONGO MASERO JOHN

1358 MAJENGO SECONDARY SCHOOL M KARSTEN M MANG''ANA

1359 LYAMUNGO SECONDARY SCHOOL M KARUME G MOMOYA

1360 RUNGWE SECONDARY SCHOOL M KASABALALA A ISSA

1361 SAME SECONDARY SCHOOL M KASABUKU K ANTHONY

1362 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M KASALA E MAKENGO

1363 JITEGEMEE SECONDARY SCHOOL M KASALA M KASALA

1364 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M KASANDA MASUNGA

1365 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M KASANDA K SAMSON

1366 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M KASANDA MARTINE KUBIGWA

1367 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M KASARA DICKSON

1368 MWEMBENI SECONDARY SCHOOL M KASARA B NGOBOKA

1369 NKASI SECONDARY SCHOOL M KASASE MATHEW

1370 USAGARA SECONDARY SCHOOL M KASAZA NELSON NASUCHIWA

1371 SONI SEMINARY M KASBERT CLAUDIUS HAULE

1372 UMBWE SECONDARY SCHOOL M KASBETH ALPHONCE PILI

1373 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M KASEMA CLEMENT

1374 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M KASENGA MIHAMBO MKINGA

1375 NSUMBA SECONDARY SCHOOL M KASHABALE N IGANGATI

1376 NEW ERA SECONDARY SCHOOL M KASHATI MALALE

1377 MILAMBO SECONDARY SCHOOL M KASHATO MICHAEL

1378 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M KASHIDYE SAMADALI

1379 IWAWA SECONDARY SCHOOL M KASHINDYE JACKSON

1380 IWALANJE SECONDARY SCHOOL M KASHINDYE JUMA

1381 BOGWE SECONDARY SCHOOL M KASHINDYE P SALUM

1382 KALIUA SECONDARY SCHOOL M KASSIMU AHMAD KALIMA

1383 KIGONSERA SECONDARY SCHOOL M KASSIMU B ALLY

1384 MEATU SECONDARY SCHOOL M KASSIMU R SHIHA

1385 MWENGE SECONDARY SCHOOL M KASSIMU S MCHUCHURI

1386 MAKITA SECONDARY SCHOOL M KASTO TWIJULEGE GEORGE

1387 MWINYI SECONDARY SCHOOL M KASTORY EPIMACK MALIGITE

1388 MINAKI SECONDARY SCHOOL M KASTORY JACOB WIMBE

1389 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M KASTORY KALOLO CHISSY

1390 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M KASULE MSAFILI

1391 MATAKA SECONDARY SCHOOL M KASUSU ROBERT

1392 LORD BADEN POWELL MEMORIAL SEC. SCHOOL M KATASIEKO M MOGITU

1393 KIBITI SECONDARY SCHOOL M KATELEMBWE ISAYA KAKEME

1394 UWEMBA SECONDARY SCHOOL M KATO MUHAMMAD

1395 KALIUA SECONDARY SCHOOL M KATOKE SIMON KATOKE

1396 KALIUA SECONDARY SCHOOL M KATUNZI L STEPHANO

1397 USAGARA SECONDARY SCHOOL M KAUNGA FY MASUNGA

1398 KANTALAMBA SECONDARY SCHOOL M KAWAWA MUSA MTAYE

1399 BINZA SECONDARY SCHOOL M KAYILA MANDI

1400 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M KAZENIELI GODRICH MNYONE

1401 MACECHU SECONDARY SCHOOL M KAZIMILI J LUCAS

1402 MAKITA SECONDARY SCHOOL M KAZIMILI MARCO BUZIZILI

1403 URU SEMINARY M LAURIAN LAZARUS

1404 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M LAURIAN MAJULA

1405 HAGAFILO SEC. SCHOOL M LAURIAN GASPAR KABONGE

1406 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M LAURIAN LEONSI AXWESO

