![]()
Uingereza
“How was Nigeria?”
“Its was fine but the search for professor Owo became unsuccessful!”(Nigeria ilikuwa nzuri lakini hatukufanikiwa kumpata profesa Owo!)
“Why?”(Kwanini?)
“They said he died in an accident while on journey in Cambodia!”(Walisema alikufa akiwa safarini huko Cambodia)
Wapelelezi wa Scortland Yard waliokuwa wametumwa nchini Nigeria kumsaka profesa Owo walimweleza mkuu wao kila kitu walichokiona nchini humo na sababu iliyowafanya washindwe kumpata profesa Owo.
“Welcome home!”(Karibuni nyumbani)Mkuu wao wa kazi aliwakaribisha nyumbani.
****
Pamoja na umri mkubwa aliokuwa nao mke wa chifu Onuku penzi kati yake na Harrison lilizidi kukomaa na mama alizidi kuchanganyikiwa zaidi kadri siku zilivyozidi kupita na Harrison nae alizidi kumpa mama mapenzi mazito zaidi ili azidi kumchanganya na kupata mzigo zaidi ya gesi bure na kusafirisha Uganda ambako alijipatia pesa nyingi na kuzidi kutajirika pamoja na kuwa afya yake hakuiamini.
Kila chifu Onuku aliposafiri mke wake alihamia nyumbani kwa Harrison ambako walitanua na kufaidi maisha!
Lagos nzima waliuelewa uhusiano uliokuwepo kati ya Harrison na mke wa chifu, ilivyoonekana ni chifu peke yake ndiye hakulielewa jambo hilo na hapakuwa na mtu wa kumpa ukweli kwa sababu watu wote walimwogopa na kumhofia! Ilikuwa si rahisi mtu kumtamkia chifu jambo hilo sababu watu wote walijua ni kiasi gani alimheshimu na kumwamini mke wake!
Ili kuondoa wasiwasi ambao alihisi ilibidi mke wa chifu amtambulishe Harrison kwa mumewe kama mteja wao wa gesi kutoka Uganda! Bila kufahamu kilichokuwa kikiendela kati yao chifu Onuku alifurahi sana kukutana na Harrison.
“Ni mteja wetu mzuri kwani ananunua gesi nyingi sana kila mwezi!”
“Kijana hongera sana ni vijana wachache sana wanaoweza kufanya biashara vizuri, wengi wanaishia kutumbua tu!”
“Ahsante sana mzee nimefurahi sana kukufahamu maana mara nyingi umekuwa safarini, muda wote nimekuwa nikifanya kazi na mama tu!”
“Hamna matatizo mama yako anaiweza kazi vizuri sana sina wasiwasi wowote juu yake, ninafikiri mnafanya kazi vizuri au siyo mama?”Chifu alimgeukia mke wake.
“Vizuri sana huyu ni kijana safi sana hana matatizo na anatulipa vizuri!”
“Kwa hivi sasa anaishi wapi hapa Lagos?”
“Yupo Lagos hoteli!”
“Kijana kwanini unaishi hotelini wakati sisi wazazi wako tuna nyumba nzuri na kubwa kiasi hiki?”
“Napenda kuishi kwa uhuru baba!”
“Lakini pia hapa kwetu unaweza kuishi vizuri kwa uhuru, tuna nyumba nyingine kubwa ipo kulee mwisho mbali kabisa na hii ya kwetu kwani mtategemea kuishi hapa kwa muda gani?”
“Mimi?”
“Ndiyo!”
“Nitakaa hapa kwa muda mrefu sana maana bado biashara yangu inaendelea!”
“Basi tafadhali naomba uhamie hapa nyumbani, mama hebu hakikisha mteja anahamia hapa leo hiihii, unataka aje kukutana na watu wengine wamchukue biashara ni ushindani!” Alisema chifu Onuku huku akitabasamu hakujua kama alilokuwa akilifanya ni kosa kubwa.
Ni siku hiyo hiyo tu mkewe alihakikisha Harrison amehamisha begi lake la nguo kutoka katika nyumba aliyokuwa amempangishia.
“Sasa itakuwaje?”
“Kwa sababu anang’ang’ania wewe hamia tu tena atakuwa ameturahisishia mambo yetu kwani kila atakapokuwa safarini wewe utakuwa mume wangu, shauri yake!”
“Sawa vipi kuhusu vitu tulivyonavyo ndani ya nyumba?”
“Nitaviuza na nyumba nitaipangisha kwa watu wengine wakae sawa darling?”
“Hakuna tatizo!”
Harrison alipoonyeshwa nyumba aliyotaka kuishi alishindwa hata kuamini, ilikuwa nyumba kubwa nzuri na yenye kila kitu cha thamini ndani yake ilijitegemea kwa kila kitu na Harrison alitambulishwa kwa Stella msichana wa kazi aliyetakiwa kumfanyia kila kitu akiwa hapo nyumbani.
