ILIPOISHIA...
“Mh! Kweli hapa nimepata mke,” akajisemea moyoni mwake Chris.
SASA ENDELEA...
HISIA za kuwa ndani ya ndoa zilimvamia Chris kwa kasi sana, ni kweli alikuwa anakimbia kuoa muda mrefu kwa sababu hakupata mwanamke ambaye amempenda kwa dhati ya moyo wake, lakini safari hii alikiri kuwa kweli Laura alikidhi vigezo vyote.
“Kama sijawahi kukuambia, naomba nikuambie leo kutoka moyoni mwangu, nakupenda sana Laura,” akasema Chris.
Laura akacheka sana!
“Mbona unacheka?”
“Ni mara ngapi baby umeniambia kuwa unanipenda? Mara nyingi tu... hata jana usiku uliniambia neno hilo.”
“Basi kama ndivyo, naomba nibadilishe maneno, leo utambue kuwa ninasema kwa kumaanisha kuliko siku zote; nakupenda sana Laura, sijajuta kuwa na wewe na kamwe sitajuta mpenzi wangu.”
“Ahsante sana mpenzi wangu kwa maneno yako mazuri.”
Kimya kifupi kilipita, wote wakiendelea kula. Kila mmoja kichwani mwake alikuwa na mawazo yake. Laura alikuwa akiota ndoa na Chris. Kijana mtanashati kama yule, maarufu anayejulikana ndani na nje ya Tanzania kwa kazi yake ya sanaa lakini zaidi ya yote daktari!
Chris yeye alikuwa akifikiria zaidi kuhusu baba yake, ni kweli amempenda sana Laura, lakini maelekezo ya baba yake ilikuwa lazima mkewe atokee kijijini kwao. Tayari alimshamdanganya kuwa mchumba amepatikana kijijini.
“Itakuwaje? Mbona naanza kuona dalili mbaya za kumkosa Laura?” akawaza Chris.
“Lakini nitajua cha kufanya, hawezi kunisumbua. Kichwa changu kinafanya kazi sawasawa,” akajiliwaza kwa maneno hayo.
Ukimya huo wa mawazo ya ndani kwa ndani huku kila mmoja akiwaza lake, ulivunjwa na Laura: “Halafu dear, kuna jambo nataka kukuuliza.”
“Uliza tu mama.”
“Imekuwaje wewe daktari mzima, ukaingia kwenye mambo ya filamu?”
“Kwanza kwa nini umesema daktari mzima? Inamaana hupendi mimi kuwa msanii?”
“Sina maana hiyo mpenzi wangu. Ninavyojua mimi, wengi wanaoingia kwenye sanaa huwa hawana elimu ya kutosha lakini wewe kitaaluma uko vizuri kabisa. Kwa nini sasa ukaingia kwenye filamu?”
“Ni habari ndefu Laura lakini jambo kubwa ambalo nataka kukuambia ujue, napenda sana sanaa na siku zote ndiyo imekuwa chanzo cha ugomvi kati yangu na mzee wangu. Baba alitaka sana niwe daktari, ndiyo maana alinilazimilisha nikazanie masomo ya Sayansi.
“Alijua kunishawishi, kweli nikajikuta taratibu nimeanza kupenda masomo ya Sayansi na nikayamudu vizuri. Baada ya kumaliza kidato cha sita, mzee alinipeleka Uingereza kusomea udaktari. Nimeishi huko kwa miaka saba.
“Pamoja na hayo, bado ndani yangu kulikuwa na chembechembe za sanaa, ndiyo maana nikaamua kurudi nchini kwa lengo hilo, lakini kwa sababu kiu ya mzee ni kutaka kusikia nikiitwa daktari tena nikiwatibu watu, nikaamua kuomba kazi Hospitali ya Kinondoni.
“Mpaka sasa nafanya kazi hapo, lakini nikiendelea na sanaa kama kawaida. Bosi wangu hana tatizo na hilo, maana nilimweleza hali halisi kabla ya kuanza kazi. Naijua vizuri taaluma yangu lakini napenda sana sanaa, vyote vinanipa fedha na ninafanya vyote kwa wakati mmoja,” alisema Chris.
“Hongera yako.”
“Ahsante.”
Walipomaliza kula, wote walitoka kwa pamoja na kuingia kwenye gari la Chris, wakaenda moja kwa moja kazini kwa Chris, akamtambulisha kwa baadhi ya wafanyakazi wenzake kisha akamruhusu aendelee na mizunguko yake mingine.
Laura hakuwa na mambo mengi sana siku hiyo, kikubwa hasa ilikuwa ni kwenda Kariakoo kufanya manunuzi ya mavazi na vitu vingine vya kwenda navyo Singida.
***
Laura alikaa Dar kwa wiki nzima akipoteza vipindi vyote kwa muda huo. Siku ya kurejea Singida ilikuwa ya huzuni sana kwake. Chris alimsindikiza mpaka kituoni, Ubungo ambapo alikuwa ameshamkatia tiketi kwenye basi la ABC.
Laura aliagana na Chris wakiwa wamekumbatiana kwa muda mrefu sana. Ilikuwa ni kama hawakuwa na mpango wa kuachiana. Mwili wa Laura ulisisimka sana, alitamani kuendelea kubaki Dar lakini haikuwezekana, alipaswa awahi masomo Singida.
Muda wa safari ulipowadia, hakuwa na jinsi – aliingia garini na kumwacha Chris akiwa anamtazama kupitia dirishani. Saa 12:00 asubuhi, gari lilianza kuondoka. Laura akampungia Chris mkono huku akitoa machozi, ni kama walikuwa wanarekodi filamu lakini ilikuwa kweli.
Waliendelea kupungiana mikono mpaka gari lilipofika mbali. Chris akaenda kwenye maegesho, akaingia kwenye gari lake, akaondoka. Ilikuwa safari ya kuelekea kazini kwake. Saa 3:00 asubuhi hiyo alikuwa na kazi ngumu sana ya kumfanyia mtu upasuaji mkubwa!