1407 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M LAURIAN PHILBERT BANTULAKI

1408 ST.MAURUS CHEMCHEMI SECONDARY SCHOOL M LAUSON DANIEL MHANGA

1409 NYERERE HIGH SCHOOL-MIGOLI M LAUSON LAULIANO NG'UMBI

1410 MALANGALI SECONDARY SCHOOL M LAUTO GERALD KYARUZI

1411 IYUNGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M LAVERN ANDREW JOHN

1412 SAME SECONDARY SCHOOL M LAWAMA STEPHEN KAGOROBA

1413 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M LAWI ISAYA

1414 MAFINGA SEMINARY M LAWI KIKOTI

1415 PIUS SECONDARY SCHOOL M LAWI MTEPA

1416 KONGWA SECONDARY SCHOOL M LAWI A MANYELEZI

1417 RUHUWIKO SECONDARY SCHOOL M LAWI DAIMON KYANDO

1418 IFUNDA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M LAWI GEORGE LUDEGE

1419 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M LAWRANCE CHARLES

1420 UWATA SECONDARY SCHOOL M LAWRANCE ERNEST KIBONA

1421 GALANOS SECONDARY SCHOOL M LAWRANCE M MWATINDILA

1422 MAKITA SECONDARY SCHOOL M LAWRANCE STANLEY NDOMBA

1423 MAHIWA SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE MAKIGI

1424 MWALIMU J K NYERERE SEC. SCHOOL M LAWRENCE BONIFACE LAUWO

1425 KYELA SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE D MWAKYAMBIKI

1426 BENJAMIN WILLIAM MKAPA HIGH SCHOOL M LAWRENCE J SIAME

1427 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE JACOB MWAKILIMA

1428 ST.ANTHONY'S SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE K LEMA

1429 KARATU SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE KALILE KAHINDI

1430 KAZIMA SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE M PETER

1431 NDANDA SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE N ALPHONCE

1432 LUBALA SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE P DAUD

1433 MSOLWA SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE RAPHAEL MURASHANI

1434 PUGU SECONDARY SCHOOL M LAWRENCE W KIHONGOSI

1435 NEW ERA SECONDARY SCHOOL M LAWRENT NGELEZYA

1436 SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M LAWRENT A MITUMBA

1437 TAMBAZA SECONDARY SCHOOL M LAWRENT D DEGERA

1438 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M LAYDA SAID LAYDA

1439 ILEJE SECONDARY SCHOOL M LAZACK K LEONARD

1440 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M LAZARO BENARD

1441 MUSOMA SECONDARY SCHOOL M LAZARO BONIPHACE

1442 ILBORU SECONDARY SCHOOL M LAZARO DONYO

1443 SONGEA BOYS SECONDARY SCHOOL M LAZARO EMMANUEL

1444 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M LAZARO FAUSTINI

1445 KIFARU SECONDARY SCHOOL M LAZARO FELIX

1446 PAMOJA SECONDARY SCHOOL M LAZARO JACOB

1447 TUNDURU SECONDARY SCHOOL M LAZARO KITWIKA

1448 TANGA TECHNICAL SECONDARY SCHOOL M LAZARO LEKOKO

1449 MADIBIRA SECONDARY SCHOOL M LAZARO MALAMLA

1450 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M LAZARO MAUGO