Watu wote nchini Nigeria waliamini chifu Onuku alikufa katika ajali ya gari na aliyeijua siri kuwa hakufa alikuwa ni mkewe peke yake na pamoja na kumpenda Harrison hakudiriki kumwambia siri hiyo hata siku moja.
*****
“Mzee yupo kweli?”
“Yupo ila huwezi kumwona huwa haonani na watu kirahisi, akiwa hapa nyumbani hupatikana nyuma ya kompyuta akifanya mahesabu yake! Na huondoka asubuhi sana kwenda kwenye shunguli zake nakurudi usiku ila anasafiri leo hii kwenda Uingereza!”
“Aisee kwa hiyo tutapata nafasi ya kuonana siyo?” Aliuliza Harrison.
“Siyo kuonana tu ila utakuwa unalala chumbani kwangu mpaka atakaporudi!”
“Hapana! Je akinikuta ndani nitafanya nini?”
“Hawezi kukukuta kwa sababu hunipigia simu kabla ya kurudi!”
“Kweli?”
“Ndiyo!”
Jioni ya siku hiyo Harrison na mke wa chifu walimsindikiza chifu Onuku uwanja wa ndege katika safari yake ya wiki tatu nchini Uingereza, kila mtu moyoni mwake siku hiyo alikuwa na furaha kupita kiasi, walifurahia safari ya chifu Onuku ili wapate nafasi ya kutanua na kufanya mambo yao vizuri na kweli siku hiyohiyo usiku Harrison alihamia katika chumba cha chifu Onuku na wakaanza kufaidi maisha pamoja.
Siku moja kabla ya chifu Onuku kurejea kutoka safarini Harrison alirejea tena chumbani kwake, hakuna mtu aliyehisi kitu chochote kati ya Harrison na mama Onuku kwa sababu ya tofauti kubwa ya umri iliyokuwepo katikati yao, kwa mama Onuku Harrison alikuwa ni kama mtoto wake wa kuzaa.
Mpaka miezi sita baadaye Harrison alikuwa bado akiishi katika himaya ya chifu Onuku, afya yake ilizidi kudhoofika siku hadi siku kwa ugonjwa wa kifua! Kwa sababu alishakuwa kama mtoto wa familia ya chifu Onuku na mkewe, walilazimika kumshughulikia kwa matibabu, alikohoa sana usiku na alipopimwa makohozi mara tatu alionekana kuwa na kifua kikuu.
Hapakuwa na suala jingine la kufanya zaidi ya kumrejesha nchini Uganda ambako miezi sita baadaye alifariki dunia kwa ugonjwa wa Ukimwi! Idadi kubwa ya vijana wa rika lake nchini Uganda walikuwa wamekufa kwa ugonjwa huo hatari.
Hivyo hakuna aliyeshangazwa sana na kifo cha Harrison, watu walishalia sana mpaka mioyo yao ikawa sugu sababu katika eneo la Mbalala alikoishi kwa mwezi mmoja walikadiriwa kufa vijana wasiopungua wawili kwa ugonjwa huo
***
Taarifa ziliporudishwa Nigeria kuwa Harrison alikufa kwa Ukimwi watu wengi waliomfahamu walisikitika sana kwani wakati huo ndio ugonjwa huo ulishaanza kuitishia nchi hiyo ingawa kulikuwa hakujawa na wagonjwa wengi sana wa Ukimwi bado.
Mke wa chifu alilia sana kusikia habari hizo na kila siku mume wake aliendelea kumfariji akijua alisikitishwa sana na kifo cha mteja wake, kumbe mama alilia kwa sababu alijua hata yeye Ukimwi alikuwa nao na angekufa muda si mrefu, kilichomuumiza zaidi ni kumwambukiza mumewe ambaye hakushtahili kabisa kushiriki katika kifo hicho.
Kwa wiki nzima mke wa chifu alilia na alikuwa na simanzi baya moyoni mwake, alishindwa kula na hata kusema chochote, ilimlazimu chifu aache kazi zake zote na kuanza kushinda nyumbani.
Siku ya sita chifu alilazimika kuondoka nyumbani kwa muda mfupi kuelekea kwenye visima vyao vya mafuta kaskazini ya Nigeria ili kuangalia shughuli zao ziliendelea vipi? Hakukaa sana lakini aliporudi nyumbani kwake muda wa saa kumi jioni aligutuka alipokuta barua ya ajabu sebuleni kwake!
Mpendwa,
Owo!
Kifo cha Harrison kinamaanisha kifo changu mimi na kifo changu kinaamisha kifo chako!.
Moyo wa chifu Onuku uliruka pigo moja alihisi kuishiwa nguvu miguuni, barua ile ilimtisha sana!