1451 LONGIDO SECONDARY SCHOOL M LAZARO MSEMELE

1452 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M LAZARO OLAIS

1453 NYAKATO SECONDARY SCHOOL M LAZARO PASTORY

1454 NYAKAHURA SECONDARY SCHOOL M LAZARO RAYMOND

1455 RORYA SECONDARY SCHOOL M LAZARO ROBERT

1456 ENGUTOTO SECONDARY SCHOOL M LAZARO SAIMALIE

1457 BINZA SECONDARY SCHOOL M LAZARO A KABATA

1458 ALFAGEMS SECONDARY SCHOOL M LAZARO A KINYELE

1459 KIGOMA SECONDARY SCHOOL M LAZARO A YUVENTINE

1460 KARATU SECONDARY SCHOOL M LAZARO ALFONCE BITANA

1461 SWILLA SECONDARY SCHOOL M LAZARO AMON SHITINDI

1462 MWAKALELI SECONDARY SCHOOL M LAZARO C MASIGE

1463 BWIRU BOYS SECONDARY SCHOOL M LAZARO CECIL MHINA

1464 SUJI SECONDARY SCHOOL M LAZARO CHARLES MKWAMA

1465 MATEMA BEACH SECONDARY SCHOOL M LAZARO CHITOJO ANDREW

1466 MWAKAVUTA SECONDARY SCHOOL M LENARD NTARISHWA MBONEA

1467 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M LENARDI FELISIAN MGAYA

1468 LULUMBA SECONDARY SCHOOL M LENGA NTEMINYANDA

1469 MEATU SECONDARY SCHOOL M LENGAY MUNGA

1470 MUHEZA HIGH SCHOOL M LENIN BARAYATA DYAGAYE

1471 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M LENNOX C LUTINWA

1472 NJOMBE SECONDARY SCHOOL M LEO MASONGELA

1473 MEATU SECONDARY SCHOOL M LEODIKARD LASWAY ALBERT

1474 MWENGE SECONDARY SCHOOL M LEON JOHN

1475 EAGLES SECONDARY SCHOOL M LEONAD T MRONDWA

1476 ST. VICENT SECONDARY SCHOOL M LEONARD ADROPH

1477 MATAI SECONDARY SCHOOL M LEONARD CHARLES

1478 HANDENI SECONDARY SCHOOL M LEONARD FRANK

1479 MANGUANJUKI SECONDARY SCHOOL M LEONARD GABRIEL

1480 MWENGE SECONDARY SCHOOL M LEONARD JOSEPH

1481 ST.MATTHEW'S SECONDARY SCHOOL M LEONARD LUTINDI

1482 RUNZEWE SECONDARY SCHOOL M MAGINA HOLELA

1483 OLD SHINYANGA SECONDARY SCHOOL M MAGINA JAMES

1484 SENGEREMA SECONDARY SCHOOL M MAGINA B JAMES

1485 MSAMALA SECONDARY SCHOOL M MAGINA I MASHAURI

1486 BEROYA SECONDARY SCHOOL M MAGINUS ZAKARIA NTILA

1487 TOSAMAGANGA SECONDARY SCHOOL M MAGNUS B SUMBE

1488 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M MAGNUS J KAMUGISHA

1489 MAUA SEMINARY M MAGNUS M GUNENA

1490 MARIAN BOYS SECONDARY SCHOOL M MAGNUS MSIGWA MUTAYOBA

1491 ULAYASI SECONDARY SCHOOL M MAGNUSI S KWAWILA

1492 ALI HASSAN MWINYI ISL. SEC. SCHOOL M MAGOHE MAJALIWA

1493 RORYA SECONDARY SCHOOL M MAGOIGA K NYAKITARE

1494 KILANGALANGA SECONDARY SCHOOL M MAGOMA HERMAN NAMGAMBWA

1495 THAQAAFA SECONDARY SCHOOL M MAGONGO HABIBU NINGA

1496 TARIME SECONDARY SCHOOL M MAGORI KICHERE

1497 KIBASILA SECONDARY SCHOOL M MAGORI MARWA

1498 IHUNGO SECONDARY SCHOOL M MAGORI NYAHOGA

1499 CHANGARAWE SECONDARY SCHOOL M MAGOTI HAMIS

1500 KIBAHA SECONDARY SCHOOL M MAGOTI A MASOTA
Viewing all 12768 articles
Browse latest View live


<script src="https://jsc.adskeeper.com/r/s/rssing.com.1596347.js" async> </script>