Nitaona aibu sana nitakapokuangalia usoni pindi nitakapoanza kuugua? Nimeamua kufa ili kujiepusha na hasira yako nakiri kwa mdomo wangu kuwa nilikutana kimwili na Harrison na nina imani nimeambukizwa Ukimwi na hiyo inaamaanisha wote ikiwemo wewe pia umeambukizwa na sote tutakufa! Nimeamua kutangulia ili kuuepuka uso wako, Ukimwi unatesa na unaumiza na mimi sitaki kufa kifo cha aina hiyo! Ninajisikia mkosaji sana moyoni mwangu na sasa ninakuomba sana uniruhusu kukutangulia!” Ilimaliza barua hiyo.
Wakati anamaliza kuisoma barua hiyo chifu mwili mzima ulikuwa ukitetemeka na jasho jingi likimtoka, aliingia moja kwa moja hadi chumbani nako pia hakumkuta mkewe, alishindwa kuelewa alikuwa wapi alianza kuita lakini hakuitikiwa.
Ghafla alisikia mkojo umembana na kuingia bafuni kukojoa ni huko bafuni ndiko alikomkuta mkewe akiwa ameanguka chini mkojo ulikatika palepale na kusahau kilichomfanya aingia bafuni!
Alimtingisha mke wake bila kuamka, aligundua mke wake tayari alishakufa, kwa haraka alitoka nje na kusogeza gari hadi mlangoni, akiwa amechanganyikiwa aliubeba mwili wa mke wake na kuuingiza ndani ya gari, wafanyakazi wote wa nyumba yake walishangaa ni nini kilikuwa kimempata mke wa bosi wao, walijaribu kumdadisi chifu lakini hakuwapa jibu badala yake aliomba geti lifunguliwe na kutoa gari nje.
Alipofika hospitali na madaktari walipopima alikuwa tayari ameshaaga dunia! Chifu aliomba mwili wa mke wake ufanyiwe uchunguzi wa kutosha kugundua ni ni hasa kilimuua, majibu yalipotoka ilibainika kuwa alikunywa kiasi kikubwa cha dawa aina ya Diazepam na kufa akiwa usingizini.
Chifu alichanganyikiwa kupita kiasi, aligundua ugonjwa alioutengeneza mwenyewe na kufikiri aliukimbia ulikuwa umeingia ndani ya damu yake, alilia sana lakini ukweli ulibaki palepale kuwa ukimwi ulikuwa umerejea tena kwake, alijilaumu mwenyewe kwa makosa mengi, kwa kuiua jamii ya watu wasiokuwa na hatia.
Hata yeye mwenyewe alishindwa kujipa msamaha! Ukimwi kufika kwake kupitia kwa mke wake aliichukulia kama adhabu kwa kazi yake haramu aliyoifanya, hakuwa na njia ya kujiokoa mwenyewe pamoja na kuwa ni yeye aliyemtengeneza mdudu huyo, aliikubali hali hiyo na kusubiri kifo.
Miaka miwili baadaye:
Hali ya chifu Onuku ilikuwa mbaya alikuwa mgonjwa taaban akiwa amelazwa katika moja ya hospitali zake, iligundulika wazi ulikuwa ni Ukimwi na alikuwa akisubiri siku zake mamia ya watu walifurika kila siku hospitalini kumsalimia chifu Onuku aliyekuwa akiugua Ukimwi.
Wengi wa walioufahamu uhusiano uliowahi kuwepo kati ya mke wa chifu na Harrison walimtupia lawama nyingi sana mkewe huyo kwa kumuua chifu wao aliyewasaidia
Siku chache kabla ya kifo chake chifu Onuku aliita waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali vya nje na vya ndani ya nchini Nigeria, alikuwa ameamua kuwaeleza ukweli juu ya ugonjwa wake.
“Nimewaita kuwaelezeni ukweli, mimi ninayeongea na nyinyi ndiye chifu Onuku mwenyewe niliyesingizia kupatwa na ajali na kufa, niliibadilisha sura yangu makusudi ili kuepuka watu waliokuwa wakinitafuta, nilisakwa sana na serikali ya Uingereza.
“Ulisakwa kwa nini?”
“Kabla ya kuja hapa Nigeria kutoka Uingereza niliitwa profesa Owo! Mimi pamoja na wenzangu wawili tulitengeneza wadudu ambao wanasababisha ugonjwa huu unaoniua mimi mwenyewe na wadudu hawa walikuwa katika chanjo ya polio na kuletwa huku Afrika nililipwa pesa nyingi sana ambazo nilikuja nazo hapa Nigeria kuanzisha biashara yangu!”
Alielezea kila kitu na mwisho aliomba dunia imsamehe kabla hajafa! Taarifa hizo zilipofika Uingereza waliletwa wapelelezi kumkamata ili akashtakiwe Uingereza lakini alifariki njiani kabla hata ya ndege kutua nchini humo.
Mwisho.